Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Nyakati na Majira Mikononi mwa Yehova
    Mnara wa Mlinzi—1998 | Septemba 15
    • Nyakati na Majira Mikononi mwa Yehova

      “Si juu yenu kupata ujuzi wa nyakati au majira ambayo Baba ameweka katika mamlaka yake mwenyewe.”—MATENDO 1:7.

      1. Yesu alijibuje maswali ya mitume wake yaliyohusiana na wakati?

      NI JAMBO lifaalo zaidi kwa wale “wanaougua na kulia kwa sababu ya machukizo yote yanayofanyika” katika Jumuiya ya Wakristo na duniani kote kuuliza ni lini mfumo huu mwovu wa mambo utakapoisha na mahali pake kuchukuliwa na ulimwengu mwadilifu wa Mungu? (Ezekieli 9:4; 2 Petro 3:13) Mitume wa Yesu walimwuliza maswali yaliyohusiana na wakati, muda mfupi kabla ya kifo chake na baada ya ufufuo wake. (Mathayo 24:3; Matendo 1:6) Hata hivyo, katika jibu lake, Yesu hakuwapa njia ya kukadiria tarehe. Katika kisa kimoja aliwapa ishara yenye mambo mengi, na katika kingine akasema kwamba ‘haikuwa juu yao kupata ujuzi wa nyakati au majira ambayo Baba ameweka katika mamlaka yake mwenyewe.’—Matendo 1:7.

      2. Kwa nini yaweza kusemwa kwamba Yesu hakujua sikuzote ratiba ya Baba yake ya matukio ambayo yangetokea wakati wa mwisho?

      2 Ingawa Yesu ni Mwana mzaliwa-pekee wa Yehova, yeye mwenyewe hakujua sikuzote ratiba ya Baba yake ya matukio. Katika unabii wake kuhusu siku za mwisho, Yesu alikiri hivi kwa unyenyekevu: “Kuhusu siku hiyo na saa hiyo hakuna mtu ajuaye, wala hao malaika wa mbingu wala Mwana, ila Baba tu.” (Mathayo 24:36) Yesu alikuwa tayari kumngojea Baba yake kwa subira ili amfunulie wakati hususa wa kuchukuliwa hatua ya kuharibu mfumo huu mwovu wa mambo.a

      3. Twaweza kujifunza nini kutokana na majibu ya Yesu kwa maswali kuhusu kusudi la Mungu?

      3 Mambo mawili yaweza kufasiriwa kutokana na njia ambayo Yesu alijibu maswali kuhusu wakati ambapo mambo yangetukia kwa utimizo wa kusudi la Mungu. Kwanza, Yehova ana ratiba; na pili, kwamba yeye pekee ndiye huiweka, nao watumishi wake hawawezi kutarajia wapashwe habari hususa kimbele kuhusu nyakati au majira yake.

      Nyakati na Majira ya Yehova

      4. Maneno ya Kigiriki yatafsiriwayo “nyakati” na “majira” kwenye Matendo 1:7 humaanisha nini?

      4 “Nyakati” na “majira” humaanisha nini? Taarifa ya Yesu iliyorekodiwa kwenye Matendo 1:7 ina sehemu mbili kuhusiana na wakati. Neno la Kigiriki litafsiriwalo “nyakati” humaanisha “wakati katika maana ya kipindi cha wakati,” muda fulani (mrefu au mfupi). “Majira” ni tafsiri ya neno linalorejezea wakati uliopangwa au uliowekwa, majira hususa, au kipindi, chenye kutambulishwa kwa mambo fulani. Kuhusu maneno hayo mawili ya awali, W. E. Vine asema: “Katika Matendo 1:7, ‘Baba ameweka kulingana na mamlaka Yake mwenyewe’ nyakati (chronos), urefu wa vipindi, na pia majira (kairos), vipindi vyenye kutambulishwa kwa matukio fulani.”

      5. Yehova alimjulisha Noa juu ya kusudi Lake la kuharibu ulimwengu mfisadi lini, naye Noa alitekeleza utume gani wenye sehemu mbili?

      5 Kabla ya Furiko, Mungu aliweka kipindi cha wakati kisichozidi miaka 120 kwa ulimwengu mfisadi uliokuwa umetokezwa na wanadamu na malaika waasi waliotwaa miili yenye kuonekana. (Mwanzo 6:1-3) Noa mwenye kumhofu Mungu alikuwa na umri wa miaka 480 wakati huo. (Mwanzo 7:6) Hakuwa na mtoto na alibaki hivyo kwa miaka mingine 20. (Mwanzo 5:32) Muda mrefu baadaye, Mungu alimjulisha Noa juu ya kusudi Lake la kuondoa uovu duniani baada tu ya wana wake kuwa watu wazima na kuoa. (Mwanzo 6:9-13, 18) Hata ingawa wakati huo Noa alikabidhiwa utume wenye sehemu mbili wa kujenga safina na kuhubiria watu wa siku yake, Yehova hakumfunulia ratiba yake.—Mwanzo 6:14; 2 Petro 2:5.

      6. (a) Noa alionyeshaje kwamba aliacha mambo yaliyohusiana na wakati mikononi mwa Yehova? (b) Twawezaje kufuata kielelezo cha Noa?

      6 Kwa miongo mingi—labda kwa nusu karne—‘Noa alifanya yote kama Mungu alivyomwamuru.’ Noa alifanya hivyo “kwa imani,” bila kujua tarehe hususa. (Mwanzo 6:22, BHN; Waebrania 11:7) Yehova hakumjulisha wakati hususa wa matukio hadi juma moja tu kabla ya wakati ambapo Gharika ingeanza. (Mwanzo 7:1-5) Tumaini na imani thabiti ya Noa katika Yehova ilimwezesha aache mambo yaliyohusiana na wakati mikononi mwa Yehova. Ni lazima Noa awe alishukuru kama nini alipohisi ulinzi wa Yehova wakati wa Furiko na baadaye akatoka katika safina kuingia kwenye dunia iliyosafishwa! Tukiwa na tumaini kama hilo la kuokolewa karibuni, je, haitupasi kudhihirisha imani sawa na hiyo katika Mungu?

      7, 8. (a) Mataifa na mamlaka za ulimwengu zilikujaje kuwako? (b) Yehova aliagizaje ‘nyakati zilizowekwa na mipaka iliyowekwa ya makao ya watu’?

      7 Baada ya Furiko, wengi wa wazao wa Noa waliacha ibada ya kweli ya Yehova. Wakinuia kubaki mahali palepale, walianza kujenga jiji na mnara kwa ajili ya ibada isiyo ya kweli. Yehova aliamua kwamba ulikuwa wakati wa kuingilia kati. Alivuruga lugha yao, ‘akawatawanya kutoka [Babeli] waende usoni pa nchi yote.’ (Mwanzo 11:4, 8, 9) Baadaye, vikundi hivyo vya lugha vilisitawi kuwa mataifa, baadhi ya hivyo vikitwaa mataifa mengine na kuwa mamlaka za kimkoa, na hata kuwa mamlaka za ulimwengu.—Mwanzo 10:32.

      8 Kwa kupatana na kutimizwa kwa kusudi lake, mara kwa mara Mungu aliamua mipaka ya kitaifa na pia wakati ambapo taifa fulani lingetawala eneo la karibu au kutawala likiwa mamlaka ya ulimwengu. (Mwanzo 15:13, 14, 18-21; Kutoka 23:31; Kumbukumbu la Torati 2:17-22; Danieli 8:5-7, 20, 21) Mtume Paulo alirejezea sehemu hii ya nyakati na majira ya Yehova alipowaambia hivi Wagiriki wenye akili huko Athene: “Mungu aliyeufanya ulimwengu na vitu vyote vilivyo katika huo . . . alifanya kutoka kwa mtu mmoja kila taifa la watu, ili wakae juu ya uso mzima wa dunia, naye aliagiza nyakati zilizowekwa na mipaka iliyowekwa ya makao ya watu.”—Matendo 17:24, 26.

      9. Yehova ‘amebadilishaje nyakati na majira’ kuhusiana na wafalme?

      9 Hilo halimaanishi kwamba Yehova ndiye husababisha ushindi mbalimbali wa kisiasa na mabadiliko miongoni mwa mataifa. Hata hivyo, ili atimize kusudi lake, yeye aweza kuingilia kati akichagua kufanya hivyo. Hivyo, nabii Danieli, ambaye angeshuhudia kuangamizwa kwa Mamlaka ya Ulimwengu ya Babiloni, na mahali pake kuchukuliwa na Umedi na Uajemi, alisema hivi kumhusu Yehova: “Hubadilisha nyakati na majira, huwaondoa na kuwatawaza wafalme. Wenye busara huwapa hekima, wenye maarifa huwaongezea ufahamu.”—Danieli 2:21, BHN; Isaya 44:24–45:7.

      ‘Wakati Ulikuwa Ukikaribia’

      10, 11. (a) Yehova aliweka kimbele kadiri gani ule wakati ambapo angekomboa wazao wa Abrahamu kutoka utumwani? (b) Ni nini kidokezacho kwamba Waisraeli hawakujua wakati hususa ambapo wangekombolewa?

      10 Zaidi ya karne nne kimbele, Yehova aliweka mwaka hususa ambapo angemtweza mfalme wa Mamlaka ya Ulimwengu ya Misri na kukomboa wazao wa Abrahamu kutoka utumwani. Akifunua kusudi lake kwa Abrahamu, Mungu aliahidi: “Ujue hakika ya kwamba wazawa wako watakaa kama wageni katika nchi isiyo yao, watakuwa watumwa na watateswa kwa muda wa miaka mia nne. Hata hivyo, nitaliadhibu taifa watakalolitumikia, na hatimaye watatoka wakiwa na mali nyingi.” (Mwanzo 15:13, 14, BHN) Katika muhtasari wake wa historia ya Israeli, alioutoa mbele ya Sanhedrini, Stefano alirejezea kipindi hicho cha miaka 400 na kusema: “Wakati ule tu ulipokuwa ukikaribia kwa ajili ya utimizo wa ahadi ambayo Mungu alikuwa amemtangazia Abrahamu waziwazi, watu walikua na kuzidi katika Misri, mpaka kukainuka mfalme tofauti juu ya Misri, ambaye hakujua habari za Yosefu.”—Matendo 7:6, 17, 18.

      11 Farao huyo mpya aliwashusha Waisraeli wakawa watumwa. Musa alikuwa bado hajaandika kitabu cha Mwanzo, ingawa yaelekea kwamba ahadi za Yehova kwa Abrahamu zilikuwa zimepitishwa ama kwa mdomo ama kwa namna ya maandishi. Hata hivyo, yaonekana kwamba habari ambazo Waisraeli walijua hazikuwawezesha kukadiria tarehe hususa ya kukombolewa kwao kutoka katika uonevu. Mungu alijua wakati ambapo angewakomboa, lakini yaonekana Waisraeli waliokuwa wakiteseka hawakuwa na habari. Twasoma: “Baada ya siku zile nyingi mfalme wa Misri akafa; wana wa Israeli wakaugua kwa sababu ya ule utumwa, wakalia; kilio chao kikafika juu kwa Mungu kwa sababu ya ule utumwa. Mungu akasikia kuugua kwao, Mungu akakumbuka agano lake alilolifanya na Ibrahimu na Isaka na Yakobo. Mungu akawaona wana wa Israeli, na Mungu akawaangalia.”—Kutoka 2:23-25.

      12. Stefano alionyeshaje kwamba Musa alitenda kabla ya wakati wa Yehova?

      12 Ukosefu huo wa ujuzi juu ya wakati hususa wa kukombolewa kwa Israeli waweza pia kufasiriwa kutokana na muhtasari wa Stefano. Akizungumza juu ya Musa, yeye alisema: “Wakati wa mwaka wake wa arobaini ulipokuwa ukitimizwa, ikaja ndani ya moyo wake kufanya ukaguzi wa ndugu zake, wana wa Israeli. Naye alipoona mara hiyo mtu fulani akitendwa isivyo haki, alimtetea na kutekeleza kisasi kwa ajili ya yule mwenye kutendwa vibaya kwa kumpiga hata chini Mmisri. Alikuwa akidhani ndugu zake wangefahamu ya kwamba Mungu alikuwa akiwapa wao wokovu kwa mkono wake, lakini hawakufahamu hilo.” (Matendo 7:23-25) Musa hapa alijaribu kukomboa Israeli, miaka 40 kabla ya wakati wa Mungu. Stefano alionyesha kwamba Musa angelazimika kungoja kwa miaka mingine 40 kabla ya Mungu ‘kuwapa Waisraeli wokovu kwa mkono wake.’—Matendo 7:30-36.

      13. Hali yetu ikoje kama ile ya Waisraeli kabla ya kukombolewa kwao kutoka Misri?

      13 Ingawa ‘wakati ulikuwa ukikaribia kwa ajili ya utimizo wa ahadi’ na kwamba Mungu alikuwa ameweka mwaka hususa, Musa na Israeli wote wangelazimika kudhihirisha imani. Wangelazimika kungojea wakati wa Yehova uliowekwa, yaonekana wakiwa bila uwezo wa kuukadiria kimbele. Sisi pia tunasadiki kwamba ukombozi wetu kutoka katika mfumo huu mwovu wa mambo unakaribia. Twajua kwamba tunaishi katika “siku za mwisho.” (2 Timotheo 3:1-5) Kwa hiyo, je, haitupasi kuwa tayari kudhihirisha imani na kungojea wakati wa Yehova uliowekwa kwa ajili ya siku yake kubwa? (2 Petro 3:11-13) Kisha, kama Musa na Waisraeli, twaweza kwa kufaa kuimba wimbo mtukufu wa ukombozi, kwa sifa ya Yehova.—Kutoka 15:1-19.

      ‘Wakati Ulipofika’

      14, 15. Twajuaje kwamba Mungu alikuwa ameweka wakati wa kuja duniani kwa Mwana wake, nao manabii na hata malaika waliendelea kulinda kuhusiana na nini?

      14 Yehova alikuwa ameweka wakati hususa wa kuja duniani kwa Mwana wake mzaliwa-pekee akiwa Mesiya. Paulo aliandika: “Kikomo kamili cha wakati kilipowasili, Mungu alimtuma Mwana wake, aliyekuja kuwa kutokana na mwanamke na aliyekuja kuwa chini ya sheria.” (Wagalatia 4:4) Hilo lilikuwa kwa utimizo wa ahadi ya Mungu ya kutuma Mbegu—‘Shilo, ambaye mataifa watamtii.’—Mwanzo 3:15; 49:10.

      15 Manabii wa Mungu—hata malaika—waliendelea kulinda kuhusiana na “majira” ambapo Mesiya angetokea duniani na ambapo wokovu ungefanywa uwezekane kwa wanadamu wenye dhambi. “Kuhusu wokovu huu wenyewe,” Petro akasema, “kuulizia habari kwa bidii yenye kuendelea na utafutaji wa uangalifu sana ulifanywa na manabii ambao walitoa unabii juu ya fadhili isiyostahiliwa iliyokusudiwa kwa ajili yenu. Walifuliza kupeleleza-peleleza ni majira gani maalumu au ni namna gani ya majira roho iliyo ndani yao ilikuwa ikionyesha kuhusu Kristo ilipokuwa ikitoa ushahidi kimbele juu ya mateso ya Kristo na juu ya matukufu ambayo yangefuata hayo. . . . Ndani ya mambo hayohayo malaika wanatamani kuchungulia.”—1 Petro 1:1-5, 10-12.

      16, 17. (a) Yehova aliwasaidia Wayahudi wa karne ya kwanza wamtarajie Mesiya kupitia unabii gani? (b) Unabii wa Danieli uliathirije tarajio la Wayahudi la Mesiya?

      16 Kupitia nabii wake Danieli—mwanamume mwenye imani isiyoyumbayumba—Yehova alikuwa ametoa unabii uliohusisha “majuma sabini.” Unabii huo ungewawezesha Wayahudi wa karne ya kwanza wajue kwamba kutokea kwa Mesiya aliyeahidiwa kulikuwa kukikaribia. Kwa sehemu, unabii huo ulisema: “Tangu kuwekwa amri ya kutengeneza na kuujenga upya Yerusalemu hata zamani zake masihi aliye mkuu; kutakuwa na majuma saba; na majuma sitini na mawili.” (Danieli 9:24, 25) Wasomi Wayahudi, Wakatoliki na Waprotestanti hukubali kwa ujumla kwamba “majuma” yaliyotajwa hapa yamaanisha majuma ya miaka. “Majuma” hayo 69 (miaka 483) ya Danieli 9:25 yalianza mwaka wa 455 K.W.K., wakati ambapo Mfalme Artashasta wa Uajemi alimwamuru Nehemia “kutengeneza na kuujenga upya Yerusalemu.” (Nehemia 2:1-8) Yaliisha miaka 483 baadaye—mwaka wa 29 W.K., Yesu alipobatizwa na kutiwa mafuta kwa roho takatifu, hivyo kuwa Mesiya, au Kristo.—Mathayo 3:13-17.

      17 Haijulikani kama Wayahudi wa karne ya kwanza walijua sawasawa wakati ambapo miaka hiyo 483 ilianza. Lakini wakati Yohana Mbatizaji alipoanza huduma yake, “watu walikuwa wakitarajia na wote walikuwa wakiwazawaza mioyoni mwao juu ya Yohana: ‘Je, labda yeye ndiye Kristo?’” (Luka 3:15) Wasomi fulani wa Biblia huhusisha tarajio hilo na unabii wa Danieli. Akieleza juu ya mstari huo Matthew Henry aliandika: “Twaambiwa hapa . . . jinsi huduma na ubatizo wa Yohana ulivyofanya watu wafikiri kuhusu Mesiya na kufikiri kuwa alikuwa karibu sana kutokea. . . . Majuma saba ya Danieli yalikuwa yakimalizika.” Kichapo cha Kifaransa, Manuel Biblique, cha Vigouroux, Bacuez, na Brassac chasema: “Watu walijua kwamba majuma sabini ya miaka yaliyowekwa na Danieli yalikuwa yakikaribia kumalizika; hakuna yeyote aliyeshangaa kumsikia Yohana Mbatizaji akitangaza kwamba ufalme wa Mungu ulikuwa umekaribia.” Msomi Myahudi Abba Hillel Silver aliandika kwamba kulingana na “kronolojia iliyopendwa na wengi” ya wakati huo, “Mesiya alitarajiwa kati ya mwaka wa 25 na 50 W.K.”

      Matukio Wala Si Ukadiriaji wa Wakati

      18. Ingawa unabii wa Danieli uliwasaidia Wayahudi watambue wakati ambapo Mesiya alitarajiwa kutokea, ni nini uliokuwa uthibitisho wenye kusadikisha zaidi wa Umesiya wa Yesu?

      18 Ingawa yaelekea kronolojia ilisaidia Wayahudi kujua kwa ujumla wakati ambapo Mesiya angetokea, matukio yaliyofuata yaonyesha kwamba wengi wao hawakusaidiwa na kronolojia kusadiki Umesiya wa Yesu. Muda unaopungua mwaka mmoja kabla ya kifo chake, Yesu aliwauliza wanafunzi wake hivi: “Umati unasema kwamba mimi ni nani?” Wakajibu: “Yohana Mbatizaji; lakini wengine, Eliya, na wengine bado, kwamba mmoja wa manabii wa kale amefufuliwa.” (Luka 9:18, 19) Hatuna rekodi yoyote kwamba Yesu aliwahi kunukuu unabii wa hayo majuma ya ufananisho ili kuthibitisha kwamba alikuwa ndiye Mesiya. Lakini katika pindi moja alisema: “Mimi nina ushahidi ulio mkubwa zaidi kuliko ule wa Yohana, kwa maana kazi zilezile ambazo Baba yangu alinigawia kutimiza, kazi hizo zenyewe ambazo ninafanya, hutoa ushahidi juu yangu kwamba Baba alinituma mimi.” (Yohana 5:36) Badala ya kronolojia yoyote iliyofunuliwa, kuhubiri kwa Yesu, miujiza yake, na matukio yaliyohusiana na kifo chake (giza la kimuujiza, kupasuka kwa pazia ya hekalu, na tetemeko la dunia), ndiyo yaliyotoa ushuhuda kwamba yeye alikuwa ndiye Mesiya aliyetumwa na Mungu.—Mathayo 27:45, 51, 54; Yohana 7:31; Matendo 2:22.

      19. (a) Wakristo wangejuaje kwamba kuharibiwa kwa Yerusalemu kulikuwa karibu? (b) Kwa nini Wakristo wa mapema waliokimbia Yerusalemu bado walihitaji imani nyingi?

      19 Vivyo hivyo, baada ya kifo cha Yesu, Wakristo wa mapema hawakupewa uwezo wa kukadiria mwisho wa mfumo wa mambo wa Kiyahudi uliokuwa karibu. Ni kweli kwamba unabii wa Danieli wa majuma ya ufananisho ulitaja kuharibiwa kwa mfumo huo. (Danieli 9:26b, 27b) Lakini hilo lingetukia baada ya mwisho wa “majuma sabini” (455 K.W.K.–36 W.K.). Yaani, baada ya watu wa kwanza Wasio Wayahudi kuwa wafuasi wa Yesu mwaka wa 36 W.K., Danieli sura ya 9 haikuwaandalia Wakristo data yoyote ya kikronolojia. Kwao, matukio wala si kronolojia, ndiyo yangeonyesha kwamba mfumo wa Kiyahudi lazima ungeisha karibuni. Matukio hayo, yaliyotabiriwa na Yesu, yalianza kufikia kilele kuanzia mwaka wa 66 W.K., wakati Waroma waliposhambulia Yerusalemu na kuondoka. Hilo liliwapa Wakristo waaminifu na wenye uangalifu wa Yerusalemu na Yudea fursa ya ‘kukimbilia milimani.’ (Luka 21:20-22) Wakiwa bila ishara zozote za kikronolojia, Wakristo hao wa mapema hawakujua wakati ambapo Yerusalemu ingeharibiwa. Walionyesha imani iliyoje kuacha nyumba zao, mashamba, na karakana na kukaa nje ya Yerusalemu kwa miaka minne hadi jeshi la Waroma liliporudi katika mwaka wa 70 W.K. na kuharibu kabisa mfumo wa Kiyahudi!—Luka 19:41-44.

      20. (a) Twaweza kunufaikaje kutokana na vielelezo vya Noa, Musa, na Wakristo wa Yudea wa karne ya kwanza? (b) Tutazungumzia nini katika makala inayofuata?

      20 Kama Noa, Musa, na Wakristo wa Yudea wa karne ya kwanza, sisi leo twaweza kwa uhakika kuacha nyakati na majira mikononi mwa Yehova. Kusadiki kwetu kwamba tunaishi wakati wa mwisho na kwamba ukombozi wetu umekaribia hakutegemei kukadiria mambo kikronolojia, bali kwategemea matukio halisi ya maisha yanayotimiza unabii mbalimbali wa Biblia. Zaidi ya hayo, ingawa tunaishi wakati wa kuwapo kwa Kristo, hilo halituondolei uhitaji wa kudhihirisha imani na kuendelea kulinda. Yatupasa tuendelee kuishi tukitarajia kwa hamu matukio yenye kusisimua yaliyotabiriwa katika Maandiko. Makala inayofuata itakuwa na habari hiyo.

  • Kungoja kwa “Taraja Lenye Hamu”
    Mnara wa Mlinzi—1998 | Septemba 15
    • Kungoja kwa “Taraja Lenye Hamu”

      “Taraja lenye hamu la viumbe linangoja kufunuliwa kwa wana wa Mungu.”—WAROMA 8:19.

      1. Ni ufanani gani uliopo baina ya hali ya Wakristo leo na ile ya Wakristo wa karne ya kwanza?

      HALI ya Wakristo wa kweli leo yafanana na ile ya Wakristo wa karne ya kwanza. Unabii fulani uliwasaidia watumishi wa Yehova wa siku hizo watambue wakati ambapo Mesiya angetokea. (Danieli 9:24-26) Unabii huohuo ulitabiri kuharibiwa kwa Yerusalemu lakini haukuwa na sehemu zozote zilizowawezesha Wakristo wajue kimbele wakati ambapo jiji hilo lingeharibiwa. (Danieli 9:26b, 27) Vivyo hivyo, unabii fulani ulioongozwa na Mungu uliwafanya wanafunzi wa Biblia wa karne ya 19 wakae wakitarajia. Kwa kuhusisha “nyakati saba” za Danieli 4:25 na “nyakati za Wasio Wayahudi,” walitazamia kwamba Kristo angepokea mamlaka ya Ufalme mwaka wa 1914. (Luka 21:24, King James Version; Ezekieli 21:25-27) Ingawa kitabu cha Danieli kina unabii mwingi mbalimbali, hakuna hata mmoja wa unabii huo ambao huwawezesha wanafunzi wa Biblia wa siku hizi wakadirie wakati hususa ambapo mfumo wote wa Shetani utaharibiwa. (Danieli 2:31-44; 8:23-25; 11:36, 44, 45) Hata hivyo, hilo litatokea karibuni kwa maana tunaishi “wakati wa mwisho.”—Danieli 12:4.a

      Kulinda Wakati wa Kuwapo kwa Kristo

      2, 3. (a) Ni nini kijumuikacho kuwa ithibati iliyo kubwa zaidi kwamba tunaishi wakati wa kuwapo kwa Kristo katika mamlaka ya kifalme? (b) Ni nini kionyeshacho kwamba Wakristo wangefuliza kulinda wakati wa kuwapo kwa Yesu Kristo?

      2 Ni kweli, unabii fulani uliwaweka Wakristo katika hali ya kutarajia kabla ya Kristo kukabidhiwa mamlaka ya Ufalme mwaka wa 1914. Lakini “ishara” ambayo Kristo alitoa kuhusu kuwapo kwake na umalizio wa mfumo wa mambo ilikazia umaana wa matukio. Na mengi ya hayo yangeonekana baada ya kuwapo kwake kuanza. Matukio hayo—vita, upungufu wa chakula, matetemeko ya dunia, magonjwa ya kuambukiza, kuongezeka kwa uasi-sheria, kunyanyaswa kwa Wakristo, na kuhubiriwa kwa habari njema ya Ufalme ulimwenguni pote—ndiyo ithibati iliyo kubwa zaidi kwamba sasa tunaishi wakati wa kuwapo kwa Kristo katika mamlaka ya kifalme.—Mathayo 24:3-14; Luka 21:10, 11.

      3 Hata hivyo, maana kamili ya shauri la Yesu la kuwaaga wanafunzi wake ilikuwa: “Fulizeni kutazama, fulizeni kuwa macho, . . . fulizeni kulinda.” (Marko 13:33, 37; Luka 21:36) Usomaji wa makini wa muktadha wa mahimizo hayo ya kuwa wenye kulinda yaonyesha kwamba, kimsingi Kristo hakuwa akizungumza juu ya kufuliza kulinda kwa makini kwa ajili ya ishara ya kuanza kwa kuwapo kwake. Badala yake, alikuwa akiwaamuru wanafunzi wake wa kweli wafulize kulinda wakati wa kuwapo kwake. Wakristo wa kweli wangefuliza kulinda juu ya nini?

      4. Ishara aliyotoa Yesu ingetimiza kusudi gani?

      4 Yesu alitoa unabii wake mkuu kwa kujibu swali hili: “Ni wakati gani mambo haya yatakuwa [matukio yaliyoongoza kwenye uharibifu wa mfumo wa mambo wa Wayahudi], nayo itakuwa ni nini ishara ya kuwapo kwako na ya umalizio wa mfumo wa mambo?” (Mathayo 24:3) Ishara hiyo iliyotabiriwa ingetambulisha kuwapo kwa Kristo na pia matukio ambayo yangetangulia mwisho wa mfumo wa mambo uliopo.

      5. Yesu alionyeshaje kwamba ingawa angekuwapo kiroho, bado angekuwa “anakuja”?

      5 Yesu alionyesha kwamba wakati wa “kuwapo” kwake (Kigiriki, pa·rou·siʹa) yeye angekuja na nguvu na utukufu. Kuhusu “kuja” (kuonyeshwako na aina za neno la Kigiriki erʹkho·mai), alitangaza: “Ndipo ishara ya Mwana wa binadamu itakapoonekana mbinguni, na ndipo makabila yote ya dunia yatakapojipiga yenyewe kwa maombolezo, nayo yatamwona Mwana wa binadamu akija juu ya mawingu ya mbinguni na nguvu na utukufu mkubwa. . . . Basi jifunzeni jambo hili kutokana na mtini kama kielezi: Mara tu tawi lao changa likuapo kuwa jororo na kutoa majani, mwajua kwamba kiangazi kiko karibu. Hivyohivyo nyinyi pia, mwonapo mambo yote hayo, jueni kwamba [Kristo] yuko karibu milangoni. . . . Fulizeni kulinda kwa sababu hamjui ni siku gani Bwana yenu anakuja. . . . Jithibitisheni wenyewe kuwa tayari, kwa sababu kwenye saa msiyoifikiri kuwa hiyo, Mwana wa binadamu anakuja.”—Mathayo 24:30, 32, 33, 42, 44.

      Kwa Nini Yesu Kristo Anakuja?

      6. Kuharibiwa kwa “Babiloni Mkubwa” kutatukiaje?

      6 Ingawa Yesu Kristo amekuwapo akiwa Mfalme tangu 1914, bado ni lazima ahukumu mashirika na watu mmoja-mmoja kabla hajawapasisha hukumu wale anaopata wakiwa waovu. (Linganisha 2 Wakorintho 5:10.) Hivi karibuni Yehova atatia katika akili za watawala wa kisiasa wazo la kuharibu “Babiloni Mkubwa,” milki ya ulimwengu ya dini isiyo ya kweli. (Ufunuo 17:4, 5, 16, 17) Mtume Paulo alisema mahususi kwamba Yesu Kristo ataharibu “mtu wa uasi-sheria”—makasisi waasi-imani wa Jumuiya ya Wakristo, iliyo sehemu mashuhuri ya “Babiloni Mkubwa.” Paulo aliandika: “Mwasi-sheria atafunuliwa, ambaye Bwana Yesu atamwondolea mbali kwa roho ya kinywa chake na kufanya awe si kitu kwa udhihirisho wa kuwapo kwake.”—2 Wathesalonike 2:3, 8.

      7. Mwana wa binadamu atatoa hukumu gani awasilipo katika utukufu wake?

      7 Hivi karibuni, Kristo atahukumu watu wa mataifa kwa kutegemea jinsi walivyowatendea ndugu zake ambao bado wako duniani. Twasoma hivi: “Wakati Mwana wa binadamu awasilipo katika utukufu wake, na malaika wote pamoja naye, ndipo atakapoketi juu ya kiti chake cha ufalme chenye utukufu. Na mataifa yote yatakusanywa mbele yake, naye atatenganisha watu mmoja na mwenzake, kama vile mchungaji atenganishavyo kondoo na mbuzi. Naye atawaweka kondoo kwenye mkono wake wa kuume, lakini mbuzi kwenye mkono wake wa kushoto. . . . Mfalme atawaambia [kondoo], ‘Kwa kweli nawaambia nyinyi, Kwa kadiri ambayo mlimfanyia hilo mmoja wa wadogo zaidi sana wa ndugu zangu hawa, mlinifanyia mimi hilo.’ . . . Na [mbuzi] wataondoka kuingia katika kukatiliwa-mbali kudumuko milele, lakini waadilifu kuingia katika uhai udumuo milele.”—Mathayo 25:31-46.

      8. Paulo afafanuaje kuja kwa Kristo ili kutekeleza hukumu juu ya wasiomwogopa Mungu?

      8 Kama ionyeshwavyo katika mfano wenye somo wa kondoo na mbuzi, Yesu atatekeleza hukumu ya mwisho juu ya wote wasiomwogopa Mungu. Paulo aliwahakikishia waamini wenzake waliokuwa wakiteseka “kitulizo pamoja nasi kwenye ufunuo wa Bwana Yesu kutoka mbinguni pamoja na malaika zake wenye nguvu katika moto wenye kuwaka mwali, aletapo kisasi juu ya wale wasiomjua Mungu na wale wasiotii habari njema juu ya Bwana wetu Yesu. Hawahawa watapatwa na adhabu ya kihukumu ya uharibifu udumuo milele kutoka mbele ya Bwana na kutoka katika utukufu wa nguvu yake, wakati ajapo kutukuzwa kuhusiana na watakatifu wake.” (2 Wathesalonike 1:7-10) Tukiwa na matukio hayo yenye kusisimua mbele yetu, je, haitupasi kudhihirisha imani na kwa hamu kufuliza kulinda kwa ajili ya kuja kwa Kristo?

      Kungojea kwa Hamu Kufunuliwa kwa Kristo

      9, 10. Kwa nini watiwa-mafuta ambao wangali duniani hungojea kwa hamu kufunuliwa kwa Yesu Kristo?

      9 ‘Kufunuliwa kwa Bwana Yesu kutoka mbinguni’ kutaleta si kuharibiwa kwa waovu tu bali pia thawabu kwa waadilifu. Wanaobaki wa ndugu watiwa-mafuta wa Kristo ambao wangali duniani huenda bado wakateseka kabla ya kufunuliwa kwa Kristo, lakini wao hushangilia tumaini lao tukufu la kimbingu. Kwa Wakristo watiwa-mafuta, mtume Petro aliandika: “Endeleeni kushangilia kwa maana nyinyi ni washiriki katika mateso ya Kristo, ili mpate kushangilia na kuwa na shangwe mno pia wakati wa ufunuo wa utukufu wake.”—1 Petro 4:13.

      10 Watiwa-mafuta wameazimia kubaki wakiwa waaminifu hadi Kristo ‘awakusanye pamoja kwake’ ili ‘ubora uliojaribiwa’ wa imani yao “upatikane kuwa sababu ya sifa na utukufu na heshima wakati wa ufunuo wa Yesu Kristo.” (2 Wathesalonike 2:1; 1 Petro 1:7) Kuhusu Wakristo hao watiwa-mafuta walio waaminifu, yaweza kusemwa: “Ushahidi juu ya Kristo umefanywa kuwa imara miongoni mwenu, ili kwamba msipungukiwe hata kidogo katika zawadi yoyote, huku mkiungoja kwa hamu ufunuo wa Bwana wetu Yesu Kristo.”—1 Wakorintho 1:6, 7.

      11. Wakristo watiwa-mafuta hufanya nini wanapongojea kufunuliwa kwa Yesu Kristo?

      11 Mabaki watiwa-mafuta wana hisi sawa na za Paulo, aliyeandika: “Nahesabu kwamba mateso ya majira yaliyopo si kitu kwa kulinganisha na utukufu utakaofunuliwa katika sisi.” (Waroma 8:18) Imani yao haihitaji kutegemezwa na makadirio ya wakati. Wao huwa na shughuli nyingi katika utumishi wa Yehova, wakiwawekea kielelezo chema waandamani wao, “kondoo wengine.” (Yohana 10:16) Watiwa-mafuta hawa wanajua kwamba mwisho wa mfumo huu mwovu umekaribia, nao husikiza himizo hili la Petro: “Kazeni akili zenu kwa ajili ya utendaji, tunzeni akili zenu kikamili; wekeni tumaini lenu juu ya fadhili isiyostahiliwa itakayoletwa kwenu wakati wa ufunuo wa Yesu Kristo.”—1 Petro 1:13.

      “Taraja Lenye Hamu la Viumbe”

      12, 13. Viumbe wa kibinadamu ‘walitiishwaje chini ya ubatili,’ nao kondoo wengine wana hamu gani?

      12 Je, kondoo wengine pia wana jambo fulani ambalo kwa ajili yake wao huishi wakiwa na taraja lenye hamu? Kwa hakika kabisa wanalo. Baada ya kuzungumza juu ya tumaini tukufu la wale waliofanywa na Yehova kuwa “wana” wake wazaliwa kwa roho na “warithi-washirika pamoja na Kristo” katika Ufalme wa Kimbingu, Paulo alisema: “Taraja lenye hamu la viumbe linangoja kufunuliwa kwa wana wa Mungu. Kwa maana viumbe vilitiishwa chini ya ubatili, si kwa mapenzi yavyo vyenyewe bali kupitia yeye aliyevitiisha hivyo, juu ya msingi wa tumaini kwamba viumbe vyenyewe pia vitawekwa huru kutoka katika utumwa wa uharibifu na kuwa na uhuru wenye utukufu wa watoto wa Mungu.”—Waroma 8:14-21; 2 Timotheo 2:10-12.

      13 Kupitia dhambi ya Adamu, wazao wake wote “[wa]litiishwa chini ya ubatili,” wakizaliwa katika utumwa wa dhambi na kifo. Wameshindwa kujiweka huru kutoka katika utumwa huo. (Zaburi 49:7; Waroma 5:12, 21) Lo, kondoo wengine wana hamu iliyoje ya “[ku]wekwa huru kutoka katika utumwa wa uharibifu”! Lakini kabla ya jambo hilo kutokea, mambo fulani lazima yatukie kulingana na nyakati na majira ya Yehova.

      14. Ni nini litakalohusika katika ‘kufunuliwa kwa wana wa Mungu,’ nalo litatokezaje ‘kuwekwa huru kwa wanadamu kutoka katika utumwa wa uharibifu’?

      14 Mabaki ya “wana wa Mungu” watiwa-mafuta lazima ‘wafunuliwe’ kwanza. Hilo litahusisha nini? Katika wakati wa Mungu uliowekwa, itadhihirika wazi kwa kondoo wengine kwamba mwishowe watiwa-mafuta ‘wametiwa muhuri’ na kutukuzwa ili kutawala na Kristo. (Ufunuo 7:2-4) “Wana wa Mungu” wenye kufufuliwa ‘watafunuliwa’ pia wakati ambapo watashirikiana na Kristo kuharibu mfumo wa mambo wa Shetani ulio mwovu. (Ufunuo 2:26, 27; 19:14, 15) Kisha, wakati wa Utawala wa Miaka Elfu wa Kristo, ‘watafunuliwa’ tena wakiwa njia ambazo kwazo manufaa za dhabihu ya fidia ya Yesu itatolewa kwa “viumbe” wa kibinadamu. Hilo litatokeza ‘kuwekwa huru kwa wanadamu kutoka katika utumwa wa uharibifu’ na hatimaye kuingia katika “uhuru wenye utukufu wa watoto wa Mungu.” (Waroma 8:21; Ufunuo 20:5; 22:1, 2) Wakiwa na matazamio hayo matukufu, je, inashangaza kwamba kondoo wengine “[wa]nangoja kufunuliwa kwa wana wa Mungu” kwa “taraja lenye hamu”?—Waroma 8:19.

      Subira ya Yehova Humaanisha Wokovu

      15. Ni jambo gani tusilopaswa kusahau kamwe kwa habari ya uwekaji wakati wa Yehova kuhusiana na matukio?

      15 Yehova ndiye Mweka-Wakati aliye mkuu zaidi. Uwekaji wake wa wakati kuhusiana na matukio utathibitika kuwa mkamilifu. Huenda mambo yasionekane sikuzote kuwa yanatukia kwa njia ambayo sisi binafsi tulitarajia. Hata hivyo, twaweza kuwa na imani thabiti kwamba ahadi zote za Mungu zitatimizwa. (Yoshua 23:14) Huenda akawa anaruhusu mambo yaendelee kwa muda mrefu zaidi ya vile watu walivyotarajia. Lakini acheni tujaribu kuelewa njia zake na kustahi hekima yake. Paulo aliandika: “Lo! kina cha utajiri wa Mungu na hekima na ujuzi! Jinsi hukumu zake zisivyotafutikana na njia zake zapita uwezo wa kufuatilia! Kwa maana ‘ni nani amekuja kuijua akili ya Yehova, au ni nani amekuwa mshauri wake?’”—Waroma 11:33, 34.

      16. Ni nani wanaoelekea kunufaika na subira ya Yehova?

      16 Petro aliandika: “Kwa sababu hiyo, wapendwa, kwa kuwa mnangojea mambo haya [kuharibiwa kwa “mbingu” na “dunia” ya zamani, ambazo mahali pake Mungu ataweka “mbingu mpya” na “dunia mpya”], fanyeni kabisa yote mwezayo ili mwishowe mpatikane naye mkiwa bila doa na bila waa na katika amani. Zaidi ya hilo, ioneni subira ya Bwana wetu kuwa wokovu.” Kwa sababu ya subira ya Yehova, mamilioni ya watu wanatolewa fursa ya kuokoka “siku ya Yehova,” itakayokuja bila kutarajiwa “kama mwizi.” (2 Petro 3:9-15) Subira yake pia inaruhusu kila mmoja wetu ‘afulize kufanyiza wokovu wake mwenyewe kwa hofu na kutetemeka.’ (Wafilipi 2:12) Yesu alisema kwamba ni lazima ‘tukazie uangalifu kwa sisi wenyewe’ na ‘kufuliza kuwa macho’ ikiwa twataka kukubalika na kufanikiwa “kusimama mbele ya Mwana wa binadamu” wakati ajapo kwa ajili ya hukumu.—Luka 21:34-36; Mathayo 25:31-33.

      Fuliza Kungojea kwa Uvumilivu

      17. Ni maneno gani ya mtume Paulo tupaswayo kusikiza?

      17 Paulo aliwahimiza ndugu zake wa kiroho wafulize ‘kuweka macho yao, si juu ya vitu vionekanavyo, bali juu ya vitu visivyoonekana.’ (2 Wakorintho 4:16-18) Hakutaka lolote lifanye thawabu yao ya kimbingu iliyowekwa mbele yao isiwe dhahiri. Tuwe Wakristo watiwa-mafuta au tuwe kondoo wengine, acheni tukumbuke tumaini zuri ajabu lililowekwa mbele yetu na tusikate tamaa. Acheni ‘tufulize kungojea kwa uvumilivu,’ tukithibitisha kwamba “sisi si namna irudiyo nyuma kwenye uangamivu, bali namna iliyo na imani kuelekea kuhifadhi hai nafsi.”—Waroma 8:25; Waebrania 10:39.

      18. Kwa nini twaweza kwa uhakika kuacha nyakati na majira mikononi mwa Yehova?

      18 Twaweza kwa uhakika kuacha nyakati na majira mikononi mwa Yehova. Kutimizwa kwa ahadi zake ‘hakutachelewa’ kulingana na ratiba yake ya wakati. (Habakuki 2:3, BHN) Wakati uleule, himizo la Paulo kwa Timotheo lina maana ya ziada kwetu. Yeye alisema: “Nakuagiza kwa uzito mbele ya Mungu na Kristo Yesu, ambaye akusudiwa kuhukumu walio hai na wafu, na kwa udhihirisho wake na ufalme wake, lihubiri neno, lifanye kwa hima katika majira yenye kufaa, katika majira yenye taabu . . . Fanya kazi ya mweneza-evanjeli, timiza kikamili huduma yako.”—2 Timotheo 4:1-5.

      19. Bado ni wakati kwa watu wa Yehova kufanya nini, na kwa nini?

      19 Uhai wetu na wa majirani wetu umo hatarini. Paulo aliandika: “Daima kaza uangalifu kwako mwenyewe na kwa kufundisha kwako. Kaa katika mambo haya, kwa maana kwa kufanya hivi utajiokoa wewe mwenyewe na wale wakusikilizao pia.” (1 Timotheo 4:16) Mfumo huu mwovu wa mambo una wakati mfupi sana. Tungojeapo kwa taraja lenye hamu matukio yenye kusisimua yaliyo mbele yetu, acheni tutambue daima kwamba bado ni wakati na majira ya Yehova kwa watu wake kuhubiri habari njema ya Ufalme. Ni lazima kazi hiyo itimizwe kwa njia inayomridhisha. “Ndipo,” kama vile Yesu alivyosema, “mwisho utakapokuja.”—Mathayo 24:14.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki