Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Miaka 30 ya Kutafsiri kwa Siri
    Amkeni!—2009 | Juni
    • Miaka 30 ya Kutafsiri kwa Siri

      Limesimuliwa na Ona Mockutė

      Mnamo Aprili (Mwezi wa 4) 1962, nilipelekwa katika mahakama iliyojaa watu huko Klaipeda, Lithuania nikiwa nimeshtakiwa kwa uhalifu dhidi ya jamii. Oktoba (Mwezi wa 10) mwaka uliotangulia, nilikuwa nimekamatwa na kushtakiwa kwa kushiriki katika utendaji wa kidini ulioonwa kuwa uhalifu dhidi ya Serikali ya Sovieti. Acheni nisimulie mambo yaliyofanya nikamatwe na kufungwa kwa sababu ya kutafsiri kisiri vichapo vya Mashahidi wa Yehova.

  • Miaka 30 ya Kutafsiri kwa Siri
    Amkeni!—2009 | Juni
    • Naanza Kutafsiri kwa Siri

      Wakati huo, kulikuwa na Mashahidi wachache tu waliokuwa wamebaki nchini Lithuania. Wengine bado walikuwa wamefungwa gerezani au kupelekwa uhamishoni huko Siberia. Mnamo 1959, Mashahidi wawili walirudi kutoka Siberia na wakapendekeza kwamba nitafsiri vichapo vyetu vya Biblia katika Kilithuania. Nilikubali kazi hiyo, na nikaiona kuwa pendeleo.

      Katika Machi (Mwezi wa 3) 1960, nilianza kutafsiri, na Julai (Mwezi wa 7), nilibatizwa kisiri katika Mto Dubysa. Kwa sababu ya upinzani kutoka kwa askari wa KGB (Shirika la Usalama wa Kitaifa la Sovieti), singeweza kupata kazi ya kunitegemeza, kwa hiyo niliishi na wazazi wangu ambao hawakuipinga imani yangu. Niliwalisha ng’ombe wa baba yangu pamoja na wa majirani. Niliendelea kutafsiri huku nikiwalisha wanyama hao. Ofisi yangu ilikuwa maridadi kwani niliketi kwenye kisiki cha mti nikiwa nimezungukwa na mkeka wa nyasi za rangi ya kijani. Juu ya kichwa changu kulikuwa na anga la bluu, na niliitumia miguu yangu kama dawati.

      Hata hivyo, baadaye nilitambua kwamba haikuwa salama kutafsiri nikiwa malishoni, kwa kuwa ingekuwa rahisi kuonekana na askari wa KGB au vibaraka wao. Hivyo nilipopata mahali pa kujificha ili nitafsiri, nilihama kutoka kwa nyumba ya baba yangu. Nyakati nyingine nilifanya kazi nikiwa zizini. Huku wanyama wakiwa upande mmoja niliketi upande ule mwingine nikichapa kwa kutumia taipureta.

      Kwa kuwa hakukuwa na umeme, nilifanya kazi wakati wa mchana. Ili sauti ya taipureta isisikike, familia niliyokuwa nikiishi nayo ilijenga kinu cha upepo nje ya zizi. Giza lilipoingia, niliingia katika nyumba kwa ajili ya chakula cha jioni. Kisha nilirudi zizini na kulala juu ya kitanda cha nyasi kavu.

      Mnamo Oktoba 1961, mimi pamoja na Mashahidi wengine wawili tulikamatwa wakati kazi yangu kutafsiri vichapo vya kidini ilipogunduliwa. Hilo lilifanya nipelekwe mahakamani mwaka wa 1962 kama nilivyotaja mwanzoni mwa simulizi hili. Tuliruhusiwa kujitetea mbele ya umma na tukafurahia kuwatolea ushahidi watu wengi waliokuja kortini. (Marko 13:9) Nilihukumiwa kifungo cha miaka mitatu na kupelekwa gerezani huko Tallinn, Estonia. Ninachojua ni kwamba, wakati huo ni mimi tu niliyekuwa nimefungwa katika gereza hilo kwa sababu ya dini yangu. Wasimamizi wa jiji walinitembelea, na niliwaambia kuhusu imani yangu.

      Narudia Kazi ya Kutafsiri

      Nilipofunguliwa kutoka gerezani huko Estonia mnamo 1964, nilirudi Lithuania. Nikiwa huko niliendelea kutafsiri vichapo vyetu, hasa kutoka Kirusi hadi Kilithuania. Nilikuwa na kazi nyingi sana. Ingawa wengine walinisaidia, mimi tu ndiye niliyetafsiri Kilithuania wakati wote. Mara nyingi nilifanya kazi siku saba kwa juma kuanzia asubuhi hadi usiku. Singeweza kupata nguvu za kufanya hivyo bila msaada wa Yehova.

      Nikitambua jinsi kazi hiyo ilivyokuwa muhimu, sikuzote nilijaribu kuwa mwangalifu. Mara nyingi ndugu na dada Wakristo walijihatarisha na kuhatarisha familia zao ili wanifiche, wanipe chakula, na kunilinda. Ushirikiano huo ulitufanya tuwe na uhusiano wa karibu sana. Nilipokuwa nikifanya kazi, familia ambayo nilikuwa nikiishi nayo ilikuwa macho ili kuona watu ambao wangenishtaki. Ili kutoa tahadhari, mtu angetumia kifaa cha chuma kugonga mabomba ya kupashia nyumba joto mara mbili. Niliposikia onyo hilo, nilificha upesi kitu chochote ambacho kingeonyesha nilikuwa nikifanya kazi gani.

      Ikiwa tungegundua kwamba askari walikuwa wakichunguza nyumba niliyokuwa nikifanyia kazi, ningehamia eneo lingine mara moja. Siku hizo ilikuwa ni kosa kubwa kupatikana na taipureta bila kibali cha serikali, kwa hiyo mtu mwingine angepeleka taipureta yangu kwenye eneo jipya la kazi. Kisha, hasa usiku, ningeelekea kwenye eneo hilo jipya.

      Yehova alinilinda sana. Ingawa maofisa hawakuwa na uthibitisho, walijua nilichokuwa nikifanya. Kwa mfano, mnamo 1973, wakati Mashahidi wanane wa Yehova waliposhtakiwa, mwendesha-mshtaka aliniita ili aniulize maswali. Aliniuliza hivi moja kwa moja, “Mockutė, umechapisha vichapo vingapi katika miaka iliyopita?”

      Nilimwambia kwamba singeweza kujibu swali hilo. Kisha akauliza, “Kwa hiyo ni swali gani unaloweza kujibu?”

      Nikamjibu, “Swali lolote ambalo halihusiani na kazi hii.”

      Hali Zabadilika

      Kufikia mwishoni mwa miaka ya 1980, hali nchini Lithuania zilianza kubadilika. Haikuwa lazima tena tujifiche kutoka kwa maofisa wa serikali. Kwa hiyo, mnamo 1990, wengine walianza kufanya kazi ya kutafsiri. Kisha, Septemba 1, 1992 (1/9/1992), ofisi ndogo ya kutafsiri ilianzishwa huko Klaipeda, jiji ambalo mwishowe nilikuja kuishi.

      Kwa ujumla, nilifanya kazi ya kutafsiri kwa miaka 30 katika maeneo 16. Sikuwa na makao yangu mwenyewe. Ninashangilia kama nini kuona matokeo ya kazi yetu! Leo kuna Mashahidi wa Yehova 3,000 hivi nchini Lithuania. Na kazi ya kutafsiri niliyofanya wakati mmoja nikijificha katika mazizi na vyumba vya darini sasa inafanywa katika ofisi ya tawi yenye starehe ya Lithuania karibu na jiji la Kaunas.

  • Miaka 30 ya Kutafsiri kwa Siri
    Amkeni!—2009 | Juni
    • [Picha katika ukurasa wa 14, 15]

      Baadhi ya vichapo vya Biblia ambavyo nilitafsiri nikihatarisha uhuru wangu

  • Miaka 30 ya Kutafsiri kwa Siri
    Amkeni!—2009 | Juni
    • [Picha katika ukurasa wa 15]

      Taipureta niliyotumia nilipokuwa nikifanya kazi wakati wa marufuku

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki