-
Tahiti2005 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
Kutafsiri Katika Kitahiti
Kadiri idadi ya wahubiri ilivyoongezeka, ndivyo kazi kwenye ofisi ya tawi ilivyoongezeka pia, hasa kazi ya kutafsiri vichapo vya Biblia katika Kitahiti, lugha kuu ya wenyeji wa Polinesia. Hata kabla ya ofisi ya tawi kufunguliwa, wahubiri wazee wachache waliojua Kitahiti vizuri walitafsiri vichapo kadhaa katika Kitahiti, wakitumia vichapo vya Kifaransa. Kwa mfano, walianza kutafsiri Huduma Yetu ya Ufalme mwaka wa 1963. Kisha, mwaka wa 1971, wakamaliza kutafsiri kitabu Kweli Iongozayo Kwenye Uzima wa Milele.
Kazi ya kutafsiri ilisonga mbele ofisi ya tawi ya Tahiti ilipofunguliwa mwaka wa 1975. Watafsiri wengi wapya walijua Kiingereza, kwa kuwa lugha hiyo inafundishwa shuleni. Kwa hiyo, waliweza kutafsiri moja kwa moja kutoka Kiingereza badala ya tafsiri za Kifaransa. Gazeti la Mnara wa Mlinzi limetolewa mara mbili kwa mwezi katika Kitahiti tangu mwaka wa 1976, nalo gazeti la Amkeni! pia lilitafsiriwa katika lugha hiyo kwa muda. Pia, kitabu “Kila Andiko, Lenye Pumzi ya Mungu, Lafaa,” Kutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko, na kitabu cha nyimbo vilitafsiriwa. Mashahidi wa Yehova ndio wamechapisha vitabu vingi zaidi vya Kitahiti kuliko kikundi kingine chochote!
Hata hivyo, kwa muda wa miaka 30 iliyopita, watu wengi wameanza kuongea sana Kifaransa badala ya Kitahiti na lugha nyingine za Polinesia. Kifaransa hupendelewa kwa kuwa ni lugha yenye maneno mengi, nacho hutumiwa kwenye vyombo vya habari na shuleni, kuanzia shule ya msingi hadi chuo kikuu.
Wenyeji wengi wa Polinesia wanakiona Kitahiti kuwa sehemu ya utamaduni wao, kwa hiyo mara nyingi ndugu hutumia lugha hiyo katika kazi ya kuhubiri. Kati ya makutaniko 26 katika eneo linalosimamiwa na ofisi ya tawi, makutaniko 5 hutumia Kitahiti. Asilimia 20 hivi ya wahubiri huhudhuria makutaniko hayo matano. Kwa hiyo, bado vichapo vya lugha hiyo vinahitajika.
-
-
Tahiti2005 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
[Picha katika ukurasa wa 126]
Watafsiri wa Kitahiti
-