Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Wakati wa Kutahini (1914-1918)
    Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
    • Katika masika ya 1918, wimbi la mnyanyaso lilianzishwa dhidi ya Wanafunzi wa Biblia katika Amerika Kaskazini na Ulaya pia. Upinzani huo wenye kuchochewa na makasisi ulifikia upeo katika Mei 7, 1918, wakati waranti za serikali ya muungano ya Marekani zilipotolewa ili kukamata J. F. Rutherford na washirika wake kadhaa wa karibu. Kufikia katikati ya 1918, Rutherford na washirika saba walijipata wakiwa katika gereza la serikali ya muungano katika Atlanta, Georgia.

      Lakini Jaji Rutherford na washirika wake wakiwa gerezani, ni nini lililoupata utendaji kwenye makao makuu?

      Kuendeleza Kazi Bila Ndugu Wenye Madaraka

      Katika Brooklyn, Halmashauri ya Utekelezi iliwekwa ili kuchukua usimamizi wa kazi. Hangaiko kuu la ndugu waliowekwa lilikuwa kuendeleza mwenezo wa The Watch Tower. Hakika Wanafunzi wa Biblia kila mahali walihitaji kitia-moyo cha kiroho chote ambacho wangeweza kupewa. Kwa kweli, muda huo wote wa “majira ya kutahini,” hakuna toleo hata moja la The Watch Tower lililokosa kutokea katika chapa!f

      Hali ilikuwaje katika makao makuu? Thomas (Bud) Sullivan ambaye baadaye alitumikia akiwa mshiriki wa Baraza Linaloongoza, alikumbuka hivi: “Lilikuwa pendeleo langu kuzuru Betheli ya Brooklyn mwishoni-mwishoni mwa kiangazi cha 1918 wakati ndugu walipokuwa kifungoni. Ndugu waliosimamia kazi kwenye Betheli hawakuwa wenye woga wala wenye huzuni hata kidogo. Kwa kweli, hali ilikuwa kinyume kabisa. Walikuwa na maoni ya kutazamia mazuri na wenye uhakika kwamba hatimaye Yehova angewapa watu wake ushindi. Nilipendelewa kuwa penye meza ya kiamshakinywa Jumatatu asubuhi wakati ndugu waliokuwa wametumwa nje katika migawo ya mwisho-juma walipotoa ripoti zao. Kulikuwa hali nzuri. Katika kila kisa ndugu walikuwa na uhakika, wakimngojea Yehova aelekeze zaidi shughuli zao.”

      Hata hivyo, matatizo mengi yalikabiliwa. Vita ya Ulimwengu 1 ilikuwa ingali inachacha. Kulikuwa upungufu wa karatasi na makaa-mawe, vilivyohitajiwa sana kwa ajili ya kazi katika makao makuu. Uzalendo ukiwa unapamba moto, kulikuwa uhasama mwingi kuelekea Sosaiti; Wanafunzi wa Biblia walionwa kuwa wasaliti. Chini ya hali hizo kali, ilionekana kwamba haiwezekani kuendeleza shughuli za kazi katika Brooklyn. Kwa hiyo, baada ya kushauriana na ndugu wengine, Halmashauri ya Utekelezi iliuza Brooklyn Tabernacle na kufunga Kao la Betheli. Katika Agosti 26, 1918, shughuli za kazi zilihamishwa kurudi Pittsburgh kwenye jengo la ofisi katika barabara za Federal na Reliance.

      Hata hivyo, kulikuwa na hali changamfu. Martha Meredith alikumbuka hivi: “Sisi tuliokuwa katika Pittsburgh tulikusanyika na kuamua kwamba tungeendelea na kazi mpaka ndugu watoke gerezani. Katika wakati huo ofisi ya Brooklyn ilihamishiwa Pittsburgh, kwa hiyo ndugu walijishughulisha kuandika makala kwa ajili ya The Watch Tower na kuhakikisha kwamba zimechapwa. Magazeti ya The Watch Tower yalipokuwa tayari kupelekwa nje, sisi akina dada tuliyafunga na kuyapeleka nje kwa watu.”

      Wanafunzi wa Biblia walikuwa wamekabili majaribu makali tangu Nyakati za Mataifa zikome katika vuli ya 1914. Je, wangeweza kuendelea kustahimili? Je, kweli walikuwa na ‘upendo wa Mungu ndani ya mioyo yao’ au la? Je, wangeshikamana kwa imara na “Bwana na Kweli Yake,” kama vile Russell alivyokuwa amewatahadharisha, au wangeacha?

  • Wakati wa Kutahini (1914-1918)
    Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
    • [Sanduku/Picha katika ukurasa wa 69]

      ‘Hakuna Wanadamu Duniani Waliopendelewa Zaidi’

      Juni 21, 1918, J. F. Rutherford na washirika wake kadhaa wa karibu walihukumiwa kifungo cha miaka 20, wakiwa wamepatikana na hatia bandia ya kufanya njama. Hisia zao zilikuwa nini? Katika barua iliyoandikwa kwa mkono yenye tarehe ya Juni 22-23 (inayoonyeshwa chini), akiwa katika jela kwenye Raymond Street katika Brooklyn, New York, Ndugu Rutherford aliandika: “Labda hakuna wanadamu duniani leo waliopendelewa zaidi na walio na furaha zaidi ya wale ndugu saba walio gerezani sasa. Wao wanajua hawana hatia kabisa ya kosa la kukusudia, na washangilia kuwa wakiteseka pamoja na Kristo kwa ajili ya kumtumikia Yeye kwa uaminifu-mshikamanifu.”

  • Wakati wa Kutahini (1914-1918)
    Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
    • [Picha katika ukurasa wa 69]

      Jela katika Raymond Street, katika Brooklyn, New York, ambamo Ndugu Rutherford na washirika wake kadhaa wa karibu walifungiwa kwa siku saba mara tu baada ya kuhukumiwa kwao

  • Tangazeni Mfalme na Ufalme! (1919-1941)
    Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
    • J. F. Rutherford na washirika wake saba walikuwa gerezani, na fungu lao la wakati ujao katika tengenezo lilielekea kutokuwa na hakika hata kidogo. Magumu hayo yalishindwaje?

      “Najua Jambo Fulani Kuhusu Sheria ya Waaminifu-Washikamanifu”

      Mkusanyiko uliratibiwa katika Pittsburgh, Pennsylvania, Januari 2-5, 1919, wakati ambao Ndugu Rutherford na washirika wake walikuwa gerezani. Lakini huu haukuwa mkusanyiko wa kawaida—uliunganishwa na mkutano wa kila mwaka wa Watch Tower Society, Jumamosi, Januari 4, 1919. Ndugu Rutherford alijua vema umaana wa mkutano huo. Alasiri ya Jumamosi hiyo yeye alimtafuta Ndugu Macmillan na kumpata kwenye uwanja wa tenisi wa gereza. Kulingana na Macmillan, ilitukia hivi:

      “Rutherford alisema, ‘Mac, nataka kuongea nawe.’

      “‘Wataka kuongea nami juu ya nini?’

      “‘Nataka kuongea nawe juu ya yale yanayotukia katika Pittsburgh.’

      “‘Ningependa kumaliza mchezo huu hapa.’

      “‘Je, wewe hupendezwi na yanayotukia? Wewe hujui leo uchaguzi wa maofisa unafanywa? Huenda ukapitwa na kukataliwa nasi tutakaa humu milele.’

      “‘Ndugu Rutherford,’ nikasema, ‘acha nikuambie jambo ambalo labda hujalifikiria. Hii ndiyo mara ya kwanza tangu Sosaiti ilipoandikishwa kuwa shirika ambapo inaweza kuwa wazi ni nani ambaye Yehova Mungu angetaka awe msimamizi.’

      “‘Wamaanisha nini?’

      “‘Namaanisha kwamba Ndugu Russell alikuwa na kura ya uamuzi naye aliweka wale maofisa mbalimbali. Sasa kwa kuwa yaonekana sisi hatuwezi kushiriki, mambo ni tofauti. Lakini, tukitoka kukiwa kungali wakati twende kwenye kusanyiko hilo kwenye mkutano huo wa mambo ya kikazi, tungeingia nasi tungekubaliwa tuchukue mahali pa Ndugu Russell kwa heshima ileile aliyopokea. Basi ingeonekana kuwa ni kazi ya mwanadamu, si ya Mungu.’

      “Rutherford alionekana kuwa mwenye kufikiri tu naye akaenda zake.”

      Siku hiyo mkutano wenye wasiwasi ulikuwa ukiendelea katika Pittsburgh. “Mvurugo, mgawanyiko, na mabishano yalikuwa mengi kwa kitambo,” akakumbuka Sara C. Kaelin, ambaye alilelewa katika eneo la Pittsburgh. “Wengine walitaka kuahirisha mkutano kwa miezi sita; wengine walitilia shaka uhalali wa kuchagua maofisa waliokuwa gerezani; wengine walidokeza maofisa wapya kabisa.”

      Baada ya mazungumzo marefu, W. F. Hudgings, mwelekezi mmoja wa Peoples Pulpit Association,a alisomea wasikilizaji barua kutoka kwa Ndugu Rutherford. Katika barua hiyo alipeleka upendo na salamu kwa wale waliokusanyika. “Silaha kuu za Shetani ni KIBURI, KUTAKA MAKUU na HOFU,” akaonya. Akionyesha tamaa ya kujitiisha kwa mapenzi ya Yehova, hata alidokeza kwa unyenyekevu wanaume wenye kufaa ikiwa wenye hisa wangeamua kuchagua maofisa wapya kwa ajili ya Sosaiti.

      Mazungumzo yaliendelea kwa kitambo kidogo zaidi, kisha E. D. Sexton, ambaye alikuwa amewekwa kuwa mwenyekiti wa halmashauri ya kutaja majina ya wachaguliwa, akasema kwa ujasiri hivi:

      “Nimewasili sasa hivi. Garimoshi nililosafiria lilichelewa saa arobaini na nane, likiwa limezuiwa na theluji. Nina jambo ambalo ni lazima niliseme na ili nistarehe afadhali niliseme sasa. Ndugu zangu wapendwa, nimekuja hapa, kama vile nyinyi wengine, nikiwa na mawazo fulani akilini—ya kuunga mkono na ya kupinga. . . . Hakuna kizuizi cha kisheria. Tukitaka kuchagua ndugu zetu walioko Kusini kwenye cheo chochote wanachoweza kushika, sioni wala sipati kutoka kwa shauri lolote [la kisheria] nililopokea, jinsi hilo, kwa namna au hali yoyote, litaingilia upande wowote wa kesi yao mbele ya Mahakama ya Serikali Kuu wala mbele ya umma.

      “Mimi naamini kwamba pongezi kubwa zaidi ambayo twaweza kumpa ndugu yetu mpendwa Rutherford ingekuwa ni kumchagua tena kuwa msimamizi wa W[atch] T[ower] B[ible] & T[ract] Society. Mimi sifikiri kwamba kuna shaka lolote katika akili za umma kwa habari ya kwamba sisi twasimama wapi katika shauri hili. Ikiwa ndugu zetu kwa njia yoyote walivunja sheria ambayo hawakuelewa, sisi twajua makusudio yao ni mema. Na mbele za [Mungu] Mweza Yote wao hawakuhalifu sheria yoyote ya Mungu wala ya mwanadamu. Tungedhihirisha utumainifu mkubwa zaidi kwa kumchagua tena Ndugu Rutherford kuwa msimamizi wa Shirika.

      “Mimi si mwanasheria, lakini inapohusu uhalali wa hali hii najua jambo fulani kuhusu sheria ya waaminifu-washikamanifu. Uaminifu-mshikamanifu ndio ambao Mungu hudai. Mimi siwezi kuwazia utumainifu mkubwa zaidi ambao tungeweza kudhihirisha kuliko kuwa na uchaguzi NA KUMCHAGUA TENA NDUGU RUTHERFORD KUWA MSIMAMIZI.”

      Kwa wazi, Ndugu Sexton alieleza hisia za walio wengi kati ya waliohudhuria. Majina yalitajwa; kura ilipigwa; na J. F. Rutherford akachaguliwa kuwa msimamizi, C. A. Wise makamu wa msimamizi, na W. E. Van Amburgh mwandishi-mweka-hazina.

      Kesho yake Ndugu Rutherford alibisha kwenye ukuta wa seli ya Macmillan na kusema: “Chomoza mkono wako nje.” Kisha akampa Macmillan barua ya simu iliyosema kwamba Rutherford alikuwa amechaguliwa tena kuwa msimamizi. “Alikuwa mwenye furaha sana,” Macmillan akakumbuka baadaye, “kuona wonyesho huo wa uhakikishio kwamba Yehova alikuwa akiendesha Sosaiti.”

      Uchaguzi ulikuwa umekwisha, lakini Ndugu Rutherford na wale wengine saba walikuwa wangali gerezani.

      “Uchochezi wa Nchini Pote” kwa Ajili ya Wafungwa

      “Wakati wa majuma machache yaliyopita uchochezi wa nchini pote umeanzishwa kwa ajili ya ndugu hao,” likataarifu The Watch Tower la Aprili 1, 1919. Magazeti fulani ya habari yalikuwa yakitoa wito J. F. Rutherford na washirika wake wafunguliwe. Wanafunzi wa Biblia katika sehemu zote za Marekani walionyesha uungaji-mkono wao kwa kuandika barua kwa wahariri wa magazeti ya habari, washiriki wa kongresi, maseneta, na magavana, wakiwahimiza wachukue hatua kwa ajili ya wafungwa hao wanane. Kwa wazi, Wanafunzi wa Biblia hawangepumzika mpaka ndugu zao wanane wawe huru.

      Kufikia Machi 1919, Wanafunzi wa Biblia katika Marekani walikuwa wakieneza ombi ambamo walimwomba Rais Woodrow Wilson atumie uvutano wake kutimiza mojapo yafuatayo kwa ajili ya ndugu waliofungwa gerezani:

      “KWANZA: Msamaha kamili, ikiwa hilo lawezekana sasa, AU

      “PILI: Kwamba uiagize Idara ya Haki iondoe mashtaka dhidi yao, na kwamba waachiliwe kabisa, AU

      “TATU: Kwamba waachiliwe mara moja kwa dhamana ikingojea uamuzi wa mwisho wa kesi yao utolewe na mahakama zilizo kuu.”

      Kwa muda wa majuma mawili Wanafunzi wa Biblia walipata sahihi 700,000. Ingawa hivyo, ombi hilo halikufikishwa kamwe kwa rais au kwa serikali. Kwa sababu gani? Kwa sababu kabla ya jambo hilo kufanywa, wanaume hao wanane waliachiliwa kwa dhamana. Basi, kazi ya kufanya ombi ilitimiza nini? The Watch Tower la Julai 1, 1919, lilitaarifu: “Uthibitisho ni mwingi mno kwamba Bwana alitaka kazi hii ifanywe, si ili sanasana kufanya ndugu hao watoke gerezani, bali kwa kusudi la kutoa ushahidi kwa ajili ya kweli.”

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki