Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Masimulizi ya Imani Kutoka Gereza Maarufu
    Amkeni!—2001 | Novemba 22
    • KWANZA labda ungependa kujua ni lini Mashahidi wa Yehova walipoingia katika gereza hilo kwa mara ya kwanza na kwa sababu gani. Ilikuwa tarehe 4 Julai mwaka wa 1918, wakati kikundi cha wahudumu wanane Wakristo mashuhuri walipopanda hatua 15 za ngazi ya mawe ya gereza hili. Ikiwa desturi ya siku hizo ilifuatwa, walikuwa wamefungwa pingu mikononi ambazo ziliunganishwa na minyororo iliyokuwa imekazwa tumboni, miguu yao ikiwa imefungwa kwa pingu vilevile. Wafungwa hao wapya walikuwa wanaume wa kiroho ambao walisimamia kazi ya Wanafunzi wa Biblia wa Kimataifa, kama vile Mashahidi wa Yehova walivyoitwa wakati huo. Wanaume hao hawakujua kwamba ingechukua karibu mwaka mzima kuthibitisha kwamba kifungo chao hakikuwa cha haki. Hatimaye, Machi 1919, Mashahidi hao wanane waliteremka ngazi iyo hiyo wakiwa huru, bila pingu. Baadaye waliondolewa hatia kabisa mahakama ilipoamua kufuta mashtaka.a

      Wanaume hao Wakristo waliofungwa huko Atlanta walifunza madarasa ya Biblia humo gerezani. Baadaye, mmoja wa wafungwa hao wanane, A. H. Macmillan, aliripoti kwamba makamu wa afisa wa gereza aliyekuwa mwenye uhasama mwanzoni, alisukumwa kusema hivi hatimaye: ‘Masomo hayo ni mazuri ajabu!’

  • Masimulizi ya Imani Kutoka Gereza Maarufu
    Amkeni!—2001 | Novemba 22
    • [Sanduku/Picha katika ukurasa wa 20, 21]

      “Mliwahi Kuwakaribisha Baadhi ya Marafiki Wangu wa Karibu”

      MNAMO Aprili 1983, Frederick W. Franz, aliyekuwa mshiriki wa Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova, alitembelea gereza la serikali ya Marekani huko Atlanta. Alikuwa na hamu sana ya kutembelea gereza hilo. Alipoingia katika jengo hilo, alipaza sauti na kumwambia hivi askari aliyeketi kwenye meza ukumbini: “Ninataka ujue kwamba mliwahi kuwakaribisha baadhi ya marafiki wangu wa karibu hapa!” Askari huyo alitatanishwa. Franz alimaanisha nini?

      Miaka 64 iliyopita Joseph F. Rutherford na washiriki wake saba walikuwa wameshtakiwa kwa wongo kwamba wamefanya njama, na kuhukumiwa isivyo haki. Baadaye, Rutherford na Franz wakawa marafiki wa karibu na walifanya kazi pamoja. Sasa, zaidi ya miaka 40 baada ya kifo cha Rutherford—na yeye mwenyewe alipokuwa na umri wa miaka 90 hivi—Franz alifurahia kutembelea mahali ambapo rafiki yake alikuwa amefungwa miaka mingi iliyopita. Bila shaka alitafakari ile kazi ambayo Rutherford na wenzake walikuwa wamefanya ndani ya gereza hilo. Hiyo ilikuwa kazi gani?

      Muda mfupi baada ya Rutherford na wenzake kuwasili, makamu wa afisa wa gereza aliwaambia hivi: “Tutawapa kazi ya kufanya. Je, Nyinyi mwaweza kufanya kazi gani?”

      A. H. Macmillan, mmojawapo wa wale wanane alijibu hivi: “Makamu, sijafanya kamwe kazi nyingine maishani mwangu isipokuwa kuhubiri. Je, kuna kazi kama hiyo huku?”

      “La, bwana! Mlihukumiwa kifungo hiki kwa sababu ya kuhubiri, nakuambia sasa, hamtahubiri hapa.”

      Majuma kadhaa yalipita. Wafungwa wote walipaswa kuhudhuria ibada iliyoendeshwa kila Jumapili penye mahali pa ibada, na wale waliotaka waliweza kuhudhuria shule ya Jumapili baadaye. Wanaume hao wanane waliamua kuanzisha funzo lao wenyewe la Biblia, ambalo kila mmoja wao alichukua zamu kuongoza. Baadaye Rutherford alisema: “Watu wachache wenye udadisi walianza kuja, na hata wengine zaidi wakaja.” Punde idadi ya kikundi hicho kidogo cha watu 8 iliongezeka kufikia watu 90!

      Wafungwa waliitikiaje masomo hayo ya Biblia? Mfungwa mmoja alisema hivi: “Mimi nina umri wa miaka 72, na ilinibidi kufungwa gerezani ili nisikie kweli. Kwa hiyo, ninafurahi kwamba nilifungwa katika gereza hili.” Mwingine alisema hivi: “Wakati wangu wa kuachiliwa umekaribia; ninasikitika kwamba nitaachiliwa . . . Niambie ninaweza kupata watu kama nyinyi wapi nitakapoachiliwa?”

      Usiku wa kuamkia kuachiliwa kwao, wanaume hao wanane walipokea barua iliyowagusa kutoka kwa mwanamume kijana aliyekuwa amehudhuria darasa lao. Aliandika hivi: “Ninataka mjue kwamba mmetia ndani yangu tamaa ya kuwa mtu bora, mwenye kustahili heshima, ikiwa itawezekana kwa mtu duni kama mimi, mwenye sifa mbaya na ambaye amekandamizwa na maisha magumu sana kubadilika hivyo. . . . Mimi ni mtu dhaifu sana, najua jambo hilo vizuri kuliko mtu yeyote mwingine, lakini nitajaribu na nitajikakamua ili mbegu ile mliyoipanda itoe mazao yake kamili, na niweze kujisaidia mimi mwenyewe na pia wale walio karibu nami. Huenda ni jambo geni kusikia mtu kama mimi akisema maneno hayo, lakini yanatoka moyoni mwangu, na ni ya kweli.”

      Leo, zaidi ya miaka 80 baadaye, mbegu za kweli ya Biblia bado hupandwa na Mashahidi wa Yehova katika gereza hilo la Atlanta, na vilevile katika magereza mengine mengi.—1 Wakorintho 3:6, 7.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki