-
Matukio Muhimu Ya Mwaka Uliopita2004 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehovah
-
-
Wale wanaotumia Lugha ya Ishara ya Marekani walipata zawadi ya pekee mnamo Septemba 2002. Kuanzia mwezi huo, makala za funzo la Mnara wa Mlinzi zinapatikana kwenye video inayotolewa kila mwezi. Video hiyo inawasaidia viziwi kwa njia ambazo watu wengine hawajawahi kufikiria.
Kwa mfano: Mashahidi wengi wasio viziwi wanaweza kukariri maandiko mengi. Wanaweza kukumbuka maandiko kwa sababu kila wanaposoma au kusomewa maandiko hayo, wao husoma au kusikia maneno yaleyale. Sivyo ilivyo na viziwi. Kwa nini? Kwa sababu Biblia haipatikani katika Lugha ya Ishara ya Marekani, na wale wanaoongoza mikutano hawatumii ishara zilezile wanapozungumzia andiko fulani. Lakini, hali hiyo ilianza kubadilika wakati video za magazeti na vitabu zilipotolewa katika Lugha ya Ishara ya Marekani. Na sasa, kwa kuwa makala za funzo la Mnara wa Mlinzi pia zinapatikana kwenye video, viziwi wanaohudhuria funzo la Mnara wa Mlinzi wanaona ishara zilezile zikitumiwa kutafsiri maandiko yaleyale ya Biblia.
Isitoshe, makutaniko na vikundi vya Lugha ya Ishara ya Marekani havihitaji tena kuwa na “wasomaji” wanaotafsiri mafungu ya Funzo la Mnara wa Mlinzi katika lugha ya ishara. Katika makutaniko ya watu wasio viziwi, huenda ndugu atakayesoma mafungu wakati wa Funzo la Mnara wa Mlinzi akatumia saa moja hivi ya ziada anapotayarisha makala ili kufanya mazoezi ya kusoma vizuri. Lakini katika kutaniko la wahubiri viziwi, mara nyingi ndugu waliotafsiri mafungu katika lugha ya ishara walikuwa wakitumia saa nyingi kufanya mazoezi. Sasa, muda huo unaweza kutumiwa katika utendaji mwingine wa kiroho. Ndugu na dada wanaonaje mpango huo mpya?
Kikundi cha wahubiri viziwi katika jimbo la Rhode Island, Marekani, waliandika hivi: “Tulifurahi sana tulipotangaziwa kwamba tungepata makala za Mnara wa Mlinzi kwenye video. Baadhi ya wahubiri waliguswa hivi kwamba walibubujikwa na machozi.” Kiongozi mmoja wa Funzo la Mnara wa Mlinzi huko Florida alisema kwamba sasa watu wengi sana huinua mikono ili watoe maelezo hivi kwamba yeye “hutatizika kuchagua atakayejibu!” Aliongeza kwamba “akina ndugu wanatoa maelezo bora.” Mzee mwingine aliandika hivi: “Matokeo yamekuwa mazuri sana! Ndugu na dada huelewa vizuri zaidi mambo magumu pia.” Naam, kwa sababu ya baraka ya Yehova, umati unaoongezeka wa viziwi hufurahia pendeleo la kumjua na kumtukuza Mungu.—Rom. 10:10.
-
-
Matukio Muhimu Ya Mwaka Uliopita2004 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehovah
-
-
Septemba 1: Makala za Mnara wa Mlinzi zapatikana kwenye video katika Lugha ya Ishara ya Marekani.
-