-
Jeuri Hutuumiza Sisi SoteAmkeni!—2012 | Agosti
-
-
Jeuri Hutuumiza Sisi Sote
NI NANI ambaye hajawahi kuathiriwa na jeuri? Tunaiona kila siku katika ripoti za habari. Tunaogopa kutendewa kwa jeuri tukiwa barabarani na kazini, na watoto huogopa kutendewa kwa jeuri na watoto wachokozi shuleni. Hata nyumbani, mahali ambapo kwa kawaida watu huhisi wakiwa salama, mamilioni ya watu—hasa wanawake—huhisi kwamba hawako salama. Kwa kweli, ikitegemea nchi, asilimia 70 hivi ya wanawake wanaripoti kwamba wameshambuliwa na mtu ambaye wanaishi pamoja kama mwenzi wa ndoa.
Katika nchi nyingi, watu wanaogopa maasi yenye jeuri ya kisiasa au kijamii au hata ugaidi. Unaweza kutambua kwamba watu wana hofu kwa sababu vifaa vya hali ya juu vya upelelezi vimeongezeka katika nchi fulani, na hasa katika nchi ambazo zimewahi kukumbwa na ugaidi.
Inaeleweka ni kwa nini biashara ya kuuza vifaa vya video vya kupeleleza inanawiri, licha ya kuzorota kwa uchumi ulimwenguni pote. Ni nani anayelipia gharama ya vifaa hivyo vyote? Sisi sote tunavilipia wakati ambapo tunalipa kodi na malipo mengine. Na gharama hizo zitaongezeka kadiri mbinu za kuimarisha usalama zitakavyozidi kuwafanyia watu upelelezi wa ndani zaidi, zitakavyozidi kuenea, na kuwa ghali zaidi.
Athari za jeuri zinapaswa kutufanya tujichunguze zaidi—tuchunguze maadili yetu na mambo tunayoamini. Makala zinazofuata zitajibu maswali haya: Vyombo vya habari vinachangiaje kuenea kwa jeuri? Ni mambo gani yanayoweza kuathiri mtazamo wetu kuelekea jeuri? Tunaweza kujilindaje dhidi ya mambo hayo yasiyofaa?
-
-
Kupumbazwa Na JeuriAmkeni!—2012 | Agosti
-
-
Kupumbazwa Na Jeuri
ULIMWENGU leo umepumbazwa na jeuri. Ni kweli kwamba siku zote kumekuwa na jeuri katika burudani. Hata hivyo, Mtandao wa Kuhamasisha Watu Kuhusu Vyombo vya Habari unasema kwamba “katika miaka ya karibuni jeuri inayoonyeshwa kwenye vyombo vya habari imebadilika. Tofauti moja ni kwamba inaonyeshwa kwa wingi zaidi.” Tofauti nyingine ni kwamba “inaonyeshwa kwa wazi zaidi, inaonyesha ngono zaidi, na ni yenye ukatili zaidi.” Fikiria mambo yafuatayo.
Muziki: Mtandao huo uliotajwa unasema kwamba nyimbo zenye maneno yenye jeuri zaidi “zimekubaliwa katika biashara ya muziki.” Waimbaji fulani hutumia lugha chafu katika nyimbo zao kutukuza uuaji na kuwalala wanawake kinguvu, kutia ndani wake zao na hata mama zao.
Michezo ya Video: “Ukweli wa mambo wenye kusikitisha ni kwamba michezo ya video inahusisha umwagaji mwingi wa damu,” linasema gazeti moja la Uingereza la watu wanaopenda michezo ya video. Liliongezea hivi: “Kwa kiasi fulani, lazima mtu apende jeuri ili afurahie michezo ya video.” Kwa mfano, mchezo mmoja unaopendwa na wengi humwezesha mchezaji kuigiza kwamba anawapiga wanawake na kuwaua akitumia magongo ya besiboli. Wataalamu fulani wanasema kwamba kwa kuwa michezo ya video humhusisha mchezaji moja kwa moja, huenda ikawa na uvutano mbaya zaidi kwa watoto kuliko televisheni.
Sinema: Utafiti unaonyesha kwamba jeuri, ngono, na matusi yameongezeka sana katika sinema, na viwango vinavyotumiwa kupima ikiwa sinema inafaa huenda visiwe vyenye kutegemeka. Isitoshe, matendo ya jeuri hayafanywi tu na wahusika wanaoigiza sehemu za “watu wabaya.” Kulingana na uchunguzi mmoja, karibu nusu ya matendo ya jeuri yanayoonyeshwa katika televisheni, sinema, na video za muziki yanafanywa na wale wanaoigiza sehemu za “watu wazuri.”
Ripoti za Habari: Watayarishaji wengi wa habari katika televisheni hufuata kanuni hii: “Habari inayovutia zaidi ni ile yenye umwagikaji mwingi wa damu.” Utangazaji wa habari ni biashara kubwa na wanahabari wanajua kwamba jeuri huwavutia sana watazamaji, nao watangazaji wa biashara huvutiwa kunapokuwa na watazamaji wengi, navyo vituo vya televisheni katika nchi nyingi hupata mapato makubwa zaidi kutokana na matangazo ya biashara.
Tovuti: Picha halisi na zile zilizofanywa zionekane kana kwamba ni halisi za watu wakiteswa, wakikatwa-katwa viungo, kulemazwa, na kuuawa zinapatikana kwenye Intaneti. Watoto wengi hutembelea tovuti hizo.
Je, Unaweza Kuathiriwa?
Je, watu wanaweza kuathiriwa na matendo ya jeuri yanayoonyeshwa kwenye televisheni, sinema, vitabu, muziki, na burudani nyingine? Wale wanaopata faida kwa kuonyesha jeuri hiyo wanadai kwamba bidhaa zao hazina madhara yoyote. Lakini fikiria hili: Ili kuwavutia watu, wafanyabiashara hulipa mabilioni ya dola ili kutokeza matangazo ya biashara, na tangazo moja linaweza kuonyeshwa kwa sekunde 30 tu. Kwa hiyo, je, inapatana na akili kufikiri kwamba sinema ya dakika 90 ambayo wahusika wake wanajihusisha katika ukosefu wa maadili na jeuri haiwezi kuwa na madhara, hasa kwa watoto ambao akili zao huathirika kwa urahisi?
Muumba wetu, Yehova Mungu anajua utu wa wanadamu vizuri zaidi kuliko sisi. Ametuambia nini kuhusu kushirikiana na watu wajeuri—kutia ndani, wale wanaotutumbuiza kupitia njia mbalimbali za burudani zinazopendwa? Fikiria maandiko ya Biblia yafuatayo:
● “Yehova humchunguza mwadilifu na pia mwovu, na mtu yeyote anayependa jeuri nafsi Yake hakika inamchukia.”—Zaburi 11:5.
● “Usishirikiane na mtu yeyote mwenye mazoea ya kukasirika; wala usiende pamoja na mtu wa mifoko ya ghadhabu, ili usizoee njia yake na hakika uiwekee nafsi yako mtego.”—Methali 22:24, 25.
Ni kweli kwamba hatuwezi kujilinda kabisa na uvutano wote mbaya. Lakini tunaweza kuchagua burudani na watu tutakaoshirikiana nao. Kwa hiyo, jiulize, ‘Mimi ninataka kuwa mtu wa aina gani? ’ Kisha shirikiana na watu walio na maadili na malengo ambayo ungependa kufikia.—Methali 13:20.
Ingawa huenda marafiki na burudani tunazochagua zikaathiri mtazamo wetu kuelekea jeuri, mambo mengine pia yanaweza kutuathiri. Mambo hayo yanaweza kutia ndani nini?
[Picha katika ukurasa wa 4]
Huenda burudani tunazochagua zikaathiri mtazamo wetu kuelekea jeuri
-
-
Visababishi Vya JeuriAmkeni!—2012 | Agosti
-
-
Visababishi Vya Jeuri
NI VIGUMU kueleza ni nini kinachosababisha jeuri. Na mara nyingi jeuri haisababishwi na jambo moja tu, kama vile marafiki, burudani, au mazingira ya kijamii. Huenda mambo mengi yakahusika, kutia ndani mambo yafuatayo.
Kuvunjika moyo na kukata tamaa. Nyakati nyingine watu hutenda kwa jeuri wanapokandamizwa, kubaguliwa, kutengwa na jamii, au kwa sababu ya umaskini au wanapoona kwamba hawawezi kujitegemeza.
Kufuata umati. Kama inavyoonekana mara nyingi katika michezo mingi, watu wanapokuwa katika vikundi au umati, wanashindwa kujizuia wasitende kwa njia isiyofaa. Kwa nini? “Huenda wakasahau viwango vyao vya maadili na yaelekea watatenda kwa jeuri au ukatili wanapochochewa,” kinasema kitabu Social Psychology. Kitabu kingine kinasema kwamba huenda watu kama hao wakaongozwa kutenda bila kufikiri na wakati huo “wakahisi kwamba hawawajibiki kwa jamii.”
Chuki na wivu. Mauaji ya kwanza kutajwa katika historia ya wanadamu yalifanywa na mtu anayeitwa Kaini. (Mwanzo 4:1-8) Akichochewa na wivu wenye chuki, Kaini alimwua ndugu yake—hata ingawa Mungu alikuwa amemwonya adhibiti hisia zake na akaahidi kumbariki ikiwa angefanya hivyo. Hilo linathibitisha ukweli wa maneno haya ya Biblia: “Mahali ambapo pana wivu na ugomvi, hapo pana machafuko na kila jambo baya”!—Yakobo 3:16.
Matumizi mabaya ya kileo na dawa za kulevya. Matumizi mabaya ya vileo huharibu afya ya kimwili na ya kiakili na pia huathiri sehemu mbalimbali za ubongo zinazodhibiti utendaji wa mwili. Kwa sababu hiyo, ni rahisi sana kwa mtu ambaye ametumia dawa za kulevya kutenda kwa jeuri na kwa ukatili anapochokozwa.
Uzembe katika mifumo ya kutekeleza sheria. “Kwa maana hukumu juu ya kazi mbaya haikutekelezwa upesi, ndiyo sababu moyo wa wana wa binadamu umeazimia kabisa ndani yao kutenda yaliyo mabaya,” inasema Mhubiri 8:11. Mifumo ya sheria iliyo dhaifu, isiyo na uwezo wa kutekeleza kazi yake, au iliyo na ufisadi huchangia jeuri kwa njia ya moja kwa moja au isiyo ya moja kwa moja.
Dini ya uwongo. Mara nyingi dini huhusianishwa na jeuri, kutia ndani jeuri ya kidini na ugaidi. Lakini si watu wanaoshikilia sana maoni yao, wenye msimamo mkali wa kidini, na washupavu peke yao wanaopaswa kulaumiwa. Wakati wa vile vita viwili vya ulimwengu, washiriki wa dini kuu—“za Kikristo” na zisizo za Kikristo—walichinjana wakiungwa mkono na viongozi wao wa kidini. Matendo kama hayo humchukiza Mungu.—Tito 1:16; Ufunuo 17:5, 6; 18:24.
Kwa kuwa kuna mambo mengi ambayo huchochea au kutukuza jeuri, je kweli mtu anaweza kuwa mwenye kufanya amani katika ulimwengu wa leo? Ndiyo, kama tutakavyoona katika makala inayofuata.
[Sanduku katika ukurasa wa 6]
JEURI HUANZIA MOYONI
Hata ingawa huenda jeuri ikasababishwa na mambo mengi, chanzo chake kikuu hutoka moyoni. Jinsi gani? Yesu Kristo ambaye aliujua vizuri moyo wa mwanadamu, alisema hivi: “Kutoka katika moyo wa watu, hutoka mawazo mabaya: uasherati, wizi, mauaji, uzinzi, kutamani, matendo ya uovu, udanganyifu, mwenendo mpotovu, jicho lenye wivu, makufuru, majivuno, ukosefu wa akili.” (Marko 7:21, 22) Tunachochea mielekeo hiyo mibaya tunapotazama, kusikiliza, au kufikiria mambo mabaya mara kwa mara.—Yakobo 1:14, 15.
Kwa upande mwingine, tunapolisha akili zetu mambo yanayofaa, kama yale yanayotajwa katika makala iliyo kwenye ukurasa wa 8, ‘tunaua’ tamaa mbaya na kukuza zile nzuri. (Wakolosai 3:5; Wafilipi 4:8) Tukifanya hivyo, Mungu atatusaidia ‘tufanywe kuwa na uwezo katika mtu tuliye kwa ndani.’—Waefeso 3:16.
[Sanduku katika ukurasa wa 7]
JEURI HUWATATANISHA WATAALAMU
Kwa nini katika nchi fulani visa vya uuaji viko juu mara 60 zaidi ya nchi nyingine? Kwa nini vita na matendo mengine ya jeuri yamekuwapo siku zote katika historia ya mwanadamu? Kuna maswali mengi yenye kutatanisha; lakini majibu yenye kusadikisha ni machache.
Wachunguzi fulani wanasema kwamba umaskini na ukosefu wa usawa husababisha jeuri. Takwimu fulani zinaonyesha kwamba karibu asilimia 90 hivi ya vifo vyote vinavyosababishwa na jeuri kutia ndani kujiua, vimetukia katika mataifa maskini ulimwenguni, na maeneo ya majijini wanamoishi watu maskini ndiyo yenye uhalifu mwingi. Lakini, je, ni kweli kwamba watu maskini ni wajeuri zaidi? Au je, wanateseka sana kutokana na jeuri kwa sababu hawawezi kulipia gharama za kupata ulinzi? Katika maeneo mengi kama vile huko Calcutta, India, mamilioni ya watu ni maskini hohehahe. Hata hivyo, Calcutta ni mojawapo ya majiji yaliyo na visa vichache sana vya mauaji ulimwenguni.
Wengine husema kwamba bunduki zinapopatikana kwa urahisi, hilo husababisha kuongezeka kwa jeuri katika jamii. Kwa kweli, bunduki hufanya watu wenye jeuri wawe hatari sana. Lakini wataalamu wana maoni yanayopingana kuhusu kinachofanya jamii fulani ziwe na idadi kubwa ya watu wenye jeuri.
-
-
Unaweza Kujifunza Kuwa Mwenye Kufanya AmaniAmkeni!—2012 | Agosti
-
-
Unaweza Kujifunza Kuwa Mwenye Kufanya Amani
INGAWA huenda tukazaliwa na mielekeo fulani isiyofaa, kwa kawaida mtu hujifunza jeuri. Ndivyo ilivyo na kuwa mwenye kufanya amani. Hata hivyo, ni nani anayeweza kutufundisha njia za amani ya kweli? Muumba wetu ndiye mtu mwenye kutegemeka zaidi, na hekima yake haina kifani. Fikiria mambo matano yafuatayo na uone hekima nyingi inayopatikana katika Biblia.
1 “Usimwonee wivu mtu mwenye jeuri.” (Methali 3:31) Tambua kwamba mtu aliye na sifa nzuri ni yule anayeweza kujizuia na mpole. “Asiye mwepesi wa hasira ni bora kuliko mwanamume mwenye nguvu,” inasema Methali 16:32. Kama kuta zenye nguvu za bwawa, mtu wa aina hiyo anaweza kustahimili anapochokozwa. Kwa kweli, badala ya kuonyesha hasira, anatenda kwa upole na hivyo “hugeuza ghadhabu.” (Methali 15:1) Hata hivyo, mtu mwenye mwelekeo wa kukasirika, hulipuka anapochokozwa kidogo.—Methali 25:28.
2 Chagua marafiki wako kwa hekima. “Mtu wa jeuri atamshawishi mwenzake,” inasema Methali 16:29. Kwa upande mwingine, “anayetembea na watu wenye hekima atakuwa na hekima.” (Methali 13:20) Naam, tukishirikiana na watu wenye kufanya amani ambao wana sifa ya kujizuia na roho ya upole, inaelekea tutajaribu kuwaiga.
3 Sitawisha upendo wa kweli kwa wengine. Ufafanuzi bora zaidi wa upendo unapatikana kwenye 1 Wakorintho 13:4-7. Sehemu fulani ya andiko hilo inasema hivi: “Upendo ni wenye ustahimilivu na wenye fadhili. . . . Hauchokozeki. Hauweki hesabu ya ubaya. . . . Huhimili mambo yote, . . . huvumilia mambo yote.” Yesu alisema kwamba ikiwa tunataka kuiga upendo wa Mungu, ni lazima tuwapende adui zetu.—Mathayo 5:44, 45.
4 Uwe na hakika kwamba Mungu atachukua hatua dhidi ya waovu. “Msimlipe yeyote uovu kwa uovu. . . . Kwa kadiri inavyowategemea ninyi, iweni wenye kufanya amani na watu wote. Wapendwa, msijilipizie kisasi wenyewe, . . . kwa maana imeandikwa: ‘Kisasi ni changu; mimi nitalipa, asema Yehova.’ ” (Waroma 12:17-19) Tunapokuwa na imani katika Mungu na ahadi zake, tunafurahia amani ya akili ambayo watu wasio na imani hawawezi kuelewa.—Zaburi 7:14-16; Wafilipi 4:6, 7.
5 Utegemee Ufalme wa Mungu ulete amani ya kweli duniani. Ufalme wa Mungu ni serikali ya kimbingu ambayo hivi karibuni itawaangamiza waovu wote na kutawala dunia yote. (Zaburi 37:8-11; Danieli 2:44) Chini ya Ufalme huo, “mwadilifu atachipuka,” na kutakuwa “na wingi wa amani mpaka mwezi utakapokuwa haupo tena.”—Zaburi 72:7.
Mafundisho kama hayo ya Biblia yamewasaidia mamilioni ya watu—kutia ndani wengine waliokuwa na mwelekeo wa jeuri—wawe wapenda amani. Soma simulizi la Salvador Garza.
-
-
Nilipenda JeuriAmkeni!—2012 | Agosti
-
-
Nilipenda Jeuri
Limesimuliwa na Salvador Garza
NILIPOKUWA mvulana, nilipenda jeuri na nilipigana na yeyote aliyenikasirisha. Bingwa fulani wa ndondi aliona hilo na akanifundisha mchezo wa kupigana ngumi. Punde si punde nilisafiri kotekote Marekani nikiwa mwanandondi wa kulipwa. Baadaye niliajiriwa kazi ya kuwa mlinzi wa jambazi mmoja.
Niliendelea kupenda jeuri hata baada ya kuoa na kupata watoto sita. Wakati huo nilimiliki klabu moja ya usiku. Ingawa watu kadhaa walijaribu kuniua, nilifurahia maisha hayo yenye msisimuko. Pindi moja niliwapiga risasi wanaume wawili tulipokuwa tukipigana na nikawajeruhi vibaya sana. Pia, mimi na rafiki zangu tulipanga njama ya kumteka nyara mwanasiasa mmoja mashuhuri. Lakini polisi waligundua njama hiyo na kunikamata. Polisi walipoenda kuwakamata rafiki zangu, walifyatuliana risasi na rafiki zangu wote wakauawa. Ninafurahi kwamba wakati huo nilikuwa gerezani!
Miaka mingi baadaye, niliachiliwa huru na nikapata kazi. Siku moja, nilipokuwa nikirudi nyumbani kutoka kazini, ghafula niliumwa sana na kichwa. Nilikuwa na wasiwasi mwingi hivi kwamba nilisali nipate msaada. Mke wangu, Dolores, ambaye alikuwa akijifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova, aliniambia kwamba Mungu ana jina, yaani Yehova. (Zaburi 83:18) Kwa hiyo nilisali nikitumia jina hilo.
Mara tu nilipopata nafuu, Dolores alinitia moyo nihudhurie mikutano ya Mashahidi wa Yehova katika Jumba lao la Ufalme. Niliguswa sana na jinsi Mashahidi walivyonionyesha fadhili na kunijali hivi kwamba nilitokwa na machozi. Jambo hilo lilifanya nianze kujifunza Biblia na mtazamo wangu kuhusu maisha ukaanza kubadilika. Nilifurahia sana mambo niliyokuwa nikifundishwa.
Hata hivyo, ilichukua muda mrefu kujifunza kudhibiti hasira yangu. Kwa mfano, siku moja mimi na rafiki yangu, Antonio, tulipokuwa tukihubiri nyumba kwa nyumba, tulikutana na mwanamume ambaye alitutukana. Nilikasirika sana karibu nimpige. Lakini Antonio akanizuia. Baadaye, kwa subira alinikumbusha jinsi ambavyo Yesu alivumilia dhihaka na matukano. Mtume Petro ambaye alikuwa mwandamani wa karibu wa Yesu, aliandika hivi: “Alipokuwa akitukanwa, hakujibu kwa matukano.” (1 Petro 2:23) Maneno hayo yalinigusa sana.
Nikitafakari maendeleo ambayo nimefanya kadiri ambavyo miaka imepita, ninamshukuru Yehova kwa kunipa roho yake takatifu, ambayo hutusaidia kujizuia na kuwa watu wenye kufanya amani. (Wagalatia 5:22, 23) Familia yangu ina furaha na tunaishi kwa utulivu na amani. Isitoshe, nikiwa mhudumu wa wakati wote, nina pendeleo la kuwasaidia watu kuwa na amani pamoja na Mungu.
[Picha katika ukurasa wa 9]
Kujifunza Biblia kulimsaidia Salvador kupata amani
-