-
Jinsi Tuwezavyo Kusitawisha Wema wa AdiliMnara wa Mlinzi—2001 | Januari 15
-
-
KAMUSI za kisasa hufasiri “wema wa adili” kuwa “ubora wa kiadili; wema.” Kuonyesha wema wa adili ni “kutenda na kufikiri ifaavyo; tabia njema.” Mtunga-kamusi Marvin R. Vincent asema kwamba maana halisi ya awali ya neno la Kigiriki linalotafsiriwa “wema wa adili” huonyesha “ubora wa aina yoyote.” Kwa hiyo si ajabu kwamba wakati fulani sifa kama vile busara, ujasiri, nidhamu, kutopendelea, huruma, uvumilivu, unyofu, unyenyekevu, na uaminifu-mshikamanifu zimetajwa kuwa wema wa adili. Wema wa adili umefasiriwa pia kuwa “kujipatanisha na kiwango cha haki.”
Twapaswa kujipatanisha na viwango vya nani vya ubora, wema, na haki? “Kulingana na wafuasi mashuhuri wa falsafa ya maadili,” likasema gazeti Newsweek, “mashaka yaliyoanzishwa na Enlightenment (Harakati ya Wanafalsafa ya Karne ya 18) yamefanya maoni yote kuhusu mema na mabaya kuwa mapendezi ya kibinafsi, mapendezi ya kihisia-moyo au uchaguzi wa kitamaduni.” Lakini, je, inaridhisha kuamua yaliyo mema na yaliyo mabaya kwa kutegemea tu mapendezi ya mtu? La. Ili tusitawishe wema wa adili, twahitaji kiwango chenye kutegemeka cha mema na mabaya—kiwango ambacho chaweza kutumiwa kuamua iwapo tendo, mtazamo, au sifa fulani ni nzuri au ni mbaya.
Chanzo cha Kweli na cha Pekee cha Viwango vya Adili
Kuna Chanzo kimoja tu cha kweli cha viwango vya adili—Muumba wa wanadamu, Yehova Mungu. Punde tu baada ya kuumba mwanadamu wa kwanza, Adamu, Yehova Mungu alitoa amri hii kwa mwanadamu huyo: “Matunda ya kila mti wa bustani waweza kula, walakini matunda ya mti wa ujuzi wa mema na mabaya usile, kwa maana siku utakapokula matunda ya mti huo utakufa hakika.” (Mwanzo 2:16, 17) Yehova Mungu aliupa mti huo jina hilo la pekee ili kuonyesha kwamba yeye pekee ndiye aliyekuwa na haki ya kuamua mema na mabaya kwa ajili ya viumbe wake. Kwa hiyo, viwango vya Mungu vya mema na mabaya vikawa msingi wa kuhukumu au kupima matendo, mtazamo, na tabia za mtu. Bila viwango hivyo hatungeweza kupambanua mema na mabaya kwa usahihi.
Amri iliyohusu mti wa ujuzi wa mema na mabaya iliwapa Adamu na Hawa uchaguzi—kutii au kutotii. Ili waonyeshe wema wa adili walihitaji kutii amri hiyo. Baada ya muda, Yehova alifunua zaidi mambo yanayompendeza na yale yasiyompendeza, na kuhakikisha yameandikwa katika Biblia kwa ajili yetu. Hivyo basi, kusitawisha wema wa adili kwahusisha kujipatanisha na viwango vya uadilifu vya Yehova vilivyo katika Maandiko.
-
-
Jinsi Tuwezavyo Kusitawisha Wema wa AdiliMnara wa Mlinzi—2001 | Januari 15
-
-
Wema wa adili si kuepuka tu lililo baya. Una nguvu za kiadili. Mtu mwenye wema wa adili ni mwema. Profesa mmoja asema kwamba “mtu ahitaji kujifunza wema wa adili kwa moyo na vilevile kwa akili.”
-