-
‘Weka Moyoni Mwako’ Hekalu la Mungu!Mnara wa Mlinzi—1999 | Machi 1
-
-
‘Weka Moyoni Mwako’ Hekalu la Mungu!
“Mwanadamu, . . . ukaweke moyoni mwako, yote nitakayokuonyesha . . . tangaza habari ya yote utakayoyaona kwa nyumba ya Israeli.” —EZEKIELI 40:4, Union Version, Chapa ya 1989.
1. Watu wa Mungu waliochaguliwa walijikuta katika hali gani mwaka wa 593 K.W.K.?
ULIKUWA mwaka wa 593 K.W.K., mwaka wa 14 wa uhamisho wa Israeli. Kwa Wayahudi walioishi Babiloni, lazima nchi ya nyumbani kwao waliyoipenda iwe ilionekana ikiwa mbali kwelikweli. Wakati wengi wao walipoliona Yerusalemu kwa mara ya mwisho, lilikuwa likichomeka, kuta zake kubwa ajabu zikiwa zimebomolewa, majengo yake yenye fahari yakiwa magofu. Hekalu la Yehova—ambalo wakati mmoja lilikuwa upeo wa fahari ya jiji hilo, na kitovu cha pekee cha ibada safi duniani pote—lilikuwa limebomolewa. Sasa sehemu kubwa ya uhamisho wa Israeli ilikuwa ingali inakuja. Miaka 56 ingepita kabla ya kutokea ukombozi ulioahidiwa.—Yeremia 29:10.
2. Kwa nini kumbukumbu juu ya hekalu la Mungu katika Yerusalemu lingemhuzunisha Ezekieli?
2 Lazima iwe nabii mwaminifu Ezekieli alihuzunika kulifikiria hekalu la Mungu lililokuwa magofu umbali wa mamia ya kilometa, likiwa makao yenye ukiwa ya wanyama-mwitu. (Yeremia 9:11) Baba yake mwenyewe, Buzi, alikuwa ametumikia akiwa kuhani huko. (Ezekieli 1:3) Ezekieli angelifurahia pendeleo ilo hilo, lakini alikuwa amepelekwa uhamishoni pamoja na jamii ya watawala wa Yerusalemu mwaka wa 617 K.W.K., akiwa angali kijana. Sasa akiwa na umri wa karibu miaka 50, yaelekea Ezekieli alijua kwamba hangeliona Yerusalemu kamwe wala hangeshiriki kamwe katika kujengwa upya kwa hekalu lake. Wazia, basi, jinsi lilivyokuwa jambo la maana sana kwa Ezekieli kupata ono juu ya hekalu lenye utukufu!
3. (a) Ni nini lililokuwa kusudi la ono la Ezekieli la hekalu? (b) Ni zipi sehemu nne kubwa za ono hilo?
3 Ono hilo lenye mambo mengi, linalojaza sura tisa za kitabu cha Ezekieli, liliwapa Wayahudi wahamishwa ahadi yenye kutia imani nguvu. Ibada safi ingerudishwa! Karne nyingi zilizopita kutoka wakati huo, hata kufikia siku yetu, ono hilo limekuwa chanzo cha kitia-moyo kwa wampendao Yehova. Jinsi gani? Acheni tuchunguze tuone ono hilo la kiunabii la Ezekieli lilimaanisha nini kwa Waisraeli waliokuwa uhamishoni. Lina sehemu nne kubwa: hekalu, ukuhani, mkuu, na nchi.
Hekalu Larudishwa
4. Ezekieli apelekwa wapi mwanzoni mwa ono lake, ni nini anachoona huko, na ni nani anayempeleka kwenye ziara hiyo ya kuongozwa?
4 Kwanza, Ezekieli aletwa kwenye “mlima mrefu sana.” Juu ya mlima huo upande wa kusini pana hekalu kubwa sana, mfano wa jiji lenye kuta. Malaika fulani, ambaye “kuonekana kwake kulikuwa kama kuonekana kwa shaba,” ampeleka nabii huyo kwenye ziara kamili ya jengo hilo. (Ezekieli 40:2, 3) Ono hilo linapoendelea, Ezekieli amwona malaika huyo akipima kwa makini jozi tatu za malango yenye kulingana pamoja na vyumba vya walinzi wa malango hayo ya hekalu, ua wa nje, ua wa ndani, vyumba vya kulia, madhabahu, na patakatifu pa hekalu hilo pamoja na vyumba vyake vya Patakatifu na Patakatifu Zaidi Sana.
5. (a) Ni uhakikisho upi ambao Yehova ampa Ezekieli? (b) “Mizoga ya wafalme wao” iliyopasa kuondolewa ndani ya hekalu ilikuwa nini, na kwa nini hilo lilikuwa muhimu?
5 Kisha, Yehova mwenyewe atokea katika ono hilo. Aingia hekaluni na kumhakikishia Ezekieli kwamba Yeye atakaa humo. Lakini Yeye aagiza nyumba Yake isafishwe, akisema: “Basi sasa wayaondoe mambo yao ya kikahaba, na mizoga ya wafalme wao, yawe mbali nami, nami nitakaa kati yao milele.” (Ezekieli 43:2-4, 7, 9) Ni dhahiri kwamba hiyo “mizoga ya wafalme wao” ilirejezea sanamu. Watawala na watu wenye kuasi wa Yerusalemu walikuwa wamelichafua hekalu la Mungu kwa sanamu na, kwa kweli, walikuwa wamezifanya sanamu hizo kuwa wafalme. (Linganisha Amosi 5:26.) Sanamu hizo hazikuwa miungu au wafalme hai, bali zilikuwa vitu vilivyokufa, vichafu machoni pa Yehova. Lazima ziondolewe.—Mambo ya Walawi 26:30; Yeremia 16:18.
6. Kupimwa kwa hekalu kulimaanisha nini?
6 Sehemu hii ya ono ilimaanisha nini? Iliwahakikishia wahamishwa hao kwamba ibada safi ingerudishwa kabisa kwenye hekalu la Mungu. Na zaidi, kupimwa kwa hekalu kuliwapa uhakikisho kamili wa kimungu kwamba ono hilo lazima lingetimizwa. (Linganisha Yeremia 31:39, 40; Zekaria 2:2-8.) Ibada ya sanamu yote ingesafishwa iondolewe mbali. Yehova angeibariki nyumba yake mara nyingine tena.
Ukuhani na Yule Mkuu
7. Ni habari gani inayotolewa kuhusu Walawi na makuhani?
7 Ukuhani pia ungepitia hatua ya kusafishwa, au kutakaswa. Walawi wangepasa kukemewa kwa kukubali ibada ya sanamu, ilhali wana wa kikuhani wa Sadoki wangepongezwa na kuthawabishwa kwa kubaki safi.a Na bado, hivyo vikundi vyote viwili vingepata vyeo vya utumishi katika nyumba ya Mungu iliyorudishwa—ikitegemea, bila shaka, uaminifu wa mtu mmoja-mmoja. Zaidi, Yehova aliamuru: “Nao watawafundisha watu wangu tofauti iliyopo kati ya vitu vitakatifu na vitu vya sikuzote [“vichafu,” NW], na kuwafundisha kupambanua kati ya yaliyo machafu na yaliyo safi.” (Ezekieli 44:10-16, 23) Hivyo ukuhani ungerudishwa, na uvumilivu wenye uaminifu wa makuhani ungethawabishwa.
8. (a) Ni nani waliokuwa wakuu wa Israeli la kale? (b) Mkuu aliye katika ono la Ezekieli alikuwa mtendaji katika ibada safi kwa njia zipi?
8 Ono hilo pia humrejezea mmoja aitwaye mkuu. Tangu siku za Musa, taifa hilo lilikuwa na wakuu. Neno la Kiebrania linalotafsiriwa mkuu, yaani na·siʼʹ, lingeweza kurejezea kichwa cha jamaa ya upande wa baba, cha kabila, au hata cha taifa. Katika ono la Ezekieli, watawala wa Israeli wakiwa jamii wanakemewa kwa kuwaonea watu na wanahimizwa sana wasipendelee na wawe wenye haki. Ijapokuwa yeye si wa jamii ya kikuhani, mkuu huyo ni mtendaji kwa njia yenye kutokeza katika ibada safi. Yeye aingia na kutokea ua wa nje akiwa pamoja na yale makabila yasiyo ya kikuhani, aketi kwenye ukumbi wa Lango la Mashariki, na kuandaa baadhi ya dhabihu ili watu wazitoe. (Ezekieli 44:2, 3; 45:8-12, 17) Hivyo, ono hilo liliwahakikishia watu wa Ezekieli kwamba taifa lililorudishwa lingebarikiwa kwa kupewa viongozi wenye kielelezo kizuri, wanaume ambao wangetegemeza ukuhani katika kusimamia watu wa Mungu na kuwa vielelezo bora katika mambo ya kiroho.
Hiyo Nchi
9. (a) Nchi hiyo ingegawanywa vipi, lakini ni nani ambao hawangepata urithi? (b) Toleo takatifu lilikuwa nini, na ni nini ambacho kilikuwa humo?
9 Hatimaye, ono la Ezekieli lilitia ndani ukaguzi wa jumla wa nchi ya Israeli. Ingegawanywa, kila kabila lipate sehemu. Yule mkuu vilevile angepata urithi. Lakini makuhani hawangepata urithi, kwa kuwa Yehova alisema, “Mimi ni urithi wao.” (Ezekieli 44:10, 28; Hesabu 18:20) Ono hilo lilionyesha kwamba sehemu ya nchi iliyogawiwa yule mkuu ingekuwa kila upande wa eneo la pekee liitwalo toleo takatifu. Hilo lilikuwa kipande cha shamba chenye umbo la mraba kilichogawanywa katika sehemu tatu—ya juu kwa Walawi waliotubu, ya katikati kwa makuhani, na ya chini kwa ajili ya jiji na mashamba yake yenye kuzaa. Hekalu la Yehova lingekuwa katika sehemu ya shamba la makuhani, katikati mwa toleo lenye umbo la mraba.—Ezekieli 45:1-7.
10. Unabii uliohusu kugawanywa kwa nchi ulimaanisha nini kwa Wayahudi waaminifu waliokuwa uhamishoni?
10 Hayo yote ni lazima yawe yaliwatia moyo wahamishwa hao kama nini! Kila familia ilihakikishiwa kupata urithi nchini humo. (Linganisha Mika 4:4.) Ibada safi ingekuwa jambo kuu, lililokwezwa mahali hapo. Na ona kwamba katika ono la Ezekieli mkuu huyo, sawa na makuhani, angeishi katika sehemu ya nchi iliyotolewa na watu. (Ezekieli 45:16) Kwa hiyo, katika nchi iliyorudishwa, watu walipaswa kuchangia kazi ya wale ambao Yehova alichagua waongoze, wakiwaunga mkono kwa kukubali mwelekezo wao. Kwa ujumla, nchi hiyo ilikuwa mfano mzuri wa utaratibu, ushirikiano, na usalama.
11, 12. (a) Yehova anawahakikishiaje kiunabii watu wake kwamba angebariki nchi yao iliyorudishwa? (b) Miti iliyo kando-kando ya kingo za mto ilifananisha nini?
11 Je, Yehova angebariki nchi yao? Unabii huo wajibu swali hili kwa ufafanuzi wenye kuchangamsha moyo. Kijito kinatiririka kutoka hekaluni, nacho kinazidi kupanuka kiendeleapo, na kinakuwa mto kufikia wakati kiingiapo Bahari ya Chumvi. Humo baharini kinayapa uhai maji yasiyo na uhai, na biashara ya kuvua samaki yasitawi kando-kando ya eneo la ufuo. Kando-kando ya kingo za mto pana miti mingi inayozaa matunda mwaka mzima, yakitoa lishe na ponyo.—Ezekieli 47:1-12.
12 Kwa wahamishwa hao, ahadi hii ilirudia na kuthibitisha unabii wa mapema wa urudisho waliouthamini sana. Zaidi ya mara moja, manabii wa Yehova waliopuliziwa walikuwa wamelifafanua kwa maneno ya kiparadiso Israeli lililorudishwa na kukaliwa na watu tena. Kichwa kilichorudiwa-rudiwa kilihusu maeneo yenye ukiwa yakirudi kwenye uhai. (Isaya 35:1, 6, 7; 51:3; Ezekieli 36:35; 37:1-14) Hivyo basi, watu wangetarajia kwamba baraka za Yehova zenye kutokeza uhai zingetiririka kama mto kutoka kwenye hekalu lililorudishwa. Matokeo ni kwamba taifa lililokuwa limekufa kiroho lingekuwa hai. Watu hao waliorudishwa wangebarikiwa kwa kupewa wanaume wa kiroho wenye kutokeza—wanaume waadilifu na walio thabiti kama miti iliyo kando-kando ya kingo za kimaono za mto huo, wanaume ambao wangeongoza katika kujenga upya nchi iliyoharibiwa. Isaya pia alikuwa ameandika kuhusu “miti mikubwa ya haki” ambao ‘wangejenga upya mahali palipokuwa pameharibiwa kwa muda mrefu.’—Isaya 61:3, 4, NW.
Ono Hilo Latimizwa Lini?
13. (a) Ni katika maana gani Yehova aliwabariki watu wake waliorudishwa kwa “miti mikubwa ya haki”? (b) Unabii unaohusu Bahari ya Chumvi ulitimizwaje?
13 Je, wahamishwa hao waliorudi walitamaushwa? La, hasha! Katika mwaka wa 537 K.W.K., baki lililorudishwa lilirudi kwenye nchi yake waliyopenda. Baada ya muda, chini ya uongozi wa hawa “miti mikubwa ya haki”—kama vile mwandishi Ezra, manabii Hagai na Zekaria, na Kuhani Mkuu Yoshua—mahali palipokuwa pameharibiwa kwa muda mrefu palijengwa upya. Wakuu, kama vile Nehemia na Zerubabeli, walitawala nchi hiyo bila upendeleo na kwa haki. Hekalu la Yehova lilirudishwa, na maandalizi yake kwa ajili ya uhai—yaani baraka za kuishi kupatana na agano lake—yakaanza kutiririka tena. (Kumbukumbu la Torati 30:19; Isaya 48:17-20) Moja ya baraka hizo ilikuwa ujuzi. Ukuhani ulirudishwa kwenye wajibu wake, na makuhani wakawafundisha watu Sheria. (Malaki 2:7) Tokeo ni kwamba watu walifanywa hai kiroho, wakawa tena watumishi wa Yehova wenye kuzaa matunda, kama ilivyofananishwa na kuponywa kwa Bahari ya Chumvi na kutokeza biashara ya uvuvi yenye matokeo.
14. Kwa nini kungekuwa na utimizo wa unabii wa Ezekieli unaopita yale yaliyofanyika baada ya Wayahudi kurudi kutoka uhamishoni Babiloni?
14 Je, matukio hayo ndiyo yaliyokuwa utimizo wa pekee wa ono la Ezekieli? La; jambo fulani kubwa zaidi laonyeshwa. Fikiria: Hekalu ambalo Ezekieli aliona kwa kweli halingeweza kujengwa kama ilivyofafanuliwa. Ni kweli, Wayahudi walilichukulia ono hilo kwa uzito na hata wakafanya mambo kadhaa kwa njia halisi.b Hata hivyo, hekalu hilo la kimaono lote lilikuwa kubwa mno lisiweze hata kutoshea juu ya Mlima Moria, mahali ambapo hekalu la kwanza lilikuwa. Kwa kuongezea, hekalu la Ezekieli halikuwa ndani ya jiji bali umbali fulani katika eneo la shamba tofauti, ilhali hekalu la pili lilijengwa mahali palipokuwa na lile la kwanza, jijini Yerusalemu. (Ezra 1:1, 2) Na zaidi, hakuna mto wowote halisi ulitokea ndani ya hekalu la Yerusalemu. Hivyo basi, Israeli la kale lilipata utimizo mdogo tu wa unabii wa Ezekieli. Hili lamaanisha kwamba lazima kuwe na utimizo wa kiroho, ulio mkubwa zaidi wa ono hilo.
15. (a) Hekalu la kiroho la Yehova lilianza kutenda lini? (b) Ni nini kinachoonyesha kwamba ono la Ezekieli halikutimizwa wakati wa maisha ya Kristo duniani?
15 Kwa wazi, lazima tutafute utimizo mkubwa wa ono la Ezekieli katika hekalu kubwa la kiroho la Yehova, ambalo mtume Paulo azungumzia kwa urefu katika kitabu cha Waebrania. Hekalu hilo lilianza kutenda wakati Yesu Kristo alipotiwa mafuta awe Kuhani wa Cheo cha Juu wake mwaka wa 29 W.K. Lakini je, ono la Ezekieli lilitimizwa katika siku ya Yesu? Yaonekana sivyo. Yesu, akiwa Kuhani wa Cheo cha Juu, alitimiza maana ya kiunabii ya Siku ya Kufunika kupitia ubatizo wake, kifo chake cha kidhabihu, na kuingia kwake ndani ya Patakatifu Zaidi Sana, mbinguni kwenyewe. (Waebrania 9:24) Hata hivyo, kwa kupendeza, ono la Ezekieli halitaji kamwe lolote kuhusu kuhani wa cheo cha juu au Siku ya Kufunika. Hivyo, haielekei kuwa ono hilo lilikuwa likielekeza kwenye karne ya kwanza W.K. Basi, ono hilo linahusu kipindi kipi cha wakati?
16. Mandhari ya ono la Ezekieli yatukumbusha juu ya unabii gani mwingine, na hilo latusaidiaje kuutambua wakati wa utimizo mkubwa wa ono la Ezekieli?
16 Ili kupata jibu, acheni tulirudie ono lenyewe. Ezekieli aliandika: “Katika maono ya Mungu alinileta mpaka nchi ya Israeli, akaniweka juu ya mlima mrefu sana, ambao juu yake palikuwapo kana kwamba ni umbo la mji upande wa kusini.” (Ezekieli 40:2) Mandhari ya ono hilo, ambayo ni “mlima mrefu sana,” hutukumbusha juu ya Mika 4:1: “Itakuwa katika siku za mwisho, ya kwamba mlima wa nyumba ya BWANA utawekwa imara juu ya milima, nao utainuliwa juu ya vilima; na watu wa mataifa watauendea makundi makundi.” Unabii huo waanza kutimizwa wakati gani? Mika 4:5 huonyesha kwamba huo waanza kutimizwa mataifa yakiwa yangali yanaabudu miungu isiyo ya kweli. Kwa kweli, imetimizwa wakati wetu wenyewe, “siku za mwisho,” ambapo ibada safi imeinuliwa juu, imerudishwa mahali pake panapofaa maishani mwa watumishi wa Mungu.
17. Unabii wa Malaki 3:1-5 watusaidiaje kutambua wakati hekalu la ono la Ezekieli liliposafishwa?
17 Ni nini kilichofanya hali hiyo ya kurudishwa iwezekane? Kumbuka, katika tukio muhimu zaidi katika ono la Ezekieli, Yehova aja kwenye hekalu na kusisitiza kwamba nyumba yake isafishwe kwa kuondolewa ibada ya sanamu. Hekalu la Mungu la kiroho lilisafishwa lini? Kwenye Malaki 3:1-5, Yehova atabiri juu ya wakati ambapo “atalijilia hekalu lake” akiandamana na “mjumbe [wake] wa agano,” Yesu Kristo. Kwa kusudi gani? ‘Yeye atakuwa mfano wa moto wa mtu asafishaye fedha, na kama mfano wa sabuni ya mtu afuaye nguo.’ Kusafishwa huko kulianza wakati wa vita ya ulimwengu ya kwanza. Tokeo lilikuwa nini? Yehova amekaa katika nyumba yake na kubariki nchi ya kiroho ya watu wake kuanzia mwaka wa 1919 na kuendelea. (Isaya 66:8) Basi, twaweza kukata kauli kwamba unabii wa hekalu wa Ezekieli unapata utimizo muhimu wakati wa siku za mwisho.
18. Ono la hekalu litakuwa na utimizo wake wa mwisho lini?
18 Kama ulivyo unabii mwingine mbalimbali wa urudisho, ono la Ezekieli lina utimizo zaidi, wa mwisho, katika Paradiso. Ni wakati huo tu ndipo wanadamu wenye mioyo minyofu watapata manufaa kamili ya mpango wa Mungu wa hekalu. Ndipo Kristo atakapotumia thamani ya dhabihu yake ya fidia, akishirikiana na ukuhani wake wa kimbingu wa 144,000. Raia watiifu wote wa kibinadamu wa utawala wa Kristo watainuliwa wafikie ukamilifu. (Ufunuo 20:5, 6) Hata hivyo, Paradiso haiwezi kuwa ndio wakati mkuu wa utimizo wa ono la Ezekieli. Kwa nini sivyo?
Ono Hilo Hukazia Siku Yetu Wenyewe
19, 20. Kwa nini ni lazima utimizo mkuu wa ono hilo utukie leo, wala si katika Paradiso?
19 Ezekieli aliona hekalu lililohitaji kusafishwa liondolewe ibada ya sanamu na uasherati wa kiroho. (Ezekieli 43:7-9) Hilo kwa kweli halingeweza kutumika kuhusu ibada ya Yehova katika Paradiso. Na zaidi, makuhani katika ono hilo hufananisha jamii ya kikuhani ya watiwa-mafuta wakiwa wangali duniani, wala si baada ya ufufuo wao wa kimbingu au wakati wa kipindi cha Milenia. Kwa nini? Ona kwamba makuhani hao wanaonyeshwa wakitumikia katika ua wa ndani. Makala katika Mnara wa Mlinzi yameonyesha kwamba ua huo hufananisha ule msimamo wa kipekee ambao makuhani wa cheo cha chini wa Kristo wanao wakiwa wangali duniani.c Pia ona kwamba ono hilo hukazia kutokamilika kwa makuhani hao. Wanaambiwa watoe dhabihu kwa ajili ya dhambi zao wenyewe. Wanaonywa juu ya hatari ya kuwa wachafu—kiroho na kiadili. Kwa hivyo, hawafananishi wale watiwa-mafuta waliofufuliwa, ambao mtume Paulo aliandika hivi kuwahusu: “Tarumbeta itavuma, na wafu watafufuliwa wakiwa wasioharibika.” (1 Wakorintho 15:52; Ezekieli 44:21, 22, 25, 27) Makuhani katika ono hilo huchangamana na kutumikia watu moja kwa moja. Haitakuwa hivyo katika Paradiso, wakati jamii ya kikuhani itakuwa mbinguni. Kwa hiyo, ono hilo hutoa mfano bora kabisa wa jinsi ambavyo watiwa-mafuta hufanya kazi kwa ukaribu na “umati mkubwa” ulio duniani leo.—Ufunuo 7:9; Ezekieli 42:14.
20 Hivyo, ono la Ezekieli la hekalu huashiria matokeo yenye mafaa yanayoletwa na usafishaji wa kiroho unaotimizwa leo. Lakini hilo lamaanisha nini kwako? Hilo sio fumbo tu la kitheolojia lisilokuhusu. Ono hilo lina mengi zaidi yanayohusu ibada yako ya siku kwa siku ya kumwabudu Mungu wa pekee wa kweli, Yehova. Tutaona jinsi jambo hilo lilivyo katika makala yetu inayofuata.
-
-
Lile “Hekalu” na Yule “Mkuu” LeoMnara wa Mlinzi—1999 | Machi 1
-
-
Lile “Hekalu” na Yule “Mkuu” Leo
“Na mukubwa [“mkuu,” “Union Version”], wakati wanapoingia, ataingia katikati yao; na wakati wanapotoka, watatoka pamoja.” —EZEKIELI 46:10, Zaire Swahili Bible.
1, 2. Ni ukweli gani muhimu unaotuwezesha kuelewa maana nyingi ya ono la Ezekieli la hekalu?
MARABI fulani wa zamani hawakuridhika kabisa na kitabu cha Ezekieli. Kulingana na Talmud, baadhi yao hata walifikiria juu ya kukiondoa kabisa kutoka kwa orodha ya Maandiko Matakatifu yaliyokubalika. Ilikuwa vigumu kwao kueleza maana ya hilo ono la hekalu na wakatangaza kwamba hakuna mwanadamu angeweza kulielewa. Wasomi wengine wa Biblia wametatanishwa na ono hilo la Ezekieli la hekalu la Yehova. Vipi sisi?
2 Tangu kurudishwa kwa ibada safi, Yehova amewabariki watu wake kwa mimweko mingi ya ufahamu wa kiroho, kutia ndani kutambua maana ya hekalu la Mungu la kiroho ni nini—mpango wa kihekalu wa Yehova kwa ajili ya ibada safi.a Ukweli huu muhimu hutuwezesha kuelewa kwa kadiri kubwa maana ya ono la Ezekieli la hekalu. Acheni tuchunguze kwa makini sehemu nne za ono hilo—hekalu, ukuhani, mkuu, na nchi. Hizo zamaanisha nini leo?
Lile Hekalu na Wewe
3. Twajifunza nini kutokana na dari refu na michoro iliyo ukutani katika vijia vya kuingia hekaluni?
3 Wazia kwamba tunazuru hekalu hilo la kimaono. Twakaribia na kupanda vipandio saba hadi kwenye moja la hayo malango makubwa mno. Tukiwa ndani ya kijia hicho cha kuingilia, twatazama juu kwa kuduwaa. Dari lake lina urefu wa meta 30 kwenda juu! Hivyo, twakumbushwa kwamba viwango vya kuingia katika mpango wa Yehova wa ibada ni vya juu sana. Miali ya nuru inayopenyeza kutoka madirishani yamulika michoro ya mitende iliyo ukutani, ambayo hutumiwa katika Maandiko kufananisha unyofu. (Zaburi 92:12; Ezekieli 40:14, 16, 22) Mahali hapo patakatifu ni pa wale walio wanyofu kiadili na kiroho. Kwa kupatana na hilo, twataka kubaki tukiwa wanyofu ili ibada yetu ikubalike kwa Yehova.—Zaburi 11:7.
4. Ni nani wanaozuiwa kuingia hekaluni, na hilo latufunza nini?
4 Kando-kando ya pande zote za kijia hicho, pana vyumba vitatu vya walinzi. Je, hao walinzi wataturuhusu tuingie ndani ya hekalu? Yehova amwambia Ezekieli kwamba hapana mgeni ambaye “moyo wake haukutahiriwa” awezaye kuingia. (Ezekieli 40:10; 44:9) Hilo lamaanisha nini? Lamaanisha kwamba Mungu hukubali tu wale wanaopenda sheria zake na kuishi kulingana nazo wamwabudu. (Yeremia 4:4; Waroma 2:29) Yeye huwakaribisha watu wa aina hiyo katika hema lake la kiroho, nyumba yake ya ibada. (Zaburi 15:1-5) Tangu ibada safi irudishwe mwaka wa 1919, tengenezo la kidunia la Yehova limetegemeza na kufafanua sheria zake za adili hatua kwa hatua. Wale wanaokataa kutii kimakusudi hawakubaliwi tena kushirikiana na watu wake. Leo, lile zoea linalotegemea Biblia la kutenga na ushirika wakosaji wasiotubu limesaidia kudumisha ibada yetu ikiwa safi na yenye utakato.—1 Wakorintho 5:13.
5. (a) Ni ufanano gani uliopo kati ya ono la Ezekieli na ono la Yohana ambalo limerekodiwa kwenye Ufunuo 7:9-15? (b) Katika ono la Ezekieli, makabila 12 yanayoabudia kwenye ua wa nje yafananisha nani?
5 Kijia hicho chaelekeza kwenye ua wa nje ambapo watu wamwabudu na kumsifu Yehova. Hilo latukumbusha juu ya ono la mtume Yohana la “umati mkubwa” ukimwabudu Yehova “mchana na usiku katika hekalu lake.” Mitende yaonyeshwa katika maono yote mawili. Katika ono la Ezekieli hiyo yapamba kuta za kijia cha kuingilia. Katika ono la Yohana waabudu wana matawi ya mitende mikononi mwao, ikionyesha shangwe yao katika kumsifu Yehova na kumkaribisha Yesu akiwa Mfalme wao. (Ufunuo 7:9-15) Katika muktadha wa ono la Ezekieli, yale makabila 12 ya Israeli yafananisha “kondoo wengine.” (Yohana 10:16; linganisha Luka 22:28-30.) Je, wewe ni mmoja wa wale wanaopata shangwe katika kumsifu Yehova kwa kutangaza Ufalme wake?
6. Kusudi la vyumba vya kulia vilivyo katika ua wa nje lilikuwa nini, na hilo laweza kuwakumbusha wale wa kondoo wengine kuhusu pendeleo jipi?
6 Tunapozuru ua wa nje, twaona vyumba vya kulia 30 ambamo watu wanashiriki kula matoleo yao ya hiari. (Ezekieli 40:17) Leo, wale walio miongoni mwa kondoo wengine hawatoi dhabihu za wanyama, lakini hawaji kwenye hekalu la kiroho mikono mitupu. (Linganisha Kutoka 23:15.) Mtume Paulo aliandika: “Kupitia [Yesu] acheni sikuzote tumtolee Mungu dhabihu ya sifa, yaani, tunda la midomo ambayo hulifanyia jina lake tangazo la hadharani. Zaidi ya hayo, msisahau kule kutenda mema na kule kushiriki vitu pamoja na wengine, kwa maana kwa dhabihu za namna hiyo Mungu hupendezwa vema.” (Waebrania 13:15, 16; Hosea 14:2) Ni pendeleo kubwa kumtolea Yehova dhabihu kama hizo.—Mithali 3:9, 27.
7. Kupimwa kwa hekalu hutupa uhakikisho juu ya nini?
7 Ezekieli atazama malaika alipimapo hekalu hilo la kimaono. (Ezekieli 40:3) Vivyo hivyo, mtume Yohana aliambiwa: “Inuka upime patakatifu pa hekalu la Mungu na madhabahu na wale wanaoabudu ndani yalo.” (Ufunuo 11:1) Kupima huko kwamaanisha nini? Katika visa vyote viwili yaonekana hilo lilikuwa uhakikisho kamili, ishara kwamba hapana chochote kiwezacho kumzuia Yehova asitimize makusudi yake yanayohusu ibada safi. Vivyo hivyo leo, twaweza kuhakikishiwa kwamba hakuna chochote—hata upinzani mkali kutoka kwa serikali zenye nguvu—kiwezacho kuzuia kurudishwa kwa ibada safi.
8. Ni nani waingiao malango yanayoelekea kwenye ua wa ndani, na malango hayo yatukumbusha nini?
8 Tunapotembea kuvuka ua wa nje, huenda tukaona kwamba kuna malango matatu ya kuingia kwenye ua wa ndani; malango ya ndani yako kwenye mpangilio mmoja na malango ya nje, nayo ni yenye kipimo kimoja na hayo ya nje. (Ezekieli 40:6, 20, 23, 24, 27) Ni makuhani tu wanaoweza kuingia katika ua wa ndani. Malango ya ndani yatukumbusha kwamba ni lazima watiwa-mafuta wafikie viwango na sheria za kimungu, viwango na sheria hizohizo huwaongoza Wakristo wote wa kweli. Lakini kazi ya makuhani ni nini, nayo yamaanisha nini leo?
Ukuhani Mwaminifu
9, 10. “Ukuhani wa kifalme,” kama ulivyotangulia kuonyeshwa na jamii ya kikuhani katika ono la Ezekieli, umetoa ufundishaji wa kiroho jinsi gani?
9 Katika nyakati za kabla ya Ukristo, makuhani walifanya kazi ngumu hekaluni. Kazi ya kuchinja wanyama wa dhabihu, kuwatoa kwenye madhabahu, na kuwatumikia makuhani wenzao na watu ilikuwa yenye kuchosha sana. Lakini walikuwa na kazi nyingine muhimu. Yehova aliamuru hivi kuhusu makuhani hao: “Watawafundisha watu wangu tofauti iliyopo kati ya vitu vitakatifu na vitu vya sikuzote [“vichafu,” NW], na kuwafundisha kupambanua kati ya yaliyo machafu na yaliyo safi.”—Ezekieli 44:23; Malaki 2:7.
10 Je, unathamini kazi ngumu na utumishi mnyenyekevu ambao watiwa-mafuta wakiwa kikundi, “ukuhani wa kifalme,” wamefanya kwa ajili ya ibada safi? (1 Petro 2:9) Kama ukuhani wa Kilawi wa zamani, wameongoza katika kutoa mafundisho ya kiroho, wakisaidia watu kuelewa kile ambacho ni safi na chenye kukubalika machoni pa Mungu na kile ambacho si safi na kisichokubalika. (Mathayo 24:45) Mafundisho hayo, yanayotolewa kupitia vichapo vinavyotegemea Biblia na mikutano ya Kikristo na mikusanyiko, yamewasaidia mamilioni ya watu kupatanishwa na Mungu.—2 Wakorintho 5:20.
11. (a) Ono la Ezekieli lilikaziaje umuhimu wa usafi kwa makuhani? (b) Katika siku za mwisho, watiwa-mafuta wamesafishwaje katika maana ya kiroho?
11 Hata hivyo, ni lazima makuhani wafanye mengi zaidi ya kufundisha wengine wawe safi; ni lazima wao wenyewe wawe safi. Hivyo basi, Ezekieli aliona kimbele hatua ya kusafishwa kwa ukuhani wa Israeli. (Ezekieli 44:10-16) Vivyo hivyo, historia yaonyesha kwamba mwaka wa 1918, Yehova aliketi “kama asafishaye” katika hekalu lake la kiroho, akiichunguza jamii ya kikuhani ya watiwa-mafuta. (Malaki 3:1-5) Wale walioonwa kuwa safi kiroho au waliotubu kuhusu ibada yao ya sanamu ya hapo awali, waliruhusiwa kuendelea na pendeleo la utumishi katika hekalu lake la kiroho. Na bado, sawa na watu wale wengine wote, watiwa-mafuta wakiwa mtu mmoja-mmoja wanaweza kuwa wachafu—kiroho na kiadili. (Ezekieli 44:22, 25-27) Imewalazimu kujitahidi sana ili kubaki “bila doa kutokana na ulimwengu.”—Yakobo 1:27; linganisha Marko 7:20-23.
12. Kwa nini twapaswa kuthamini kazi ya watiwa-mafuta?
12 Kila mmoja wetu aweza kujiuliza, ‘Je, ninathamini kielelezo kilichowekwa na watiwa-mafuta kwa miaka mingi ya utumishi wao mwaminifu? Je, ninaiga imani yao?’ Ni vizuri kwa wale wa umati mkubwa kukumbuka kwamba hawatakuwa na watiwa-mafuta sikuzote hapa duniani. Yehova alisema hivi kuhusu makuhani katika ono la Ezekieli: “Wala hamtawapa milki [ya nchi] iwayo yote katika Israeli; mimi ni milki yao.” (Ezekieli 44:28) Vivyo hivyo, watiwa-mafuta hawana sehemu yoyote yenye kudumu milele hapa duniani. Wao wana urithi wa kimbingu, na wale wa umati mkubwa huliona kuwa pendeleo kuwaunga mkono na kuwatia moyo wakiwa wangali hapa duniani.—Mathayo 25:34-40; 1 Petro 1:3, 4.
Yule Mkuu—Yeye Ni Nani?
13, 14. (a) Ni kwa nini yule mkuu lazima awe mmoja wa kondoo wengine? (b) Mkuu hufananisha nani?
13 Sasa swali lenye kuamsha udadisi lazuka. Basi, mkuu huyo anawakilisha nani? Kwa kuwa yeye huzungumziwa akiwa kama mtu mmoja na vilevile kama kikundi, twaweza kukata kauli kwamba anawakilisha jamii ya watu. (Ezekieli 44:3; 45:8, 9) Lakini watu gani? Kwa hakika si watiwa-mafuta. Katika ono hilo, yeye anafanya kazi kwa kushirikiana na ukuhani, lakini yeye si mmoja wao. Tofauti na jamii ya kikuhani, yeye apewa urithi katika nchi hiyo na kwa hiyo wakati wake ujao upo hapa duniani, wala si mbinguni. (Ezekieli 48:21) Na zaidi, Ezekieli 46:10 (ZSB), lasema: “Na mukubwa [“mkuu,” UV], wakati wanapoingia [yale makabila yasiyo ya kikuhani yanapoingia kwenye ua wa nje wa hekalu], ataingia katikati yao; na wakati wanapotoka, watatoka pamoja.” Yeye haingii katika ua wa ndani bali huabudia katika ua wa nje, akiingia na kutoka hekaluni pamoja na hao watu. Kwa wazi mambo hayo ya hakika humweka mkuu huyo miongoni mwa umati mkubwa wa kondoo wengine.
14 Kwa wazi, mkuu huyo ana daraka fulani miongoni mwa watu wa Mungu. Katika ua wa nje, yeye aketi katika ukumbi wa Lango la Mashariki. (Ezekieli 44:2, 3) Hilo lingeonyesha cheo cha uangalizi, kinachofanana na kile cha wanaume wazee katika Israeli walioketi kwenye lango la jiji na kutoa hukumu. (Ruthu 4:1-12; Mithali 22:22) Ni nani miongoni mwa kondoo wengine walio na vyeo vya uangalizi leo? Ni wazee walio na tumaini la kidunia ambao wamewekwa rasmi na roho takatifu. (Matendo 20:28) Hivyo, jamii ya mkuu sasa inatayarishwa kwa tazamio la kutumikia baadaye katika cheo cha usimamizi katika ulimwengu mpya.
15. (a) Ono la Ezekieli hutufafanuliaje uhusiano uliopo baina ya wazee ambao ni wa umati mkubwa na jamii ya kikuhani ya watiwa-mafuta? (b) Wazee watiwa-mafuta wamechukua uongozi upi katika tengenezo la Mungu la kidunia?
15 Lakini je, ni uhusiano gani uliopo baina ya jamii ya kikuhani ya watiwa-mafuta na wanaume wazee hao ambao, wakiwa sehemu ya umati mkubwa, wanatumikia katika vyeo vya usimamizi? Ono la Ezekieli ladokeza kwamba fungu la wazee hao walio washiriki wa umati mkubwa ni la chini na la kuunga mkono, huku watiwa-mafuta wakichukua uongozi wa kiroho. Jinsi gani? Kumbuka, makuhani katika ono hilo walipewa daraka la kufundisha watu mambo ya kiroho. Pia waliambiwa watumikie wakiwa mahakimu katika kesi za kisheria. Kwa kuongezea, Walawi walipewa kazi ya kuwa “wasimamizi” katika malango ya hekalu. (Ezekieli 44:11, 23, 24) Kwa wazi, mkuu huyo alipaswa kujitiisha kwa utumishi wa kiroho na uongozi wa hao makuhani. Basi, inafaa kwamba katika nyakati za kisasa watiwa-mafuta wamechukua uongozi katika ibada safi. Kwa mfano, washiriki wa Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova wamechaguliwa kutoka miongoni mwao. Wazee hao waaminifu, watiwa-mafuta, wamekuwa wakiizoeza kwa makumi ya miaka jamii ya mkuu huyo inayokua. Washiriki hao wa Baraza Linaloongoza wanawatayarisha wale wanaotazamia kuwa washiriki wa jamii hii kwa ajili ya siku watakapoachiwa mamlaka kamili ya madaraka yao katika ulimwengu mpya wa Mungu unaokuja.
16. Kulingana na Isaya 32:1, 2, ni lazima wazee wote watendeje?
16 Je, hawa wanaotazamia kuwa washiriki, ambao wako katika mstari wa kupata madaraka yaliyoongezeka wakiwa kama jamii ya mkuu, ni waangalizi wa aina gani? Unabii ulio kwenye Isaya 32:1, 2 wasema hivi: “Tazama, mfalme atamiliki kwa haki, na wakuu [“wana-wafalme,” NW] watatawala kwa hukumu. Na mwanadamu atakuwa kama mahali pa kujificha na upepo, na mahali pa kujisitiri na dhoruba; kama mito ya maji mahali pakavu, kama kivuli cha mwamba mkubwa katika nchi yenye uchovu.” Unabii huo unatimizwa sasa, wazee Wakristo—watiwa-mafuta na kondoo wengine—wanapofanya kazi ili kulinda kundi dhidi ya “dhoruba” kama vile mnyanyaso na kuvunjika moyo.
17. Wachungaji Wakristo wapaswa kujionaje, na kundi lapaswa kuwaonaje?
17 Maneno “mwana-mfalme” na “mkuu,” ambayo yana maana sawa katika lugha ya Kiebrania, hayatumiwi kama majina ya vyeo vinavyokusudiwa kuwatukuza wanadamu. Badala yake, yanafafanua daraka ambalo wanaume hawa wanalo katika kutunza kondoo za Mungu. Yehova aonya kwa ukali hivi: “Na iwatoshe ninyi, enyi wakuu wa Israeli; ondoeni dhuluma na unyang’anyi; fanyeni hukumu na haki.” (Ezekieli 45:9) Yafaa wazee wote leo wazingatie shauri hilo. (1 Petro 5:2, 3) Kwa upande mwingine, kundi hutambua kwamba Yesu ameandaa wachungaji, ambao ni “zawadi zikiwa wanadamu.” (Waebrania 4:8) Sifa zao za ustahili zimeandikwa katika Neno la Mungu mwenyewe lililopuliziwa. (1 Timotheo 3:1-7; Tito 1:5-9) Hivyo basi, Wakristo hufuata mwongozo wa wazee.—Waebrania 13:7.
18. Ni nini baadhi ya madaraka ya wale wanaotazamia kuwa jamii ya mkuu sasa, na wakati ujao daraka lake litakuwa nini?
18 Katika nyakati za Biblia wakuu fulani walikuwa na uwezo mkubwa, na wengine uwezo mdogo. Leo, wazee wa ule umati mkubwa wana madaraka mengi mbalimbali. Baadhi yao hutumikia kutaniko moja; wengine hutumikia makutaniko mengi wakiwa waangalizi wasafirio; wengine hutumikia nchi nzimanzima wakiwa washiriki wa Halmashauri ya Tawi; wengine husaidia moja kwa moja halmashauri mbalimbali za Baraza Linaloongoza. Katika ulimwengu mpya, Yesu ataweka rasmi “wakuu katika nchi zote” ili waongoze miongoni mwa waabudu wa Yehova duniani. (Zaburi 45:16) Yaelekea atateua wengi wao kutoka miongoni mwa wazee waaminifu wa siku hizi. Kwa kuwa hawa wanaume wanajithibitisha wenyewe sasa, ataamua kuwakabidhi wengi mapendeleo makubwa zaidi wakati ujao anapofunua daraka la jamii ya mkuu katika ulimwengu mpya.
Nchi ya Watu wa Mungu Leo
19. Nchi iliyo kwenye ono la Ezekieli huwakilisha nini?
19 Pia, ono la Ezekieli laonyesha nchi iliyorudishwa ya Israeli. Sehemu hii ya ono huwakilisha nini? Unabii mwingine mbalimbali wa urudisho ulitabiri kwamba nchi hiyo, Israeli, ingekuwa paradiso kama Edeni. (Ezekieli 36:34, 35) Leo, twafurahia “nchi” iliyorudishwa, na hii pia ni ya Kiedeni kwa njia fulani. Vivyo hivyo, mara nyingi sisi husema juu ya paradiso yetu ya kiroho. Gazeti la Mnara wa Mlinzi limefafanua “nchi” yetu kuwa “eneo la utendaji” la watu wa Mungu waliochaguliwa.b Kokote ambako huenda mtumishi wa Yehova yuko, yeye yumo katika nchi hiyo iliyorudishwa maadamu anajitahidi kutegemeza ibada ya kweli kwa kutembea katika hatua za Kristo Yesu.—1 Petro 2:21.
20. Twaweza kujifunza kanuni ipi kutokana na “toleo takatifu” kwenye ono la Ezekieli, nasi huenda tukaitumiaje kanuni hii?
20 Vipi juu ya sehemu ya nchi iitwayo “toleo takatifu”? Hiyo ilikuwa toleo la watu ili kutegemeza ukuhani na jiji. Vivyo hivyo, “watu wote wa nchi” wangepaswa kutoa sehemu ya nchi kwa ajili ya mkuu. Hilo lamaanisha nini leo? Bila shaka, halimaanishi kwamba watu wa Mungu watwikwe mzigo wa kulipa jamii ya makasisi mshahara. (2 Wathesalonike 3:8) Badala yake, utegemezo unaotolewa kwa wazee hasa ni wa kiroho. Unatia ndani kusaidia katika kazi iliyopo na kuonyesha roho ya ushirikiano, na ya kujitiisha. Hata hivyo, kama ilivyokuwa katika siku ya Ezekieli, toleo hili hutolewa “kwa BWANA [“Yehova,” NW], wala si kwa mwanadamu yeyote.—Ezekieli 45:1, 7, 16.
21. Huenda tukajifunza nini kutokana na kugawanywa kwa nchi katika ono la Ezekieli?
21 Si mkuu na makuhani pekee waliogawiwa mahali katika nchi hiyo iliyorudishwa. Kugawanywa kwa nchi kwaonyesha kwamba kila moja la yale makabila 12 lina urithi ulio salama. (Ezekieli 47:13, 22, 23) Hivyo, wale wa umati mkubwa wana sehemu katika paradiso ya kiroho iliyopo sasa na pia watagawiwa nchi watakaporithi sehemu katika eneo la kidunia la Ufalme wa Mungu.
22. (a) Jiji kwenye ono la Ezekieli huwakilisha nini? (b) Ni nini tunachoweza kujifunza kutokana na jiji kuwa na malango pande zote?
22 Hatimaye, jiji kwenye ono hilo huwakilisha nini? Hilo si jiji la kimbingu, kwa kuwa limo katikati mwa sehemu ya nchi “chafu” (isiyo takatifu). (Ezekieli 48:15-17, NW) Hivyo, ni lazima liwe la kidunia. Naam, jiji ni nini? Je, hilo halitoi wazo la watu kuja pamoja wakiwa kikundi na kufanyiza kitu fulani kilichoundwa na kilichopangwa kitengenezo? Ndiyo. Hivyo, yaonekana jiji hilo hufananisha usimamizi wa kidunia unaowafaidi wote watakaofanyiza jamii yenye uadilifu ya kidunia. Jiji hilo litatenda kikamilifu katika “dunia mpya” itakayokuja. (2 Petro 3:13) Malango yaliyo pande zote za jiji hilo, moja kwa kila kabila, yaonyesha vizuri uwazi wa mambo. Leo, watu wa Mungu hawako chini ya usimamizi fulani wa kisiri na wa kichinichini. Ndugu walio na madaraka lazima wawe wenye kufikika; wote wanajua vizuri kanuni zinazowaongoza. Uhakika wa kwamba watu kutoka makabila yote hulima shamba linalotegemeza jiji hilo hutukumbusha kwamba kondoo wengine huunga mkono, hata kwa njia ya kimwili, mipango ya usimamizi ambayo imefanywa kwa ajili ya watu wa Mungu ulimwenguni pote.—Ezekieli 48:19, 30-34.
23. Tutachunguza nini katika makala inayofuata?
23 Lakini, vipi juu ya mto unaotiririka kutoka patakatifu pa hekalu? Kile ambacho huo huwakilisha leo na wakati ujao ndilo litakalokuwa jambo kuu la makala ya tatu na ya mwisho katika mfululizo huu.
-
-
Baraka ya Yehova Juu ya “Nchi” YetuMnara wa Mlinzi—1999 | Machi 1
-
-
Baraka ya Yehova Juu ya “Nchi” Yetu
“Kila kitu kitaishi po pote utakapofikilia mto huo.”—EZEKIELI 47:9.
1, 2. (a) Maji yana umuhimu gani? (b) Maji kwenye mto wa kimaono wa Ezekieli hufananisha nini?
MAJI ni kitu cha ajabu. Uhai wote duniani huyategemea. Hakuna yeyote kati yetu awezaye kuishi kwa muda mrefu bila maji. Pia twayatumia kwa kusafisha, kwa kuwa maji yaweza kufyonza na kuondolea mbali uchafu. Hivyo, sisi hutumia maji kuogea, kufulia nguo, na hata kuoshea vyakula. Kufanya hivyo kwaweza kuokoa uhai wetu.
2 Biblia hutumia maji kufananisha maandalizi ya Yehova ya kiroho kwa ajili ya uhai. (Yeremia 2:13; Yohana 4:7-15) Maandalizi haya yatia ndani kusafishwa kwa watu wake kupitia fidia ya dhabihu ya Kristo na ujuzi juu ya Mungu ulio katika Neno lake. (Waefeso 5:25-27) Katika ono la Ezekieli la hekalu, mto wa kimwujiza unaotiririka kutoka kwenye hekalu hufananisha baraka hizo zinazotokeza uhai. Lakini mto huo hutiririka lini, nao wamaanisha nini kwetu leo?
Mto Watiririka Katika Nchi Iliyorudishwa
3. Ezekieli aliona nini, kama ilivyoripotiwa kwenye Ezekieli 47:2-12?
3 Wakiwa mateka huko Babiloni, watu wa Ezekieli walihitaji sana maandalizi ya Yehova. Basi ilimtia Ezekieli moyo kama nini kuona mchuruziko wa maji ukitokea mahali patakatifu na kutiririka kutoka ndani ya hekalu la kimaono! Malaika fulani akipima kijito hicho baada ya kila dhiraa 1,000. Kina chake chaongezeka kutoka kifundo cha mguu hadi kufikia magotini, kutoka magotini hadi kiunoni, halafu unakuwa mto ambao mtu ahitaji kuogelea. Mto huo hutokeza uhai na mazao. (Ezekieli 47:2-11) Ezekieli aambiwa: “Na karibu na mto, juu ya ukingo wake, upande huu na upande huu, utamea kila mti wa chakula.” (Ezekieli 47:12a) Mto huo unapoingia Bahari ya Chumvi—maji yasiyo na uhai—uhai waanza! Samaki watokea kwa wingi. Biashara ya uvuvi yasitawi.
4, 5. Ni jinsi gani unabii wa Yoeli unaohusu mto unafanana na ule wa Ezekieli, na kwa nini hilo ni muhimu?
4 Huenda unabii huo mzuri uliwakumbusha Wayahudi wahamishwa unabii mwingine uliorekodiwa zaidi ya karne mbili mapema: “Chemchemi itatokea katika nyumba ya BWANA, na kulinywesha bonde la Shitimu.”a (Yoeli 3:18) Unabii wa Yoeli, kama ulivyo wa Ezekieli, unatabiri kwamba mto ungetiririka kutoka kwenye nyumba ya Mungu, lile hekalu, na kutokeza uhai katika eneo la ukame.
5 Kwa muda mrefu gazeti Mnara wa Mlinzi limeeleza kwamba unabii wa Yoeli unatimizwa siku zetu.b Kwa hakika basi, iko vivyo hivyo kwa habari ya ono la Ezekieli linalofanana na unabii huo. Katika nchi iliyorudishwa ya watu wa Mungu leo, kama tu katika Israeli la kale, baraka za Yehova zimetiririka kwelikweli.
Mtiririko Mkubwa wa Baraka
6. Kunyunyizwa kwa damu katika madhabahu ya kimaono kulipaswa kuwakumbusha Wayahudi juu ya nini?
6 Ni nini chanzo cha baraka ambazo watu wa Mungu waliorudishwa wanazo? Naam, ona kwamba maji hayo hutiririka kutoka hekalu la Mungu. Vivyo hivyo leo, baraka hizo huja kutoka kwa Yehova kupitia hekalu lake kubwa la kiroho—mpango kwa ajili ya ibada safi. Ono la Ezekieli laongezea jambo fulani muhimu. Katika ua wa ndani, kijito hicho chatiririka kupitia kusini mwa madhabahu. (Ezekieli 47:1) Madhabahu imo katikati hasa mwa hekalu hilo la kimaono. Yehova amfafanulia Ezekieli kwa makini kuihusu na aamuru kwamba damu ya dhabihu inyunyizwe juu yake. (Ezekieli 43:13-18, 20) Madhabahu hiyo ilikuwa na maana kubwa sana kwa Waisraeli wote. Agano lao na Yehova lilikuwa limehalalishwa muda mrefu mapema wakati Musa aliponyunyiza damu juu ya madhabahu iliyokuwa chini ya Mlima Sinai. (Kutoka 24:4-8) Kunyunyizwa kwa damu juu ya madhabahu hiyo ya kimaono kulipaswa kuwakumbusha kwamba mara warudipo kwenye nchi yao iliyorudishwa, baraka za Yehova zingetiririka maadamu wangeishi kulingana na agano lao naye.—Kumbukumbu la Torati 28:1-14.
7. Wakristo leo wanapata maana gani katika madhabahu ya ufananisho?
7 Hali kadhalika, watu wa Mungu leo wanabarikiwa kupitia agano—lililo bora, agano jipya. (Yeremia 31:31-34) Hilo pia lilihalalishwa muda mrefu uliopita kwa damu ya Yesu Kristo. (Waebrania 9:15-20) Leo, tuwe miongoni mwa watiwa-mafuta, ambao ni washiriki wa agano hilo, au miongoni mwa “kondoo wengine,” ambao wanafaidika kutokana nalo, twapata maana kubwa katika madhabahu hiyo ya mfano. Hiyo hufananisha mapenzi ya Mungu kuhusiana na dhabihu ya Kristo. (Yohana 10:16; Waebrania 10:10) Kama tu vile madhabahu hiyo ya ufananisho imo katikati hasa mwa hekalu la kiroho, dhabihu ya fidia ya Kristo ni ya umuhimu mkubwa katika ibada safi. Hiyo ndiyo msingi wa msamaha wa dhambi zetu na kwa sababu hiyo, dhabihu hiyo inakuwa pia msingi wa matumaini yetu yote ya wakati ujao. (1 Yohana 2:2) Hivyo, twajitahidi kuishi kulingana na sheria inayohusishwa na hilo agano jipya, “sheria ya Kristo.” (Wagalatia 6:2) Maadamu twafanya hivyo, tutafaidika kutokana na maandalizi ya Yehova ya uhai.
8. (a) Ni nini ambacho ua wa ndani wa hekalu la kimaono ulikosa? (b) Makuhani kwenye hekalu la kimaono wangejisafisha kwa njia gani?
8 Faida moja ya aina hiyo ni msimamo safi mbele za Yehova. Katika hekalu hilo la kimaono, ua wa ndani unakosa kitu fulani ambacho kilitokeza sana katika ua wa tabenakulo na katika hekalu la Solomoni—beseni kubwa, ambayo baadaye iliitwa bahari, kwa ajili ya makuhani kuogea ndani. (Kutoka 30:18-21; 2 Mambo ya Nyakati 4:2-6) Je, makuhani katika hekalu la kimaono la Ezekieli wangetumia nini kusafishia? Naam, kijito kile cha kimwujiza kinachotiririka kupitia ua wa ndani! Ndiyo, Yehova angewabariki kwa kuwawezesha kufurahia msimamo safi, au mtakatifu.
9. Ni jinsi gani watiwa-mafuta na umati mkubwa waweza kuwa na msimamo safi leo?
9 Vivyo hivyo leo, watiwa-mafuta wamebarikiwa kwa kupewa msimamo safi mbele za Yehova. Yehova huwaona kuwa watakatifu, akiwatangaza kuwa waadilifu. (Waroma 5:1, 2) Vipi juu ya “umati mkubwa,” unaofananishwa na yale makabila yasiyo ya kikuhani? Wao wanaabudia katika ua wa nje, na kijito kile kile hupitia ndani ya sehemu hiyo ya hekalu la kimaono. Basi, yafaa kama nini, kwamba mtume Yohana aliona umati mkubwa ukiwa umevaa kanzu safi nyeupe wanapoabudia katika ua wa hekalu la kiroho! (Ufunuo 7:9-14) Haidhuru wametendewa vipi katika ulimwengu huu ulioshuka kiadili, wanaweza kuwa na uhakika kwamba maadamu wanazoea imani katika dhabihu ya fidia ya Kristo, Yehova awaona kuwa safi na wenye kutakata. Wanajizoezaje imani? Kwa kufuata hatua za Yesu, wakiwa na uhakika kamili katika dhabihu ya fidia.—1 Petro 2:21.
10, 11. Ni ipi iliyo sehemu moja muhimu ya maji ya ufananisho, na hiyo yahusuje mpanuko wa ajabu wa mto huo?
10 Kama ilivyotangulia kutajwa, kuna sehemu nyingine muhimu ya maji haya ya ufananisho—ujuzi. Katika Israeli lililorudishwa, Yehova aliwabariki watu wake kwa mafundisho ya Kimaandiko kupitia ukuhani. (Ezekieli 44:23) Kwa njia kama hiyo, Yehova amewabariki watu wake leo kwa mafundisho tele juu ya Neno lake la kweli, kupitia ule “ukuhani wa kifalme.” (1 Petro 2:9) Ujuzi juu ya Yehova Mungu, juu ya makusudi yake kwa wanadamu, na hasa juu ya Yesu Kristo na Ufalme wa Kimesiya umetiririka kwa wingi unaozidi kuongezeka daima wakati huu wa siku za mwisho. Burudisho la mbubujiko wa kiroho tunaopata na ambao unazidi kuongezeka ni tukufu jinsi gani!—Danieli 12:4.
11 Kama vile ule mto ambao malaika aliupima ulivyoendelea kuongezeka kina hatua kwa hatua, ndivyo mtiririko wa baraka zinazotokeza uhai kutoka kwa Yehova umeongezeka sana ili kutosheleza mmiminiko wa watu wanaoingia katika nchi yetu ya kiroho iliyobarikiwa. Unabii mwingine wa urudisho ulitabiri hivi: “Mdogo atakuwa elfu, na mnyonge atakuwa taifa hodari; mimi, BWANA, nitayahimiza hayo wakati wake.” (Isaya 60:22) Maneno hayo yametimia—mamilioni ya watu wamemiminika makundi makundi na kujiunga nasi katika ibada safi! Yehova amefanya “maji” mengi sana yapatikane kwa wote wanaomjia. (Ufunuo 22:17) Yeye huhakikisha kwamba tengenezo lake la kidunia hugawa Biblia na fasihi za Biblia ulimwenguni pote, katika mamia ya lugha. Vivyo hivyo, mikutano ya Kikristo na mikusanyiko imepangwa ulimwenguni pote ili wote waweze kupewa maji safi kabisa ya kweli. Maandalizi hayo huwaathirije watu?
Maji Yatokeza Uhai!
12. (a) Ni kwa nini miti iliyo katika ono la Ezekieli yaweza kuzaa kama ifanyavyo? (b) Miti hiyo yenye kuzaa sana huwakilisha nini katika siku za mwisho?
12 Mto katika ono la Ezekieli watokeza uhai na afya. Ezekieli anapopata kujua juu ya miti ambayo ingekua kando-kando ya mto huo, aambiwa: “Majani yake hayatanyauka, wala matunda yake hayatatindika kamwe; . . . na matunda yake yatakuwa chakula; na majani yake yatakuwa ni dawa.” Kwa nini miti hiyo huzaa kwa njia hii yenye kustaajabisha? “Kwa sababu maji yake yanatoka mahali patakatifu.” (Ezekieli 47:12b) Miti hiyo ya mfano hufananisha kimbele maandalizi yote ya Mungu kwa ajili ya kurudisha wanadamu kwenye ukamilifu kwa msingi wa dhabihu ya fidia ya Yesu. Hapa duniani wakati huu, baki la watiwa-mafuta huongoza katika kuandaa lishe na ponyo la kiroho. Baada ya wale 144,000 wote kupokea thawabu yao ya kimbingu, faida zinazotokana na utumishi wao wa kikuhani wakiwa watawala-wenzi pamoja na Kristo zitaenea hadi wakati ujao, hatimaye zikiongoza kwenye kushindwa kabisa kwa kifo cha Kiadamu.—Ufunuo 5:9, 10; 21:2-4.
13. Ni ponyo gani limetimizwa wakati wetu?
13 Mto huo wa kimaono unaingia katika Bahari ya Chumvi isiyo na uhai na kuponya chochote ambacho hukifikia. Bahari hiyo hufananisha mazingira yaliyokufa kiroho. Lakini uhai watokea kwa wingi ‘kila mahali ufikapo mto huo.’ (Ezekieli 47:9) Vivyo hivyo, katika siku za mwisho, watu wamefanywa hai kiroho kokote ambako maji ya uhai yamepenyeza. Watu wa kwanza kutiwa uhai mpya jinsi hiyo ni baki la watiwa-mafuta mwaka wa 1919. Walirudishwa kighafula kwenye uhai wa kiroho kutoka hali iliyo kama kifo, ya kutotenda. (Ezekieli 37:1-14; Ufunuo 11:3, 7-12) Tangu wakati huo maji hayo ya uhai yamewafikia watu wengine walio wafu kiroho, nao wamekuwa hai na kufanyiza umati mkubwa wa kondoo wengine unaozidi kuongezeka daima, wanaompenda na kumtumikia Yehova. Hivi karibuni, uandalizi huu utafikia halaiki ya watu watakaofufuliwa.
14. Biashara ya uvuvi inayositawi sehemu fulani ya ufuo wa Bahari ya Chumvi yaonyesha vizuri jambo gani leo?
14 Uhai wa kiroho hutokeza uzalishaji. Hilo laonyeshwa kwa biashara ya uvuvi inayositawi kwenye fuo za bahari ambayo hapo kwanza ilikuwa imekufa. Yesu aliwaambia wafuasi wake hivi: “Nitawafanya nyinyi kuwa wavuvi wa watu.” (Mathayo 4:19) Katika siku za mwisho, kazi ya uvuvi ilianza kwa kukusanywa kwa mabaki ya watiwa-mafuta, lakini haijakomea hapo. Maji yenye kutokeza uhai yatokayo katika hekalu la kiroho la Yehova, kutia ndani baraka ya ujuzi sahihi, yaathiri watu wa mataifa yote. Kokote ambako mto huo umefikia, uhai wa kiroho umetokezwa.
15. Ni nini kionyeshacho kwamba si kila mtu atakayekubali maandalizi ya Mungu ya uhai, nalo tokeo la mwisho ni nini kwa watu kama hao?
15 Bila shaka, si wote huitikia ujumbe wa uhai ifaavyo sasa; wala si wote watakaofufuliwa wakati wa Utawala wa Milenia wa Kristo wataitikia ifaavyo. (Isaya 65:20; Ufunuo 21:8) Malaika atangaza kwamba sehemu fulani za bahari haziponywi. Sehemu hizo zenye matope, zisizo na uhai ‘zaachwa ziwe za chumvi.’ (Ezekieli 47:11) Kwa habari ya watu wa siku yetu, si wote huyakubali maji ya Yehova yenye kutokeza uhai wanayopewa. (Isaya 6:10) Kwenye Har–Magedoni, wale wote ambao wamechagua kubaki katika hali isiyo na uhai na yenye ugonjwa kiroho wataachiwa chumvi, yaani, wataharibiwa milele. (Ufunuo 19:11-21) Hata hivyo, wale ambao wamekuwa wakinywa maji hayo kwa uaminifu wanaweza kutumaini kuokoka na kuona utimizo wa mwisho wa unabii huu.
Mto Huo Watiririka Katika Paradiso
16. Ni lini na jinsi gani ono la Ezekieli la hekalu litakuwa na utimizo wake wa mwisho?
16 Kama ulivyo unabii mwingine mbalimbali wa urudisho, ono la Ezekieli la hekalu hupata utimizo wake wa mwisho wakati wa ile Milenia. Wakati huo jamii ya kikuhani haitakuwa tena hapa duniani. “Watakuwa makuhani wa Mungu na wa Kristo, na watatawala wakiwa wafalme pamoja naye [mbinguni] kwa miaka elfu.” (Ufunuo 20:6) Makuhani hawa wa kimbingu watashirikiana na Kristo katika kutoa manufaa kamili ya fidia ya dhabihu ya Kristo. Hivyo, wanadamu waadilifu wataokolewa, wakiwa wamerudishwa kwenye ukamilifu!—Yohana 3:17.
17, 18. (a) Mto unaotokeza uhai unafafanuliwaje kwenye Ufunuo 22:1, 2, na wakati muhimu wa utimizo wa ono hilo ni lini? (b) Ni kwa nini mto huo wa maji ya uhai utaingia kipindi cha mpanuko ulio mkubwa zaidi katika Paradiso?
17 Kwa kweli, ndipo mto ambao Ezekieli aliona utatiririka kwa maji ya uhai yenye nguvu nyingi. Huo ndio wakati muhimu wa utimizo wa unabii uliorekodiwa kwenye Ufunuo 22:1, 2: “Akanionyesha mto wa maji ya uhai, mwangavu kama fuwele, ukitiririka kutoka katika kiti cha ufalme cha Mungu na cha Mwana-Kondoo kuteremka katikati ya njia pana yalo. Na upande huu wa mto na upande ule kulikuwa na miti ya uhai yenye kutokeza mazao kumi na mawili ya matunda, ikitoa matunda yayo kila mwezi. Na majani ya hiyo miti yalikuwa ya kuponya mataifa.”
18 Wakati wa Milenia, magonjwa yote—ya kimwili, ya kiakili, na ya kihisia-moyo—yataponywa. Hilo laonyeshwa vyema kwa ‘kuponywa kwa mataifa’ kupitia miti hiyo ya ufananisho. Kwa sababu ya maandalizi yatakayotolewa na Kristo pamoja na wale 144,000, “hapana mwenyeji atakayesema, Mimi mgonjwa.” (Isaya 33:24) Nao mto huo utaingia kipindi cha mpanuko wake ulio mkubwa zaidi. Utalazimika kupanuka na kuongezeka kina ili kuwatosheleza mamilioni, labda mabilioni, ya wanadamu waliofufuliwa ambao watayanywa maji hayo safi ya uhai. Mto wa kimaono uliponya Bahari ya Chumvi, ukitokeza uhai popote maji yake yalipotiririka kuelekea. Katika Paradiso, wanaume na wanawake watakuja kwenye uhai kwa maana iliyo kamili zaidi, wakiponywa kutokana na kifo cha Kiadamu kilichorithiwa ikiwa watajizoeza imani katika manufaa za fidia watakazopewa. Ufunuo 20:12 hutabiri kwamba “hati-kunjo” zitafunguliwa katika siku hizo, zikiandaa nuru zaidi ya uelewevu ambao utawanufaisha wale watakaofufuliwa. Kwa kuhuzunisha, hata katika Paradiso, watu fulani watakataa kuponywa. Waasi hao ndio wale ‘walioachiwa chumvi’ ya uharibifu wa milele.—Ufunuo 20:15.
19. (a) Kugawanywa kwa nchi kutatimizwaje katika Paradiso? (b) Jiji lafananisha kitu gani kikuu katika Paradiso? (c) Ni nini umuhimu wa jiji kuwa umbali fulani kutoka kwenye hekalu?
19 Pia, wakati huo, kugawanywa kwa nchi katika ono la Ezekieli kutakuwa na utimizo wake wa mwisho. Ezekieli aliona nchi ikigawanywa ifaavyo; vivyo hivyo, kila Mkristo mwaminifu aweza kuwa na uhakika kwamba atakuwa na sehemu, yaani urithi, katika Paradiso. Yaonekana, ile tamaa ya mtu kuwa na nyumba yake mwenyewe ya kuishi na kuitunza itatimizwa kwa utaratibu. (Isaya 65:21; 1 Wakorintho 14:33) Lile jiji ambalo Ezekieli aliona hufananisha kwa kufaa mpango wa usimamizi ambao Yehova akusudia kwa ajili ya dunia mpya. Jamii ya kikuhani ya watiwa-mafuta haitakuwapo kimwili tena miongoni mwa wanadamu. Ono hilo ladokeza hilo kwa kulionyesha jiji likiwa katika nchi “chafu” umbali fulani kutoka kwa hekalu. (Ezekieli 48:15, linganisha NW.) Wale 144,000 watakapokuwa wakitawala na Kristo mbinguni, Mfalme hatakosa waakilishi duniani. Raia zake wa kibinadamu watanufaika kwa njia kubwa kutokana na mwongozo na mwelekezo wenye upendo wa ile jamii ya mkuu. Hata hivyo, kitovu halisi cha serikali kitakuwa, si duniani, bali mbinguni. Kila mtu duniani, kutia ndani jamii ya mkuu, atakuwa katika ujitiisho kwa Ufalme wa Kimesiya.—Danieli 2:44; 7:14, 18, 22.
20, 21. (a) Kwa nini jina la jiji hilo lafaa? (b) Kuelewa kwetu ono la Ezekieli kwapaswa kutufanya tujiulize maswali gani?
20 Ona maneno ya kumalizia ya unabii wa Ezekieli: “Jina la mji huo tangu siku hiyo litakuwa Yehova Mwenyewe Yupo Hapo.” (Ezekieli 48:35, NW) Kusudi la jiji hilo halitakuwa kuwapa wanadamu nguvu au mamlaka; wala kusudi halitakuwa kutekeleza mapenzi ya binadamu yeyote. Hilo ni jiji la Yehova, daima likidhihirisha akili zake na njia zake zenye upendo na zenye kiasi. (Yakobo 3:17) Hilo latupa uhakikisho wenye kuchangamsha moyo kwamba Yehova ataibariki, hadi kufikia wakati ujao udumuo kwa muda usio dhahiri, jamii ya kibinadamu iliyopangwa ya “dunia mpya.”—2 Petro 3:13.
21 Je, hatushangilii juu ya tumaini hilo lililo mbele yetu? Kwa kufaa, basi, kila mmoja wetu atafanya vema kuuliza: ‘Je, mimi naitikiaje baraka nzuri ajabu zinazofunuliwa katika ono la Ezekieli? Je, naunga mkono kwa uaminifu kazi inayofanywa na waangalizi wenye upendo, kutia ndani wale mabaki watiwa-mafuta na wale wanaotazamia kuwa washiriki wa jamii ya mkuu? Je, nimeifanya ibada safi kuwa jambo muhimu kabisa katika maisha yangu? Je, ninatumia kwa ukamili maji ya uhai yanayotiririka kwa wingi sana leo?’ Acheni kila mmoja wetu aendelee kufanya hivyo na kupendezwa na maandalizi ya Yehova kwa umilele wote!
-