-
“Nilitumwa Kufanya Hivyo”‘Njoo Uwe Mfuasi Wangu’
-
-
Sura ya 8
“Nilitumwa Kufanya Hivyo”
1-4. (a) Yesu anamfundisha mwanamke Msamaria kwa ustadi jinsi gani, na anapata matokeo gani? (b) Mitume wake wana maoni gani juu ya jambo hilo?
YESU na mitume wake wamekuwa wakitembea kwa muda fulani. Wanaelekea kaskazini, kutoka Yudea kwenda Galilaya. Njia fupi zaidi, inayochukua siku tatu hivi, inapitia Samaria. Saa sita hivi mchana, wanakaribia jiji dogo linaloitwa Sikari ambapo wanapumzika.
2 Mitume wake wanapoenda kununua chakula, Yesu anapumzika kando ya kisima kilicho nje ya jiji hilo. Mwanamke fulani anakuja kuchota maji. Ikiwa Yesu angetaka, angempuuza kwa kuwa “amechoka kwa sababu ya safari hiyo.” (Yohana 4:6) Ingeeleweka ikiwa Yesu angempuuza mwanamke huyo Msamaria na kuendelea na shughuli zake. Kama tulivyoona katika Sura ya 4 ya kitabu hiki, mwanamke huyo angetazamia mtu yeyote ambaye ni Myahudi ampuuze. Hata hivyo, Yesu anaanzisha mazungumzo pamoja naye.
3 Anaanza kwa mfano unaohusu maisha ya kila siku ya mwanamke huyo. Anazungumzia jambo ambalo mwanamke huyo anafanya sasa hivi. Amekuja kuchota maji, naye Yesu anazungumza kuhusu maji ya uzima yatakayomaliza kiu yake ya kiroho. Mara kwa mara mwanamke huyo anataja mambo yanayoweza kutokeza mabishano.a Kwa busara, Yesu anaepuka mambo hayo na kuzungumzia habari aliyokuwa nayo akilini. Anakazia mambo ya kiroho, yale yanayohusu ibada safi na Yehova Mungu. Maneno yake yana matokeo sana, kwa maana mwanamke huyo anawasimulia watu wa jiji hilo, nao pia wanataka kumsikiliza Yesu.—Yohana 4:3-42.
4 Mitume wanaporudi, wana maoni gani kuhusu ushahidi wa pekee ambao Yesu anatoa? Hawachangamki hata kidogo. Wanashangaa kumwona Yesu akizungumza na mwanamke huyo, na inaonekana kwamba hawaongei na mwanamke huyo hata kidogo. Mwanamke huyo anapoondoka, wanamsihi Yesu tena na tena ale chakula ambacho wameleta. Hata hivyo, Yesu anawaambia: “Nina chakula ambacho hamkijui.” Wanashangaa! Mwanzoni, wanafikiri kwamba Yesu anazungumzia chakula cha kimwili. Kisha, anaeleza hivi: “Chakula changu ni mimi kufanya mapenzi yake aliyenituma na kuimaliza kazi yake.” (Yohana 4:32, 34) Hivyo, Yesu anawafundisha kwamba anaiona kazi yake kuu maishani kuwa jambo la maana kuliko kula. Anataka wawe na maoni hayohayo kuhusu kazi hiyo.
-
-
“Nilitumwa Kufanya Hivyo”‘Njoo Uwe Mfuasi Wangu’
-
-
a Kwa mfano, mwanamke huyo anapotaka kujua kwa nini Myahudi anazungumza na Msamaria, anataja ugomvi ambao umekuwako kwa karne nyingi kati ya watu wa jamii hizo mbili. (Yohana 4:9) Pia, anakazia kwamba wao ni wazao wa Yakobo, jambo ambalo Wayahudi wa wakati huo wanapinga vikali. (Yohana 4:12) Wayahudi wanawaita Wasamaria, Wakutha, ili kukazia kwamba wametokana na jamii ya kigeni.
-