-
Aina Mpya ya ChakulaKitabu Changu cha Hadithi za Biblia
-
-
HADITHI YA 34
Aina Mpya ya Chakula 34
UNAJUA watu wanaokota nini chini? Ni cheupe, na chembamba na chenye kupasuka vipande vyembamba. Ni chakula.
Umekuwa karibu mwezi mmoja tu tangu Waisraeli waondoke Misri. Wamo jangwani. Humo chakula kidogo kinamea, watu wanalia, wakisema: ‘Afadhali Yehova angetuua huko Misri. Tulikula huko kila chakula tulichotaka.’
Basi Yehova asema: ‘Nitatelemsha chakula kutoka angani.’ Ndivyo Yehova anafanya. Kesho yake Waisraeli wanapoona chakula hicho cheupe kilichoanguka, wanaulizana hivi: ‘Ni nini hiki?’
Musa anajibu: ‘Ndicho chakula ambacho Yehova amewapa mle.’ Watu wanakiita MANA. Utamu wake ni kama keki (mkate) nyembamba zenye asali.
‘Kila mtu aokote anachoweza kula,’ Musa anawaambia watu. Basi kila asubuhi wanaokota hivyo. Jua linapokuwa kali, ile mana iliyoachwa chini inayeyuka.
Pia Musa anasema: ‘Mtu asiweke mana ikae mpaka kesho.’ Lakini watu wengine hawasikii. Unajua inavyokuwa? Kesho yake ile mana waliyoweka inajaa wadudu, inaanza kunuka vibaya!
Walakini kuna siku moja katika juma ambayo Yehova anawaambia watu wakusanye mana nyingi mara mbili. Siku hiyo ni ya sita. Yehova anawaambia waweke akiba ya kesho, kwa sababu hataangusha mana yoyote siku ya saba. Wanapoweka akiba ya siku ya saba, haijai wadudu wala kunuka! Huo ni mwujiza mwingine.
Miaka yote ambayo Waisraeli walikuwa jangwani Yehova aliwalisha mana.
-
-
Yehova Anatoa Sheria Zake 35Kitabu Changu cha Hadithi za Biblia
-
-
HADITHI YA 35
Yehova Anatoa Sheria Zake 35
KARIBU miezi miwili baada ya Waisraeli kuondoka Misri, wanakuja kwenye Mlima Sinai unaoitwa pia Horebu. Ni pale pale ambapo Yehova alisema na Musa katika mti mdogo uliowaka moto. Watu wanapiga kambi hapa na kukaa kidogo.
Watu wanapongojea chini, Musa apanda mlima. Katika mlima, Yehova anamwambia Musa kwamba Yeye anataka Waisraeli wamtii na kuwa watu Wake wa pekee. Musa anaposhuka, anawaambia Waisraeli maneno ya Yehova. Watu hao wanasema kwamba watamtii Yehova, kwa sababu wanataka kuwa watu wake.
Sasa Yehova anafanya mwujiza. Anafanya kilele cha mlima kitoke moshi, na kufanyiza ngurumo yenye sauti kubwa. Pia anawaambia watu hivi: ‘Mimi ni Yehova Mungu wenu niliyewatoa Misri.’ Kisha anawaamuru hivi: ‘Usiabudu miungu mingine isipokuwa mimi.’
Mungu anawapa Waisraeli amri nyingine tisa, au sheria. Watu wanaogopa sana. Wanamwambia Musa hivi: ‘Wewe sema na sisi, kwa sababu Mungu akisema na sisi huenda tukafa.’
Baadaye Yehova anamwambia Musa hivi: ‘Njoo kwangu mlimani. Nitakupa mabamba mawili ya mawe ambapo nimeandika sheria ninazotaka watu washike.’ Tena Musa anapanda mlimani. Anakaa huko muda wa siku 40 mchana na usiku.
Mungu ana sheria nyingi nyingi za kuwapa watu. Musa anaziandika sheria hizo. Pia Mungu anampa Musa mabamba mawili ya mawe. Juu ya hayo, Mungu mwenyewe ameandika sheria 10 alizowaambia watu wote. Zinaitwa Amri Kumi.
Amri Kumi ni sheria za maana. Hata sheria nyingine nyingi ambazo Mungu anawapa Waisraeli ni za maana. Moja ya hizo sheria ni hii: ‘Inakupasa umpende Yehova Mungu wako kwa moyo wako wote, kwa akili zako zote, kwa nafsi yako yote na nguvu zako zote.’ Nyingine ni hii: ‘Inakupasa umpende jirani yako kama unavyojipenda.’ Yesu Kristo, Mwana wa Mungu, alisema kwamba hizo ndizo sheria mbili zilizo kubwa kuliko zote ambazo Yehova aliwapa watu wake Waisraeli. Baadaye tutajifunza mambo mengi juu ya Mwana wa Mungu na mafundisho yake.
-
-
Ndama ya Dhahabu 36Kitabu Changu cha Hadithi za Biblia
-
-
HADITHI YA 36
Ndama ya Dhahabu 36
MAMA WEE! Sasa watu wanafanya nini? Wanaabudu ndama! Kwa nini wanafanya hivyo?
Musa anapokawia mlimani, watu wasema hivi: ‘Hatujui yaliyompata Musa. Basi na tufanye mungu atutoe katika nchi hii.’
‘Vema,’ Haruni ndugu yake Musa asema. ‘Vueni pete zenu za dhahabu masikioni mniletee.’ Haruni anaziyeyusha na kufanya ndama ya dhahabu. Kisha watu wasema hivi: ‘Huyu ni Mungu wetu, aliyetutoa katika Misri!’ Halafu Waisraeli wanafanya karamu kubwa, na kuiabudu ndama hiyo ya dhahabu.
Yehova anapoona hayo, anakasirika sana. Anamwambia Musa hivi: ‘Fanya haraka ushuke. Watu wanafanya vibaya sana. Wamesahau sheria zangu nao wanaabudu ndama ya dhahabu.’
Musa anashuka haraka mlimani. Anapokaribia, anaona hivi. Watu wanaimba na kucheza wakizunguka ndama ya dhahabu! Musa anakasirika sana hata anayatupa chini mabamba mawili ya mawe yenye kuandikwa sheria, nayo yanavunjika-vunjika. Kisha anachukua ndama ya dhahabu na kuiyeyusha kabisa. Halafu anaisaga kuwa unga.
Watu wamefanya jambo baya sana. Musa anawaambia wanaume kati yao wachukue panga zao. ‘Wale watu wabaya walioiabudu ndama ya dhahabu lazima wafe,’ Musa anasema. Basi wanaume hao wanawaua watu 3,000! Inatupasa tumwabudu Yehova pekee kuliko miungu ya uongo, sivyo?
-
-
Hema ya IbadaKitabu Changu cha Hadithi za Biblia
-
-
HADITHI YA 37
Hema ya Ibada
UNAJUA jengo hili? Ni hema ya pekee ya kuabudia Yehova. Watu walimaliza kuijenga mwaka mmoja baada ya kuondoka Misri. Unajua aliyetoa wazo la kuijenga?
Ni Yehova. Musa alipokuwa katika Mlima Sinai, Yehova alimwambia namna ya kuijenga. Alimwambia ijengwe ili iwe vyepesi kubomolewa. Kwa njia hiyo sehemu zake zingeweza kuchukuliwa mahali pengine, na kuunganishwa tena. Basi Waisraeli walipokuwa wakihama hapa na pale jangwani, walichukua hema hiyo.
Ukitazama ndani ya chumba kidogo mwishoni mwa hema, unaweza kuona sanduku, au kasha. Hilo laitwa sanduku la agano. Kila upande ulikuwa na malaika au kerubi mmoja wa dhahabu. Tena Mungu aliziandika Amri Kumi juu ya mabamba mawili ya mawe, kwa sababu Musa alikuwa ameyavunja yale ya kwanza. Na mawe hayo yalitunzwa ndani ya sanduku la agano. Pia, mtungi wa mana ulitunzwa ndani yake. Unakumbuka mana ni nini?
Yehova anachagua Haruni ndugu yake Musa awe kuhani mkuu. Anawaongoza watu wamwabudu Yehova. Na wanawe ni makuhani pia.
Sasa kitazame chumba kikubwa zaidi cha hema hiyo. Ni kikubwa mara mbili kuliko kile chumba kidogo. Unaliona lile sanduku au kasha dogo, na moshi kidogo ukipanda kutoka ndani yake? Ndiyo madhabahu ambapo makuhani wanachoma uvumba. Halafu kuna kinara cha taa chenye taa saba. Na kitu cha tatu chumbani ni meza. Mikate 12 inatunzwa juu yake.
Uani mwa hema mna bakuli kubwa, au birika, iliyojaa maji. Makuhani wanaitumia kwa kuogea. Pia kuna madhabahu kubwa. Hapo ndipo wanyama wafu wanapochomwa wawe toleo kwa Yehova. Hema iko katikati ya kambi, na Waisraeli wanakaa katika hema zao kuizunguka.
-
-
Wapelelezi 12Kitabu Changu cha Hadithi za Biblia
-
-
HADITHI YA 38
Wapelelezi 12
TAZAMA matunda ambayo wanaume hawa wanabeba. Tazama kichala kile cha zabibu kilivyo kikubwa. Kinataka wanaume wawili wakibebe kwa mti. Zitazame tini na yale makomamanga. Matunda hayo mazuri yalitoka wapi? Nchi ya Kanaani. Kumbuka, wakati mmoja Ibrahimu, Isaka na Yakobo walikaa Kanaani. Lakini kwa sababu kulikuwako njaa kuu, Yakobo na jamaa yake, walihama wakaenda Misri. Sasa, miaka kama 216 baadaye, Musa anawarudisha Waisraeli Kanaani. Wamefika mahali panapoitwa Kadeshi huko jangwani.
Watu wabaya wanakaa Kanaani. Basi Musa anawatuma wapelelezi 12, akiwaambia: ‘Nendeni mkaone ni watu wangapi wanaokaa huko, na wana nguvu gani. Mjue kama udongo unafaa mimea. Mhakikishe kurudisha matunda fulani.’
Wapelelezi hao wanaporudi Kadeshi, wanamwambia Musa hivi: ‘Ni nchi nzuri kweli kweli.’ Na kama ushuhuda wa hayo, wanamwonyesha Musa matunda fulani. Lakini wapelelezi 10 wanasema hivi: ‘Watu wanaokaa huko ni wakubwa na wenye nguvu sana. Tutauawa tukijaribu kuichukua nchi hiyo.’
Waisraeli wanaogopa kwa kusikia hayo. ‘Afadhali tungefia Misri au hata humu jangwani,’ wanasema. ‘Tutauawa vitani, wake zetu na watoto watatekwa nyara. Na tuchague kiongozi mpya mahali pa Musa, turudi Misri!’
Lakini wapelelezi wawili wanamtumaini Yehova, wanajaribu kuwatuliza watu. Ni Yoshua na Kalebu. Wanasema: ‘Msiogope. Yehova yuko pamoja na sisi. Itakuwa rahisi kuichukua nchi hiyo.’ Lakini watu hawasikii. Hata wanataka kuwaua Yoshua na Kalebu. Hilo lamkasirisha Yehova sana, anamwambia Musa hivi: ‘Hakuna yeyote kati ya watu hao kuanzia wale wenye miaka 20 na zaidi watakaoingia Kanaani. Wamekwisha kuiona miujiza niliyofanya huko Misri na jangwani, lakini bado hawanitumaini. Basi watatanga-tanga jangwani muda wa miaka 40 mpaka mtu wa mwisho afe. Yoshua (Yosua) na Kalebu peke yao wataingia Kanaani.’
-
-
Fimbo ya Haruni Inamea MauaKitabu Changu cha Hadithi za Biblia
-
-
HADITHI YA 39
Fimbo ya Haruni Inamea Maua
YATAZAME maua na lozi hizo zilizoiva zikimea katika fimbo hiyo. Hiyo ni fimbo ya Haruni. Maua na matunda hayo yalimea katika fimbo ya Haruni usiku mmoja tu! Ebu tuone sababu yake.
Waisraeli wamekuwa wakitanga-tanga jangwani kwa muda fulani sasa. Wengine kati ya watu hawataki Musa awe kiongozi, wala Haruni kuwa kuhani mkuu. Kora anafikiri hivyo, pia Dathani, Abiramu na viongozi wa watu 250. Wote hao wanakuja kumwambia Musa hivi: ‘Kwa nini wewe unajiweka juu ya wengine wetu?’
Musa anamwambia Kora na wafuasi wake hivi: ‘Kesho asubuhi mchukue makoleo ya moto mweke uvumba ndani yake. Ndipo mje kwenye hema ya Yehova. Tutaona ni nani ambaye Yehova atachagua.’
Kesho yake Kora na wafuasi wake 250 wanafika kwenye hema. Wengine wengi wanafuata ili wawaunge mkono wanaume hao. Yehova anakasirika sana. ‘Ondokeni kwenye hema za watu hao wabaya,’ Musa anasema. ‘Msishike mali yao.’ Watu wanasikiliza, na kuondoka kwenye hema za Kora, Dathani na Abiramu.
Kisha Musa anasema hivi: ‘Kwa hili mtajua ni nani ambaye Yehova amechagua. Ardhi itafunguka na kuwameza watu hawa wabaya.’
Mara Musa anapomaliza kusema, ardhi inafunguka. Hema ya Kora na mali yake na Dathani na Abiramu na wale walio pamoja nao wanazama, nayo ardhi inawafunika. Watu wanaposikia kilio cha hao wanaotumbukia katika ardhi, wanapiga kelele hivi: ‘Kimbieni! Ardhi isitumeze sisi pia!’
Kora na wafuasi wake 250 bado wako karibu na hema. Basi Yehova anapeleka moto, na wote wanateketezwa. Kisha Yehova anamwambia Eleazari mwana wa Haruni achukue makoleo ya moto ya watu hao waliokufa ayafanye yawe kifuniko chembamba cha madhabahu.
Yehova anataka wafahamu sana kwamba Haruni na wanawe ndio amechagua wawe makuhani. Basi anamwambia Musa hivi: ‘Mwambie kiongozi wa kila kabila la Israeli alete fimbo yake. Kisha weka kila moja ya fimbo hizo katika hema mbele ya sanduku la agano. Ile fimbo ya mtu niliyemchagua awe kuhani itamea maua.’
Musa anapotazama kesho yake, lo! fimbo ya Haruni imemea maua hayo na lozi zilizoiva! Basi unaona sasa kwa nini Yehova alifanya fimbo ya Haruni imee maua?
-
-
Musa Anaupiga MwambaKitabu Changu cha Hadithi za Biblia
-
-
HADITHI YA 40
Musa Anaupiga Mwamba
MWAKA baada ya mwaka unapita—miaka 10, miaka 20, miaka 30, miaka 39! Waisraeli wangali jangwani. Lakini miaka hiyo yote Yehova anawaangalia watu wake. Anawalisha mana. Anawaongoza mchana kwa nguzo ya wingu, na usiku kwa nguzo ya moto. Na wakati wa miaka yote hiyo mavazi yao hayamaliziki na miguu haipati vidonda.
Sasa ndio mwezi wa kwanza wa mwaka wa 40 tangu waondoke Misri. Tena Waisraeli wanapiga kambi katika Kadeshi. Hapo ndipo walipokuwa wakati wapelelezi 12 walipotumwa kwenda kwenye nchi ya Kanaani karibu miaka 40 iliyopita. Miriamu dada yake Musa anakufa katika Kadeshi. Na kama zamani, matata yanatokea hapa.
Watu hawawezi kupata maji. Hivyo wanamlilia Musa hivi: ‘Afadhali tungekufa. Kwa nini ukatutoa Misri kuja mahali hapa pabaya pasipomea kitu? Hakuna nafaka, hakuna tini, hakuna zabibu, hakuna komamanga. Wala hakuna maji ya kunywa.’
Musa na Haruni wanapokwenda kwenye hema wakasali, Yehova anamwambia Musa hivi: ‘Wakusanye watu. Kisha mbele yao wote useme na mwamba ule. Maji mengi yatatoka watu na wanyama wao wote wanywe.’ Basi Musa anakusanya watu, na kusema: ‘Sikilizeni, ninyi msiomtumaini Mungu! Je! Haruni na mimi tuwatolee maji katika mwamba huu?’ Kisha Musa anaupiga mwamba huo mara mbili kwa fimbo, maji mengi yatiririka katika mwamba huo. Kuna maji mengi ya kunywa watu wote na wanyama.
Lakini Yehova anawakasirikia Musa na Haruni. Unajua kwa nini? Kwa sababu Musa na Haruni walisema kwamba wao watatoa maji katika mwamba. Lakini Yehova ndiye aliyetoa. Na kwa vile Musa na Haruni hawakusema kweli hiyo, Yehova anasema kwamba atawaadhibu. ‘Hamtawaingiza watu wangu Kanaani,’ anasema.
Upesi Waisraeli wanaondoka Kadeshi. Baada ya kitambo kidogo wanafika kwenye Mlima Hori. Huko ndiko Haruni alikufa juu ya kilele cha mlima. Anakufa akiwa mwenye miaka 123. Waisraeli wanahuzunika sana, na watu wote wanamlilia Haruni muda wa siku 30. E·le·aʹzari mwanawe anakuwa kuhani mkuu wa pili wa taifa la Israeli.
-
-
Nyoka wa ShabaKitabu Changu cha Hadithi za Biblia
-
-
HADITHI YA 41
Nyoka wa Shaba
JE! HUYO anaonekana kama nyoka wa kweli aliyezungushwa juu ya mti? Hapana. Nyoka huyo amefanyizwa kwa shaba. Yehova alimwambia Musa amweke juu ya mti ili watu wamtazame waishi. Lakini nyoka wengine chini ni wa kweli. Wamewauma watu na kuwafanya wagonjwa. Unajua kwa nini?
Ni kwa sababu Waisraeli wamempinga Mungu na Musa. Wanalaumu hivi: ‘Kwa nini ulitutoa Misri ili tufe huku jangwani? Hakuna chakula wala maji huku. Tumechoka kula mana hii.’
Lakini mana hiyo ni chakula kizuri. Yehova amewapa mana hiyo kwa mwujiza. Na kwa mwujiza amewapa maji pia lakini watu hawamshukuru Mungu kwa vile alivyowaangalia. Basi Yehova anawapeleka nyoka hao wenye sumu ili awaadhibu Waisraeli. Nyoka hao wanawauma, na wengi wao wanakufa.
Mwishowe watu wanamwendea Musa na kusema: ‘Tumefanya dhambi, kwa sababu tumepinga Yehova na wewe. Basi mwombe Yehova awaondoe nyoka hawa.’
Musa anaombea watu. Naye Yehova anamwambia Musa afanyize nyoka huyu wa shaba. Anamwambia amweke juu ya mti, ili mtu anayeumwa amtazame. Musa anafanya kama anavyoambiwa na Mungu. Watu walioumwa wanamtazama nyoka wa shaba wanapona.
Kuna jambo la kujifunza kutokana na hayo. Sote tuko kama Waisraeli hao walioumwa na nyoka hao. Sote tuko katika hali ya kufa. Ebu tazama huku na huku, utaona kwamba watu wanazeeka, wanakuwa wagonjwa, na kufa. Ni kwa sababu yule mwanamume na mwanamke wa kwanza, Adamu na Hawa walijitenga na Yehova, na sote ni watoto wao. Lakini Yehova amefanya njia ili tuweze kuishi milele.
Yehova alimtuma Mwanawe, Yesu Kristo, duniani. Yesu aliwekwa juu ya mti, kwa sababu watu wengi walidhani alikuwa mbaya. Lakini Yehova alimtoa Yesu atuokoe. Tukimtazama, tukimfuata, ndipo twaweza kuwa na uzima wa milele. Lakini tutajifunza zaidi juu ya hilo baadaye.
-
-
Punda AnasemaKitabu Changu cha Hadithi za Biblia
-
-
HADITHI YA 42
Punda Anasema
JE! UMEPATA kusikia kwamba punda anasema? ‘Hapana,’ labda unasema. ‘Wanyama hawawezi kusema.’ Lakini Biblia inasimulia hivyo. Na tuone ilivyokuwa.
Waisraeli wako karibu sana kuingia nchi ya Kanaani. Balaki, mfalme wa Moabu, anawaogopa Waisraeli. Basi anapeleka habari ili mtu mwerevu jina lake Balaamu awalaani Waisraeli. Balaki anaahidi kumpa Balaamu fedha nyingi sana, basi Balaamu anapanda punda wake kwenda kumwona Balaki.
Yehova hataki Balaamu alaani watu wake. Basi anamtuma malaika mwenye upanga mrefu akasimame njiani amzuie Balaamu. Balaamu hawezi kumwona malaika, lakini punda anamwona. Basi punda huyo anaepa-epa huyo malaika, na mwishowe analala njiani. Balaamu anakasirika sana, na kumpiga punda wake kwa fimbo.
Ndipo Yehova anamfanya Balaamu asikie punda wake akisema naye. ‘Nimekukosea nini hata unipige?’ punda anauliza.
‘Umenifanya mpumbavu,’ Balaamu anasema. ‘Kama ningekuwa na upanga ningekuua!’
‘Je! nimekufanyia hivyo zamani?’ punda anauliza.
‘Hapana,’ Balaamu anajibu.
Ndipo Yehova anamwonyesha Balaamu malaika aliye na upanga anasimama njiani. Malaika anasema hivi: ‘Kwa nini umempiga punda wako? Nimekuja nikuzuie njia usiende kulaani Waisraeli. Kama punda wako hangeniepa, ningekupiga ufe.’
Balaamu anasema: ‘Nimefanya dhambi. Sikujua kama ulikuwa ukisimama njiani.’ Malaika huyo anamruhusu Balaamu aende, naye Balaamu anaendelea na safari ya kumwona Balaki. Bado anajaribu kulaani Waisraeli, lakini, badala yake, Yehova anamwongoza abariki Waisraeli mara tatu.
-
-
Yoshua Anakuwa KiongoziKitabu Changu cha Hadithi za Biblia
-
-
HADITHI YA 43
Yoshua Anakuwa Kiongozi
MUSA anataka kuingia Kanaani pamoja na Waisraeli. Hivyo anauliza hivi: ‘Yehova, uniruhusu nivuke Mto Yordani, niione nchi nzuri.’ Lakini Yehova anasema: ‘Basi! usiseme tena hivyo?’ Unajua kwa nini Yehova alisema hivyo?
Ni kwa sababu ya jambo lililotokea wakati Musa alipoupiga mwamba. Kumbuka, yeye na Haruni hawakumheshimu Yehova. Hawakuwaambia watu kwamba ni Yehova aliyekuwa akiwaletea maji katika mwamba ule. Kwa sababu hiyo Yehova alisema hangewaruhusu waingie Kanaani.
Basi miezi michache baada ya Haruni kufa Yehova anamwambia Musa hivi: ‘Mchukue Yoshua umsimamishe mbele ya E·le·aʹzari kuhani na watu. Na mbele ya wote mwambie kila mtu kwamba Yoshua ndiye kiongozi mpya.’ Musa anafanya kama Yehova anavyosema, kama unavyoona katika picha.
Kisha Yehova anamwambia Yoshua hivi: ‘Uwe hodari, usiogope. Utawaingiza Waisraeli katika nchi ya Kanaani niliyowaahidi, mimi nitakuwa na wewe.’
Baadaye Yehova anamwambia Musa apande juu ya Mlima Nebo katika nchi ya Moabu. Musa anatazama ng’ambo ya Mto Yordani na kuiona nchi nzuri ya Kanaani. Yehova anasema hivi: ‘Hii ndiyo nchi niliyoahidi kuwapa wana wa Ibrahimu, Isaka na Yakobo. Nimekuruhusu uione, lakini sitakubali uingie ndani yake.’
Huko juu ya Mlima Nebo Musa anakufa. Alikuwa mwenye miaka 120. Alikuwa bado ana nguvu, macho yake yalikuwa bado yakiona vizuri. Watu wanahuzunika sana na kulia kwa sababu Musa amekufa. Lakini wanafurahi kuwa na Yoshua kiongozi wao mpya.
-
-
Rahabu Anaficha WapeleleziKitabu Changu cha Hadithi za Biblia
-
-
HADITHI YA 44
Rahabu Anaficha Wapelelezi
WANAUME hao wana taabu. Lazima waondoke, ama watauawa. Ni wapelelezi Waisraeli, na anayewasaidia ni Rahabu. Rahabu anakaa katika nyumba hiyo juu ya ukuta wa mji wa Yeriko. Ebu tuone sababu gani wanaume hao wana taabu.
Waisraeli wako tayari kuvuka Mto Yordani waingie Kanaani. Lakini kwanza, Yoshua anatuma wapelelezi wawili. Anawaambia hivi: ‘Nendeni mkaitazame nchi na mji wa Yeriko.’
Wapelelezi hao wanapoingia Yeriko, wanakwenda nyumbani kwa Rahabu. Lakini mtu fulani anamwambia mfalme hivi: ‘Waisraeli wawili waliingia mjini usiku huu ili wapeleleze nchi.’ Anaposikia hivyo, mfalme anatuma watu kwa Rahabu, wakimwambia hivi: ‘Watoe wale wanaume walioingia nyumbani mwako!’ Lakini Rahabu ameficha wapelelezi hao juu ya dari lake. Anasema: ‘Wanaume fulani walikuja kwangu, lakini sijui walikotoka. Waliondoka kulipoanza kuwa usiku, kabla ya kufungwa lango. Mkifanya haraka, mtawakuta!’ Watu hao wanaanza kuwafuata.
Wakiisha kuondoka, Rahabu anapanda haraka juu ya dari. ‘Najua Yehova atawapa ninyi nchi hii,’ anawaambia wapelelezi hao. ‘Tulisikia alivyoikausha Bahari Nyekundu mlipoondoka Misri, na alivyowaua wafalme Sihoni na Ogu. Nimewahurumia ninyi, basi tafadhali mnipe ahadi, ya kwamba mtanihurumia mimi. Mwokoe baba na mama yangu, ndugu na dada zangu.’
Wapelelezi hao wanaahidi kufanya hivyo, lakini inampasa Rahabu atende jambo fulani. ‘Chukua kamba hii nyekundu uifunge katika dirisha,’ wapelelezi wanamwambia, ‘kisha ukusanye watu wako wote wa ukoo ndani ya nyumba yako pamoja nawe. Tutakaporudi sote kuutwaa Yeriko, tutaiona kamba hii katika dirisha lako tusimwue yeyote nyumbani mwako.’ Wapelelezi hao wanaporudi kwa Yoshua, wanamwambia kila jambo lililotokea.
-