Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Tazameni Mtekelezaji wa Mambo ya Ajabu!
    Mnara wa Mlinzi—2001 | Aprili 15
    • Tazameni Mtekelezaji wa Mambo ya Ajabu!

      “Simama kimya, uzifikiri [“uzizingatie,” “NW”] kazi za Mungu za ajabu.”—AYUBU 37:14.

      1, 2. Ni uvumbuzi gani wa ajabu uliofanywa mwaka wa 1922, nao ulionwaje?

      MWAKIOLOJIA mmoja na mheshimiwa mmoja Mwingereza walikuwa wameshirikiana kwa miaka mingi kutafuta hazina. Hatimaye, Novemba 26, 1922, katika makaburi ya mafarao wa Misri kwenye Bonde maarufu la Wafalme, mwakiolojia Howard Carter na Mheshimiwa Carnarvon walipata hazina hiyo—kaburi la Farao Tutankhamen. Walitoboa shimo kwenye mlango uliokuwa umezibwa kabisa kisha Carter akaingiza mshumaa na kuchungulia ndani.

      2 Baadaye Carter alisema: “Wakati Mheshimiwa Carnarvon, aliyekuwa na hamu kubwa sana ya kujua yaliyokuwemo ndani, aliponiuliza, ‘Unaona nini humo ndani?’ ningeweza kujibu tu, ‘Naona vitu vya ajabu.’” Ndani ya kaburi hilo kulikuwemo jeneza la dhahabu tupu miongoni mwa vitu vingi vyenye thamani. Labda umeona baadhi ya ‘vitu hivyo vya ajabu’ kwenye picha au kwenye maonyesho katika jumba la makumbusho. Lakini hata vitu hivyo viwe vya ajabu namna gani, yaelekea havina thamani yoyote kwako. Kwa hiyo acheni tuzingatie mambo ya ajabu ambayo bila shaka yanakuhusu na ni yenye thamani kwako.

      3. Tutapata wapi habari kuhusu mambo ya ajabu ambayo yanaweza kutunufaisha?

      3 Kwa mfano, hebu mfikirie mwanamume aliyeishi karne nyingi zilizopita, mtu mashuhuri kuliko mcheza-sinema, mwanamichezo, mwanasiasa, au mtu yeyote kutoka katika familia ya kifalme. Alisemwa kuwa mkuu sana kuliko watu wote wa upande wa Mashariki. Jina lake ni Ayubu. Kitabu kizima cha Biblia kiliandikwa kumhusu. Hata hivyo, mmoja wa watu walioishi wakati wake, kijana aitwaye Elihu, aliona ni lazima kumsahihisha. Elihu alisema kwamba Ayubu alikuwa akijifikiria mwenyewe na wengine kupita kiasi. Katika Ayubu sura ya 37, twaona ushauri mwingine hususa na wenye hekima, ambao unaweza kutunufaisha sana.—Ayubu 1:1-3; 32:1–33:12.

      4. Nini kilichomfanya Elihu atoe himizo lililo kwenye Ayubu 37:14?

      4 Watu watatu waliodai kuwa marafiki wa Ayubu walizungumzia kirefu makosa ambayo walidhani Ayubu alikuwa amefanya kwa kuwaza ama kutenda. (Ayubu 15:1-6, 16; 22:5-10) Elihu alisubiri hadi mazungumzo hayo yakaisha. Kisha akaongea kwa hekima na ufahamu wenye kina. Alizungumzia mambo mengi yenye manufaa kubwa, lakini ona wazo hili muhimu: “Sikiliza neno hili, Ee Ayubu; simama kimya, uzifikiri [“uzizingatie,” NW] kazi za Mungu za ajabu.”—Ayubu 37:14.

      Aliyezitekeleza Kazi Hizo

      5. “Kazi za Mungu za ajabu” ambazo Elihu alirejezea zatia ndani nini?

      5 Ona kwamba Elihu hakuwa anadokeza kwamba Ayubu ajizingatie mwenyewe, wala amzingatie yeye Elihu, wala azingatie wanadamu wengine. Kwa hekima Elihu alimhimiza Ayubu—hata sisi pia—azingatie kazi za Yehova Mungu za ajabu. Je, unafikiri usemi “kazi za Mungu za ajabu” watia ndani nini? Isitoshe, kwa nini uzingatie kazi za Mungu ilhali huenda ukawa na mahangaiko kuhusu afya, hali ya kifedha, wakati ujao, familia yako, wafanyakazi wenzako, na majirani? Bila shaka, kazi za ajabu za Yehova Mungu zatia ndani hekima yake na mamlaka yake juu ya uumbaji wote unaotuzunguka. (Nehemia 9:6; Zaburi 24:1; 104:24; 136:5, 6) Ili kuelewa vizuri zaidi jambo hilo, ona yanayosemwa katika kitabu cha Yoshua.

      6, 7. (a) Yehova alitekeleza kazi gani za ajabu siku za Musa na Yoshua? (b) Kama ungalishuhudia mojawapo ya kazi hizo wakati wa Musa au wa Yoshua, ungaliitikiaje?

      6 Yehova alileta mapigo dhidi ya Misri ya kale kisha akatenganisha maji ya Bahari Nyekundu ili Musa awakomboe Waisraeli wa kale. (Kutoka 7:1–14:31; Zaburi 106:7, 21, 22) Yoshua sura ya 3 inasimulia tukio linalofanana na hilo. Yoshua, mwandamizi wa Musa, alipaswa kuwaongoza watu wa Mungu wavuke mto fulani na kuingia katika Bara Lililoahidiwa. Yoshua alisema: “Jitakaseni; maana kesho BWANA atatenda mambo ya ajabu kati yenu.” (Yoshua 3:5) Mambo gani ya ajabu?

      7 Simulizi hilo laonyesha kwamba Yehova alifungua njia katikati ya Mto Yordani ili mamia ya maelfu ya wanaume, wanawake, na watoto wavuke wakitembea pakavu. (Yoshua 3:7-17) Kama tungalikuwa huko na kutazama maji ya mto yakitengana na watu wote hao wakivuka salama, tungaliona utimizo huo kuwa wa ajabu kama nini! Lilionyesha nguvu za Mungu juu ya uumbaji. Hata hivyo, leo hii—nyakati zetu—kuna mambo ya ajabu pia. Ili kuona baadhi ya mambo hayo na kuona ni kwa nini mimi na wewe twapaswa kuyazingatia, ona andiko la Ayubu 37:5-7.

      8, 9. Andiko la Ayubu 37:5-7 lazungumzia kazi gani za ajabu na kwa nini tuzifikirie?

      8 Elihu alitangaza: “Mungu hunguruma kwa kustaajabisha kwa sauti yake; hufanya mambo makuu, ambayo hatuwezi kuelewa nayo.” Elihu alimaanisha nini aliposema Mungu hufanya mambo “kwa kustaajabisha”? Elihu alikuwa anazungumza juu ya theluji na mvua. Vitu hivyo vingemzuia mkulima asifanye kazi shambani mwake na kumpa wakati na sababu ya kuzizingatia kazi za Mungu. Huenda tusiwe wakulima, lakini sote tunaweza kuathiriwa na mvua na theluji. Ikitegemea tunakoishi duniani, theluji na mvua zaweza kuvuruga shughuli zetu pia. Je, sisi huchukua wakati kutafakari ni nani asababishaye maajabu hayo nayo yanamaanisha nini? Je, umewahi kutafakari juu ya mambo hayo?

      9 Kama tusomavyo katika kitabu cha Ayubu sura ya 38, ni jambo lenye kutokeza kwamba Yehova Mungu mwenyewe ana maoni kama hayo kuhusu kutafakari anapomwuliza Ayubu maswali muhimu. Ingawa Muumba wetu alimwuliza Ayubu maswali hayo, ni wazi kwamba yanatuhusu—yanahusu mtazamo wetu, kuwapo kwetu, na wakati wetu ujao. Kwa hiyo, hebu tuchunguze maswali ambayo Mungu aliuliza na kufikiria maana yake, naam, na tufanye yale ambayo andiko la Ayubu 37:14 latuhimiza tufanye.

      10. Ayubu sura ya 38 yapasa kuwa na matokeo gani kwetu, nayo yazusha maswali gani?

      10 Sura ya 38 yaanza hivi: “BWANA akamjibu Ayubu katika upepo wa kisulisuli, na kusema, Ni nani huyu atiaye mashauri giza kwa maneno yasiyo na maarifa? Basi jifunge viuno kama mwanamume, maana nitakuuliza neno, nawe niambie.” (Ayubu 38:1-3) Utangulizi huo ulimsaidia Ayubu arekebishe maoni yake na kutambua kwamba anasimama mbele za Muumba wa ulimwengu wote, na anawajibika mbele zake. Yafaa sisi na wengine wanaoishi wakati huu tufanye hivyo pia. Kisha, Mungu azungumzia mambo yaleyale ambayo Elihu alikuwa amezungumzia. “Ulikuwa wapi nilipoiweka misingi ya nchi? Haya! sema, kama ukiwa na ufahamu. Ni nani aliyeamrisha vipimo vyake, kama ukijua? Au ni nani aliyenyosha kamba juu yake? Misingi yake ilikazwa juu ya kitu gani? Au ni nani aliyeliweka jiwe lake la pembeni?”—Ayubu 38:4-6.

      11. Twapaswa kung’amua nini kutokana na andiko la Ayubu 38:4-6?

      11 Ayubu alikuwa wapi, sisi tulikuwa wapi dunia ilipoumbwa? Je, yeyote kati yetu alichora ramani za ujenzi za dunia yetu, na kutumia ramani hiyo kupima vipimo mbalimbali kana kwamba kwa rula? Bila shaka la. Wanadamu hata hawakuwepo wakati huo. Akiifananisha dunia yetu na jengo, Mungu aliuliza hivi: “Ni nani aliyeliweka jiwe lake la pembeni?” Tunajua kwamba dunia imewekwa umbali hususa kutoka kwa jua, umbali unaotuwezesha kuishi na kufurahia maisha. Nayo dunia ina ukubwa ufaao. Kama dunia yetu ingalikuwa kubwa zaidi ya vile ilivyo sasa, gesi ya hidrojeni haingeweza kutoka katika angahewa letu nayo dunia haingekalika. Ni wazi kwamba mtu fulani ‘aliliweka jiwe lake la pembeni’ mahali pafaapo. Je, Ayubu alistahili sifa kwa jambo hilo? Je, sisi twastahili sifa? Au Yehova Mungu ndiye anayestahili sifa?—Mithali 3:19; Yeremia 10:12.

      Ni Mwanadamu Gani Awezaye Kutoa Majibu?

      12. Swali linalopatikana kwenye Ayubu 38:6 lafanya tufikirie nini?

      12 Mungu aliuliza hivi pia: “Misingi yake ilikazwa juu ya kitu gani?” Je, hilo si swali zuri? Huenda twajua nguvu za uvutano, jambo ambalo Ayubu hakujua. Wengi wetu twafahamu kwamba nguvu za uvutano za jua huwezesha dunia idumu mahali ilipo, kana kwamba misingi yake imekazwa. Hata hivyo, je, kuna yeyote kati yetu awezaye kuzielewa kikamili nguvu za uvutano?

      13, 14. (a) Ni lazima tukiri nini kuhusu nguvu za uvutano? (b) Tuoneje hali inayokaziwa na andiko la Ayubu 38:6?

      13 Kitabu kilichochapishwa hivi majuzi, The Universe Explained, chakiri kwamba ‘watu wengi wanazijua nguvu za uvutano, lakini hawazielewi vizuri kama wanavyoelewa nguvu nyinginezo za asili.’ Kitabu hicho chaendelea kusema: “Yaonekana kwamba nguvu za uvutano husafiri kasi angani, bila kufuata njia yoyote mahususi. Hata hivyo, katika miaka ya majuzi, wanafizikia wameanza kukisia kwamba huenda ikawa nguvu za uvutano husafiri kwa mawimbi ya chembe ndogo ziitwazo graviton . . . Lakini hakuna yeyote aliye na uhakika kwamba chembe hizo zipo.” Hebu wazia hilo lamaanisha nini.

      14 Sayansi imepiga hatua kubwa kwa miaka 3,000 tangu Yehova alipomwuliza Ayubu maswali hayo. Hata hivyo, wala sisi wala wataalamu wa fizikia hawawezi kueleza kikamili jinsi nguvu za uvutano zidumishavyo dunia katika mzunguko wake, mahali hasa ipaswapo kuwa ili kutuwezesha kufurahia maisha. (Ayubu 26:7; Isaya 45:18) Kusema hivyo hakudokezi kwamba sote tunahitaji kuanza uchunguzi wenye kina juu ya mambo tusiyoelewa kuhusu nguvu za uvutano. Hata hivyo, kuzingatia hata sehemu hii moja tu ya kazi za Mungu za ajabu kwapasa kuathiri maoni yetu kumhusu. Je, unastaajabia hekima yake na ujuzi wake, na je, unaelewa ni kwa nini twahitaji kujifunza mengi zaidi juu ya mapenzi yake?

      15-17. (a) Andiko la Ayubu 38:8-11 lakazia nini na linazusha maswali gani? (b) Twapaswa kukiri nini juu ya yale tunayojua kuhusu bahari na mahali zilipo duniani?

      15 Muumba aliendelea kuuliza hivi: “Ni nani aliyeifunga bahari kwa milango, hapo ilipofurika kana kwamba imetoka tumboni. Nilipolifanya wingu kuwa vazi lake, na giza zito kuwa nguo ya kuifungia, nikaiagiza amri yangu; nikaiwekea makomeo na milango, nikasema, Utafika mpaka hapa, lakini hutapita, na hapa mawimbi yako yanyetayo yatazuiliwa?”—Ayubu 38:8-11.

      16 Kufungwa kwa bahari kwahusisha mabara, bahari, na mawimbi. Mwanadamu amechunguza na kuchanganua vitu hivyo kwa muda mrefu kadiri gani? Amefanya hivyo kwa maelfu ya miaka na kwa makini zaidi hasa katika karne iliyopita. Unaweza kuwazia kwamba kufikia sasa lazima mwanadamu awe anajua mambo mengi ambayo anapaswa kujua kuhusu vitu hivyo. Lakini, katika mwaka huu wa 2001, ungepata habari gani za karibuni zaidi kama ungechunguza juu ya vitu hivyo kwenye maktaba kubwa au kwenye Internet yenye uwezo mkubwa wa kufanya utafiti?

      17 Kichapo kimoja maarufu cha marejezo, chakiri hivi: ‘Ni vigumu sana kwa wanasayansi kuchunguza kikamili au kutoa nadharia inayoweza kueleza ni kwa nini mabara, bahari na uumbaji mwingine, upo mahali ulipo.’ Baada ya kusema hayo, ensaiklopidia hiyo ilitoa mambo manne ambayo yawezekana yalisababisha hali hiyo, lakini ikasema kwamba mambo hayo ni “baadhi ya zile nadharia tete nyingi.” Huenda ukafahamu kwamba usemi nadharia tete “wamaanisha uthibitisho usiotosha ambao watoa ufafanuzi uwezao kubadilika.”

      18. Andiko la Ayubu 38:8-11 lafanya tufikie mkataa gani?

      18 Je, mambo hayo hayakazii kwamba maswali tusomayo kwenye Ayubu 38:8-11 yaliulizwa wakati ufaao? Bila shaka, hatuwezi kupokea sifa kwa kuwa sio sisi tulioviweka vitu hivyo mahali vilipo duniani. Hatukuuweka mwezi mahali ulipo ili nguvu zake za uvutano zisaidie kutokeza mawimbi ambayo kwa kawaida hayaharibu mwambao wala kutuathiri sisi binafsi. Tunajua kwamba Mtekelezaji wa mambo ya ajabu ndiye aliyefanya hayo yote.—Zaburi 33:7; 89:9; Mithali 8:29; Matendo 4:24; Ufunuo 14:7.

      Mpe Yehova Sifa Anayostahili

      19. Semi za kishairi kwenye Ayubu 38:12-14 zafanya tuzingatie mambo gani halisi?

      19 Mzunguko wa dunia unaorejezewa kwenye andiko la Ayubu 38:12-14 haukutokezwa na wanadamu. Mzunguko huo wa dunia husababisha mapambazuko ambayo mara nyingi huvutia kwa uzuri. Jua lichomozapo, vitu vilivyomo katika dunia yetu huonekana vizuri zaidi na zaidi kama vile alama kwenye udongo laini. Tunapozingatia kwa kiasi kidogo mwendo wa dunia twastaajabu kuona kwamba haizunguki kwa kasi sana, jambo ambalo kama tujuavyo lingeleta madhara. Wala dunia haizunguki polepole sana hivi kwamba mchana na usiku zawa ndefu sana. Jambo hilo laweza kusababisha joto na baridi zinazopita kiasi na kufanya wanadamu wasiweze kuishi. Kusema kweli, yatupasa kufurahi kwamba Mungu ndiye aliyeanzisha mwendo wa mzunguko huo, wala si wanadamu fulani.—Zaburi 148:1-5.

      20. Ungejibuje maswali yaliyoulizwa kwenye Ayubu 38:16, 18?

      20 Sasa, hebu wazia Mungu akikuuliza maswali zaidi: “Je! umeziingia chemchemi za bahari, au umetembea mahali pa siri pa vilindi?” Hata mtaalamu wa mambo ya bahari hangeweza kutoa jibu kamili! “Umeyafahamu mapana ya dunia? Haya! sema, ikiwa unayajua hayo yote.” (Ayubu 38:16, 18) Je, umezuru na kutembelea sehemu zote za dunia au angalau sehemu nyingi za dunia? Kutembelea sehemu nzuri mbalimbali na kuona maajabu ya dunia yetu kungechukua muda mrefu kadiri gani? Nao ungekuwa wakati mzuri kama nini!

      21. (a) Maswali yaliyoulizwa kwenye Ayubu 38:19 yanaweza kutokeza maoni gani ya kisayansi? (b) Mambo halisi kuhusu nuru yapasa kutuchochea tufanye nini?

      21 Pia, tazama maswali mazito katika Ayubu 38:19: “Iko wapi njia ya kuyafikia makao ya nuru? Na giza pia, mahali pake ni wapi?” Huenda ikawa wajua kwamba kwa muda mrefu, wanasayansi walidhani kwamba nuru husafiri kama wimbi, kama viwimbi tuonavyo kwenye kidimbwi. Kisha katika mwaka wa 1905, Albert Einstein akaeleza kwamba nuru ni kama chembechembe za nishati. Je, ufafanuzi wa Einstein ulitoa jibu? Ensaiklopidia ya karibuni iliuliza hivi: “Je, nuru ni wimbi au ni chembechembe?” Nayo yajibu hivi: “Yaonekana kwamba, [nuru] haiwezi kuwa [wimbi na wakati uleule ikawa chembechembe] kwa sababu vitu hivyo viwili vyatofautiana sana. Jibu lifaalo kabisa ni kwamba nuru si wimbi wala si chembechembe.” Hata hivyo, ingawa mwanadamu hawezi kufafanua kikamili kazi hizo za Mungu jua bado laendelea kupasha joto (kwa njia ya moja kwa moja au kwa njia nyingineyo). Twapata chakula na oksijeni kwa sababu mimea hupata nuru. Twaweza kusoma, kuona nyuso za wapendwa wetu, kutazama machweo, na kadhalika. Tufanyapo hivyo, je, hatupaswi kushukuru kwa sababu ya kazi za Mungu za ajabu?—Zaburi 104:1, 2; 145:5; Isaya 45:7; Yeremia 31:35.

      22. Daudi aliyeishi zamani alizionaje kazi za Mungu za ajabu?

      22 Je, tunatafakari kazi za Yehova za ajabu kusudi tu tustaajabu au kuduwaa? La, hasha. Mtunga-zaburi aliyeishi zamani alikiri kwamba haiwezekani kufahamu au kueleza kazi zote za Mungu. Daudi aliandika: “Ee BWANA, Mungu wangu, umefanya kwa wingi miujiza yako; [“kazi zako za ajabu,” NW] . . . Kama ningependa kuyatangaza na kuyahubiri, ni mengi sana hayahesabiki.” (Zaburi 40:5) Bila shaka Daudi hakumaanisha kwamba hangezungumza kuhusu kazi hizo zenye kuvutia. Daudi alithibitisha hilo kwa azimio lake linalotajwa kwenye Zaburi 9:1: “Nitamshukuru BWANA kwa moyo wangu wote; nitayasimulia matendo yako yote ya ajabu.”

      23. Unazionaje kazi za Mungu za ajabu, na unaweza kuwasaidiaje wengine?

      23 Je, hatupaswi kuchochewa vivyo hivyo? Je, kustaajabia kwetu kazi za Mungu zenye kuvutia hakupasi kutuchochea kuzungumza juu yake, juu ya yale ambayo amefanya, na yale ambayo bado atafanya? Jibu ni wazi—tunapaswa ‘kuwahubiri mataifa habari za utukufu wake, na watu wote habari za maajabu yake.’ (Zaburi 96:3-5) Naam, tunaweza kuonyesha uthamini wetu wenye unyenyekevu kwa kazi za Mungu za ajabu kwa kujulisha wengine yale ambayo tumejifunza kumhusu. Hata wawe walilelewa katika jamii ambayo haimtambui Muumba, huenda maneno yetu yenye kujenga na yenye kuelimisha yakawaamsha fikira watambue kuna Mungu. Isitoshe, huenda yakawachochea kutaka kujifunza na kumtumikia yule ambaye ‘aliumba vitu vyote,’ Yehova, Mtekelezaji wa kazi za ajabu.—Ufunuo 4:11.

  • Zingatia Kazi za Mungu za Ajabu
    Mnara wa Mlinzi—2001 | Aprili 15
    • Zingatia Kazi za Mungu za Ajabu

      “Ee BWANA, Mungu wangu, umefanya kwa wingi miujiza yako [“kazi zako za ajabu,” “NW”] na mawazo yako kwetu; hakuna awezaye kufananishwa nawe.”—ZABURI 40:5.

      1, 2. Tuna uthibitisho gani wa kazi za Mungu za ajabu, na hilo lapasa kutuchochea tufanye nini?

      USOMAPO Biblia unaweza kuona kwa urahisi kwamba Mungu alifanya mambo ya ajabu kwa ajili ya watu wake Waisraeli walioishi zamani. (Yoshua 3:5; Zaburi 106:7, 21, 22) Hata ingawa sasa Yehova haingilii shughuli za wanadamu kwa njia hiyo, tunaona uthibitisho mwingi wa kazi zake za ajabu. Kwa hiyo tuna sababu ya kujiunga na mtunga-zaburi kusema: “Ee BWANA, jinsi yalivyo mengi matendo yako! Kwa hekima umevifanya vyote pia. Dunia imejaa mali zako.”—Zaburi 104:24; 148:1-5.

      2 Watu wengi leo hupuuza au hukataa uthibitisho huo ulio wazi wa matendo ya Muumba. (Waroma 1:20) Hata hivyo, ingefaa tuyatafakari na kufanya maamuzi yanayopatana na msimamo wetu na wajibu wetu mbele za Muumba. Ayubu sura ya 38 hadi 41 yaweza kutusaidia sana katika jambo hilo, kwa kuwa kwenye sura hizo Yehova alimjulisha Ayubu baadhi ya kazi Zake za ajabu. Fikiria masuala fulani yafaayo ambayo Mungu alizusha.

      Kazi za Ajabu na Zenye Nguvu

      3. Mungu aliuliza juu ya mambo gani kwenye Ayubu 38:22-23, 25-29?

      3 Wakati mmoja, Mungu alimwuliza Ayubu hivi: “Je! umeziingia ghala za theluji, au umeziona ghala za mvua ya mawe, nilizoziweka akiba kwa wakati wa misiba, kwa siku ya mapigano na vita?” Theluji na mvua ya mawe hutokea katika sehemu nyingi za dunia yetu. Mungu aliendelea kumwuliza: “Ni nani aliyepasua mfereji kwa maji ya gharika, au njia kwa umeme wa radi; kunyesha mvua juu ya nchi isiyo na watu; juu ya jangwa asiyokaa mwanadamu; kuishibisha nchi iliyo kame na ukiwa, na kuyameza majani yaliyo mororo? Je! mvua ina baba au ni nani aliyeyazaa matone ya umande? Barafu ilitoka katika tumbo la nani na sakitu ya mbinguni ni nani aliyeizaa?”—Ayubu 38:22, 23, 25-29.

      4-6. Ni katika maana gani mwanadamu amekosa ujuzi kamili kuhusu theluji?

      4 Huenda watu fulani wanaoishi katika jamii zenye hekaheka nyingi, ambao ni lazima wasafiri, wakaiona theluji kuwa kizuizi. Hata hivyo, watu wengine huvutiwa sana na theluji wakati wa majira ya baridi kali kwa kuwa hiyo huwapa fursa ya kufanya mambo ya pekee. Unapofikiria swali ambalo Mungu aliuliza, je, wewe unaijua theluji vizuri, na je, umewahi kuiona? Tunajua jinsi rundo kubwa la theluji lilivyo, aidha kwa kuwa tumeliona kwa macho yetu wenyewe au tumeona picha zake. Lakini namna gani chembe za theluji? Je, wajua chembe za theluji zinafananaje, labda kwa kuchunguza jinsi zinavyotokea?

      5 Watu fulani wamechunguza na kupiga picha chembe za theluji kwa makumi ya miaka. Chembe moja ya theluji inaweza kuwa na chembe ndogondogo mia moja za barafu zenye maumbo mbalimbali yenye kupendeza. Kitabu kiitwacho Atmosphere chasema: ‘Namna nyingi za chembe za theluji zajulikana sana, na ingawa wanasayansi wanasisitiza kwamba hakuna sheria ya asili ambayo huzuia chembe hizo zisifanane, hawajawahi kupata chembe mbili zinazofanana. Wilson A. Bentley alifanya uchunguzi mkubwa uliochukua muda wa miaka 40 kwa kutumia darubini kupiga picha chembe za theluji, lakini hakupata chembe mbili zinazofanana.’ Na hata kama angalipata chembe mbili zinazofanana, jambo ambalo ni nadra, je, hilo lingebadili kwa njia yoyote maajabu tunayoona katika namna nyingi za chembe za barafu?

      6 Kumbuka swali la Mungu: “Je! umeziingia ghala za theluji?” Wengi hufikiria mawingu kuwa ghala za theluji. Je, waweza kuwazia ukiingia katika ghala hizo kuhesabu chembe za theluji za namna nyingi sana na kuchunguza jinsi zilivyotokea? Ensaiklopidia moja ya sayansi yasema hivi: ‘Asili ya kiini cha barafu, ambacho husababisha matone ya maji kwenye mawingu yagande wakati wa baridi kali, haijulikani bado.’—Zaburi 147:16, 17; Isaya 55:9, 10.

      7. Mwanadamu ana ujuzi mwingi kadiri gani kuhusu mvua?

      7 Namna gani mvua? Mungu alimwuliza Ayubu hivi: “Je! mvua ina baba? Au ni nani aliyeyazaa matone ya umande?” Ensaiklopidia hiyohiyo yasema hivi: ‘Ni vigumu kwa wanasayansi kueleza jinsi ambavyo mawingu na matone ya mvua hutokea kwa sababu kuna utendaji mwingi tata katika angahewa na kiwango cha mvuke na chembe zilizo hewani hubadilika-badilika.’ Kwa maneno sahili, wanasayansi wametoa dhana zenye maelezo mengi, lakini hawawezi kueleza kikamili jinsi ambavyo mvua hutokea. Hata hivyo, unajua kwamba mvua ambayo ni muhimu hunyesha na kuitia dunia maji. Husitawisha mimea na hutuwezesha kuishi na kufurahia maisha.

      8. Kwa nini maneno ya Paulo kwenye Matendo 14:17 yafaa?

      8 Je, hukubaliani na kauli aliyokata mtume Paulo? Aliwahimiza wengine waone kazi za Mungu za ajabu kuwa zatoa ushuhuda juu ya Yule aliyezifanya. Paulo alisema hivi kumhusu Yehova Mungu: “Hakujiacha mwenyewe bila ushahidi kwa kuwa alitenda mema, akiwapa nyinyi mvua kutoka mbinguni na majira yenye kuzaa matunda, akijaza mioyo yenu kikamili kwa chakula na uchangamfu.”—Matendo 14:17; Zaburi 147:8.

      9. Kazi za Mungu za ajabu hudhihirishaje nguvu zake kuu?

      9 Bila shaka Mtekelezaji wa mambo hayo ya ajabu na yenye kunufaisha ana hekima na nguvu nyingi sana. Fikiria jambo hili kuhusu nguvu zake: Yasemekana kwamba kuna mvua za umeme na ngurumo zipatazo 45,000 zinazotokea kila siku, zaidi ya milioni 16 kwa mwaka. Hilo lamaanisha kwamba kuna mvua za aina hiyo zipatazo 2,000 zinazonyesha sasa hivi. Mawingu tata ya mvua moja ya umeme na ngurumo hutokeza nguvu zinazotoshana na nguvu za mabomu kumi au zaidi ya nyuklia yaliyoangushwa katika Vita ya Ulimwengu ya Pili. Baadhi ya nguvu hizo huonekana zikiwa umeme. Licha ya kuwa yenye kuogofya, mimweko ya umeme husaidia hasa kutokeza nitrojeni za namna mbalimbali zinazoufikia udongo na kufyonzwa na mimea zikiwa mbolea ya asili. Kwa hiyo umeme ni nguvu ionekanayo, yenye manufaa halisi.—Zaburi 104:14, 15.

      Unafikia Mkataa Gani?

      10. Ungejibuje maswali yanayoulizwa kwenye Ayubu 38:33-38?

      10 Hebu wazia kuwa wewe ni Ayubu na unaulizwa maswali na Mungu Mweza Yote. Yaelekea utakubali kwamba watu wengi hawazingatii sana kazi za Mungu za ajabu. Yehova anatuuliza maswali tusomayo kwenye Ayubu 38:33-38. “Je! unazijua amri zilizoamuriwa mbingu? Waweza kuyathibitisha mamlaka yake juu ya dunia? Waweza kuiinua sauti yako mpaka mawinguni, ili wingi wa maji ukufunikize? Waweza kuutuma umeme, nao ukaenda, ukakuambia, Sisi tupo hapa? Je! ni nani aliyetia hekima moyoni? Au ni nani aliyetia ufahamu rohoni? Ni nani awezaye kuyahesabu mawingu kwa hekima? Au ni nani awezaye kuzimimina chupa za mbinguni? Wakati mavumbi yagandamanapo, na madongoa kushikamana pamoja?”

      11, 12. Ni baadhi ya mambo gani yanayothibitisha kwamba Mungu ni Mtekelezaji wa kazi za ajabu?

      11 Tumezungumzia mambo machache tu ambayo Elihu alimwuliza Ayubu, kisha tumeona baadhi ya maswali ambayo Yehova alimwuliza Ayubu ajibu “kama mwanamume.” (Ayubu 38:3) Twasema “baadhi” kwa sababu katika Ayubu sura ya 38 na 39, Mungu alikazia fikira uumbaji mwingine mbalimbali wenye kutokeza. Kwa mfano, alitaja makundi ya nyota yaliyo katika mbingu. Ni nani ajuaye amri au sheria zake zote? (Ayubu 38:31-33) Yehova alimtajia Ayubu wanyama fulani—simba na kunguru, mbuzi-mwitu na punda-milia, nyati na mbuni, kisha farasi na tai. Ni kana kwamba Mungu alimwuliza Ayubu iwapo alikuwa amewapa wanyama hao mbalimbali tabia zao na kuwawezesha kuishi na kusitawi. Huenda ukafurahia kusoma sura hizo, hasa ikiwa wewe unapendezwa na farasi au wanyama wengineo.—Zaburi 50:10, 11.

      12 Waweza pia kuchunguza Ayubu sura ya 40 na 41, ambapo Yehova amwomba tena Ayubu ajibu maswali yake juu ya viumbe wawili hususa. Twawajua viumbe hao, nao ni kiboko (Behemothi), mwenye mwili mkubwa na mwenye nguvu, na mamba wa Naili (Leviathani) mwenye kuogofya. Kila mmoja wao ni kiumbe wa ajabu asiyepasa kupuuzwa. Acheni sasa tuone yatupasa kukata kauli gani.

      13. Maswali ya Mungu yalikuwa na matokeo gani kwa Ayubu, nayo yapasa kuwa na matokeo gani kwetu?

      13 Ayubu sura ya 42 yatuonyesha maswali ya Mungu yalikuwa na matokeo gani kwa Ayubu. Awali, Ayubu alikuwa akijifikiria mwenyewe na wanadamu wengine kupita kiasi. Lakini, kwa kuwa alikubali sahihisho lililodokezwa na maswali ya Mungu, Ayubu alibadili maoni yake. Alikiri hivi: “Najua ya kuwa [wewe Yehova] waweza kufanya mambo yote, na ya kuwa makusudi yako hayawezi kuzuilika. Ni nani huyu afichaye mashauri bila maarifa? Kwa maana, nimesema maneno nisiyoyafahamu, mambo ya ajabu ya kunishinda mimi, nisiyoyajua.” (Ayubu 42:2, 3) Naam, baada ya kuzingatia kazi za Mungu, Ayubu alisema kwamba kazi hizo zilikuwa za ajabu sana. Baada ya kuzungumzia maajabu hayo ya uumbaji, sisi pia twapaswa kuvutiwa na hekima na nguvu za Mungu. Kwa madhumuni gani? Je, ni ili tu tuvutiwe na nguvu na uwezo mwingi wa Yehova? Au twapaswa kuchochewa kufanya mengi zaidi?

      14. Daudi alizionaje kazi za Mungu za ajabu?

      14 Katika Zaburi 86, tunapata maneno yanayofanana na hayo ambayo yalisemwa na Daudi katika Zaburi fulani iliyotangulia: “Mbingu zauhubiri utukufu wa Mungu, na anga laitangaza kazi ya mikono yake. Mchana husemezana na mchana, usiku hutolea usiku maarifa.” (Zaburi 19:1, 2) Lakini Daudi alisema mengi zaidi. Kwenye Zaburi 86:10, 11 twasoma hivi: “[Wewe] ndiwe uliye mkuu, wewe ndiwe mfanya miujiza, ndiwe Mungu peke yako. Ee BWANA, unifundishe njia yako; nitakwenda katika kweli yako; moyo wangu na ufurahi kulicha jina lako.” Daudi alikuwa na hofu yenye staha kwa Muumba kwa sababu ya kazi Zake zote za ajabu. Waweza kuona ni kwa nini. Daudi hakutaka kumchukiza Yule awezaye kufanya kazi hizo za ajabu. Wala sisi hatupaswi kumchukiza.

      15. Kwa nini hofu yenye staha ya Daudi kwa Mungu ilifaa?

      15 Ni lazima Daudi awe alitambua kwamba kwa kuwa Mungu ana nguvu nyingi anazoweza kutumia vile atakavyo, aweza kuzitumia dhidi ya yeyote asiyestahili fadhili zake. Hilo ni onyo kwao. Mungu alimwuliza Ayubu hivi: “Je! umeziingia ghala za theluji, au umeziona ghala za mvua ya mawe, nilizoziweka akiba kwa wakati wa misiba, kwa siku ya mapigano na vita?” Theluji, mvua ya mawe, dhoruba za mvua, upepo, na umeme, zote hizo ni silaha za Mungu. Nazo ni kani za asili zilizo nyingi kama nini!—Ayubu 38:22, 23.

      16, 17. Nguvu kuu za Mungu hudhihirishwa na nini, naye ametumiaje nguvu hizo wakati uliopita?

      16 Huenda wakumbuka msiba fulani uliosababishwa na mojawapo ya mambo hayo—iwe kimbunga, dhoruba ya mvua ya mawe, au furiko la ghafula. Kwa mfano, mwishoni mwa mwaka wa 1999, dhoruba kubwa ilikumba kusini-magharibi mwa Ulaya. Iliwashangaza hata wataalamu wa hali ya anga. Pepo zenye nguvu zilifikia mwendo wa kilometa 200 kwa saa, ziking’oa maelfu ya paa, zikiangusha nguzo za chuma za kuegemeza nyaya za nguvu za umeme, na kuangusha magari. Hebu wazia hili: Dhoruba hiyo iling’oa au kuvunja miti ipatayo milioni 270. Miti 10,000 kati ya hiyo ilikuwa katika bustani ya Versailles, nje ya Paris. Mamilioni ya nyumba yaliachwa bila umeme. Karibu watu 100 walikufa. Uharibifu wote huo ulichukua muda mfupi sana. Ni nguvu zilizoje!

      17 Mtu anaweza kuita dhoruba tukio lisilo la kawaida, lisilo na mwelekezo na lisilodhibitiwa. Hata hivyo, hali ingekuwaje iwapo Yule mwenye nguvu zote, angefanya kazi za ajabu kwa kutumia kani hizo kwa njia inayodhibitiwa, chini ya mwelekezo wake? Alifanya jambo kama hilo zama za Abrahamu, ambaye alijifunza kwamba Hakimu wa dunia yote alikuwa amezingatia uovu wa majiji mawili, Sodoma na Gomora. Majiji hayo yalikuwa na ufisadi mwingi sana hivi kwamba malalamiko mengi dhidi yake yalimfikia Mungu, ambaye aliwasaidia waadilifu wote kukimbia majiji hayo yaliyohukumiwa adhabu. Historia yasema hivi: ‘Ndipo BWANA akanyesha kiberiti na moto toka mbinguni,’ juu ya miji hiyo ya kale. Ilikuwa kazi ya ajabu kuwahifadhi waadilifu na kuwaharibu watu hao waliokuwa waovu kupita kiasi.—Mwanzo 19:24.

      18. Isaya sura ya 25 inazungumzia mambo gani ya ajabu?

      18 Baadaye, Mungu alikata kauli kuhukumu Babiloni, mji wa kale ambao waweza kuwa ndio mji unaorejezewa kwenye Isaya sura ya 25. Mungu alitabiri kwamba mji huo ungekuwa magofu: “Umefanya mji kuwa ni chungu; mji wenye boma kuwa ni magofu; jumba la wageni kuwa si mji; hautajengwa tena milele.” (Isaya 25:2) Watu wanaozuru leo mahali ulipokuwa Babiloni wa kale waweza kuthibitisha kwamba ndivyo ilivyo. Je, kuharibiwa kwa Babiloni kulitukia kiaksidenti tu? La. Badala yake twaweza kukubali maoni ya Isaya: “Ee BWANA, wewe u Mungu wangu; nitakutukuza na kulihimidi jina lako; kwa kuwa umetenda mambo ya ajabu, mashauri ya kale, kwa uaminifu na kweli.”—Isaya 25:1.

      Kazi za Ajabu Wakati Ujao

      19, 20. Tunaweza kutarajia utimizo gani wa Isaya 25:6-8?

      19 Mungu alitimiza unabii ambao umetajwa hapo juu wakati uliopita, naye atafanya hivyo kwa njia ya ajabu wakati ujao. Katika muktadha huo, ambapo Isaya anataja “mambo ya ajabu” ya Mungu, tunapata unabii wenye kutegemeka ambao utatimizwa, kama vile tu hukumu dhidi ya Babiloni ilivyotimizwa. Ni ‘jambo gani la ajabu’ linaloahidiwa? Andiko la Isaya 25:6 lasema hivi: “Katika mlima huu BWANA wa majeshi atawafanyia mataifa yote karamu ya vitu vinono, karamu ya divai iliyokaa juu ya urojorojo wake, karamu ya vinono vilivyojaa mafuta, karamu ya divai iliyokaa juu ya urojorojo wake, iliyochujwa sana.”

      20 Bila shaka unabii huo utatimizwa katika ulimwengu mpya ulio karibu, ambao Mungu ameahidi. Wakati huo, wanadamu wataondolewa matatizo yanayowalemea wengi leo. Kwa kweli unabii wa Isaya 25:7, 8 wahakikisha kwamba Mungu atatumia nguvu zake za uumbaji kufanya mojawapo ya kazi za ajabu zaidi zisizo na kifani: “Amemeza mauti hata milele; na Bwana MUNGU atafuta machozi katika nyuso zote; na aibu ya watu wake ataiondoa katika ulimwengu wote; maana BWANA amenena hayo.” Baadaye mtume Paulo alinukuu andiko hilo na kulitumia kuonyesha jinsi Mungu atakavyowafufua wafu. Hiyo itakuwa kazi ya ajabu kama nini!—1 Wakorintho 15:51-54.

      21. Ni kazi gani za ajabu ambazo Mungu atawafanyia wafu?

      21 Jambo jingine litakalofanya machozi ya huzuni yaishe ni kwamba magonjwa yataondolewa. Yesu alipokuwa duniani aliwaponya wengi, akawawezesha vipofu kuona, viziwi kusikia, na kuwapa nguvu walemavu. Andiko la Yohana 5:5-9 lasema kwamba alimponya mtu aliyekuwa kilema kwa miaka 38. Watazamaji waliona jambo hilo kuwa kazi ya ajabu sana. Nalo kwa kweli lilikuwa kazi ya ajabu! Lakini Yesu aliwaambia kwamba kufufuliwa kwa wafu ndilo litakalokuwa jambo la ajabu zaidi: “Msistaajabie hili, kwa sababu saa inakuja ambayo katika hiyo wote wale waliomo ndani ya makaburi ya ukumbusho watasikia sauti yake na kutoka, wale waliofanya mambo mema kwenye ufufuo wa uhai, wale waliozoea kufanya mambo maovu kwenye ufufuo wa hukumu.”—Yohana 5:28, 29.

      22. Kwa nini maskini na wenye kuonewa watazamie wakati ujao kwa matumaini?

      22 Bila shaka hilo litatukia kwa kuwa Yehova ndiye anayetoa ahadi hiyo. Waweza kuwa na hakika kwamba atumiapo na kuelekeza kwa uangalifu nguvu zake kuu za kuponya, matokeo yatakuwa ya ajabu. Andiko la Zaburi 72 hutaja atakayofanya kupitia Mwanaye Mfalme. Kisha waadilifu watasitawi na amani itakuwa tele. Mungu atawakomboa maskini na watu walioonewa. Anaahidi hivi: “Na uwepo wingi wa nafaka katika ardhi juu ya milima; matunda yake na yawaye-waye kama Lebanoni [ya kale], na watu wa mjini wasitawi kama majani ya nchi.”—Zaburi 72:16.

      23. Kazi za Mungu za ajabu zapasa kutuchochea tufanye nini?

      23 Ni wazi kwamba tuna sababu nyingi za kuzingatia kazi za Yehova za ajabu—mambo aliyofanya wakati uliopita, anayofanya leo na atakayofanya karibuni. “Na ahimidiwe BWANA, Mungu, Mungu wa Israeli, atendaye miujiza [“kazi za ajabu,” NW] Yeye peke yake; jina lake tukufu na lihimidiwe milele; dunia yote na ijae utukufu wake. Amina na Amina.” (Zaburi 72:18, 19) Yatupasa kuzungumzia mambo hayo kwa ukawaida na kwa shauku pamoja na jamaa zetu na wengineo. Naam, acheni ‘tuwahubiri mataifa habari za utukufu wake, na watu wote habari za maajabu yake.’—Zaburi 78:3, 4; 96:3, 4.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki