Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Yehova Ni Msaidizi Wetu
    Mnara wa Mlinzi—2004 | Desemba 15
    • Yehova Ni Msaidizi Wetu

      “Msaada wangu unatoka kwa Yehova, Mtengenezaji wa mbingu na dunia.”—ZABURI 121:2.

      1, 2. (a) Kwa nini tunaweza kusema kwamba nyakati nyingine sisi sote huhitaji msaada? (b) Yehova ni Msaidizi wa aina gani?

      NI NANI kati yetu asiyehitaji msaada kamwe? Kwa kweli, nyakati nyingine sisi sote huhitaji msaada ili kukabiliana na tatizo zito, kuvumilia huzuni ya kufiwa, na kustahimili jaribu gumu. Wanapohitaji msaada, mara nyingi watu humwendea rafiki anayejali. Huenda kumwambia rafiki huyo tatizo lako kukafanya iwe rahisi kulistahimili. Lakini msaada ambao mwanadamu mwenzetu anaweza kutoa una mipaka. Isitoshe, huenda sikuzote wengine wasiweze kutoa msaada unapohitajiwa.

      2 Hata hivyo, kuna Msaidizi ambaye ana nguvu na uwezo usio na mipaka. Zaidi ya hayo, yeye anatuhakikishia kwamba hatatuacha kamwe. Yeye ndiye anayetajwa na mtunga-zaburi ambaye alisema hivi kwa uhakika kabisa: “Msaada wangu unatoka kwa Yehova.” (Zaburi 121:2) Kwa nini mtunga-zaburi huyo alisadiki kwamba Yehova angemsaidia? Ili kujibu swali hilo, acheni tuchunguze Zaburi ya 121. Kufanya hivyo kutatusaidia kuona kwa nini sisi pia tunaweza kwa uhakika kumtegemea Yehova kuwa Msaidizi wetu.

      Chanzo Kinachotegemeka cha Msaada

      3. Huenda mtunga-zaburi aliinua macho yake kuelekea milima gani, na kwa nini?

      3 Mtunga-zaburi alianza kwa kueleza kwamba kwa kuwa Yehova ndiye aliyeumba kila kitu, tuna msingi wa kuwa na uhakika. Alisema hivi: “Nitainua macho yangu milimani. Msaada wangu utatoka wapi? Msaada wangu unatoka kwa Yehova, Mtengenezaji wa mbingu na dunia.” (Zaburi 121:1, 2) Mtunga-zaburi aliinua macho yake kuelekea milima fulani hususa. Maneno hayo yalipoandikwa, hekalu la Yehova lilikuwa Yerusalemu. Jiji hilo lililokuwa juu ya milima ya Yuda, lilifananisha makao ya Yehova. (Zaburi 135:21) Huenda mtunga-zaburi aliinua macho yake kuelekea milima ya Yerusalemu ambako hekalu la Yehova lilijengwa, huku akitegemea msaada wa Yehova akiwa na uhakika. Kwa nini mtunga-zaburi alikuwa na uhakika sana kwamba Yehova angemsaidia? Kwa sababu Yeye ndiye “Mtengenezaji wa mbingu na dunia.” Kwa kweli, mtunga-zaburi alikuwa akisema, ‘Hakika hakuna chochote kinachoweza kumzuia Muumba mwenye nguvu zote kunisaidia!’—Isaya 40:26.

      4. Mtunga-zaburi alionyeshaje kwamba sikuzote Yehova yuko macho kuona mahitaji ya watumishi wake, na kwa nini jambo hilo linafariji?

      4 Kisha mtunga-zaburi alieleza kwamba sikuzote Yehova huwa macho kuona mahitaji ya watumishi wake: “Hawezi kamwe kuruhusu mguu wako utikisike. Yeye anayekulinda hawezi kamwe kusinzia. Tazama! Hatasinzia wala kulala usingizi, yeye anayelinda Israeli.” (Zaburi 121:3, 4) Mungu hawezi kamwe kuruhusu wale wanaomtumaini ‘watikisike’ au waanguke na kushindwa kusimama. (Methali 24:16) Kwa nini? Kwa sababu Yehova ni kama mchungaji aliye macho kabisa anayechunga kondoo zake. Jambo hilo linafariji kama nini! Hatakosa kamwe kuangalia mahitaji ya watu wake. Yeye huwaangalia mchana na usiku.

      5. Kwa nini Yehova anasemwa kuwa yuko kwenye ‘mkono wa kuume’?

      5 Akiwa na uhakika kwamba Yehova huwalinda kwa ushikaminifu watu wake, mtunga-zaburi aliandika hivi: “Yehova anakulinda. Yehova ni kivuli chako kwenye mkono wako wa kuume. Wakati wa mchana, jua halitakupiga, wala mwezi wakati wa usiku.” (Zaburi 121:5, 6) Kwa msafiri anayetembea kwa miguu huko Mashariki ya Kati, kivuli kingemkinga na jua kali. Yehova ni kama kivuli kwa watu wake, akiwalinda na maafa yaliyo kama joto lenye kuunguza. Ona kwamba Yehova anasemwa kuwa yuko kwenye ‘mkono wa kuume.’ Katika vita vya kale, kwa kadiri fulani, mkono wa kuume wa askari-jeshi haukukingwa na ngao ambayo aliishika kwa mkono wa kushoto. Rafiki mshikamanifu angeweza kumkinga kwa kusimama na kupigana akiwa kwenye mkono wa kuume wa askari-jeshi huyo. Kama rafiki huyo, Yehova anasimama kwa ushikamanifu kando ya waabudu wake, sikuzote akiwa tayari kuwasaidia.

      6, 7. (a) Mtunga-zaburi anatuhakikishiaje kwamba Yehova hataacha kamwe kuwasaidia watu wake? (b) Kwa nini tunaweza kuwa na uhakika kama mtunga-zaburi?

      6 Je, Yehova ataacha kamwe kuwasaidia watu wake? Hawezi kufanya hivyo kamwe. Mtunga-zaburi alimalizia hivi: “Yehova mwenyewe atakulinda na misiba yote. Atailinda nafsi yako. Yehova mwenyewe atalinda kuondoka kwako na kuingia kwako tangu sasa na mpaka wakati usio na kipimo.” (Zaburi 121:7, 8) Ona kwamba mwandikaji alikazia njeo ya wakati ujao badala ya njeo ya wakati uliopo. Mapema katika mstari wa 5, mtunga-zaburi alisema: “Yehova anakulinda.” Lakini katika mistari hii, mtunga-zaburi aliandika: “Yehova mwenyewe atakulinda.” Hivyo waabudu wa kweli wanahakikishiwa kwamba Yehova atawasaidia hata wakati ujao. Hata waende wapi, au wakabili misiba gani, mkono wa Yehova utawasaidia sikuzote.—Methali 12:21.

      7 Kwa kweli, mwandikaji wa Zaburi ya 121 alikuwa na uhakika kwamba Muumba mweza-yote huwaangalia watumishi wake kwa wororo kama mchungaji anayejali na kwa uangalifu kama mlinzi aliye macho. Tuna kila sababu ya kuwa na uhakika kama mtunga-zaburi, kwa kuwa Yehova habadiliki. (Malaki 3:6) Je, hilo linamaanisha kwamba sikuzote tutalindwa kimwili? La, lakini maadamu tunamtegemea Yehova kuwa Msaidizi wetu, yeye atatulinda na mambo yote yanayoweza kutudhuru kiroho. Ni jambo la kawaida kuuliza, ‘Yehova hutusaidiaje?’ Hebu tuchunguze njia nne anazotumia kufanya hivyo. Katika makala hii, tutazungumzia jinsi alivyowasaidia watumishi wake katika nyakati za Biblia. Katika makala inayofuata, tutazungumzia jinsi anavyowasaidia watu wake leo.

      Msaada Kutoka kwa Malaika

      8. Kwa nini haishangazi kwamba malaika wanapendezwa sana na hali ya watumishi wa Mungu duniani?

      8 Yehova ana mamlaka juu ya mamilioni na mamilioni ya malaika. (Danieli 7:9, 10) Wana hao wa roho wanafanya mapenzi yake kwa uaminifu. (Zaburi 103:20) Wanajua vizuri sana kwamba Yehova anawapenda sana wanadamu wanaomwabudu naye anataka kuwasaidia. Haishangazi kwamba malaika wanapendezwa sana na hali ya watumishi wa Mungu duniani. (Luka 15:10) Bila shaka, malaika hufurahia sana kutumiwa na Yehova kuwasaidia wanadamu. Yehova aliwatumiaje malaika kuwasaidia watumishi wake wanadamu katika nyakati za kale?

      9. Toa mfano unaoonyesha jinsi malaika walivyopewa na Mungu mamlaka na nguvu ili kuwalinda wanadamu waaminifu.

      9 Malaika walipewa na Mungu mamlaka na nguvu ili kuwalinda na kuwaokoa wanadamu waaminifu. Malaika wawili walimsaidia Loti na binti zake kuponyoka uharibifu wa Sodoma na Gomora. (Mwanzo 19:1, 15-17) Malaika mmoja aliwaua askari-jeshi Waashuru 185,000 waliokuwa wakitisha Yerusalemu. (2 Wafalme 19:35) Danieli alipotupwa ndani ya shimo la simba, Yehova “alimtuma malaika wake na kufunga vinywa vya simba.” (Danieli 6:21, 22) Malaika alimfungua mtume Petro kutoka gerezani. (Matendo 12:6-11) Biblia inataja mifano mingine mingi ya jinsi malaika walivyotoa ulinzi, na hivyo kuthibitisha yale yanayosemwa na Zaburi 34:7: “Malaika wa Yehova anapiga kambi pande zote kuwazunguka wanaomwogopa, na yeye huwaokoa.”

      10. Yehova alitumiaje malaika kumtia moyo nabii Danieli?

      10 Pindi fulani, Yehova alitumia malaika ili kuwatia moyo na kuwaimarisha wanadamu waaminifu. Mfano mmoja unaogusa moyo unapatikana katika Danieli sura ya 10. Wakati huo, pengine Danieli alikuwa na umri wa miaka 100 hivi. Nabii huyo alikuwa amevunjika moyo sana, yaelekea kwa sababu ya hali ya ukiwa ya Yerusalemu na kucheleweshwa kujengwa upya kwa hekalu. Pia aliogopa sana baada ya kuona maono yenye kutisha. (Danieli 10:2, 3, 8) Kwa upendo, Mungu alimtuma malaika kumtia moyo. Zaidi ya mara moja, malaika huyo alimkumbusha Danieli kwamba alikuwa mwenye “kutamanika sana” machoni pa Mungu. Ikawaje? Nabii huyo mzee alimwambia malaika huyo hivi: “Umenitia nguvu.”—Danieli 10:11, 19.

      11. Ni mfano gani unaoonyesha jinsi malaika walivyotumiwa kuelekeza kazi ya kuhubiri habari njema?

      11 Yehova pia alitumia malaika kuelekeza kazi ya kuhubiri habari njema. Malaika mmoja alimwelekeza Filipo kumhubiria towashi Mwethiopia kuhusu Kristo, na baadaye towashi huyo akabatizwa. (Matendo 8:26, 27, 36, 38) Muda mfupi baadaye, ilikuwa mapenzi ya Mungu kwamba habari njema ihubiriwe kwa watu wasio Wayahudi ambao hawakuwa wametahiriwa. Katika maono, malaika alimtokea Kornelio, mtu ambaye hakuwa Myahudi na aliyemwogopa Mungu, naye akamwelekeza atume watu wakamwite mtume Petro. Walipompata Petro, wajumbe waliotumwa na Kornelio walisema: ‘Kornelio alipewa maagizo matakatifu na malaika wa Mungu kwamba atume watu ili uitwe uje nyumbani kwake apate kuyasikia mambo utakayosema.’ Petro alikubali kwenda, na hivyo watu wa kwanza wasio Wayahudi ambao hawakuwa wametahiriwa wakawa sehemu ya kutaniko la Kikristo. (Matendo 10:22, 44-48) Hebu wazia jinsi ambavyo ungehisi kujua kwamba malaika alikusaidia kukutana na mtu mwenye mwelekeo unaofaa!

      Msaada Kupitia Roho Takatifu

      12, 13. (a) Kwa nini mitume wa Yesu walikuwa na sababu nzuri ya kuamini kwamba roho takatifu ingewasaidia? (b) Ni katika njia gani roho takatifu iliwapa Wakristo wa karne ya kwanza mamlaka na nguvu?

      12 Muda mfupi kabla ya kufa, Yesu aliwahakikishia mitume wake kwamba hangewaacha bila msaada. Baba angewapa “msaidizi, roho takatifu.” (Yohana 14:26) Mitume walikuwa na sababu nzuri ya kuamini kwamba roho takatifu ingewasaidia. Maandiko yaliyoongozwa na roho ya Mungu yana mifano mingi ya jinsi Yehova alivyotumia roho takatifu, nguvu iliyo kuu kupita zote, kuwasaidia watu wake.

      13 Pindi nyingi, roho takatifu ilitumiwa kuwapa wanadamu mamlaka na nguvu ili kufanya mapenzi ya Yehova. Roho takatifu iliwapa Waamuzi mamlaka na nguvu za kuwaokoa Waisraeli. (Waamuzi 3:9, 10; 6:34) Roho hiyohiyo iliwapa Wakristo wa karne ya kwanza mamlaka na nguvu za kuendelea kuhubiri kwa ujasiri licha ya upinzani wa kila namna. (Matendo 1:8; 4:31) Mafanikio waliyopata katika huduma yao yalitoa uthibitisho wenye nguvu wa utendaji wa roho takatifu. Ndiyo sababu watu “wasio na elimu na wa kawaida tu” wangeweza kufanikiwa kueneza ujumbe wa Ufalme katika ulimwengu wote uliojulikana wakati huo.—Matendo 4:13; Wakolosai 1:23.

      14. Yehova ametumiaje roho yake takatifu ili kuwapa watu wake uelewaji zaidi?

      14 Pia Yehova alitumia roho yake takatifu ili kuwapa watu wake uelewaji zaidi. Kwa msaada wa roho ya Mungu, Yosefu aliweza kufasiri ndoto za kinabii za Farao. (Mwanzo 41:16, 38, 39) Kupitia roho yake, Yehova alifanya makusudi yake yafunuliwe kwa wanyenyekevu lakini yakafichwa kwa wenye kiburi. (Mathayo 11:25) Hivyo, mtume Paulo alisema hivi kuhusu mambo ambayo Yehova huwaandalia “wale wanaompenda”: “Ni kwetu sisi Mungu ameyafunua kupitia roho.” (1 Wakorintho 2:7-10) Mtu anaweza tu kuelewa mapenzi ya Mungu kikweli kwa msaada wa roho takatifu.

      Msaada Kutoka kwa Neno la Mungu

      15, 16. Yoshua aliambiwa afanye nini ili atende kwa hekima?

      15 Neno la Yehova lililoongozwa na roho yake ni “lenye faida kwa kufundisha,” nalo huwawezesha watumishi wa Mungu wawe na ‘uwezo kamili, wakiwa na vifaa kamili kwa ajili ya kila kazi njema.’ (2 Timotheo 3:16, 17) Biblia ina mifano mingi ya jinsi watu wa Mungu katika nyakati za kale walivyosaidiwa na sehemu za Neno lake ambazo zilikuwa tayari zimeandikwa.

      16 Maandiko yalisaidia kutoa mwongozo unaofaa kwa waabudu wa Mungu. Yoshua aliambiwa hivi alipopewa daraka la kuwaongoza Waisraeli: “Kitabu hiki cha sheria [ambacho kiliandikwa na Musa] kisiondoke katika kinywa chako, nawe ukisome kwa sauti ya chini mchana na usiku, upate kuangalia kufanya kulingana na yote ambayo yameandikwa ndani yake; kwa maana ndipo utakapoifanikisha njia yako, kisha utatenda kwa hekima.” Ona kwamba Mungu hakumwahidi Yoshua kwamba angempa hekima kimuujiza. Badala yake, Yoshua angetenda kwa hekima ikiwa angesoma na kutafakari ‘kitabu cha sheria.’—Yoshua 1:8; Zaburi 1:1-3.

      17. Danieli na Mfalme Yosia walisaidiwaje na sehemu za Maandiko zilizokuwapo wakati huo?

      17 Pia Neno la Mungu lililoandikwa lilisaidia kufunua mapenzi na kusudi lake. Kwa mfano, kupitia maandishi ya Yeremia, Danieli alitambua muda ambao Yerusalemu lingebaki ukiwa. (Yeremia 25:11; Danieli 9:2) Fikiria pia yale yaliyotukia wakati wa utawala wa Mfalme Yosia wa Yuda. Kufikia wakati huo, taifa hilo lilikuwa limemwacha Yehova, na yaelekea wafalme hawakujiandikia nakala ya Sheria na kuifuata. (Kumbukumbu la Torati 17:18-20) Lakini hekalu lilipokuwa likirekebishwa, “kile kitabu chenyewe cha sheria,” ambacho yaelekea kiliandikwa na Musa, kilipatikana. Huenda kitabu hicho kilikuwa maandishi ya awali yaliyokamilishwa miaka 800 hivi mapema. Baada ya kusikia maneno yote ya kile kitabu yakisomwa, Mfalme Yosia alitambua jinsi taifa hilo lilivyokuwa limekiuka sana mapenzi ya Yehova, naye akachukua hatua thabiti kufanya yaliyokuwa yameandikwa katika kitabu hicho. (2 Wafalme 22:8; 23:1-7) Je, si wazi kwamba watu wa Mungu katika nyakati za kale walisaidiwa na sehemu za Maandiko Matakatifu zilizokuwapo wakati huo?

      Msaada Kupitia Waamini Wenzao

      18. Kwa nini tunaweza kusema kwamba Yehova anahusika mwabudu wa kweli anapomsaidia mwenzake?

      18 Mara nyingi Yehova hutoa msaada kupitia waamini wenzetu. Kwa kweli, Mungu anahusika mwabudu mmoja anapomsaidia mwenzake. Kwa nini tunaweza kusema hivyo? Kuna sababu mbili. Kwanza, roho takatifu ya Mungu inahusika. Roho hiyo hutokeza matunda, kutia ndani upendo na wema katika wale wanaotafuta mwongozo wake. (Wagalatia 5:22, 23) Kwa hiyo, mtumishi wa Mungu anapochochewa kumsaidia mwenzake, hilo huthibitisha kwamba roho ya Yehova inafanya kazi. Pili, tumeumbwa kwa mfano wa Mungu. (Mwanzo 1:26) Hiyo inamaanisha kwamba tunaweza kuonyesha sifa zake, kutia ndani fadhili na huruma zake. Kwa hiyo, mtumishi wa Yehova anapomsaidia mwenzake, Chanzo halisi cha msaada huo ni yule ambaye tumeumbwa kwa mfano wake.

      19. Kulingana na yale yaliyoandikwa katika Biblia, Yehova aliwasaidiaje watu wake kupitia waamini wenzao?

      19 Katika nyakati za Biblia, Yehova aliwasaidiaje watu wake kupitia waamini wenzao? Mara nyingi Yehova alifanya mmoja wa watumishi wake amshauri mwenzake, kama vile Yeremia alivyompa Baruku mashauri yenye kuokoa uhai. (Yeremia 45:1-5) Mara kwa mara, waabudu wa kweli walichochewa kutoa msaada wa kimwili kwa waamini wenzao, kama vile Wakristo huko Makedonia na Akaya walivyoonyesha tamaa ya kuwasaidia ndugu zao wenye uhitaji huko Yerusalemu. Mtume Paulo alisema kwamba kwa kweli ukarimu huo ulitokeza “wonyesho wa shukrani kwa Mungu.”—2 Wakorintho 9:11.

      20, 21. Mtume Paulo aliimarishwa na ndugu kutoka Roma chini ya hali gani?

      20 Masimulizi yenye kugusa moyo hasa ni yale yanayohusu jinsi watumishi wa Yehova walivyojitahidi kuimarishana na kutiana moyo. Fikiria mfano unaomhusu mtume Paulo. Alipokuwa safarini kuelekea Roma akiwa mfungwa, Paulo alipitia barabara kuu ya Roma iliyoitwa Njia ya Apio. Sehemu ya mwisho ya safari hiyo ilikuwa ngumu hasa kwa kuwa iliwabidi wasafiri kupitia eneo tambarare lenye majimaji.a Akina ndugu katika kutaniko la Roma walijua kwamba Paulo alikuwa anakuja. Wangefanya nini? Je, wangeendelea kustarehe katika nyumba zao jijini hadi Paulo afike ndipo waende kumpokea?

      21 Luka, mwandikaji wa Biblia, aliyeandamana na Paulo katika safari hiyo, anatuambia yaliyotukia: “Kutoka huko [Roma] akina ndugu, waliposikia habari juu yetu, wakaja kukutana nasi mpaka Soko la Apio na Mikahawa Mitatu.” Je, unaweza kuwazia yaliyotukia? Walipojua kwamba Paulo alikuwa anakuja, kikundi cha akina ndugu walisafiri kutoka Roma ili kukutana naye. Baadhi ya ndugu hao walikuwa wakimngojea katika Soko la Apio, kituo mashuhuri cha kupumzikia kilichokuwa umbali wa kilometa 74 hivi nje ya Roma. Ndugu wale wengine walikuwa wakimngojea kwenye Mikahawa Mitatu, kituo cha kupumzikia kilichokuwa umbali wa kilometa 58 hivi nje ya jiji. Paulo aliitikiaje? Luka anaripoti hivi: “Alipowaona, Paulo akamshukuru Mungu na kujipa moyo.” (Matendo 28:15) Hebu wazia jambo hilo, Paulo aliimarika na kutiwa moyo alipowaona ndugu hao waliojitahidi kufunga safari hiyo ndefu! Naye Paulo alimshukuru nani kwa msaada huo? Alimshukuru yule aliyehusika, Yehova Mungu.

      22. Andiko letu la mwaka wa 2005 ni lipi, na tutazungumzia nini katika makala inayofuata?

      22 Ni wazi kwamba yale ambayo Biblia husema kuhusu jinsi ambavyo Mungu alishughulika na watu huthibitisha kwamba yeye ni Msaidizi asiye na kifani. Kwa kufaa, andiko la Zaburi 121:2: “Msaada wangu unatoka kwa Yehova” litakuwa andiko la mwaka wa 2005 la Mashahidi wa Yehova. Lakini Yehova hutusaidiaje leo? Hilo litazungumziwa katika makala inayofuata.

      [Maelezo ya Chini]

      a Mtunga-mashairi Mroma Horace (65—8 K.W.K.), aliyesafiri katika njia hiyohiyo, alieleza kuhusu magumu ya sehemu ya mwisho ya safari hiyo. Horace alisema kwamba Soko la Apio lilikuwa “limesongamana na wenye mashua na wenye mikahawa wachoyo.” Alilalamika kuhusu “chawa na vyura waliolaaniwa” na maji “mabaya sana.”

  • Yehova Ni Msaidizi Wetu
    Mnara wa Mlinzi—2004 | Desemba 15
    • [Blabu katika ukurasa wa 15]

      Andiko la mwaka wa 2005 litakuwa: “Msaada wangu unatoka kwa Yehova.”—Zaburi 121:2.

  • Je, Wewe Hukubali Msaada wa Yehova?
    Mnara wa Mlinzi—2004 | Desemba 15
    • Je, Wewe Hukubali Msaada wa Yehova?

      “Yehova ni msaidizi wangu; sitaogopa.”—WAEBRANIA 13:6.

      1, 2. Kwa nini ni muhimu kukubali msaada na mwongozo wa Yehova maishani mwetu?

      HEBU wazia unapanda mlima fulani. Hata hivyo, huko peke yako, kwa kuwa mtu fulani amejitolea kuambatana nawe ili akuongoze, naye ni kiongozi bora sana. Yeye ana ujuzi na nguvu nyingi kuliko wewe, lakini yeye anatembea kando yako bila kulalamika. Anaona kwamba unajikwaa mara kwa mara. Kwa kuwa anajali usalama wako, anakunyoshea mkono ili kukusaidia kupita mahali hatari. Je, utakataa msaada wake? Hapana! Usalama wako uko hatarini.

      2 Tukiwa Wakristo, tuna njia ngumu ya kufuata. Je, ni lazima tutembee peke yetu katika barabara hiyo yenye nafasi ndogo? (Mathayo 7:14) La, Biblia inaonyesha kwamba tuna Kiongozi bora zaidi, Yehova Mungu, ambaye huwaruhusu wanadamu watembee pamoja naye. (Mwanzo 5:24; 6:9) Je, Yehova huwasaidia watumishi wake wanapotembea? Anasema: “Mimi, Yehova Mungu wako, ninaushika mkono wako wa kuume, Mwenye kukuambia, ‘Usiogope. Mimi mwenyewe nitakusaidia.’” (Isaya 41:13) Kama kiongozi aliyetajwa katika mfano wetu, kwa fadhili Yehova huwasaidia na huwa rafiki ya wale wanaojitahidi kutembea pamoja naye. Kwa kweli, hakuna hata mmoja wetu angetaka kukataa msaada wake!

      3. Tutachunguza maswali gani katika mazungumzo haya?

      3 Katika makala iliyotangulia, tulizungumzia njia nne ambazo Yehova alitumia kuwasaidia watu wake katika nyakati za kale. Je, yeye huwasaidia watu wake katika njia hizohizo leo? Na tunawezaje kuhakikisha kwamba tunakubali msaada wowote kati ya misaada hiyo? Acheni tuchunguze maswali hayo. Kwa kuyachunguza, tunaweza kuwa na uhakika zaidi kwamba Yehova ni Msaidizi wetu.—Waebrania 13:6.

      Msaada Kutoka kwa Malaika

      4. Kwa nini watumishi wa Mungu leo wanaweza kuwa na uhakika kwamba malaika wanawasaidia?

      4 Je, malaika huwasaidia watumishi wa Yehova leo? Ndiyo. Ni kweli kwamba leo malaika hawaonekani waziwazi ili kuwakomboa waabudu wa kweli kutokana na hatari. Hata katika nyakati za Biblia, walifanya hivyo mara chache sana. Kama ilivyo leo, mambo mengi waliyofanya hayakuonekana na wanadamu. Hata hivyo, watumishi wa Mungu walitiwa moyo sana walipojua kwamba malaika walikuwa tayari kuwasaidia. (2 Wafalme 6:14-17) Tuna sababu nzuri ya kuhisi vivyo hivyo.

      5. Biblia inaonyeshaje kwamba malaika wanahusika katika kazi ya kuhubiri leo?

      5 Malaika wa Yehova wanapendezwa hasa na kazi fulani ya pekee inayotuhusu. Ni kazi gani hiyo? Tunaweza kupata jibu katika andiko la Ufunuo 14:6: “Nikamwona malaika mwingine akiruka katikati ya mbingu, naye alikuwa na habari njema ya milele ili aitangaze kuwa habari za furaha kwa wale wanaokaa duniani, na kwa kila taifa na kabila na lugha na watu.” Hii “habari njema ya milele” inahusianishwa na “habari njema ya ufalme” ambayo kama Yesu alivyotabiri “itahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa ili kuwa ushahidi kwa mataifa yote” kabla ya mwisho wa mfumo huu wa mambo. (Mathayo 24:14) Bila shaka, malaika hawahubiri moja kwa moja. Yesu aliwapa wanadamu kazi hiyo muhimu. (Mathayo 28:19, 20) Je, si jambo lenye kutia moyo kujua kwamba tunapofanya kazi hiyo, tuna msaada wa malaika watakatifu, ambao ni viumbe wa roho wenye hekima na nguvu?

      6, 7. (a) Ni nini kinachoonyesha kwamba malaika wanatusaidia katika kazi yetu ya kuhubiri? (b) Tunaweza kufanya nini ili tuwe na uhakika wa kupokea msaada wa malaika wa Yehova?

      6 Kuna uthibitisho mwingi unaoonyesha kwamba malaika wanatusaidia katika kazi yetu. Kwa mfano, mara nyingi tunasikia kwamba Mashahidi wa Yehova walipokuwa wakihubiri walikutana na mtu fulani aliyekuwa ametoka tu kusali kwa Mungu amsaidie kupata kweli. Mambo hayo hutukia mara nyingi sana hivi kwamba hayawezi kupuuzwa kuwa mambo ya kawaida tu. Kwa sababu ya msaada huo wa malaika, watu wengi zaidi wanajifunza kufanya yale ambayo ‘malaika anayeruka katikati ya mbingu’ alitangaza: “Mwogopeni Mungu na kumpa utukufu.”— Ufunuo 14:7.

      7 Je, unatamani kupata msaada wa malaika wa Yehova wenye nguvu? Basi fanya yote uwezayo katika huduma yako. (1 Wakorintho 15:58) Tunapojitoa wenyewe kwa hiari kufanya kazi hii ya pekee kutoka kwa Yehova, tunaweza kuwa na uhakika wa kupokea msaada wa malaika wake.

      Msaada Kutoka kwa Mkuu wa Malaika

      8. Yesu ana cheo gani cha juu huko mbinguni, na kwa nini jambo hilo linatutia moyo?

      8 Yehova pia hutupatia msaada mwingine wa kimalaika. Andiko la Ufunuo 10:1 linamtaja ‘malaika mwenye nguvu’ ambaye “uso wake ulikuwa kama jua.” Ni wazi kwamba malaika huyo aliyeonwa katika maono anawakilisha Yesu Kristo aliyetukuzwa akiwa katika mamlaka ya kimbingu. (Ufunuo 1:13, 16) Je, kweli Yesu ni malaika? Ndiyo, katika maana fulani, kwa kuwa yeye ni malaika mkuu. (1 Wathesalonike 4:16) Yesu ndiye mwenye nguvu zaidi kati ya wana wote wa roho wa Yehova. Yehova amempa mamlaka juu ya jeshi Lake lote la kimalaika. Kwa kuwa yeye ni malaika mkuu, yeye ni chanzo cha msaada wenye nguvu nyingi kwelikweli. Katika njia zipi?

      9, 10. (a) Yesu anakuwaje “msaidizi” wetu tunapotenda dhambi? (b) Tunaweza kupata msaada gani katika kielelezo cha Yesu?

      9 Mtume Yohana aliyezeeka aliandika hivi: “Yeyote akitenda dhambi, tuna msaidizi kwa Baba, Yesu Kristo, mtu mwadilifu.” (1 Yohana 2:1) Kwa nini Yohana alidokeza kwamba Yesu ni “msaidizi” wetu hasa wakati ‘tunapotenda dhambi’? Sisi hutenda dhambi kila siku, nayo dhambi huongoza kwenye kifo. (Mhubiri 7:20; Waroma 6:23) Hata hivyo, Yesu alitoa uhai wake kuwa dhabihu kwa ajili ya dhambi zetu. Naye yuko kando ya Baba yetu mwenye rehema ili kutuombea. Sote tunahitaji msaada huo. Tunawezaje kuukubali? Tunahitaji kutubu dhambi zetu na kuomba msamaha kwa msingi wa dhabihu ya Yesu. Pia tunahitaji kuepuka kurudia dhambi zetu.

      10 Mbali na kufa kwa ajili yetu, Yesu alituwekea kielelezo kikamilifu. (1 Petro 2:21) Kielelezo chake hutuongoza na kutusaidia tuishi kwa njia ambayo tunaweza kuepuka dhambi nzito na hivyo kumpendeza Yehova Mungu. Tunafurahi sana kuwa na msaada huo. Yesu aliahidi kuwapa wafuasi wake msaada mwingine.

      Msaada wa Roho Takatifu

      11, 12. Roho ya Yehova ni nini, nayo ina nguvu kiasi gani, na kwa nini tunaihitaji leo?

      11 Yesu aliahidi hivi: “Nitamwomba Baba naye atawapa ninyi msaidizi mwingine awe pamoja nanyi milele, roho ya ile kweli, ambayo ulimwengu hauwezi kuipokea.” (Yohana 14:16, 17) “Roho ya ile kweli” au roho takatifu, si mtu bali ni nguvu, yaani nguvu ya utendaji ya Yehova. Nguvu hiyo haina mipaka. Ni nguvu ambayo Yehova alitumia kuumba ulimwengu, kufanya miujiza yenye kustaajabisha, na kufunua mapenzi yake kupitia maono. Kwa kuwa leo Yehova hatumii roho yake katika njia hizo hususa, je, hilo lamaanisha kwamba hatuhitaji nguvu hiyo?

      12 Sivyo kabisa! Katika ‘nyakati hizi za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo,’ tunahitaji roho ya Yehova zaidi kuliko wakati mwingine wowote. (2 Timotheo 3:1) Hiyo hutuimarisha kuvumilia majaribu. Inatusaidia kusitawisha sifa nzuri ambazo hutufanya tumkaribie Yehova na ndugu na dada zetu wa kiroho. (Wagalatia 5:22, 23) Hivyo basi, tunawezaje kufaidika na msaada huo bora kutoka kwa Yehova?

      13, 14. (a) Kwa nini tunaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova huwapa watu wake roho yake takatifu kwa kupenda? (b) Tunaweza kuonyesha kwa tendo gani kwamba kwa kweli hatukubali zawadi ya roho takatifu?

      13 Kwanza tunahitaji kusali tupewe roho takatifu. Yesu alisema: “Ikiwa ninyi, mjapokuwa waovu, mnajua jinsi ya kuwapa watoto wenu zawadi zilizo njema, je, Baba aliye mbinguni hatawapa hata zaidi roho takatifu wale wanaomwomba!” (Luka 11:13) Naam, Yehova ndiye Baba bora zaidi. Ikiwa tunamwomba kwa unyoofu na kwa imani atupe roho yake takatifu, kwa hakika atatupatia zawadi hiyo. Basi swali ni, Je, sisi humwomba roho takatifu? Tuna sababu nzuri ya kuomba roho hiyo kila siku tunaposali.

      14 Pili, tunakubali zawadi hiyo kwa kutenda kupatana nayo. Kwa mfano: Tuseme Mkristo anajaribu kuacha zoea la kutazama picha chafu. Amesali apewe roho takatifu ili imsaidie kushinda zoea hilo chafu. Ametafuta mashauri kutoka kwa wazee Wakristo, nao wamemshauri achukue hatua thabiti na hata aepuke kukaribia mambo hayo machafu. (Mathayo 5:29) Namna gani akipuuza mashauri yao na kuendelea kutazama picha chafu anaposhawishiwa? Je, anatenda kupatana na sala yake kwamba roho takatifu imsaidie? Au badala yake, je, anaelekea kukabili hatari ya kuhuzunisha roho ya Mungu na kupoteza zawadi hiyo? (Waefeso 4:30) Kwa kweli, sote tunahitaji kufanya yote tuwezayo ili kuhakikisha kwamba tunaendelea kupokea msaada huo bora kutoka kwa Yehova.

      Msaada Kutoka kwa Neno la Mungu

      15. Tunawezaje kuonyesha kwamba hatuioni Biblia kuwa kitabu cha kawaida tu?

      15 Biblia imewasaidia watumishi waaminifu wa Yehova kwa karne nyingi. Badala ya kuiona Biblia kuwa kitabu cha kawaida tu, tunahitaji kukumbuka kwamba kitabu hicho ni chanzo chenye nguvu cha msaada. Jitihada inahitajiwa ili kukubali msaada huo. Tunapaswa kuwa na ratiba ya kusoma Biblia kwa ukawaida.

      16, 17. (a) Zaburi 1:2, 3 inaelezaje thawabu za kusoma sheria ya Mungu? (b) Zaburi 1:3 inaonyeshaje kwamba tunapaswa kufanya kazi kwa bidii?

      16 Zaburi 1:2, 3 inasema hivi kumhusu mtu anayempendeza Mungu: “Mapendezi yake ni katika sheria ya Yehova, naye huisoma sheria yake kwa sauti ya chini mchana na usiku. Naye hakika atakuwa kama mti uliopandwa kando ya vijito vya maji, ambao hutoa matunda yake katika majira yake na ambao majani yake hayanyauki, na kila jambo analofanya litafanikiwa.” Je, unaona jambo lililo muhimu zaidi katika mistari hiyo? Ni rahisi kusoma maneno hayo na kukata kauli kwamba yanafafanua tu hali nzuri yenye utulivu, yaani, mti wenye kivuli unaokua kando ya mto. Ingeburudisha kama nini kulala kidogo chini ya mti huo wakati wa alasiri! Lakini zaburi hii haitutii moyo tufikirie kupumzika. Inazungumzia kufanya kazi kwa bidii. Jinsi gani?

      17 Ona kwamba mti unaotajwa hapa si mti wa kivuli ambao umekua wenyewe tu kando ya mto. Ni mti unaozaa matunda, “uliopandwa” mahali fulani palipochaguliwa, yaani, “kando ya vijito vya maji.” Mti mmoja ungewezaje kukua karibu na vijito vingi vya maji? Katika shamba la miti ya matunda, huenda mwenye shamba akachimba mitaro ya kuleta maji kwenye mizizi ya miti hiyo yenye thamani. Ah! sasa jambo hilo liko wazi kabisa. Ikiwa katika maana ya kiroho tunasitawi kama mti huo, ni kwa kuwa mtu fulani amefanya kazi nyingi ili kutusaidia. Tunashirikiana na tengenezo ambalo linatuletea maji safi ya kweli, lakini lazima tutimize sehemu yetu. Tunahitaji kufyonza maji hayo yenye thamani kwa kutafakari na kufanya utafiti unaohitajiwa ili kweli za Neno la Mungu zipenye katika akili na moyo wetu. Kwa kufanya hivyo, sisi pia tutazaa matunda mazuri.

      18. Tunahitaji kufanya nini ili kupata majibu ya Biblia kwa maswali yetu?

      18 Biblia haiwezi kutufaidi ikiwa hatuisomi. Hiyo si hirizi, kwani hatuwezi tu kufumba na kufumbua macho na kutazamia Biblia ijifungue na kujibu swali letu. Tunapokabili maamuzi, tunahitaji kuchimba kana kwamba tunachimba hazina iliyofichwa ili kupata “kumjua Mungu.” (Methali 2:1-5) Mara nyingi, tunahitaji kufanya utafiti kwa bidii na kwa makini ili tupate shauri la Biblia linalozungumzia mahitaji yetu hususa. Tuna vichapo vingi vya Biblia vinavyoweza kutusaidia katika utafiti wetu. Tunapotumia vichapo hivyo kuchimba kwa bidii hekima ya Neno la Mungu ambayo ni kama mawe ya thamani, tunafaidika kikweli na msaada wa Yehova.

      Msaada Kupitia Waamini Wenzetu

      19. (a) Kwa nini huenda makala fulani katika Mnara wa Mlinzi na Amkeni! zikaonwa kuwa msaada ulioandaliwa kupitia waamini wenzetu? (b) Umesaidiwaje na makala fulani katika mojawapo ya magazeti yetu?

      19 Sikuzote watumishi wa Yehova duniani wamekuwa wakisaidiana. Je, Yehova amebadilika? Hata kidogo. Bila shaka, sote tunaweza kukumbuka pindi ambazo tulipokea msaada tuliohitaji kutoka kwa waamini wenzetu kwa wakati unaofaa. Kwa mfano, je, unaweza kukumbuka makala fulani katika Mnara wa Mlinzi au Amkeni! ambayo ilikufariji ulipohitaji faraja au ilikusaidia kutatua tatizo fulani au kukabiliana na jaribu la imani yako? Yehova alikupa msaada huo kupitia “mtumwa mwaminifu na mwenye busara” ambaye amepewa kazi ya kuandaa ‘chakula kwa wakati unaofaa.’—Mathayo 24:45-47.

      20. Wazee Wakristo huwa “zawadi katika wanadamu” katika njia zipi?

      20 Hata hivyo, mara nyingi sisi hupokea msaada wa moja kwa moja kutoka kwa waamini wenzetu. Mzee Mkristo anatoa hotuba inayotuchochea, au anafanya ziara ya uchungaji inayotusaidia kukabiliana na hali ngumu, au anatupa shauri lenye fadhili linalotusaidia kutambua na kushinda udhaifu fulani. Mkristo mmoja mwenye shukrani aliandika hivi kuhusu msaada aliopewa na mzee fulani: “Tukiwa katika huduma ya shambani alinitia moyo nieleze yaliyokuwa moyoni mwangu. Usiku uliotangulia, nilisali kwa Yehova, nikimwomba anipe mtu wa kuongea naye. Siku iliyofuata, ndugu huyo aliongea nami kwa huruma. Alinisaidia nione jinsi ambavyo Yehova amekuwa akinisaidia kwa miaka mingi. Ninamshukuru Yehova kwa kumtuma mzee huyo kwangu.” Katika njia hizo zote, wazee Wakristo huonyesha kwamba wao ni “zawadi katika wanadamu” zinazoandaliwa na Yehova kupitia Yesu Kristo ili kutusaidia tuendelee kutembea katika barabara ya uzima.—Waefeso 4:8.

      21, 22. (a) Kunakuwa na matokeo gani washiriki wa kutaniko wanapofuata shauri la Wafilipi 2:4? (b) Kwa nini hata matendo madogo ya fadhili ni muhimu?

      21 Mbali na wazee, kila Mkristo mwaminifu anataka kufuata amri iliyoongozwa na roho ya Mungu ya kuendelea ‘kuangalia, si faida za kibinafsi za mambo yake mwenyewe tu, bali pia faida za kibinafsi za wengine.’ (Wafilipi 2:4) Wale walio katika kutaniko la Kikristo wanapofuata shauri hilo, kunakuwa na matendo mazuri ya fadhili. Kwa mfano, familia moja ilipatwa na misiba kadhaa kwa ghafula. Baba alikuwa amempeleka binti yake mchanga dukani. Walipokuwa wakirudi nyumbani, walipatwa na aksidenti ya gari. Binti huyo alikufa; naye baba akajeruhiwa vibaya sana. Alipotoka hospitali, alikuwa amelemaa sana hivi kwamba hangeweza kujifanyia chochote. Mke wake alikuwa amefadhaika sana kihisia-moyo hivi kwamba hangeweza kumtunza akiwa peke yake. Hivyo, wenzi fulani wa ndoa katika kutaniko waliwachukua na kuwapeleka nyumbani kwao na kuwatunza kwa majuma kadhaa.

      22 Bila shaka, matendo yote ya fadhili hayahusu tu misiba kama hiyo na kujidhabihu. Msaada fulani tunaopokea ni mdogo zaidi. Lakini hata kama tendo la fadhili ni dogo sana, tunalithamini, sivyo? Je, unaweza kufikiria pindi ambazo ulipata msaada uliohitaji kupitia neno au tendo fulani la fadhili kutoka kwa ndugu au dada? Mara nyingi Yehova hututunza katika njia kama hizo.—Methali 17:17; 18:24.

      23. Yehova huonaje jitihada zetu za kusaidiana?

      23 Je, ungependa Yehova akutumie kuwasaidia wengine? Unaweza kuwa na pendeleo hilo. Kwa kweli, Yehova anathamini jitihada unayofanya kusaidia. Neno lake linasema hivi: “Anayemwonyesha kibali mtu wa hali ya chini anamkopesha Yehova, na Yeye atamlipa matendo yake.” (Methali 19:17) Tunapata shangwe nyingi tunapojitolea kuwasaidia ndugu na dada zetu. (Matendo 20:35) Wale wanaojitenga kimakusudi na wengine hawapati shangwe inayotokana na kusaidia au kitia-moyo kinachotokana na kupokea msaada. (Methali 18:1) Kwa hiyo, na tukutanike kwa uaminifu na kwa ukawaida katika mikutano ya Kikristo ili tutiane moyo.—Waebrania 10:24, 25.

      24. Kwa nini hatupaswi kuhisi kwamba tunakosa chochote kwa sababu hatujashuhudia miujiza yenye kustaajabisha ambayo Yehova alifanya zamani?

      24 Inapendeza kama nini kutafakari njia ambazo Yehova hutumia kutusaidia. Ingawa hatuishi wakati ambao Yehova anafanya miujiza yenye kustaajabisha ili kutimiza makusudi yake, hatupaswi kuhisi kuwa tunakosa chochote. Jambo muhimu ni kwamba Yehova anatupatia msaada wowote tunaohitaji ili tuendelee kuwa waaminifu. Na tukivumilia pamoja katika imani, tutashuhudia matendo matukufu na yenye kustaajabisha ya Yehova katika historia yote! Basi na tuazimie kukubali na kutumia kabisa msaada wenye upendo kutoka kwa Yehova ili tuonyeshe kwamba tunakubaliana na maneno haya ya andiko letu la mwaka wa 2005: “Msaada wangu unatoka kwa Yehova.”—Zaburi 121:2.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki