-
“Mkaribieni Mungu”Mnara wa Mlinzi—2002 | Desemba 15
-
-
“Mkaribieni Mungu”
“Mkaribieni Mungu, naye atawakaribia.”—YAKOBO 4:8.
1, 2. (a) Wanadamu hudai nini mara kwa mara? (b) Yakobo alitoa ushauri gani, na kwa nini ulihitajika?
“MUNGU yu pamoja nasi.” Maneno hayo yamepamba nembo za kitaifa na hata yunifomu za askari. Maneno “twamtumaini Mungu” yameandikwa kwenye sarafu na noti nyingi sana za kisasa. Ni kawaida kwa wanadamu kudai kwamba wana uhusiano wa karibu na Mungu. Hata hivyo, je, hungekubali kwamba ili kuwa na uhusiano huo na Mungu tunahitaji kufanya mengi zaidi ya kusema au kuandika maneno tu?
2 Biblia inaonyesha kwamba inawezekana kuwa na uhusiano pamoja na Mungu. Hata hivyo, jitihada zinahitajiwa. Hata Wakristo fulani watiwa-mafuta wa karne ya kwanza walihitaji kuimarisha uhusiano wao pamoja na Yehova Mungu. Mwangalizi Mkristo Yakobo alilazimika kuwashauri baadhi yao kuhusu mielekeo ya kimwili na ukosefu wa usafi wa kiroho. Aliambatanisha ushauri huo na himizo hili lenye nguvu: “Mkaribieni Mungu, naye atawakaribia.” (Yakobo 4:1-12) Yakobo alimaanisha nini aliposema “mkaribieni”?
3, 4. (a) Huenda maneno ya Yakobo “mkaribieni Mungu” yakawa yaliwakumbusha nini wale waliosoma barua yake katika karne ya kwanza? (b) Kwa nini tunaweza kuwa na hakika kwamba inawezekana kumkaribia Mungu?
3 Yakobo alitumia usemi uliofahamika na wengi waliosoma barua yake. Sheria ya Musa iliwapa makuhani maagizo hususa kuhusu “kumkaribia” Yehova kwa niaba ya watu wake. (Kutoka 19:22) Hivyo, huenda ikawa Yakobo aliwakumbusha wasomaji wa barua yake kwamba kumkaribia Yehova ni jambo linalopaswa kuchukuliwa kwa uzito. Yehova peke yake ndiye mwenye cheo kilichotukuka zaidi ulimwenguni.
4 Kwa upande mwingine, kama vile msomi mmoja wa Biblia anavyosema, “himizo hilo [la andiko la Yakobo 4:8] linatoa tumaini kubwa.” Yakobo alijua kwamba siku zote Yehova amewaalika wanadamu wasio wakamilifu wamkaribie. (2 Mambo ya Nyakati 15:2) Dhabihu ya Yesu imewawezesha kumkaribia Yehova kikamili zaidi. (Waefeso 3:11, 12) Leo, mamilioni ya watu wana fursa ya kumkaribia Mungu! Lakini, tunaweza kufanyaje ili kutumia fursa hiyo nzuri? Tutachunguza kwa ufupi njia tatu zinazoweza kutusaidia kumkaribia Yehova Mungu.
Endeleeni “Kutwaa Ujuzi” Juu ya Mungu
5, 6. Mfano wa kijana Samweli unaonyeshaje maana ya “kuendelea kutwaa ujuzi” juu ya Mungu?
5 Kulingana na Yohana 17:3, Yesu alisema: ‘Hii yamaanisha uhai udumuo milele, wao kuendelea kutwaa ujuzi juu yako wewe, Mungu pekee wa kweli, na juu ya yule uliyemtuma, Yesu Kristo.’ Biblia nyingi zinatafsiri andiko hilo kwa njia iliyo tofauti kidogo na tafsiri ya New World Translation. Biblia hizo zinataja tu “kumjua” Mungu badala ya kusema “kuendelea kutwaa ujuzi” juu ya Mungu. Hata hivyo, wasomi kadhaa wanasema kwamba neno lililotumiwa katika Kigiriki cha awali lina maana pana zaidi—linamaanisha tendo linaloendelea, ambalo linaweza kumsaidia mtu amjue mwingine kwa undani zaidi.
6 Katika siku za Yesu watu walielewa maana ya kumjua Mungu kwa undani zaidi. Kwa mfano, tunasoma katika Maandiko ya Kiebrania kwamba Samweli “alikuwa hamjui BWANA bado” alipokuwa kijana. (1 Samweli 3:7) Je, hilo lilimaanisha kwamba Samweli alijua mambo machache tu kumhusu Mungu? La. Bila shaka, wazazi wake na makuhani walikuwa wamemfundisha mambo mengi. Lakini msomi mmoja anasema kwamba neno la Kiebrania lililotumiwa katika mstari huo linaweza “kumaanisha kumjua mtu kwa undani zaidi.” Hivyo Samweli hakuwa amemjua Yehova kwa undani zaidi, kama alivyokuja kumjua alipokuwa akitumika akiwa msemaji wake. Samweli alipozidi kukua, alikuja kumjua Yehova vizuri, na kuwa na uhusiano wa karibu pamoja naye.—1 Samweli 3:19, 20.
7, 8. (a) Kwa nini hatupaswi kuogopa kujifunza mambo yenye kina ya Biblia? (b) Ni kweli gani zenye kina za Neno la Mungu tunazopaswa kujifunza?
7 Je, unaendelea kutwaa ujuzi juu ya Yehova ili umjue kwa undani zaidi? Ili kufanya hivyo, unahitaji ‘kufanyiza hamu’ ya chakula cha kiroho ambacho Mungu hutoa. (1 Petro 2:2) Usitosheke tu kujua mambo ya msingi. Jitahidi kujifunza mambo yenye kina ya Biblia. (Waebrania 5:12-14) Je, unaogopa kujifunza mambo hayo, ukiyaona kuwa magumu mno? Ikiwa ndivyo, kumbuka kwamba Yehova ndiye “Mfundishaji Mkuu.” (Isaya 30:20, NW) Anajua jinsi ya kuwafundisha kweli zenye kina wanadamu wasio wakamilifu. Naye anaweza kubariki jitihada zako za unyofu za kutaka kuelewa mambo anayokufundisha.—Zaburi 25:4.
8 Kwa nini usijichunguzie baadhi ya “mambo yenye kina kirefu ya Mungu”? (1 Wakorintho 2:10) Hayo si mambo yasiyopendeza kama yale yanayozungumziwa na wanatheolojia na makasisi fulani. Hayo ni mafundisho yanayofaa ambayo yanaweza kutusaidia kujifunza mambo yenye kupendeza kuhusu akili na moyo wa Baba yetu mwenye upendo. Kwa mfano, inafurahisha na kunufaisha kujifunza na kufanya utafiti kuhusu fidia, “siri takatifu,” maagano mbalimbali ambayo Yehova alitumia kulinda watu wake na kutimiza makusudi yake, na pia mambo mengine yanayohusiana na hayo. —1 Wakorintho 2:7.
9, 10. (a) Kwa nini kiburi ni hatari, na nini kitakachotusaidia kukiepuka? (b) Kwa nini tunapaswa kujitahidi kuwa wanyenyekevu kuhusiana na ujuzi juu ya Yehova?
9 Unapoendelea kuongeza ujuzi wa kweli za kiroho zenye kina, jihadhari na hatari ambayo huenda ikaambatana na ujuzi—kiburi. (1 Wakorintho 8:1) Kiburi ni hatari kwa kuwa hututenganisha na Mungu. (Mithali 16:5; Yakobo 4:6) Kumbuka, hakuna mtu anayepaswa kujigamba kwa sababu ana ujuzi. Kwa mfano, fikiria maneno haya yaliyonukuliwa kutoka katika utangulizi wa kitabu kimoja kinachochanganua maendeleo ya mwanadamu ya kisayansi ya karibuni zaidi: “Kadiri ujuzi wetu uongezekavyo, ndivyo tuzidivyo kutambua kwamba tuna ujuzi kidogo sana. . . . Yote tuliyojifunza ni bure yakilinganishwa na yale ambayo bado hatujajifunza.” Sifa hiyo ya unyenyekevu inatia moyo. Hivyo, tuna sababu kubwa zaidi ya kuwa wanyenyekevu hasa kuhusiana na ujuzi ulio mkubwa zaidi—ujuzi juu ya Yehova Mungu. Kwa nini?
10 Ona vile Biblia inavyosema kumhusu Yehova. “Mawazo yako ni mafumbo makubwa.” (Zaburi 92:5) “Akili za [Yehova] hazina mipaka.” (Zaburi 147:5) “Akili za [Yehova] hazichunguziki.” (Isaya 40:28) “Lo! kina cha utajiri wa Mungu na hekima na ujuzi!” (Waroma 11:33) Ni wazi kwamba hatuwezi kumjua Yehova kabisa. (Mhubiri 3:11) Ametufundisha mambo mengi mazuri, hata hivyo sikuzote tutakuwa na habari chungu nzima za kujifunza kumhusu. Je, tazamio hilo halitusisimui na kutunyenyekeza? Basi, tunapojifunza sikuzote na tutumie ujuzi wetu kama msingi wa kumkaribia Yehova na kuwasaidia wengine wafanye hivyo, na tusiutumie kamwe kama njia ya kujisifu mbele za wengine.—Mathayo 23:12; Luka 9:48.
Onyesha Upendo Wako kwa Yehova
11, 12. (a) Mambo tunayojifunza kumhusu Yehova yapasa kuwa na matokeo gani kwetu? (b) Ni nini kinachoonyesha kama mtu anampenda Mungu kikweli?
11 Kwa kufaa, mtume Paulo alihusianisha ujuzi na upendo. Aliandika: “Hili ndilo mimi huendelea kusali, kwamba upendo wenu upate kuzidi bado hata zaidi na zaidi pamoja na ujuzi sahihi na ufahamu kamili.” (Wafilipi 1:9) Kila kweli yenye thamani tunayojifunza kumhusu Yehova na makusudi yake inapasa kuzidisha upendo wetu kwa Baba yetu wa mbinguni bali si kutututumua kwa kiburi.
12 Hapana shaka kwamba wengi wanaodai kuwa wanampenda Mungu hawampendi kwa kweli. Huenda mioyo yao imejaa hisia zenye nguvu kumhusu Mungu. Hisia hizo ni nzuri, hata zenye kusifika, zinapopatana na ujuzi sahihi. Lakini hisia peke yake hazitoshi kuonyesha kwamba tunampenda Mungu kikweli. Kwa nini? Ona jinsi Neno la Mungu linavyofafanua upendo huo: “Hivi ndivyo kumpenda Mungu humaanisha, kwamba tushike amri zake.” (1 Yohana 5:3) Basi, tunaonyesha kwamba tunampenda Yehova kikweli kupitia kutii kwa vitendo.
13. Kumwogopa Yehova kutatusaidiaje kumwonyesha upendo?
13 Kumwogopa Yehova kutatusaidia tumtii. Kuendelea kutwaa ujuzi juu ya Yehova, kujifunza juu ya utakatifu wake, utukufu, uwezo, haki, hekima, na upendo wake usio na mipaka, kutafanya tumwogope na kumheshimu sana. Woga huo ni muhimu ili kumkaribia. Ona andiko la Zaburi 25:14, Zaire Swahili Bible linavyosema: “Siri ya BWANA ni pamoja nao wanaomwogopa.” Kwa hiyo, tunaweza kumkaribia Baba yetu mpendwa wa mbinguni ikiwa tuna woga unaofaa wa kutomchukiza. Kumwogopa Mungu kutatusaidia kufuata ushauri wa hekima unaopatikana kwenye Mithali 3:6: “Katika njia zako zote mkiri yeye, naye atayanyosha mapito yako.” Hiyo inamaanisha nini?
14, 15. (a) Tunakabili maamuzi gani kila siku? (b) Tunawezaje kufanya maamuzi kwa njia inayoonyesha kwamba tunamwogopa Mungu?
14 Ni lazima ufanye maamuzi kila siku, makubwa kwa madogo. Kwa mfano, utazungumzia nini pamoja na wafanyakazi, wanashule, na majirani wako? (Luka 6:45) Je, utafanya kazi uliyopewa kwa bidii, au utatafuta mbinu za kufanya kazi polepole ili kupisha wakati? (Wakolosai 3:23) Je, utakuwa na uhusiano wa karibu na wale wasiompenda Yehova, au utajitahidi kuimarisha uhusiano wako na watu wa kiroho? (Mithali 13:20) Utafanya nini, hata katika mambo madogo-madogo ili kuendeleza mambo yanayohusiana na Ufalme wa Mungu? (Mathayo 6:33) Ikiwa kanuni kama hizi za Kimaandiko zilizotajwa hapa zitakuongoza unapofanya maamuzi yako ya kila siku, basi hapana shaka kwamba unamkiri Yehova “katika njia zako zote.”
15 Tunapaswa kufikiria mambo haya kila tunapofanya uamuzi: ‘Yehova angetaka nifanye nini? Ni mwenendo gani ambao ungempendeza zaidi?’ (Mithali 27:11) Kuonyesha woga wetu kwa Mungu kwa njia hiyo, ni njia bora sana ya kudhihirisha upendo wetu kwake. Kumwogopa Mungu pia kutatuchochea tuendelee kuwa safi—kiroho, kiadili, na kimwili. Kumbuka kwamba mbali na kuwahimiza Wakristo ‘wamkaribie Mungu,’ Yakobo anawahimiza hivi katika mstari huohuo: “Safisheni mikono yenu, nyinyi watenda-dhambi, na takaseni mioyo yenu, nyinyi wenye kusitasita kuamua.”—Yakobo 4:8.
16. Ni nini ambacho hatuwezi kutimiza hata tukimpa Yehova mali, wakati, na nguvu zetu, lakini tunaweza kufanikiwa kufanya nini?
16 Bila shaka, kuonyesha upendo kwa Yehova kunatia ndani mengi zaidi ya kuepuka maovu tu. Upendo pia hutuchochea kufanya yaliyo mema. Kwa mfano, tunaitikiaje ukarimu mwingi ambao Yehova ametuonyesha? Yakobo aliandika: “Kila zawadi njema na kila upaji mkamilifu ni kutoka juu, kwa maana huteremka kutoka kwa Baba wa mianga ya kimbingu.” (Yakobo 1:17) Ni kweli kwamba tunapompa Yehova mali zetu, hatumtajirishi kwa kuwa vitu vyote ni mali yake. (Zaburi 50:12) Na tunapompa Yehova wakati na nguvu zetu, hiyo haimaanishi kwamba tunatimiza uhitaji asioweza kutimiza. Hata kama tungekataa kuhubiri habari njema ya Ufalme wa Mungu, angefanya mawe yapaaze sauti! Kwa nini basi tumpe Yehova mali, wakati na nguvu zetu? Hasa ni kwa sababu kwa kufanya hivyo tunaonyesha tunampenda kwa moyo, nafsi, akili, na nguvu zetu zote.—Marko 12:29, 30.
17. Ni nini kinachoweza kutuchochea tumpe Yehova kwa uchangamfu?
17 Tunapompa Yehova, tunapaswa kufanya hivyo kwa furaha, “kwa maana Mungu hupenda mpaji mchangamfu.” (2 Wakorintho 9:7) Kanuni inayopatikana kwenye Kumbukumbu la Torati 16:17 inaweza kutusaidia kutoa kwa uchangamfu: ‘Kila mtu atoe kama awezavyo, kwa kadiri ya baraka ya BWANA, Mungu wake, alivyompa.’ Tunapotafakari ukarimu wa Yehova kwetu, sisi hutamani kumpa kwa uchangamfu na kwa ukarimu. Utoaji huo humfurahisha moyo, kama vile mzazi anavyofurahia zawadi ndogo kutoka kwa mtoto wake mpendwa. Kuonyesha upendo wetu kwa njia hiyo kutatusaidia kumkaribia Yehova.
Sitawisha Uhusiano wa Karibu Kupitia Sala
18. Kwa nini inafaa kufikiria jinsi ya kuboresha sala zetu?
18 Tunakuwa na fursa muhimu sana tunaposali faraghani—fursa ya kuwa na mazungumzo ya faragha na ya kindani pamoja na Baba yetu wa mbinguni. (Wafilipi 4:6) Kwa kuwa sala ni njia muhimu ya kumkaribia Mungu, inafaa kutua kidogo na kufikiria ubora wa sala zetu. Si lazima sala hilo ziwe na maneno ya ufasaha yenye mpangilio wa kipekee, lakini zinapaswa kuwa za unyofu, zinazotoka moyoni. Tunawezaje kuboresha sala zetu?
19, 20. Kwa nini tutafakari kabla ya kusali, na inafaa kutafakari juu ya mambo gani?
19 Tunaweza kujaribu kutafakari kabla ya kusali. Tukitafakari mapema, tunaweza kutoa sala zinazotaja mambo hususa na yenye maana na hivyo kuepuka kurudia-rudia maneno fulani tunayokumbuka kwa urahisi. (Mithali 15: 28, 29) Huenda ikasaidia kutafakari mambo fulani ambayo Yesu alitaja katika sala yake ya kielelezo na kisha kufikiria jinsi mambo hayo yanavyohusiana na hali zetu. (Mathayo 6:9-13) Kwa mfano, huenda tukajiuliza tunataka kutimiza sehemu gani ndogo kuhusiana na mapenzi ya Yehova hapa duniani. Je, tunaweza kumweleza Yehova kwamba tunatamani kutumiwa naye kikamili na kumwomba atusaidie kutimiza migawo yoyote ambayo ametupatia? Je, mahitaji yetu ya kimwili yanatuhangaisha sana? Tunahitaji msamaha kwa dhambi gani, na tunahitaji kuwasamehe zaidi watu gani? Tunakabili vishawishi gani, na je, tunatambua kwamba tunahitaji ulinzi wa Yehova haraka ili kukabiliana na vishawishi hivyo?
20 Zaidi ya hayo, tunaweza kuwafikiria watu ambao tunajua wanahitaji msaada hususa kutoka kwa Yehova. (2 Wakorintho 1:11) Hata hivyo, hatupaswi kusahau kwamba tunahitaji kutoa shukrani. Tukitua kidogo na kufikiria jambo hilo, bila shaka tunaweza kupata sababu nyingi za kumshukuru na kumsifu Yehova kila siku kwa wema wake mwingi. (Kumbukumbu la Torati 8:10; Luka 10:21) Kufanya hivyo kunatunufaisha sana—kunaweza kutusaidia kuwa na mwelekeo unaofaa na kuwa wenye shukrani kuhusu maisha.
21. Ni mifano gani ya Kimaandiko tunayoweza kuchunguza ili itusaidie tunapomfikia Yehova kwa sala?
21 Kujifunza pia kunaweza kuboresha sala zetu. Katika Neno la Mungu, kuna sala nzuri sana zilizotolewa na wanaume na wanawake waaminifu. Kwa mfano, ikiwa tunakabili tatizo gumu, linalotutia wasiwasi na hata kutufanya tuhofie hali yetu au ya wapendwa wetu, tunaweza kuchunguza kwa makini sala ambayo Yakobo alitoa kabla ya kukutana na ndugu yake Esau, aliyetaka kulipiza kisasi. (Mwanzo 32:9-12) Au tunaweza pia kuchunguza sala iliyotolewa na Mfalme Asa wakati jeshi la Waethiopia milioni moja lilipotisha kuwashambulia watu wa Mungu. (2 Mambo ya Nyakati 14:11, 12) Ikiwa tuna tatizo linalotusumbua ambalo linaweza kuleta suto kwa jina zuri la Yehova, basi inafaa tuchunguze sala ambayo Eliya alitoa mbele ya waabudu wa Baali kwenye Mlima Karmeli. Inafaa pia kuchunguza sala ya Nehemia kuhusu hali mbaya ya Yerusalemu. (1 Wafalme 18:36, 37; Nehemia 1:4-11) Kusoma na kutafakari sala hizo kunaweza kuimarisha imani yetu na kutusaidia kuona jinsi tunavyoweza kumweleza Yehova mahangaiko yanayotulemea.
22. Andiko la mwaka wa 2003 ni gani, na tunaweza kujiuliza maswali gani mara kwa mara katika mwaka huo wote?
22 Bila shaka, hakuna jambo lenye kuleta heshima na hakuna mradi ulio mkubwa kuliko kutii maneno ya Yakobo ya ‘kumkaribia Mungu.’ (Yakobo 4:8) Na tufanye hivyo kwa kuendelea kutwaa ujuzi juu ya Mungu, kwa kujitahidi kumwonyesha upendo zaidi, na kwa kusitawisha urafiki pamoja naye kupitia sala. Tufikiriapo andiko la Yakobo 4:8 katika mwaka wote wa 2003, na tuendelee kujichunguza tuone kama kwa kweli tunamkaribia Yehova. Namna gani sehemu ya pili ya andiko hilo? Ni katika maana gani Yehova ‘atakukaribia,’ akikuletea baraka gani? Makala inayofuata itazungumzia jambo hilo.
-
-
“Naye Atawakaribia”Mnara wa Mlinzi—2002 | Desemba 15
-
-
“Naye Atawakaribia”
“[Mungu] hayuko mbali sana na kila mmoja wetu.”—MATENDO 17:27.
1, 2. (a) Tunapotazama anga lililojaa nyota, tunaweza kuuliza maswali gani kumhusu Muumba? (b) Biblia hutuhakikishiaje kwamba wanadamu ni wenye thamani sana machoni pa Yehova?
JE, UMEWAHI kutazama anga lililojaa nyota usiku usiokuwa na mawingu na kustaajabu? Idadi hiyo kubwa ya nyota na ukubwa wa anga unastaajabisha. Katika ulimwengu huu mkubwa, dunia ni kama doa tu. Je, hilo linamaanisha kwamba Muumba, ‘Aliye juu, juu ya nchi yote,’ yuko juu sana asiweze kujishughulisha na wanadamu, au yuko mbali sana asiweze kueleweka au kufahamiwa na wanadamu?—Zaburi 83:18.
2 Biblia yatuhakikishia kwamba wanadamu ni wenye thamani sana machoni pa Yehova. Hata Neno la Mungu hututia moyo tumtafute, likisema: “Yeye hayuko mbali sana na kila mmoja wetu.” (Matendo 17:27; 1 Mambo ya Nyakati 28:9) Naam, tukichukua hatua kumkaribia Mungu, atatenda kulingana na jitihada zetu. Kwa njia gani? Maneno ya andiko letu la mwaka wa 2003 hutoa jibu hili lenye kutia moyo: “Naye atawakaribia.” (Yakobo 4:8) Na tuzungumzie baadhi ya baraka ambazo Yehova huwamwagia wale wanaomkaribia.
Zawadi Kutoka kwa Yehova Mwenyewe
3. Yehova huwapa wale wanaomkaribia zawadi gani?
3 Kwanza, watumishi wa Yehova wana zawadi yenye thamani ambayo ameitenga kwa ajili ya watu wake. Uwezo, mali, au elimu ambazo ulimwengu huu unatoa haziwezi kumsaidia mtu kupata zawadi hiyo. Hiyo ni zawadi kutoka kwa Yehova mwenyewe, naye huwapa wale wanaomkaribia. Hiyo ni zawadi gani? Neno la Mungu linajibu: ‘Ukipaza sauti yako upate ufahamu; ukiutafuta kama fedha, na kuutafutia kama hazina iliyositirika; ndipo utakapofahamu kumcha BWANA, na kupata kumjua Mungu. Kwa kuwa BWANA huwapa watu hekima.’ (Mithali 2:3-6) Hebu wazia wanadamu wasio wakamilifu wakiwa na uwezo wa “kumjua Mungu”! Zawadi hiyo—ujuzi unaopatikana katika Neno la Mungu—inalinganishwa na “hazina iliyositirika.” Kwa nini?
4, 5. Kwa nini “kumjua Mungu” kunaweza kulinganishwa na “hazina iliyositirika”? Toa mfano.
4 Sababu moja ni kwamba kumjua Mungu kuna thamani kubwa. Mojawapo ya baraka zenye thamani zaidi za kumjua Mungu ni taraja la uhai udumuo milele. (Yohana 17:3) Lakini ujuzi huo huboresha maisha yetu hata sasa. Kwa mfano, kutokana na uchunguzi wa makini wa Neno la Mungu, tumejibiwa maswali muhimu kama: Mungu anaitwa nani? (Zaburi 83:18) Wafu wako katika hali gani? (Mhubiri 9:5, 10) Kusudi la Mungu ni nini kwa dunia na wanadamu? (Isaya 45:18) Tumekuja kujua kwamba njia bora ya maisha ni kufuata ushauri wenye hekima wa Biblia. (Isaya 30:20, 21; 48:17, 18) Hivyo, tuna mwongozo mzuri unaotusaidia kukabili mahangaiko ya maisha na kujiendesha katika njia inayoleta furaha na uradhi. Zaidi ya yote, kujifunza Neno la Mungu kumetuwezesha kujua sifa nzuri za Yehova na kumkaribia. Je, kuna kitu kingine chochote chenye thamani zaidi ya kuwa na uhusiano wa karibu pamoja na Yehova unaotokana na “kumjua”?
5 Kuna sababu nyingine inayoweza kufanya tulinganishe kumjua Mungu na “hazina iliyositirika.” Kama ilivyo na hazina nyingi, ujuzi huo haupatikani kwa urahisi. Kati ya wakazi wa dunia bilioni sita, waabudu wa Yehova wapatao milioni sita au karibu mtu mmoja kati ya kila watu 1,000 ndio wamepata “kumjua Mungu.” Ili kudhihirisha kwamba kujua kweli ya Neno la Mungu ni pendeleo la pekee, fikiria swali hili moja tu la Biblia: Ni nini hupata wanadamu wanapokufa? Kulingana na Maandiko, tunajua kwamba nafsi hufa na wafu hawafahamu lolote. (Ezekieli 18:4, ZSB) Hata hivyo, dini nyingi za ulimwengu zinaamini isivyo kweli kwamba kitu fulani ndani ya mtu huendelea kuishi baada ya mtu kufa. Hilo ni fundisho la msingi la dini nyingi zinazojiita za Kikristo. Fundisho hilo linapatikana pia katika dini nyingine kama za Wabudha, Wahindu, Wajaini, Waislamu, Washinto, Wasikh, Watao, na Wayahudi. Hebu wazia—mabilioni ya watu ambao wamepotoshwa na fundisho hilo moja lisilo la kweli!
6, 7. (a) Ni nani pekee wanaoweza kupata “kumjua Mungu”? (b) Ni mfano gani unaoonyesha kwamba Yehova ametupatia ufahamu ambao watu wengi “wenye hekima na wenye akili” wamekosa?
6 Kwa nini watu wengi hawajapata “kumjua Mungu”? Kwa sababu mtu hawezi kulielewa Neno la Mungu kabisa bila msaada Wake. Kumbuka kwamba ujuzi huo ni zawadi ambayo Yehova huwapa wale tu walio tayari kuchunguza Neno lake kwa unyofu na kwa unyenyekevu. Huenda watu hao wasiwe “wenye hekima katika njia ya kimwili.” (1 Wakorintho 1:26) Huenda hata wengi wao wakaonwa kuwa watu “wasio na elimu na wa kawaida tu” kulingana na viwango vya ulimwengu. (Matendo 4:13) Hata hivyo, hilo si muhimu. Yehova hututhawabisha kwa kutuwezesha “kumjua,” naye hufanya hivyo kwa sababu ya sifa anazoona moyoni mwetu.
7 Fikiria mfano mmoja. Wasomi wengi wa zile dini zinazojiita za Kikristo wametoa vichapo vingi sana vinavyofafanua Biblia. Huenda vichapo hivyo vya marejeo vikaeleza mambo ya kihistoria kuhusu vitabu vya Biblia, maana ya maneno ya Kiebrania na Kigiriki, na kadhalika. Licha ya elimu yao, je, wasomi hao wamepata “kumjua Mungu” kweli? Je, wanaelewa vizuri kichwa cha Biblia—kutetewa kwa haki ya Yehova ya kutawala kupitia Ufalme wake wa mbinguni? Je, wanajua kwamba Yehova Mungu si sehemu ya Utatu? Sisi tunayafahamu mambo hayo. Kwa nini tuseme hivyo? Kwa sababu Yehova ametupatia ufahamu wa kweli za kiroho ambazo watu wengi “wenye hekima na wenye akili” wamekosa. (Mathayo 11:25) Yehova huwabariki sana wale wanaomkaribia!
‘Yehova Huwalinda Wote Wampendao’
8, 9. (a) Daudi alifafanuaje baraka nyingine ambayo wale wanaomkaribia Yehova hupata? (b) Kwa nini Wakristo wa kweli wanahitaji ulinzi wa Mungu?
8 Wale wanaomkaribia Yehova hufurahia baraka nyingine—ulinzi wake. Mtunga-zaburi Daudi, ambaye alipatwa na magumu na matatizo mengi, aliandika: “BWANA yu karibu na wote wamwitao, wote wamwitao kwa uaminifu. Atawafanyia wamchao matakwa yao, naye atakisikia kilio chao na kuwaokoa. BWANA huwahifadhi [“huwalinda,” NW] wote wampendao.” (Zaburi 145:18-20) Naam, Yehova yu karibu na wale wampendao kwa hiyo anaweza kuitikia upesi vilio vyao wanapoomba msaada.
9 Kwa nini tunahitaji ulinzi wa Mungu? Mbali na kuathiriwa na hali katika ‘nyakati hizi za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo,’ Wakristo wa kweli hushambuliwa sana na Shetani Ibilisi, ambaye ni Adui mkubwa wa Yehova. (2 Timotheo 3:1) Adui huyo mwenye ujanja ameazimia ‘kutunyafua.’ (1 Petro 5:8) Shetani hutunyanyasa, hutuletea mikazo, na kutushawishi. Yeye pia hutafuta mitazamo fulani ya akili na ya moyo anayoweza kuitumia vibaya. Lengo lake ni: kudhoofisha imani yetu na kutuangamiza kiroho. (Ufunuo 12:12, 17) Kwa kuwa tunakabiliana na adui huyo mwenye nguvu nyingi, je, si jambo lenye kutia moyo kujua kwamba ‘Yehova huwalinda wote wampendao’?
10. (a) Yehova huwalindaje watu wake? (b) Ni ulinzi gani ulio muhimu zaidi, na kwa nini?
10 Lakini Yehova hawalindaje watu wake? Ingawa ameahidi kwamba atatulinda, hiyo haimaanishi kwamba hatutapatwa na matatizo yoyote katika ulimwengu huu; wala haimaanishi kwamba atalazimika kufanya miujiza kwa niaba yetu. Hata hivyo, Yehova hutoa ulinzi wa kimwili kwa watu wake kwa ujumla, kwa kuwa hawezi kumruhusu Ibilisi awaangamize waabudu wa kweli duniani! (2 Petro 2:9) Zaidi ya yote, Yehova hutulinda kiroho. Yeye hutuandalia tunachohitaji ili kuvumilia majaribu na kulinda uhusiano wetu pamoja naye. Ulinzi wa kiroho ndio hasa muhimu zaidi. Kwa nini? Maadamu tuna uhusiano na Yehova, hakuna chochote—hata kifo—kinachoweza kutuletea madhara ya kudumu.—Mathayo 10:28.
11. Yehova amefanya maandalizi gani ili kuwalinda watu wake kiroho?
11 Yehova amefanya maandalizi mengi ya kuwalinda kiroho wale wanaomkaribia. Kupitia Neno lake Biblia, yeye hutupatia hekima ya kushinda majaribu mbalimbali. (Yakobo 1:2-5) Tunapata ulinzi kwa kufuata ushauri unaofaa unaopatikana katika Maandiko. Zaidi ya hayo, Yehova ‘huwapa roho takatifu wale wanaomwomba.’ (Luka 11:13) Hiyo ndiyo roho yenye nguvu zaidi ulimwenguni, kwa hiyo inaweza kutusaidia kushinda jaribu au kishawishi chochote kinachoweza kutupata. Yehova hutoa “zawadi zikiwa wanadamu” kupitia Kristo. (Waefeso 4:8) Wanaume hao wanaostahili kiroho hujitahidi kuiga huruma nyingi ya Yehova wanapowasaidia waabudu wenzao.—Yakobo 5:14, 15.
12, 13. (a) Yehova hutumia njia zipi kutuandalia chakula cha kiroho kwa wakati unaofaa? (b) Unahisije kuhusu maandalizi ambayo Yehova amefanya ili kuboresha hali yetu ya kiroho?
12 Kuna uandalizi mwingine ambao Yehova amefanya ili kutulinda: chakula cha kiroho kwa wakati unaofaa. (Mathayo 24:45) Kupitia vichapo, kutia ndani magazeti ya Mnara wa Mlinzi na Amkeni!, na pia mikutano na makusanyiko, Yehova hutuandalia tunachohitaji wakati tunapokihitaji. Je, unaweza kukumbuka pindi ambapo ulisikia jambo fulani lililokutia nguvu au kukufariji kwenye mikutano ya Kikristo au kwenye kusanyiko? Je, umewahi kusoma makala fulani katika magazeti yaliyotajwa juu na kuhisi kwamba iliandikwa kwa ajili yako?
13 Silaha ambayo Shetani hutumia kwa matokeo sana ni kivunja-moyo, nasi tunaweza kuathiriwa. Yeye anajua vizuri kwamba tukivunjika moyo kwa muda mrefu, tunaweza kudhoofika na hata kufanya iwe rahisi kwake kutushambulia. (Mithali 24:10) Kwa sababu Shetani anajaribu kutumia vibaya hali hiyo ya kuvunjika moyo, tunahitaji msaada. Mara kwa mara, magazeti ya Mnara wa Mlinzi na Amkeni! yamekuwa na makala zinazotusaidia kukabiliana na kuvunjika moyo. Dada mmoja Mkristo aliandika hivi kuhusu makala moja inayozungumzia jambo hilo: “Ninasoma makala hiyo karibu kila siku, na bado mimi hulia ninapoisoma. Naiweka karibu na kitanda changu, mahali ninapoweza kuipata kwa urahisi ninapovunjika moyo. Kwa kusoma makala kama hizi, ninaweza kuhisi mikono ya Yehova ikinikumbatia.”a Je, hatumshukuru Yehova kwa kutuandalia chakula cha kiroho kwa wakati unaofaa? Kumbuka kwamba maandalizi anayofanya ili kuboresha hali yetu ya kiroho ni uthibitisho kuwa yeye yu karibu nasi na anatulinda.
Kumfikia “Msikiaji wa Sala”
14, 15. (a) Ni baraka gani ambayo Yehova huwapa wale wanaomkaribia? (b) Kwa nini ni pendeleo la pekee sana kuweza kumfikia Yehova kwa sala bila kizuizi?
14 Je, umegundua kwamba kadiri uwezo na mamlaka ya wanadamu yanavyoongezeka, ndivyo mara nyingi inavyokuwa vigumu zaidi kwa wale walio chini yao kuwafikia? Namna gani Yehova Mungu? Je, yeye yuko mbali sana na wanadamu asipendezwe na sala zao? La, hasha! Zawadi ya sala ni baraka nyingine ambayo Yehova huwapa wale wanaomkaribia. Ni pendeleo la pekee sana kuweza kumfikia “Msikiaji wa sala” bila kizuizi. (Zaburi 65:2, NW) Kwa nini?
15 Ona mfano ufuatao: Mkurugenzi mkuu wa kampuni kubwa huwa na shughuli nyingi. Yeye huamua ni mambo gani atakayoshughulikia mwenyewe na ni mambo gani atakayowapa wengine wafanye. Vivyo hivyo, Mtawala Mkuu wa ulimwengu anaweza kuamua ni mambo gani atakayofanya na ni gani atakayowapa wengine wafanye. Fikiria mambo ambayo Yehova amempa Yesu, Mwana wake mpendwa, afanye. Mwana amepewa “mamlaka kufanya kazi ya kuhukumu.” (Yohana 5:27) Malaika ‘wametiishwa kwake.’ (1 Petro 3:22) Yehova amempa Yesu roho Yake takatifu na yenye nguvu ili imsaidie kuwaongoza wanafunzi wake duniani. (Yohana 15:26; 16:7) Kwa hiyo Yesu angeweza kusema: “Nimepewa mamlaka yote mbinguni na juu ya dunia.” (Mathayo 28:18) Hata hivyo, kwa habari ya sala, Yehova amechagua kujihusisha kibinafsi. Hiyo ndiyo sababu Biblia hutuagiza tusali kwa Yehova peke yake, kupitia jina la Yesu.—Zaburi 69:13; Yohana 14:6, 13.
16. Kwa nini tunaweza kuwa na hakika kwamba Yehova husikiliza sala zetu?
16 Je, kweli Yehova husikiliza sala zetu? Kama hangejali sala zetu, hangetuhimiza “tudumu katika sala” au tumtwike mizigo na mahangaiko yetu. (Waroma 12:12; Zaburi 55:22; 1 Petro 5:7) Watumishi waaminifu wa nyakati za Biblia walikuwa na hakika kabisa kwamba Yehova husikiliza sala. (1 Yohana 5:14) Hivyo, mtunga-zaburi Daudi alisema: “[Yehova] ataisikia sauti yangu.” (Zaburi 55:17) Sisi pia tuna sababu nzuri za kuwa na hakika kwamba Yehova yu karibu na tayari kusikiliza mawazo na mahangaiko yetu yote.
Yehova Huwathawabisha Watumishi Wake
17, 18. (a) Yehova huhisije kuhusu utumishi wa viumbe wake wenye akili—wanadamu na malaika? (b) Eleza jinsi Mithali 19:17 inavyoonyesha kwamba Yehova huthamini matendo yetu ya huruma.
17 Cheo cha Yehova akiwa Mwenye Enzi Kuu ya Ulimwengu wote hakiathiriwi na yale ambayo wanadamu wanaweza kufanya au kukataa kufanya. Hata hivyo, Yehova ni Mungu mwenye uthamini. Yeye huthamini na hupendezwa na utumishi mwaminifu wa viumbe wake wenye akili—wanadamu na malaika. (Zaburi 147:11) Kuna baraka nyingine pia ambayo wale wanaomkaribia Yehova hupata: Yeye huwathawabisha watumishi wake.—Waebrania 11:6.
18 Biblia huonyesha wazi kwamba Yehova huthamini yale ambayo waabudu wake hufanya. Kwa mfano, tunasoma: “Amhurumiaye maskini humkopesha BWANA; naye atamlipa kwa tendo lake jema.” (Mithali 19:17) Sheria ya Musa ilionyesha jinsi Yehova anavyowahurumia watu wa hali ya chini. (Mambo ya Walawi 14:21; 19:15) Yehova huhisije tunapomwiga kwa kuwaonyesha huruma watu wa hali ya chini? Tunapompa mtu wa hali ya chini kitu pasipo kutazamia aturudishie, Yehova huona ni kama tumemkopesha Yeye. Yehova anaahidi kulipa deni hilo kwa kutuonyesha kibali na kutubariki. (Mithali 10:22; Mathayo 6:3, 4; Luka 14:12-14) Naam, tunapomwonyesha huruma mwabudu mwenzetu aliye na uhitaji, jambo hilo hugusa moyo wa Yehova. Tunashukuru kama nini kujua kwamba matendo yetu ya huruma yanathaminiwa na Baba yetu wa mbinguni!—Mathayo 5:7.
19. (a) Kwa nini tunaweza kuwa na hakika kwamba Yehova huthamini tunayofanya katika kazi ya kuhubiri na kufanya wanafunzi? (b) Yehova hututhawabishaje kwa utumishi tunaofanya ili kutegemeza Ufalme wake?
19 Yehova hasa huthamini yale tunayofanya kwa ajili ya Ufalme wake. Tunapomkaribia Yehova, ni jambo la kawaida kutaka kutumia wakati, nguvu, na mali zetu ili tushiriki kikamili iwezekanavyo katika kazi ya kuhubiri Ufalme na kufanya wanafunzi. (Mathayo 28:19, 20) Nyakati nyingine, huenda tukahisi kwamba tunatimiza kazi hiyo kwa kiwango kidogo sana. Huenda hata moyo wetu usio mkamilifu ukafanya tuwe na shaka kama Yehova anapendezwa na jitihada zetu. (1 Yohana 3:19, 20) Lakini Yehova huthamini kila zawadi—hata iwe ndogo—ambayo inatolewa kwa moyo wa upendo. (Marko 12:41-44) Biblia hutuhakikishia hivi: “Mungu si asiye mwadilifu ili asahau kazi yenu na upendo mlioonyesha kwa ajili ya jina lake.” (Waebrania 6:10) Naam, Hata utumishi wetu uwe mdogo kadiri gani, Yehova hutukumbuka na kututhawabisha kwa yote tunayofanya ili kutegemeza Ufalme wake. Mbali na baraka tele za kiroho, tunaweza kutazamia maisha yenye furaha katika ulimwengu mpya unaokuja, ambapo Yehova atatoa kwa ukarimu na kutosheleza tamaa za watu wote waadilifu wanaomkaribia!—Zaburi 145:16; 2 Petro 3:13.
20. Katika mwaka wote wa 2003, tunawezaje kuendelea kufikiria maneno ya andiko la mwaka, na matokeo yatakuwa nini?
20 Katika mwaka wote wa 2003, na tujichunguze wenyewe tuone kama tunaendelea kujitahidi kumkaribia Baba yetu wa mbinguni. Tukifanya hivyo, tunaweza kuwa na hakika kwamba atatenda kulingana na ahadi yake, kwa kuwa ‘Mungu hawezi kusema uwongo.’ (Tito 1:2) Ukimkaribia, atakukaribia. (Yakobo 4:8) Matokeo yatakuwa nini? Baraka nyingi sasa na tazamio la kuendelea kumkaribia Yehova milele!
[Maelezo ya Chini]
a Barua iliyoandikwa kuhusu makala yenye kichwa “Yehova Ni Mkubwa Zaidi Kuliko Mioyo Yetu,” katika toleo la Mnara wa Mlinzi la Mei 1, 2000, ukurasa wa 28-31.
-