Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Hisia Zako
    Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, Buku la 2
    • SEHEMU YA 7

      Hisia Zako

      Kati ya taarifa zifuatazo, ni taarifa gani inayokufafanua vizuri?

      □ Siwezi kuzuia hasira yangu.

      □❏ Mimi ni bure kabisa—siwezi kufanya lolote.

      □ Nina huzuni saa zote. Sina furaha kamwe maishani.

      □ Daima, nawafikiria watu wa jinsia tofauti.

      □ Nyakati nyingine mimi huvutiwa na watu wa jinsia yangu.

      Ikiwa ulichagua yoyote ya taarifa hizo, usikate tamaa! Sura ya 26-29 zitakusaidia kujua jinsi unavyoweza kudhibiti hisia zako ili zisikutawale.

      [Picha katika ukurasa wa 216, 217

  • Ninaweza Kudhibiti Jinsi Gani Hisia Zangu?
    Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, Buku la 2
    • SURA YA 26

      Ninaweza Kudhibiti Jinsi Gani Hisia Zangu?

      UNAONAJE—moto ni mzuri au ni mbaya? Huenda ukajibu kwamba inategemea hali. Usiku wenye baridi kali, moto wa kuni unaweza kukupasha joto. Katika hali hiyo, moto ni mzuri. Hata hivyo, usipodhitiwa, moto huo unaweza kuenea na kuteketeza nyumba nzima. Sasa, moto ni mbaya.

      Ndivyo pia na hisia zako. Zinapodhibitiwa, zina manufaa, zinakuwezesha kukuza urafiki mzuri. Zisipodhibitiwa, zinaweza kutokeza madhara, si kwako tu, lakini pia kwa wengine.

      Ukiwa kijana, huenda nyakati nyingine ukalemewa na hasira au huzuni. Unaweza kudhibiti hisia hizo jinsi gani? Acha tuzungumzie kila moja kivyake.

      Kudhibiti Hasira

      Si rahisi kuvumilia uchungu na maumivu yanayotokea unapotendewa isivyofaa. Watu fulani hushindwa kujidhibiti wanapotendewa hivyo. Hata Biblia inasema kwamba kuna watu wenye “mazoea ya kukasirika” na wenye “mifoko ya ghadhabu.” (Methali 22:24; 29:22) Hilo si jambo dogo. Hasira isiyodhibitiwa inaweza kukufanya utende kwa njia ambayo itakufanya ujute baadaye. Kwa hiyo, unaweza kudhibiti hisia zako jinsi gani unapotendewa isivyofaa?

      Kwanza, changanua vizuri hali hiyo, uone ikiwa unaweza kutatua jambo hilo moyoni mwako.a (Zaburi 4:4) Kumbuka kulipa “ubaya kwa ubaya” kutafanya mambo yawe mabaya zaidi. (1 Wathesalonike 5:15) Baada ya kufikiria jambo hilo kwa uzito na kusali, huenda ukaona kwamba unaweza kusahau jambo hilo. Ukiondoa kinyongo moyoni, hutakuwa tena mtumwa wa jambo hilo.—Zaburi 37:8

      Lakini namna gani ikiwa bado una uchungu mwingi? Biblia inasema kuna “wakati wa kukaa kimya na wakati wa kusema.” (Mhubiri 3:7) Je, unaweza kuzungumza na mtu aliyekuumiza? Ikiwa haingefaa kufanya hivyo, unaweza kufaidika kwa kuzungumza na wazazi wako au rafiki mkomavu na kumweleza unavyohisi. Ikiwa mtu fulani anakusumbua kimakusudi, jitahidi kushughulika naye kwa fadhili. Chati iliyo katika ukurasa wa 221 inaweza kukusaidia kufikiria jinsi unavyoweza kushughulikia hali ambazo zimekuwa zikikufanya utende kwa hasira.

      Vyovyote vile, mwombe Yehova akusaidie kuepuka kumwekea kinyongo mtu aliyekuumiza. Kumbuka hili: Ijapokuwa huwezi kubadili lililotokea, unaweza kubadili utakavyoshughulika na hali hiyo. Ukijiacha ulemewe na kinyongo, utakuwa hoi kama samaki aliyenaswa kwenye ndoano. Unamruhusu mtu mwingine aongoze fikira na hisia zako. Ingekuwa afadhali kama wewe mwenyewe ungekuwa kwenye usukani, sivyo?—Waroma 12:19.

      Kuvumilia Huzuni

      “Hivi majuzi nimekuwa nikijiona sifai kitu, tena sina furaha,” asema Laura, mwenye umri wa miaka 16. “Sifurahii maisha hata kidogo. Mimi hulia sana kitandani.” Kama Laura, vijana wengi huhisi kwamba wanalemewa na ugumu wa maisha. Namna gani wewe? Mikazo mingi sana kutoka kwa wazazi wako, marafiki, walimu; mabadiliko ya kimwili na kihisia ya wakati wa kubalehe; au kuhisi kwamba hufai kitu kwa sababu ya kosa fulani dogo—yote hayo yanaweza kukufanya ujisikie vibaya sana.

      Vijana fulani hata huanza kujiumiza ili kupunguza huzuni hiyo.b Ikiwa umetumbukia katika zoea hilo, jaribu kujua ni kwa nini. Kwa mfano, mara nyingi watu ambao hujiumiza, hufanya hivyo wanapokuwa na mkazo. Je, kuna hali fulani—labda inayohusisha familia au marafiki—inayokufanya uwe na mkazo?

      Njia moja nzuri ya kushughulika na hisia zinazosumbua ni kuzungumza na mzazi au mshiriki mkomavu wa kutaniko anayeweza kuwa ndugu “aliyezaliwa kwa ajili ya wakati wa taabu.” (Methali 17:17) Liliana, mwenye umri wa miaka 16, alizungumza na akina dada fulani wakomavu. “Kwa kuwa wana umri mkubwa kuliko wangu,” anasema, “wana mashauri mazuri. Wamekuja kuwa rafiki zangu.”c Dana, mwenye umri wa miaka 15, anasema kwamba alipata nafuu kwa kushiriki zaidi katika huduma ya Kikristo. “Hilo ndilo jambo bora ambalo ningeweza kufanya,” anasema. “Huo ndio wakati nilipokuwa na furaha zaidi maishani!”

      Zaidi ya yote, ikiwa una huzuni au umeshuka moyo, usipuuze sala. Mtunga-zaburi Daudi, aliyekumbwa na taabu nyingi, aliandika: “Mtupie Yehova mzigo wako, naye mwenyewe atakutegemeza.” (Zaburi 55:22) Yehova anajua jinsi unavyoteseka. Isitoshe, ‘anakujali.’ (1 Petro 5:7) Ikiwa moyo wako unakulaumu, kumbuka kwamba ‘Mungu ni mkuu kuliko moyo wako naye anajua mambo yote.’ (1 Yohana 3:20) Anaelewa vizuri zaidi kuliko wewe ni kwa nini unafadhaika, naye anaweza kukuondolea mzigo wa kihisia unaokulemea.

      Huzuni ikiendelea, inawezekana kwamba una tatizo fulani la afya, kama vile ugonjwa wa kushuka moyo.d Ikiwa hivyo ndivyo ilivyo, ingefaa umwone daktari. Kupuuza hali hiyo ni kama kuongeza sauti ya redio katika gari ili usisikie makelele yanayotoka katika injini ya gari. Ingefaa zaidi ushughulikie hali hiyo. Kwa kweli, hakuna haja ya kuonea aibu hali yako. Vijana wengi walio na ugonjwa wa kushuka moyo au matatizo mengine kama hayo wanapata msaada kupitia matibabu.

      Kumbuka kwamba hisia ni kama moto. Zikidhibitiwa zinaweza kuwa na manufaa; zisipodhibitiwa, zinaweza kutokeza madhara. Fanya yote uwezayo ili kudhibiti hisia zako. Ni kweli kwamba huenda wakati mwingine ukasema au kufanya jambo ambalo utajuta baadaye. Lakini uwe na subira. Kadiri muda unavyopita, utajizoeza kudhibiti hisia ili usitawaliwe na hisia.

      KATIKA SURA INAYOFUATA

      Je, wewe ni mtu asiyeridhika? Ikiwa ndivyo, unaweza kujifunza jinsi gani kushughulika na hisia hizo?

      [Maelezo ya Chini]

      a Ikiwa unanyanyaswa pia, unaweza kupata mapendekezo ya kushughulika na hali hiyo katika Sura ya 14 ya kitabu hiki. Kwa upande mwingine, ikiwa umekasirishwa na rafiki yako, habari iliyo katika Sura ya 10 inaweza kukusaidia.

      b Watu wanaojiumiza hufanya hivyo kimakusudi kwa njia mbalimbali, kama vile kujikata-kata, kujichoma kwa moto, kujichubua, au kujikwaruza ngozi.

      c Ukishindwa kuzungumza na mtu uso kwa uso, jaribu kumwandikia barua au kumpigia simu. Mara nyingi, kuzungumza na mtu ni hatua ya kwanza ya kuondolea mbali maumivu ya moyoni.

      d Unaweza kupata habari zaidi kuhusu kushuka moyo, katika Buku la 1, sura ya 13.

      MAANDIKO MUHIMU

      “Usiache ushindwe na uovu, bali endelea kuushinda uovu kwa wema.”—Waroma 12:21.

      PENDEKEZO

      Kila siku mwambie mzazi (wazazi) wako jambo fulani zuri lililokufurahisha—hata kama ni dogo. Hivyo, tatizo zito litakapotokea, itakuwa rahisi zaidi kwako kuzungumza nao. Nao watakuwa tayari kukusikiliza

      JE, WAJUA . . .?

      Usipopumzika vya kutosha na kula vizuri, huenda ukashindwa kudhibiti hisia zako.

      HATUA ZA KUCHUKUA!

      Hisia isiyofaa ambayo ni vigumu sana kwangu kuidhibiti ni ․․․․․

      Nitashughulikia hisia hiyo kwa ․․․․․

      Mambo ambayo ningependa kuuliza mzazi (wazazi) wangu kuhusu habari hii ni ․․․․․

      UNA MAONI GANI?

      ● Kwa nini hasira isiyodhibitiwa humchukiza Mungu?

      ● Kushindwa kuzuia hasira kunaweza kukuumiza jinsi gani?

      ● Ni nini kinachoweza kukusaidia kuvumilia huzuni?

      [Blabu katika ukurasa wa 223]

      ‘‘Jambo kuu lilikuwa kujua kwamba mtu fulani ananijali kwelikweli, na kwamba kuna mtu ninayeweza kuzungumza naye wakati mambo yanapokwenda mrama.’’—Jennifer

      [Chati/Picha katika ukurasa wa 221]

      Ukurasa wa Mazoezi

      Dhibiti hasira yako

      Malizia chati hii

      Tukio

      Mwanafunzi mwenzangu ananidhihaki

      Itikio la hasira

      Kumtukana

      Itikio bora zaidi

      Kupuuza dhihakaka zake, na kumwonyesha na kumwonyesha kwamba hujakasirika

      Tukio

      Dada yangu “alichukua” viatu vyangu ninavyovipenda sana bila kuniomba

      Itikio la hasira

      Kulipiza kisasi kwa “kuchukua” kitu chake

      Itikio bora zaidi

      ․․․․․

      Tukio

      Dada yangu wananinyima ruhusa

      Itikio la hasira

      ․․․․․

      Itikio bora zaidi

      ․․․․․

      [Picha katika ukurasa wa 220]

      Mtu anayeweka kinyongo ni kama samaki aliyenaswa katika ndoano—wote wawili wanaongozwa na mtu mwingine

  • Kwa Nini Siridhiki?
    Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, Buku la 2
    • SURA YA 27

      Kwa Nini Siridhiki?

      Wewe hukasirika usipopita mtihani kwa alama za juu zaidi?

      □ Ndiyo

      □ Hapana

      Wewe hujiona kuwa bure kabisa ukikosolewa hata kidogo tu?

      □ Ndiyo

      □ Hapana

      Wewe huona ni vigumu kupata au kudumisha marafiki kwa sababu hakuna anayefikia kiwango chako?

      □ Ndiyo

      □ Hapana

      IKIWA umejibu ndiyo katika swali moja au zaidi, huenda una tatizo la kutoridhika. ‘Kwani kuna ubaya gani kujaribu kufanya mambo yote kikamilifu?’ huenda ukauliza. Bila shaka, hakuna ubaya! Biblia humsifu mtu ambaye ni “stadi katika kazi yake.” (Methali 22:29) Hata hivyo, mtu asiyeridhika, hufanya mambo kupita kiasi.

      Kwa mfano, Jason, mwenye umri wa miaka 19 anakiri hivi: “Mwaka wa mwisho nilipokuwa shuleni, nilihisi kana kwamba, ikiwa singeweza kupita mtihani kwa alama za juu zaidi, basi nilikuwa mwanafunzi mjinga. Pia, mimi hupiga piano, nami nilikuwa nikihisi kwamba lazima nipige piano kwa ustadi kama ule wa wapiga-piano katika maonyesho ya muziki.”

      Kutoridhika kwaweza hata kuathiri ibada ya mtu. Fikiria kinachoweza kumpata kijana ambaye sikuzote huonwa kuwa mfano mzuri kwa wengine. Kwa kuwa sikuzote anasifiwa, huenda akaanza kuhisi ni kana kwamba anatembea juu ya kamba, kila mtu akichunguza kila kitu anachofanya. Bila shaka, Wakristo, vijana kwa wazee, hufaidika kutokana na mifano mizuri kutanikoni. Hata hivyo, kujaribu kuishi maisha yasiyo na dosari kwaweza kumfanya kijana asiwe na shangwe katika utumishi wa Mungu. Inapofikia hatua hiyo, kijana huyo anahitaji msaada. Lakini huenda asiombe msaada, akihofia kwamba atawavunja moyo wale wanaomwona kuwa ‘mkamilifu.’ Huenda hata akakata tamaa, akifikiri, ‘Ikiwa siwezi kudumisha kiwango changu kikamilifu, kuna haja gani kujisumbua?’

      Kupambana na Kutoridhika

      Watu wasioridhika huamini kwamba mtu hapaswi kukosea hata kidogo. Lakini, kwa kweli, maoni hayo yana kasoro. Biblia inasema hivi waziwazi: “Wote wamefanya dhambi na kupungukiwa na utukufu wa Mungu.” (Waroma 3:23) Kwa hiyo, hakuna mwanadamu yeyote anayeweza kutenda mambo kikamilifu kabisa. Kuamini kwamba unaweza kutenda mambo kikamilifu ni sawa na kuamini kwamba unaweza kuruka kama ndege. Hata uamini hivyo kadiri gani, ni jambo lisilowezekana!

      Unaweza kufanya nini ili kuepuka kuwa mtu asiyeridhika na chochote? Jaribu mambo yafuatayo:

      Badili maoni yako kuhusu “mafanikio.” Je, unajichosha kwa kujaribu kuwa bora kuliko wengine wote? Biblia inaonyesha kwamba kufanya hivyo kwaweza kuwa kama “kuwinda upepo.” (Mhubiri 4:4, Verbum Bible) Ukweli ni kwamba, ni watu wachache sana wanaofikia kiwango cha kuwa “bora kuliko wote.” Na hata mtu anapofikia kiwango hicho, kwa kawaida muda si muda mwingine hutokea na kuvunja rekodi yake. Mafanikio ni kufanya yote uwezayo—wala si kumshinda mtu mwingine.—Wagalatia 6:4.

      Ona mambo kihalisi. Unapaswa kuwa na matazamio yanayolingana na uwezo na mipaka yako. Kujiwekea mradi ulio juu sana ni kukosa kiasi, au hata ni kiburi. Mtume Paulo anatoa shauri zuri: “Namwambia kila mtu hapo kati yenu asijifikirie mwenyewe zaidi kuliko ilivyo lazima kufikiri.” (Waroma 12:3) Kwa hiyo, ona mambo kihalisi. Changanua matarajio yako. Jitahidi kufanya yote uwezayo bali si kuwa mkamilifu.

      Legeza kamba! Jaribu kufanya mambo ambayo hujui kufanya, kama vile kupiga chombo fulani cha muziki. Ni kweli kwamba utakosea mara nyingi. Hata hivyo, wakati huu, jitahidi kuyaona makosa yako kwa njia tofauti. Biblia inasema kwamba kuna “wakati wa kucheka.” (Mhubiri 3:4) Kwa hiyo, kwa nini usijifunze kutochukua mambo kwa uzito sana? Kufanya hivyo kutakusaidia kuona kwamba kupotea njia ndiyo kujua njia. Ni kweli kwamba haitakuwa rahisi kwako kuridhika na kazi isiyofikia kiwango unachotaka. Lakini jitahidi kuondoa akilini mwako mawazo yasiyofaa, ya kuchambua-chambua.

      Sikuzote kumbuka kwamba Yehova hadai ukamilifu; anataka tu tumtumikie kwa uaminifu. (1 Wakorintho 4:2) Ikiwa unajitahidi kuwa mwaminifu, unaweza kuwa na furaha ya kweli—hata ikiwa hufanyi mambo kikamilifu.

      KATIKA SURA INAYOFUATA

      Watu wengi leo wanaona ngono kati ya watu wa jinsia moja kuwa jambo linalokubalika. Unaweza kuepuka zoea hilo namna gani? Utafanya nini ukivutiwa na mtu wa jinsia yako?

      MAANDIKO MUHIMU

      “Hakuna mwanadamu aliye mwadilifu duniani ambaye huendelea kufanya mema na asifanye dhambi.”—Mhubiri 7:20.

      PENDEKEZO

      Fikiria jambo fulani ambalo umekuwa ukiahirisha-ahirisha kulifanya, kwa sababu tu hutaki kukosea. Kisha weka tarehe ya kumaliza kulifanya.

      JE, WAJUA . . .?

      Yehova ni mkamilifu, lakini anaposhughulika na wanadamu ambao si wakamilifu, hatazamii ukamilifu kutoka kwao. Anajua na kuzingatia uwezo na mipaka yetu.

      HATUA ZA KUCHUKUA!

      Nikianza kujiona kwamba sifai, nita ․․․․․

      Nikianza kuwa mwenye kudai mengi mno kutoka kwa wengine nita ․․․․․

      Mambo ambayo ningependa kuuliza mzazi (wazazi) wangu kuhusu habari hii ni ․․․․․

      UNA MAONI GANI?

      ● Ni katika mambo gani maishani wewe hujiwekea miradi isiyoweza kufikika?

      ● Ni maandiko gani yanayokusaidia kuona waziwazi kwamba Yehova hatazamii watumishi wake wafanye mambo yanayopita uwezo wao?

      ● Kwa nini huenda wengine wakajitenga nawe ikiwa unadai mengi mno kutoka kwao?

      ● Wakati ujao utafanya nini ukikosea?

      [Blabu katika ukurasa wa 226]

      ‘‘Kufanya yote uwezayo na kufanya mambo kikamilifu ni mambo mawili tofauti; la kwanza linaonyesha usawaziko na la pili ukosefu wa usawaziko.’’—Megan

      [Sanduku katika ukurasa wa 228]

      Kutazamia mengi mno kunaweza kuharibu urafiki

      Je, umewahi kuwaepuka watu kwa sababu hawafai machoni pako? Au, je, watu wazuri wamewahi kukuepuka kwa sababu viwango vyako vya urafiki ni vya juu mno visiweze kufikiwa? Biblia inashauri hivi: “Usiwe mwadilifu kupita kiasi, wala kujionyesha kuwa na hekima kupita kiasi. Kwa nini ujiletee ukiwa?” (Mhubiri 7:16) Njia moja ambayo mtu hujiletea ukiwa ni kwa kutoa visingizio mbalimbali ili kuwaepuka watu ambao wangependa kuwa rafiki zake. “Hakuna mtu anayependa kuwa rafiki ya watu wanaomfanya aone hafai,” anasema msichana mmoja anayeitwa Amber, “nami nimeona watu ambao hudai mengi kutoka kwa rafiki zao wakipoteza marafiki wazuri kwa sababu ya mambo madogo sana.”

      [Picha katika ukurasa wa 229]

      Kujaribu kuwa mkamilifu ni kazi bure kama vile kujaribu kuruka kama ndege

  • Mfano wa Kuigwa—Paulo
    Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, Buku la 2
    • Mfano wa Kuigwa—Paulo

      Mtume Paulo anaelewa vizuri hisia zake. Anakiri hivi waziwazi: “Ninapotaka kufanya yaliyo sawa, yaliyo mabaya yapo pamoja nami.” Paulo ana moyo mzuri. Anasema: “Kwa kweli naipenda sheria ya Mungu kulingana na mtu niliye kwa ndani.” Shida ni nini basi? Paulo anasema: “Naona . . . sheria nyingine ikipigana na sheria ya akili yangu na kunichukua mateka kwa sheria ya dhambi iliyo ndani ya viungo vyangu.” Paulo hafurahii kuwa katika hali hiyo. Anasema hivi kwa majuto: “Maskini mimi!”—Waroma 7:21-24.

      Je, wewe huvunjika moyo kwa sababu ya makosa unayofanya? Ikiwa ndivyo, kumbuka kwamba hata Paulo alihisi hivyo nyakati fulani. Lakini Paulo alijua kwamba Kristo alikufa kwa ajili ya watu kama yeye. Hivyo, angeweza kusema: “Shukrani kwa Mungu kupitia Yesu Kristo Bwana wetu!” (Waroma 7:25) Paulo aliiona fidia kuwa zawadi yake binafsi. Aliandika: ‘Mwana wa Mungu, alinipenda mimi na kujitoa mwenyewe kwa ajili yangu.’ (Wagalatia 2:20) Unaposhuka moyo, tafakari kuhusu fidia. Na ikiwa makosa yako yanakuvunja moyo, usisahau kamwe kwamba Kristo alikufa kwa ajili ya wakosaji, bali si watu wakamilifu.

  • Nifanye Nini Ikiwa Ninavutiwa na Watu wa Jinsia Yangu?
    Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, Buku la 2
    • sura ya 28

      Nifanye Nini Ikiwa Ninavutiwa na Watu wa Jinsia Yangu?

      “Nilipokuwa kijana, nilipambana na hisia za kuvutiwa na wavulana wenzangu. Moyoni mwangu nilijua kwamba hisia hizo si za kawaida.”—Olef.

      “Mimi na rafiki yangu mmoja msichana tulipigana busu mara moja, mbili hivi. Kwa kuwa ninavutiwa na wavulana pia, sijui ikiwa nina hisia za kingono kuelekea watu wa jinsia zote mbili.”—Sarah.

      SI SIRI kwamba leo ngono kati ya watu wa jinsia moja huzungumziwa waziwazi kuliko ilivyokuwa miaka kadhaa iliyopita. Na ukithubutu kusema kwamba hilo ni zoea lenye kuchukiza, utakiona! Amy, msichana mwenye umri wa miaka 16 anasema: “Msichana mmoja aliniambia kwamba haikosi ninawachukia watu wa rangi nyingine kwa sababu maoni yangu kuhusu ngono kati ya watu wa jinsia moja hayana tofauti—yote ni ubaguzi.”

      Uhuru wa kufanya mambo uliopo leo umewachochea vijana fulani kuwa na mahusiano ya kingono pamoja na wengine wa jinsia yao. “Wasichana wengi shuleni wanadai kwamba wao hufanya ngono na wasichana wenzao, wengine hudai kwamba wao hufanya ngono na wasichana kwa wavulana, nao wengine husema kwamba wangependa kujaribu mahusiano yote hayo,” anasema Becky mwenye umri wa miaka 15. Naye Christa, mwenye umri wa miaka 18, anasema kwamba hali iko hivyohivyo shuleni kwao. Anasema: “Tayari wasichana wawili katika darasa langu wameniomba nifanye ngono nao. Mmoja aliniandikia maneno machache akiniuliza ikiwa ningependa ‘kuonja’ ngono na msichana mwenzangu.”

      Wakati huu ambapo ngono kati ya watu wa jinsia moja inapigiwa debe sana, huenda ukaanza kujiuliza: ‘Kwa kweli, ni dhambi kuwa na uhusiano wa kingono na mtu wa jinsia yako? Namna gani ikiwa ninavutiwa na mtu wa jinsia yangu? Je, hilo linamaanisha kwamba mimi ni shoga?’

      Mungu Anaonaje Ngono Kati ya Watu wa Jinsia Moja?

      Watu wengi leo, kutia ndani viongozi fulani wa dini, huona ngono kati ya watu wa jinsia moja kuwa jambo la kawaida. Hata hivyo, Neno la Mungu, Biblia inataja mambo waziwazi. Inatuambia kwamba Yehova Mungu aliumba mwanamume na mwanamke na kwamba alikusudia tamaa za ngono zitoshelezwe kati ya mume na mke tu. (Mwanzo 1:27, 28; 2:24) Hivyo basi, haishangazi kwamba Biblia inashutumu ngono kati ya watu wa jinsia moja.—Waroma 1:26, 27.

      Huenda watu wengi wakasema kwamba Neno la Mungu limepitwa na wakati. Lakini unafikiri ni kwa nini wengi huwa na maoni kama hayo? Inawezekana ni kwa sababu Biblia inapinga maoni yao? Wengi wanakataa Neno la Mungu kwa sababu tu linafundisha tofauti na vile wanavyotaka kuamini. Lakini maoni hayo yamepotoka, nasi hatupaswi kuruhusu yatupotoshe!

      Namna gani ikiwa unavutiwa na mtu wa jinsia yako? Je, hilo linamaanisha kwamba wewe ni shoga? Hapana. Kumbuka, uko katika “upeo wa ujana,” wakati ambapo tamaa za ngono hutokea zenyewe. (1 Wakorintho 7:36) Ikiwa nyakati nyingine unahisi ukivutiwa na mtu wa jinsia yako, uwe na hakika kwamba hilo halimaanishi kwamba wewe ni shoga. Kwa kawaida hisia hizo huisha baada ya muda. Kwa sasa unapaswa kujiepusha na mambo hayo. Jinsi gani?

      Sali. Msihi Yehova kama Daudi alivyofanya: “Unichunguze kabisa, Ee Mungu, uujue moyo wangu. Unichunguze, na uzijue fikira zangu zinazofadhaisha, na uone kama ndani yangu mna njia yoyote yenye kuumiza, na uniongoze katika njia ya mpaka wakati usio na kipimo.” (Zaburi 139:23, 24) Yehova anaweza kukuimarisha kwa kukupa amani “yenye ubora unaozidi fikira zote.” Amani hiyo inaweza ‘kuulinda moyo wako na nguvu zako za akili’ na pia kukupa “nguvu zinazopita zile za kawaida” ili usitende kulingana na tamaa zisizofaa.—Wafilipi 4:6, 7; 2 Wakorintho 4:7

      Kazia fikira mambo yenye kujenga. (Wafilipi 4:8) Soma Biblia kila siku. Usipuuze kamwe uwezo wa Biblia wa kufinyanga akili na moyo wako ili utende mema. (Waebrania 4:12) Kijana mmoja anayeitwa Jason anasema: “Biblia—kutia ndani maandiko kama vile 1 Wakorintho 6:9, 10; na Waefeso 5:3—imenisaidia sana. Mimi husoma maandiko haya kila wakati ninapoanza kuwa na tamaa mbaya.”

      Epuka ponografia, yaani picha au habari za ngono na propaganda za ngono kati ya watu wa jinsia moja. (Wakolosai 3:5) Epuka chochote kinachoweza kuchochea tamaa zisizofaa. Vitu hivyo vinatia ndani ponografia, vipindi fulani vya televisheni na sinema, na huenda hata magazeti ya mitindo ya kujenga mwili yanayoonyesha wanamitindo wakiwa nusu uchi. Ondoa maoni yasiyofaa akilini na kukaza fikira juu ya mambo yanayofaa. Mvulana mmoja tineja anasema: “Ninapoanza kuwa na tamaa za kufanya ngono na mtu wa jinsia yangu, mimi huanza kutafakari andiko fulani ninalopenda katika Biblia.”

      Bila shaka, huenda wengine wakasema kwamba hakuna haja ya kuchukua hatua zote hizo, badala yake unapaswa ‘kutosheleza tamaa ulizo nazo’ na ‘kukubali kwamba ndivyo ulivyoumbwa.’ Lakini, Biblia haisemi hivyo! Kwa mfano, inasema kwamba baadhi ya Wakristo wa karne ya kwanza ambao walikuwa na mazoea ya kulala na watu wa jinsia yao walibadilika. (1 Wakorintho 6:9-11) Wewe pia unaweza kushinda vita hivyo—ingawa kwa sasa bado ni jambo lililo katika mawazo yako.

      Namna gani tamaa hizo zikizidi? Usisalimu amri! Yehova anashutumu matendo ya ngono kati ya watu wa jinsia moja. Kwa hiyo, mtu anayepambana na tamaa za kufanya ngono na mtu wa jinsia moja anaweza kuamua kutotosheleza tamaa hizo.

      Kwa mfano: Huenda mtu akawa na “mwelekeo wa ghadhabu,” au kukasirika-kasirika. (Methali 29:22) Huenda wakati uliopita alikuwa akijiachilia tu na kulipuka kwa hasira. Ingawa hivyo, baada ya kujifunza Biblia, anatambua kwamba anahitaji kujizoeza sifa ya kujizuia. Inamaanisha kwamba hakuna wakati atakapojisikia akiwaka kwa hasira? Hapana. Lakini, kwa sababu anajua Biblia inasema nini kuhusu hasira isiyozuiliwa, atajitahidi kutolemewa na hisia hizo.

      Ndivyo pia na mtu anayevutiwa na wengine wa jinsia yake ambaye amejifunza jinsi Biblia inavyosema kuhusu mazoea ya kufanya ngono na watu wa jinsia moja. Huenda bado akawa na tamaa zisizofaa mara mojamoja. Lakini akijitahidi kuwa na maoni kama ya Yehova, anaweza kupata nguvu za kushinda tamaa hizo.

      Usikate Tamaa!

      Ikiwa unapambana na hisia za kuvutiwa na watu wa jinsia yako, huenda ukahisi kama alivyohisi kijana mmoja, aliyesema: “Nimejaribu kuondolea mbali tamaa hizo. Nimemwomba Yehova anisaidie. Nimesoma Biblia. Nimesikiliza hotuba mbalimbali kuhusu habari hiyo. Lakini sijui nifanye nini.”

      Ikiwa uko katika hali kama hiyo, bila shaka una pambano kali kwelikweli. Hakuna njia ya mkato. Lakini, yeyote anayetamani kumpendeza Mungu lazima ashikamane na viwango Vyake vya maadili na kuepuka mwenendo mpotovu, ijapokuwa huenda ikawa vigumu sana kufanya hivyo. Usisahau kamwe kwamba Mungu anajua jinsi unavyopambana na tamaa hizo naye anawahurumia wale wanaomtumikia.a (1 Yohana 3:19, 20) Ukitii amri za Mungu, utapata baraka. Biblia inasema kwamba kuzishika amri za Mungu “kuna thawabu kubwa.” (Zaburi 19:11) Hata sasa, utafurahia maisha bora zaidi katika ulimwengu huu wenye taabu.

      Kwa hiyo, mtegemee Mungu na kupambana na tamaa zisizofaa. (Wagalatia 6:9) Jitahidi ‘kuchukia maovu’ na ‘kushikamana na mema.’ (Waroma 12:9) Ukitia bidii, baada ya muda tamaa hizo zisizofaa zitaisha. Zaidi ya yote, ukiepuka mazoea hayo machafu, utakuwa na tumaini la kuishi milele katika ulimwengu mpya wenye uadilifu wa Mungu.

      KATIKA SURA INAYOFUATA

      Unaweza kufanya nini unapovutiwa na watu wa jinsia tofauti?

      [Maelezo ya Chini]

      a Mkristo ambaye ametumbukia katika matendo mapotovu katika ngono anapaswa kuwaendea wazee wa kutaniko wamsaidie.—Yakobo 5:14, 15.

      MAANDIKO MUHIMU

      “Unichunguze, na uzijue fikira zangu zinazofadhaisha, na uone kama ndani yangu mna njia yoyote yenye kuumiza.”—Zaburi 139:23, 24.

      PENDEKEZO

      Ili kuwa na maoni yanayofaa kuhusu sifa za kiume, chunguza kielelezo cha Yesu. (1 Petro 2:21) Alikuwa kielelezo kikamilifu cha mwanamume hodari lakini mpole.

      JE, WAJUA . . .?

      Ijapokuwa huwezi kujizuia kabisa usiwe na tamaa, unaweza kuzuia matendo yako. Unaweza kuamua kutotosheleza tamaa mbaya.

      HATUA ZA KUCHUKUA!

      Mtu akiniuliza kwa nini Biblia inashutumu ngono kati ya watu wa jinsia moja nitajibu ․․․․․

      Ikiwa mtu anasema kwamba maoni ya Biblia yamepita kiasi, nitamsadikisha kwa kusema ․․․․․

      Mambo ambayo ningependa kuuliza mzazi (wazazi) wangu kuhusu jambo hili ni ․․․․․

      UNA MAONI GANI?

      ● Kwa nini Mungu anakataza ngono kati ya watu wa jinsia moja?

      ● Unaweza kuchukua hatua gani ili usinaswe na mtego wa ngono kati ya watu wa jinsia moja?

      ● Kuwa na maoni kama ya Mungu kuhusu ngono kati ya watu wa jinsia moja kunamaanisha kwamba wewe ni mtu mwenye ubaguzi au chuki kali kuelekea watu wenye mazoea hayo?

      [Blabu katika ukurasa wa 236]

      ‘‘Maoni mapotovu ya ulimwengu yaliathiri sana akili yangu, na kufanya nichanganyikiwe. Sasa mimi huepuka kabisa kitu chochote au mtu yeyote ambaye anaunga mkono ngono kati ya watu wa jinsia moja.’’—Anna

      [Picha katika ukurasa wa 233]

      Vijana wote wanahitaji kufanya uamuzi—ikiwa watafuata maoni mapotovu ya ulimwengu kuhusu ngono au ikiwa watafuata viwango vilivyo katika Neno la Mungu

  • Nifanye Nini Ili Niache Kufikiria Ngono Saa Zote?
    Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, Buku la 2
    • SURA YA 29

      Nifanye Nini Ili Niache Kufikiria Ngono Saa Zote?

      “MIMI hujikuta nikifikiria wasichana saa zote—hata wakati ambapo hawapo,” asema kijana mmoja anayeitwa Michael. “Sielewi. Nyakati nyingine siwezi kukazia fikira jambo lolote!”

      Je, wewe hutumia saa nyingi ukiwaza juu ya watu wa jinsia tofauti, kama anavyofanya Michael? Ikiwa ndivyo, huenda ukahisi kana kwamba unapigana vita na akili yako. Fikira za ngono huingia akilini mwako kama jeshi la adui. “Fikira hizo zinaweza kukutawala,” asema Michael. “Zinaweza kukufanya uzunguke njia ndefu ili tu umtupie jicho msichana fulani mrembo, au kutembea-tembea dukani wakati ambapo hukusudii kununua chochote ili tu umtazame mtu fulani kwa ukaribu.”

      Hata hivyo, kumbuka kwamba kuwa na hisia za ngono si dhambi. Mungu alimuumba mwanamume na mwanamke wakiwa na uvutano wenye nguvu kati yao, na hakuna ubaya wa kutosheleza tamaa za ngono katika mpango wa ndoa. Kabla ya kufunga ndoa, huenda ukawa na tamaa kali za ngono. Hilo likitokea, usidhani kwamba wewe ni mtu mwovu au kwamba huwezi kuishi maisha safi. Unaweza kudumisha usafi wa kiadili ukiamua kufanya hivyo! Lakini ili ufanikiwe, utahitaji kudhibiti mawazo yako kuhusu watu wa jinsi tofauti. Unaweza kufanya hivyo jinsi gani?

      Angalia watu unaoshirikiana nao. Wanafunzi wenzako wakianza kuzungumzia mambo ya ngono, huenda ukataka kuchangia mazungumzo hayo—ili tu usionekane mshamba. Hata hivyo, kwa kweli kushiriki mazungumzo hayo kutafanya iwe vigumu zaidi kwako kudhibiti mawazo yako. Ufanye nini? Usimame tu na kuondoka? Ndiyo, na usione aibu kufanya hivyo! Mara nyingi inawezekana kuondoka pasipo kuonekana “mtakatifu” au kuwafanya wenzako wakucheke.

      Epuka kujifurahisha kwa mambo machafu. Bila shaka, haimaanishi kwamba sinema zote, au miziki yote ni mibaya. Hata hivyo, katika ulimwengu wa leo burudani nyingi zimekusudiwa kuamsha tamaa zisizofaa za ngono. Biblia inatoa shauri gani? “Acheni tujisafishe wenyewe kila unajisi wa mwili na roho, tukiukamilisha utakatifu katika kumwogopa Mungu.” (2 Wakorintho 7:1) Epuka kabisa burudani zote zinazoweza kuchochea tamaa zisizofaa za ngono.a

      Tatizo la Kupiga Punyeto

      Vijana fulani hujaribu kupunguza tamaa ya ngono kwa kupiga punyeto. Lakini kufanya hivyo kunaweza kutokeza matatizo makubwa. Biblia inawahimiza Wakristo hivi: “Viueni viungo vya mwili wenu vilivyo duniani kwa habari ya uasherati, uchafu, hamu ya ngono, tamaa yenye madhara, na kutamani.” (Wakolosai 3:5) Kupiga punyeto ni kinyume kabisa cha ‘kuua hamu ya ngono.’ Kwa kweli, kupiga punyeto huchochea na kukuza hamu hiyo!

      Kupiga punyeto kwaweza kukufanya kuwa mtumwa wa tamaa zako. (Tito 3:3) Hatua moja unayoweza kuchukua ili kushinda zoea hilo ni kuzungumza na mtu unayemtumaini. Mkristo aliyekuwa na tatizo la kupiga punyeto kwa miaka mingi anasema hivi: “Laiti ningeweza kupata ujasiri wa kuzungumza na mtu fulani kuhusu tatizo hilo nilipokuwa kijana! Kwa miaka mingi nilisumbuliwa na hisia za hatia, nazo ziliathiri sana uhusiano wangu na wengine, na zaidi ya yote, uhusiano wangu na Yehova.”

      Ni nani unayeweza kuongea naye? Mara nyingi ingefaa kuzungumza na mzazi. Au huenda Mkristo mkomavu kutanikoni anaweza kukusaidia. Unaweza kuanza kwa kusema, “Ningependa kuzungumza nawe kuhusu tatizo linalonisumbua sana.”

      André aliongea na mzee Mkristo, naye anafurahi kwamba alifanya hivyo. “Mzee huyo alipokuwa akinisikiliza, alilengwa-lengwa na machozi,” André anasema. “Nilipomaliza kuzungumza, alinihakikishia kwamba Yehova ananipenda. Aliniambia kwamba watu wengi wana tatizo kama langu. Aliahidi kwamba atakuwa akizungumza nami mara kwa mara kuona nimefanya maendeleo kiasi gani na kuniletea habari zaidi kutoka katika vitabu vinavyotegemea Biblia. Baada ya kuongea naye, niliazimia kupiga vita zoea hilo—hata ikiwa ningeanguka mara moja moja.”

      Mário aliamua kuongea na baba yake, aliyemjali sana na kuelewa hali yake. Hata alikiri mbele za Mário kwamba alipokuwa kijana haikuwa rahisi kwake kushinda zoea hilo. “Nilitiwa moyo sana na mazungumzo hayo ya waziwazi na unyoofu wa baba yangu,” asema Mário. “Nilijiambia, ikiwa alifaulu, hata mimi nitafaulu. Niliguswa moyo sana na mtazamo wa baba yangu hivi kwamba sikujizuia kulia.”

      Kama André na Mário, wewe pia unaweza kupata msaada wa kushinda zoea la kupiga punyeto. Hata ukijikuta umetumbukia tena, usikate tamaa! Uwe na hakika kwamba unaweza kushinda vita hivyo.b

      Dhibiti Fikira Zako

      Mtume Paulo alisema: “Naupigapiga mwili wangu na kuuongoza kama mtumwa.” (1 Wakorintho 9:27) Vivyo hivyo, huenda wewe pia ukahitaji kujitia nidhamu wakati mawazo yasiyofaa kuhusu watu wa jinsia tofauti yanapoingia katika akili yako. Mawazo hayo yakiendelea, jaribu kufanya mazoezi ya kimwili. Biblia inasema: “Mazoezi ya kimwili ni yenye faida kidogo.” (1 Timotheo 4:8) Kutembea kasi kwa muda au kufanya mazoezi ya kimwili kwa dakika chache kwaweza kukusaidia kuondolea mbali mawazo hayo yasiyofaa.

      Zaidi ya yote, usipuuze msaada kutoka kwa Baba yako wa mbinguni. Mkristo mmoja anasema hivi: “Tamaa za ngono zinapoanza kuamka najilazimisha kusali.” Si kwamba Mungu atakufanya uache kupendezwa na watu wa jinsia tofauti. Lakini anaweza kukusaidia kuona kwamba kuna mambo mengine mengi unayoweza kukazia fikira zako.

      [Maelezo ya Chini]

      a Tafrija na burudani zinazungumziwa kwa mapana na marefu katika Sehemu ya 8 ya kitabu hiki.

      b Habari zaidi kuhusu zoea la kupiga punyeto zinazungumziwa katika Buku la 1, sura ya 25.

      MAANDIKO MUHIMU

      “Wema wa adili wowote ulioko na jambo lolote la kustahili sifa lililoko, endeleeni kuyafikiria mambo hayo.”—Wafilipi 4:8.

      PENDEKEZO

      Ikiwa umetumbukia tena katika zoea la kupiga punyeto, endelea kupambana! Chunguza kwa makini kilichokufanya urudie zoea hilo, na ujaribu kukiepuka.

      JE, WAJUA . . .?

      Mambo unayoruhusu yakae akilini mwako yanaweza kuwa na uvutano juu ya utu wako na kuathiri matendo yako.—Yakobo 1:14, 15.

      HATUA ZA KUCHUKUA!

      Ili niache kufikiria sana watu wa jinsia tofauti, nita ․․․․․

      Wanafunzi wenzangu wakianza kuzungumzia mambo yasiyofaa au machafu kiadili, nita ․․․․․

      Mambo ambayo ningependa kuuliza mzazi (wazazi) wangu kuhusu habari hii ni ․․․․․

      UNA MAONI GANI?

      ● Kwa nini hisia za ngono hazipaswi kuonwa kuwa “adui” nyakati zote?

      ● Kwa nini unahitaji kudhibiti hisia zako za ngono?

      ● Ni burudani za aina gani zinazoweza kukufanya ukazie fikira watu wa jinsia tofauti?

      ● Kwa nini ni muhimu kuondoka wakati mazungumzo yanapoanza kuwa yasiyofaa au machafu?

      [Blabu katika ukurasa wa 240]

      ‘‘Kinachonisaidia ni kuanza kufikiria mambo mengine—kutoa fikira zangu katika mambo yanayoamsha tamaa za ngono. Mimi hujikumbusha kwamba hisia na tamaa hizo zitakwisha mwishowe.’’—Scott

      [Picha katika ukurasa wa 239]

      Ungekubali kompyuta yako iingiwe na virusi? Basi kwa nini uingize mawazo yasiyofaa akilini mwako?

  • Daftari—Hisia Zako
    Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, Buku la 2
    • SEHEMU YA 7

      Daftari—Hisia Zako

      Ni hisia gani inayokulemea sana, nayo inakuathiri jinsi gani?

      ․․․․․

      Habari iliyo katika sehemu hii inaweza kukusaidia jinsi gani kushughulikia hisia hiyo wakati ujao?

      ․․․․․

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki