Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Mungu Anataka Tufanye Nini?
    Mnara wa Mlinzi—1997 | Januari 15
    • Mungu Anataka Tufanye Nini?

      “Hivi ndivyo kumpenda Mungu humaanisha, kwamba tushike amri zake; na bado amri zake si zenye kulemea.”—1 YOHANA 5:3.

      1, 2. Kwa nini haishangazi kwamba Mungu ana matakwa kwa wale watakao kumwabudu kwa njia ya kukubalika?

      “DINI yangu yanipendeza!” Je, sivyo wasemavyo watu mara nyingi? Lakini, kwa kweli, swali lapaswa liwe, “Je, dini yangu inampendeza Mungu?” Ndiyo, Mungu ana matakwa kwa wale wanaotaka kumwabudu kwa kukubalika. Je, hilo litushangaze? Sivyo hasa. Tuseme ungekuwa na nyumba yenye kupendeza, ambayo ulirekebisha upya hivi majuzi kwa gharama kubwa. Je, ungemruhusu mtu yeyote yule aishi huko? Bila shaka la! Yeyote yule ambaye angekuwa mpangaji angelazimika kutimiza matakwa yako.

      2 Vivyo hivyo, Yehova ameandalia familia ya kibinadamu makao haya ya kidunia. Chini ya utawala wa Ufalme wake, karibuni dunia ‘itarekebishwa upya’—itageuzwa kuwa paradiso yenye kupendeza. Yehova atatimiza hili. Kwa gharama kubwa kwake mwenyewe, alimtoa Mwanaye mzaliwa-pekee ili kuwezesha hilo. Kwa hakika, ni lazima Mungu awe ana matakwa kwa wale watakaoishi huko!—Zaburi 115:16; Mathayo 6:9, 10; Yohana 3:16.

      3. Solomoni alitoaje muhtasari wa yale ambayo Mungu atazamia tufanye?

      3 Twaweza kupataje kujua matakwa ya Mungu? Yehova alimpulizia Mfalme Solomoni mwenye hekima atoe muhtasari wa yale ambayo Yeye atazamia tufanye. Baada ya kutafakari juu ya mambo yote aliyokuwa amefuatia—kutia na utajiri, miradi ya ujenzi, upendezi wa muziki mbalimbali, na upendo wa kimahaba—Solomoni alifikia utambuzi huu: “Hii ndiyo jumla ya maneno; yote yamekwisha sikiwa; mche Mungu, nawe uzishike amri zake, maana kwa jumla ndiyo impasayo mtu.”—Mhubiri 12:13, italiki ni zetu.

      “Amri Zake Si Zenye Kulemea”

      4-6. (a) Ni nini maana halisi ya neno la Kigiriki linalotafsiriwa ‘-enye kulemea’? (b) Kwa nini twaweza kusema kwamba amri za Mungu si zenye kulemea?

      4 “Uzishike amri zake.” Kwa msingi, hilo ndilo Mungu atazamia tufanye. Je, anaomba mengi mno? La hasha. Mtume Yohana atuambia jambo fulani lenye kutia moyo sana juu ya amri, au matakwa, ya Mungu. Aliandika hivi: “Hivi ndivyo kumpenda Mungu humaanisha, kwamba tushike amri zake; na bado amri zake si zenye kulemea.”—1 Yohana 5:3.

      5 Neno la Kigiriki linalotafsiriwa ‘-enye kulemea’ lamaanisha kihalisi “-zito.” Laweza kurejezea jambo lililo gumu kuishi kulingana nalo au lililo gumu kufuata. Kwenye Mathayo 23:4, neno lilo hilo linatumiwa kufafanua ile “mizigo mizito,” yaani amri na mapokeo ya kufanywa na wanadamu, ambayo waandishi na Mafarisayo waliwekea watu. Je, unapata maana ya mkataa unaofikiwa na mtume Yohana mwenye umri mkubwa? Amri za Mungu si mzigo mzito wenye kulemea, wala si ngumu sana tusiweze kuzitimiza. (Linganisha Kumbukumbu la Torati 30:11.) Kinyume cha hilo, tunapompenda Mungu, kutimiza matakwa yake hutufurahisha. Hutupa sisi fursa yenye thamani ya kuonyesha kumpenda kwetu Yehova.

      6 Ili kuonyesha kumpenda kwetu Mungu, twahitaji kujua kimahususi yale ambayo yeye atazamia tufanye. Acheni sasa tuchunguze matano kati ya matakwa ya Mungu. Tufanyapo hivyo, kumbuka yale aliyoandika Yohana: ‘Amri za Mungu si zenye kulemea.’

      Kuendelea Kutwaa Ujuzi juu ya Mungu

      7. Wokovu wetu wategemea nini?

      7 Takwa la kwanza ni kuendelea kutwaa ujuzi juu ya Mungu. Fikiria maneno ya Yesu yaliyorekodiwa katika Yohana sura ya 17. Kikao kilikuwa usiku wa mwisho wa uhai wa Yesu akiwa binadamu. Yesu alikuwa ametumia sehemu kubwa ya jioni hiyo akiwatayarisha mitume wake kwa ajili ya kuondoka kwake. Yesu alihangaikia wakati ujao wao, wakati ujao wao udumuo milele. Akiinua macho yake mbinguni, yeye alisali kwa ajili yao. Katika mstari wa 3, twasoma hivi: ‘Hii yamaanisha uhai udumuo milele, wao kuendelea kutwaa ujuzi juu yako wewe, Mungu pekee wa kweli, na juu ya yule uliyemtuma, Yesu Kristo.’ Ndiyo, wokovu wao ulitegemea ‘kuendelea kwao kutwaa ujuzi’ juu ya Mungu na pia Kristo. Hilo latuhusu sisi pia. Ili tupate wokovu, ni lazima tuendelee kutwaa ujuzi huo.

      8. ‘Kuendelea kutwaa ujuzi’ juu ya Mungu kwamaanisha nini?

      8 “Kuendelea kutwaa ujuzi” juu ya Mungu kwamaanisha nini? Neno la Kigiriki linalotafsiriwa hapa “kuendelea kutwaa ujuzi” lamaanisha “kupata kujua, kufahamu,” au “kuelewa kikamili.” Ona pia, kwamba ufasiri “kuendelea kutwaa ujuzi” wadokeza kwamba hiyo ni hatua yenye kuendelea. Hivyo, kuendelea kutwaa ujuzi juu ya Mungu kwamaanisha kupata kumjua si kijuujuu bali kindani, kusitawisha urafiki wenye uelewevu pamoja naye. Uhusiano wenye kuendelea pamoja na Mungu huleta ujuzi wenye kuongezeka daima juu yake. Hatua hiyo yaweza kuendelea milele, kwani hatutajifunza kamwe mambo yote juu ya Yehova.—Waroma 11:33.

      9. Twaweza kujifunza nini juu ya Yehova kutoka kitabu cha uumbaji?

      9 Twaendeleaje kutwaa ujuzi juu ya Mungu? Kuna vitabu viwili viwezavyo kutusaidia. Kimoja ni kitabu cha uumbaji. Vitu ambavyo Yehova ameumba—vyenye uhai na pia visivyo na uhai—hutupa sisi ufahamu fulani wenye kina juu ya aina ya mtu alivyo. (Waroma 1:20) Fikiria vielelezo fulani. Kunguruma kwa poromoko la maji lenye fahari, kuponda-ponda kwa mawimbi wakati wa dhoruba, mwono wa mbingu zenye nyota katika usiku usio na mawingu—je, mambo kama hayo hayatufundishi kwamba Yehova ni Mungu aliye “hodari kwa nguvu”? (Isaya 40:26) Mtoto achekaye aonapo kitoto cha mbwa kikifuata-fuata mkia wacho au kitoto cha paka kikicheza na tufe la uzi wa sufu—je, hilo halidokezi kwamba Yehova, “Mungu mwenye furaha,” ana ucheshi? (1 Timotheo 1:11) Ladha ya mlo mtamu, harufu yenye kupendeza ya maua shambani, rangi nyangavu za kipepeo mwororo, sauti za ndege wakiimba wakati wa masika, kumbatio changamfu la mpendwa—je, hatutambui kutokana na mambo haya kwamba Muumba wetu ni Mungu mwenye upendo, anayetaka tufurahie uhai?—1 Yohana 4:8.

      10, 11. (a) Ni mambo gani juu ya Yehova ambayo hatuwezi kujifunza kutoka kitabu cha uumbaji? (b) Ni majibu ya maswali yapi yanayopatikana katika Biblia tu?

      10 Hata hivyo, kuna mpaka kwa yale tuwezayo kujifunza juu ya Yehova kutokana na kitabu cha uumbaji. Kwa kielelezo: Jina la Mungu ni nani? Kwa nini aliumba dunia akawaweka wanadamu juu yayo? Kwa nini Mungu anaruhusu uovu? Wakati ujao una nini kwa ajili yetu? Ili kupata majibu kwa maswali hayo, ni lazima tuendee kile kitabu kingine kinachotoa ujuzi juu ya Mungu—Biblia. Katika kurasa zacho, Yehova hufunua mambo juu yake mwenyewe, kutia na jina lake, utu wake, na makusudi yake—habari ambayo hatuwezi kupata kutoka chanzo kingine chochote.—Kutoka 34:6, 7; Zaburi 83:18; Amosi 3:7.

      11 Katika Maandiko, Yehova hutoa pia ujuzi muhimu juu ya watu wengine ambao twahitaji kujua juu yao. Kwa kielelezo, Yesu Kristo ni nani, naye ana sehemu gani katika kutimizwa kwa makusudi ya Yehova? (Matendo 4:12) Shetani Ibilisi ni nani? Yeye huwaongoza watu vibaya katika njia zipi? Twaweza kuepukaje kuongozwa vibaya naye? (1 Petro 5:8) Majibu yenye kuokoa uhai ya maswali haya yanapatikana katika Biblia tu.

      12. Ungeelezaje ni kwa nini kuendelea kutwaa ujuzi juu ya Mungu na makusudi yake si mzigo wenye kulemea?

      12 Je, kuendelea kutwaa ujuzi huo juu ya Mungu na makusudi yake ni mzigo wenye kulemea? La hasha! Je, waweza kukumbuka jinsi ulivyohisi ulipojifunza kwa mara ya kwanza kwamba jina la Mungu ni Yehova, kwamba Ufalme wake utarudisha Paradiso kwenye dunia hii, kwamba alimtoa Mwana wake mpendwa awe fidia kwa ajili ya dhambi zetu, pamoja na kweli nyinginezo zenye thamani? Je, hilo halikuwa kama kuondoa shela ya ukosefu wa ujuzi na kuona mambo kwa wazi kwa mara ya kwanza? Kuendelea kutwaa ujuzi juu ya Mungu si mzigo wenye kulemea. Ni jambo lenye kupendeza!—Zaburi 1:1-3; 119:97.

      Kufikia Viwango vya Mungu

      13, 14. (a) Tuendeleapo kutwaa ujuzi juu ya Mungu, ni mabadiliko gani tunayohitaji kufanya maishani mwetu? (b) Mungu anataka kwamba tuepuke mazoea gani yasiyo safi?

      13 Tuendeleapo kutwaa ujuzi juu ya Mungu, twapata kung’amua kwamba twahitaji kufanya mabadiliko katika maisha zetu. Hilo latuleta kwenye takwa la pili. Ni lazima tufikie viwango vya Mungu vya mwenendo sawa na kukubali kweli yake. Kweli ni nini? Je, kwa kweli Mungu hujali kile tunachoamini na kile tunachofanya? Ni wazi kwamba watu wengi leo hawaoni kwamba anajali. Ripoti iliyochapishwa na Kanisa la Uingereza katika 1995 ilidokeza kwamba kuishi pamoja bila kufunga ndoa hakupasi kuonwa kuwa dhambi. “Maneno ‘kuishi katika dhambi’ yaaibisha na si yenye kusaidia,” akasema askofu mmoja wa kanisa.

      14 Kwa hiyo basi, je, “kuishi katika dhambi” si dhambi tena? Yehova hutuambia kwa udhahiri kabisa jinsi ahisivyo juu ya mwenendo wa aina hiyo. Neno lake, Biblia, hutaarifu hivi: “Acheni ndoa iwe yenye kuheshimika miongoni mwa wote, na kitanda cha ndoa kiwe bila kutiwa unajisi, kwa maana Mungu atawahukumu waasherati na wazinzi.” (Waebrania 13:4) Kufanya ngono kabla ya ndoa huenda kusiwe dhambi kwa maoni ya makasisi na waenda-kanisani wasio na uzuizi kiadili, lakini ni dhambi nzito machoni pa Mungu! Ndivyo na uzinzi, ngono ya maharimu (watu wa ukoo), na ugoni-jinsia-moja. (Mambo ya Walawi 18:6; 1 Wakorintho 6:9, 10) Mungu ataka kwamba tuepuke mazoea ya aina hiyo, anayoona kuwa yasiyo safi.

      15. Matakwa ya Mungu huhusishaje njia tunayowatendea wengine na pia kile tunachoamini?

      15 Hata hivyo, haitoshi kuepuka tu mazoea ambayo Mungu huona kuwa yenye dhambi. Matakwa ya Mungu hutia ndani pia njia tunayotendea wengine. Katika familia, yeye atazamia mume na mke wapendane na kustahiana. Mungu anataka wazazi watunze mahitaji ya watoto wao ya kimwili, ya kiroho, na ya kihisia-moyo. Anawaambia watoto wawe watiifu kwa wazazi wao. (Mithali 22:6; Wakolosai 3:18-21) Na namna gani itikadi zetu? Yehova Mungu anataka tuepuke itikadi na desturi zinazotokana na ibada isiyo ya kweli au ambazo hupinga ile kweli safi inayofundishwa katika Biblia.—Kumbukumbu la Torati 18:9-13; 2 Wakorintho 6:14-17.

      16. Eleza ni kwa nini kufikia viwango vya Mungu vya mwenendo sawa na kukubali kweli yake si mzigo wenye kulemea.

      16 Je, kufikia kwetu viwango vya Mungu vya mwenendo sawa na kukubali kweli yake ni mzigo wenye kulemea? Sivyo tunapofikiria manufaa—ndoa ambazo katika hizo mume na mke wanapendana na wana itibari katika mmoja na mwenzake badala ya ndoa ambazo zimevunjika kwa sababu ya ukosefu wa uaminifu; makao ambako watoto huhisi wanapendwa na wanatakwa na wazazi wao badala ya familia ambazo katika hizo watoto wanahisi hawapendwi, wanapuuzwa, na hawatakwi; dhamiri safi na afya njema badala ya hisia za kuwa na hatia na mwili uliokumbwa na UKIMWI au maradhi mengine ya kupitishwa kingono. Kwa hakika, matakwa ya Yehova hayatunyimi chochote kile tunachohitaji ili kufurahia uhai!—Kumbukumbu la Torati 10:12, 13.

      Stahi Uhai na Damu

      17. Yehova huonaje uhai na damu?

      17 Upatanishapo maisha yako na viwango vya Mungu, unapata kuthamini jinsi uhai ulivyo wenye thamani kikweli. Acheni sasa tuzungumzie takwa la tatu la Mungu. Ni lazima tustahi uhai na damu. Uhai ni mtakatifu kwa Yehova. Wapaswa uwe hivyo, kwa maana yeye ndiye Chanzo cha uhai. (Zaburi 36:9) Kwani, hata uhai wa mtoto asiyezaliwa bado aliye ndani ya mama yake ni wenye thamani kwa Yehova! (Kutoka 21:22, 23) Damu huwakilisha uhai. Kwa hiyo, damu ni takatifu pia machoni pa Mungu. (Mambo ya Walawi 17:14) Basi, si ajabu kwamba Mungu atazamia tuone uhai na damu jinsi anavyoviona.

      18. Maoni ya Yehova juu ya uhai na damu yataka tufanye nini?

      18 Kustahi uhai na damu kwataka tufanye nini? Tukiwa Wakristo, sisi hatuhatarishi uhai wetu bure ili kupata msisimko tu. Sisi ni wenye kujali usalama, kwa hiyo tunahakikisha kwamba magari yetu na nyumba zetu ni salama. (Kumbukumbu la Torati 22:8) Hatutumii tumbaku, hatutafuni miraa, au kutumia dawa zisababishazo uraibu au za kulevya ili kuona raha. (2 Wakorintho 7:1) Kwa sababu twamsikiliza Mungu asemapo ‘jiepusheni na damu,’ haturuhusu damu itiwe miilini mwetu. (Matendo 15:28, 29) Ingawa twapenda uhai, hatutajaribu kuokoa uhai wetu wa sasa kwa kuvunja sheria ya Mungu na hivyo kuhatarisha taraja letu la uhai udumuo milele!—Mathayo 16:25.

      19. Eleza jinsi tunavyonufaika kutokana na kustahi uhai na damu.

      19 Je, kuona kwetu uhai na damu kuwa takatifu ni mzigo wenye kulemea? La, hasha! Ebu fikiria. Je, uhuru pasipo kansa ya mapafu inayosababishwa na kuvuta tumbaku ni mzigo wenye kulemea? Je, kuponyoka uraibu wa kiakili na wa kimwili wa madawa yenye kudhuru ni mzigo wenye kulemea? Je, kuepuka kupatwa na UKIMWI, mchochota wa ini, au maradhi mengine yanayotokana na utiaji-damu mishipani ni mzigo wenye kulemea? Kwa wazi, kujiepusha kwetu na tabia na mazoea yenye kudhuru ni kwa faida yetu.—Isaya 48:17.

      20. Familia moja ilinufaikaje kutokana na kuwa na maoni ya Mungu juu ya uhai?

      20 Fikiria ono hili. Miaka kadhaa iliyopita, mwanamke Shahidi aliyekuwa na mimba ya karibu miezi mitatu na nusu alianza kutokwa na damu jioni moja naye akapelekwa hospitali mbio. Baada ya daktari kumchunguza, mwanamke huyo alimsikia akimwambia mmoja wa wauguzi kwamba wangelazimika kuikomesha mimba hiyo. Akijua maoni ya Yehova juu ya uhai wa watoto wasiozaliwa bado, yeye alikataa katakata utoaji-mimba akimwambia daktari hivi: “Ikiwa yu hai, mwache humo!” Aliendelea kutokwa na damu mara kwa mara, lakini miezi kadhaa baadaye alizaa kabla ya wakati wake, kitoto kivulana chenye afya, ambaye sasa ni mwenye umri wa miaka 17. Alieleza hivi: “Mwana wetu aliambiwa haya yote, naye alisema anaterema kwamba hakutupwa. Ajua kwamba sababu tu ya yeye hata kuwa hai ni kumtumikia kwetu Yehova.” Kwa hakika, kuwa na maoni ya Mungu juu ya uhai hakukuwa mzigo wenye kulemea kwa familia hii!

      Kutumikia Pamoja na Watu wa Yehova Waliofanywa Kuwa Tengenezo

      21, 22. (a) Yehova atazamia tumtumikie pamoja na nani? (b) Watu wa Mungu waliofanywa kuwa tengenezo wanaweza kutambuliwaje?

      21 Sisi hatuko peke yetu katika kufanya mabadiliko yanayohitajiwa ili kuzipatanisha maisha zetu na viwango vya Mungu. Yehova ana watu kwenye dunia hii, naye atazamia tumtumikie pamoja nao. Hilo latuleta kwenye takwa la nne. Ni lazima tumtumikie Yehova pamoja na tengenezo lake lenye kuelekezwa kwa roho.

      22 Lakini, watu wa Mungu waliofanywa kuwa tengenezo wanaweza kutambuliwaje? Kulingana na viwango vilivyomo katika Maandiko, wao wana upendo halisi miongoni mwao wenyewe, wana staha yenye kina kuelekea Biblia, wanaheshimu jina la Mungu, wanahubiri juu ya Ufalme wake, nao si sehemu ya ulimwengu huu mwovu. (Mathayo 6:9; 24:14; Yohana 13:34, 35; 17:16, 17) Kuna tengenezo moja tu la kidini kwenye dunia hii lililo na alama hizi zote za Ukristo wa kweli—Mashahidi wa Yehova!

      23, 24. Twaweza kuonyesha kwa kielezi gani kwamba kumtumikia Yehova pamoja na watu wake waliofanywa kuwa tengenezo si mzigo wenye kulemea?

      23 Je, kumtumikia Yehova pamoja na watu wake waliofanywa kuwa tengenezo ni mzigo wenye kulemea? La hasha! Kinyume cha hilo, ni pendeleo lenye thamani kuwa na upendo na utegemezo wa familia ya ulimwenguni pote ya ndugu na dada Wakristo! (1 Petro 2:17) Ebu wazia umeokoka mvunjiko wa meli na wajipata majini, uking’ang’ana kuelea. Unapohisi kwamba huwezi kuvumilia zaidi, mkono wakufikilia kutoka katika mashua ya kuokolea uhai. Ndiyo, kuna waokokaji wengine! Katika mashua hiyo ya kuokolea uhai, wewe na wengine mnapiga makasia kwa zamu hadi pwani mkiwachukua waokokaji wengine njiani.

      24 Je, sisi hatumo katika hali iyo hiyo? Tumevutwa kutoka katika “maji” yenye hatari ya ulimwengu huu mwovu kuingia katika “mashua ya kuokolea uhai” ya tengenezo la kidunia la Yehova. Humo, twatumikia sambamba tuelekeapo “pwani” ya ulimwengu mpya wenye uadilifu. Misongo ya maisha haya ikitufanya tuchoke njiani, twashukuru kama nini kwa msaada na faraja ya waandamani Wakristo wa kweli!—Mithali 17:17.

      25. (a) Tuna wajibu gani kuelekea wale ambao wangali katika “maji” ya ulimwengu huu mwovu? (b) Ni takwa gani la Mungu litakalozungumziwa katika makala inayofuata?

      25 Namna gani wengine—watu wenye mioyo ya haki ambao wangali katika “maji”? Tuna wajibu wa kuwasaidia waingie katika tengenezo la Yehova, sivyo? (1 Timotheo 2:3, 4) Wanahitaji msaada ili wajifunze yale ambayo Mungu anataka. Hilo latuleta kwenye takwa la Mungu la tano. Ni lazima tuwe wapiga-mbiu waaminifu-washikamanifu wa Ufalme wa Mungu. Yanayohusishwa katika hilo yatazungumziwa katika makala ifuatayo.

  • Kusaidia Wengine Wajifunze Matakwa ya Mungu
    Mnara wa Mlinzi—1997 | Januari 15
    • Kusaidia Wengine Wajifunze Matakwa ya Mungu

      “Nimewekewa sharti. Kwa kweli, ole wangu mimi ikiwa sikutangaza habari njema!”—1 WAKORINTHO 9:16.

      1, 2. (a) Yehova anataka tushiriki katika kazi gani yenye sehemu mbili? (b) Ni lazima watu wenye mioyo ya haki wajifunze nini ili wapate kuwa raia wa Ufalme wa Mungu?

      YEHOVA ana habari njema kwa ajili ya wanadamu. Yeye ana Ufalme, naye ataka watu kila mahali wasikie juu yao! Mara tunapojifunza habari njema hiyo, Mungu anataka tuishiriki na wengine. Hii ni kazi yenye sehemu mbili. Kwanza, ni lazima tupige mbiu ya habari njema ya Ufalme wa Mungu. Katika unabii wake juu ya “umalizio wa mfumo wa mambo,” Yesu alisema hivi: “Habari njema hii ya ufalme itahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa kwa ajili ya kuwa ushahidi kwa mataifa yote; na ndipo mwisho utakapokuja.”—Mathayo 24:3, 14.

      2 Sehemu ya pili ya kazi hiyo yahusisha kufundisha wale wanaoitikia vizuri kupigwa mbiu kwa Ufalme. Baada ya ufufuo wake, Yesu aliambia kikundi kikubwa cha wanafunzi wake hivi: “Kwa hiyo nendeni mkafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote, kuwabatiza katika jina la Baba na la Mwana na la roho takatifu, kuwafundisha kushika mambo yote ambayo mimi nimewaamuru nyinyi. Na, tazameni! mimi nipo pamoja nanyi siku zote hadi umalizio wa mfumo wa mambo.” (Mathayo 28:19, 20) ‘Mambo ambayo Kristo alikuwa ameamuru’ hayakutokana naye; aliwafundisha wengine washike amri, au matakwa ya Mungu. (Yohana 14:23, 24; 15:10) Hivyo, kuwafundisha wengine ‘washike mambo ambayo Kristo ameamuru’ kwahusisha kuwasaidia wajifunze matakwa ya Mungu. Ni lazima watu wenye mioyo ya haki watimize matakwa ya Mungu ili wapate kuwa raia wa Ufalme wake.

      3. Ufalme wa Mungu ni nini, nao utatimiza nini kifanyacho ujumbe wa Ufalme uwe habari njema hivyo?

      3 Ufalme wa Mungu ni nini? Nao utatimiza nini kifanyacho ujumbe wa Ufalme uwe habari njema hivyo? Ufalme wa Mungu ni serikali ya kimbingu. Huo ni wenye thamani sana moyoni mwa Yehova, kwani ndiyo njia atakayotumia ili kulitakasa jina lake, na kuliondolea suto lote. Ufalme ndio chombo ambacho Yehova atatumia kufanya mapenzi yake yatimizwe duniani kama mbinguni. Hiyo ndiyo sababu Yesu alitufundisha tusali kwamba Ufalme wa Mungu uje na alitusihi sana kuutanguliza katika maisha zetu. (Mathayo 6:9, 10, 33) Je, wewe waona ni kwa sababu gani ni jambo la maana sana kwa Yehova kwamba tuwafundishe wengine juu ya Ufalme wake?

      Jambo Gumu Lakini Si Mzigo Wenye Kulemea

      4. Ni kielezi gani kiwezacho kutumiwa ili kuonyesha kwamba wajibu wetu wa kuhubiri habari njema si mzigo wenye kulemea?

      4 Je, kuhubiri habari njema hii ni mzigo wenye kulemea? Sivyo hata kidogo! Kwa kutoa kielezi: Baba ana wajibu wa kuiandalia familia yake kimwili. Akishindwa kufanya hivyo ni kama ameikana imani ya Kikristo. Mtume Paulo aliandika hivi: “Hakika ikiwa yeyote hawaandalii kitu wale walio wake mwenyewe, na hasa kwa ajili ya wale walio washiriki wa nyumbani mwake, ameikana imani naye ni mbaya zaidi kuliko mtu asiye na imani.” (1 Timotheo 5:8) Lakini je, wajibu huo ni mzigo wenye kulemea kwa mwanamume Mkristo? Sivyo ikiwa anaipenda familia yake, kwa maana ikiwa aipenda yeye ataka kuiandalia.

      5. Ingawa kazi ya kuhubiri na kufanya wanafunzi ni wajibu, kwa nini twapaswa kufurahia kuifanya?

      5 Vivyo hivyo, kazi ya kuhubiri na kufanya wanafunzi ni wajibu, ni takwa, ambao uhai wetu wenyewe wategemea. Paulo alieleza hivi: “Nimewekewa sharti. Kwa kweli, ole wangu mimi ikiwa sikutangaza habari njema!” (1 Wakorintho 9:16; linganisha Ezekieli 33:7-9.) Hata hivyo, nia yetu ya kuhubiri ni upendo, si wajibu tu. Kwanza kabisa twampenda Mungu, lakini pia twawapenda majirani wetu, na twajua jinsi lilivyo jambo la maana kwao kuisikia habari njema. (Mathayo 22:37-39) Inawapa tumaini la wakati ujao. Karibuni Ufalme wa Mungu utasahihisha udhalimu mbalimbali, utaondoa uonevu wote, na kurudisha amani na muungano—yote kwa baraka idumuyo milele ya wale wanaojitiisha chini ya utawala wao mwadilifu. Je, hatufurahi, ndiyo kusisimka, kushiriki na wengine habari njema hiyo?—Zaburi 110:3.

      6. Kwa nini kazi ya kuhubiri na kufanya wanafunzi hutokeza ugumu halisi?

      6 Wakati uleule, kazi hii ya kuhubiri na kufanya wanafunzi hutokeza ugumu halisi. Watu wako tofauti. Wote hawapendezwi na mambo yaleyale wala hawana uwezo uleule. Watu fulani ni wataalamu, hali wengine wana elimu kidogo sana. Kusoma—kulikokuwa wakati mmoja burudisho lililopendwa sana—sasa huonwa mara nyingi kuwa kazi ngumu isiyopendeza. Kutopenda kusoma, kunakofasiliwa kuwa “ubora au hali ya kujua kusoma lakini kutopendezwa kufanya hivyo,” ni tatizo linaloongezeka, hata katika nchi zenye watu wengi wanaojua kusoma na kuandika. Basi, twaweza kuwasaidiaje watu wenye malezi tofauti hivyo na wale wanaopendezwa na mambo tofauti wajifunze yale ambayo Mungu anataka?—Linganisha 1 Wakorintho 9:20-23.

      Wenye Kuandaliwa Vifaa Vifaavyo ili Kusaidia Wengine

      7. “Mtumwa mwaminifu na mwenye busara” ametuandaliaje vifaa ili kusaidia wengine wajifunze matakwa ya Mungu?

      7 Kazi ngumu hurahisishwa ukiwa na vyombo au vifaa vifaavyo. Chombo kifaacho kazi fulani leo huenda kikarekebishwa kwa njia fulani kesho au hata kutotumiwa tena kwa sababu ya mahitaji yanayobadilika. Ndivyo ilivyo kwa habari ya utume wetu wa kupiga mbiu ya ujumbe juu ya Ufalme wa Mungu. Katika miaka iliyopita, “mtumwa mwaminifu na mwenye busara” ametuandalia vyombo sahihi barabara, vichapo vilivyokusudiwa hasa kutumiwa katika kuongoza mafunzo ya Biblia nyumbani. (Mathayo 24:45) Hivyo tumeandaliwa vifaa ili kuwasaidia watu wa “mataifa yote na makabila na . . . lugha” wajifunze matakwa ya Mungu. (Ufunuo 7:9) Mara kwa mara, vyombo vipya vimeandaliwa ili kutosheleza mahitaji yanayobadilika katika shamba la ulimwengu. Ebu tufikirie vielelezo vichache.

      8. (a) Kitabu “Let God Be True” kilikuwa na sehemu gani katika kuendeleza elimu ya Biblia? (b) Ni chombo kipi cha kufanyia kazi ya funzo la Biblia kilichoandaliwa katika mwaka 1968, na kilitungwaje hasa? (c) Kitabu Kweli kilisaidiaje katika kazi ya kufanya wanafunzi?

      8 Tangu mwaka 1946 hadi 1968, kitabu “Let God Be True” kilitumiwa kuwa chombo chenye nguvu cha elimu ya Biblia, na nakala zipitazo 19,250,000 zilichapishwa katika lugha 54. Kitabu Kweli Iongozayo kwenye Uzima wa Milele kilichotolewa mwaka 1968, kilitumiwa miaka mingi kwa matokeo katika kujifunza Biblia pamoja na wenye kupendezwa. Hapo awali, lilikuwa jambo la kawaida kwa watu fulani kujifunza pamoja na Mashahidi wa Yehova kwa miaka mingi bila kubatizwa. Lakini chombo hicho kilitungwa ili kumhusisha mwanafunzi, na kumtia moyo atumie yale aliyokuwa akijifunza. Tokeo likawa nini? Kitabu Jehovah’s Witnesses—Proclaimers of God’s Kingdom chataarifu hivi: “Kwa ile miaka mitatu ya utumishi kuanzia Septemba 1, 1968, na kumalizika Agosti 31, 1971, jumla ya watu 434,906 walibatizwa—zaidi ya mara mbili ya idadi iliyobatizwa wakati wa miaka mitatu ya utumishi iliyotangulia!” Tangu kutolewa kwacho, kitabu Kweli kimekuwa na idadi ya kushangaza ya nakala zinazogawanywa—zaidi ya 107,000,000 katika lugha 117.

      9. Kitabu Kuishi Milele kina jambo gani la pekee, na kilikuwa na matokeo gani juu ya idadi ya wapiga-mbiu wa Ufalme?

      9 Katika 1982 kitabu Unaweza Kuishi Milele Katika Paradiso Duniani kilipata kuwa kitabu kikuu kilichotumiwa katika kuongoza mafunzo ya Biblia. Chombo hicho kina picha zaidi ya 150, kila moja yenye maelezo ya maana yanayokazia somo la picha kwa ufupi. Toleo la Huduma ya Ufalme Yetu la Oktoba 1982 katika Kiingereza, lilitaarifu hivi: “Katika ile miaka ipatayo 20 ambayo kitabu ‘Let God Be True’ kilikuwa kitabu chetu kikuu cha funzo (kutoka 1946 hadi katikati ya miaka ya 1960) tulipata ongezeko la wapiga-mbiu wapya zaidi ya 1,000,000. Kisha kukawa na ongezeko la watangazaji 1,000,000 wakati kitabu Kweli Iongozayo Kwenye Uzima wa Milele kilipopata kuwa kitabu chetu kikuu cha funzo baada ya kutolewa kwacho mwaka 1968. Kwa kutumia kitabu chetu kipya cha funzo, Unaweza Kuishi Milele Katika Paradiso Duniani, je, tutaona upanuzi uo huo katika idadi ya watangazaji wa Ufalme? Kwa hakika, ikiwa hayo ni mapenzi ya Yehova!” Ni wazi kwamba hayo yalikuwa mapenzi ya Yehova, kwa sababu kutoka 1982 hadi 1995, kulikuwako na ongezeko la zaidi ya 2,700,000 katika idadi ya wapiga-mbiu wa Ufalme!

      10. Ni chombo gani kipya kilichoandaliwa katika mwaka 1995, na kwa nini kwapaswa kuwezesha wanafunzi wa Biblia wafanye maendeleo ya kiroho upesi zaidi?

      10 “Mavuno ni mengi, lakini wafanyakazi ni wachache,” akasema Yesu. (Mathayo 9:37) Kwa kweli, mavuno ni mengi. Kuna mengi ya kufanywa bado. Katika nchi fulani lazima watu wanaongoja funzo la Biblia waandikwe majina katika orodha ya kungojea. Kwa hiyo ili kuweza kueneza ujuzi juu ya Mungu upesi zaidi, katika mwaka 1995 “mtumwa mwaminifu na mwenye busara” aliandaa chombo kipya, kile kitabu cha kurasa 192 chenye kichwa Ujuzi Uongozao Kwenye Uhai Udumuo Milele. Chombo hicho chenye thamani hakikazii mafundisho yasiyo ya kweli. Kinatoa kweli za Biblia katika njia chanya. Inatazamiwa kwamba kitawezesha wanafunzi wa Biblia wafanye maendeleo ya kiroho upesi zaidi. Kitabu Ujuzi tayari kimekuwa na matokeo juu ya shamba la ulimwengu kukiwa na uchapaji wa nakala 45,500,000 katika lugha 125 na utafsiri ukiendelea katika lugha nyingine 21.

      11. Ni chombo kipi chenye matokeo kilichoandaliwa ili kuwasaidia wasioweza kusoma wala kuandika au wale wasiojua kusoma vizuri, na kimechangiaje programu yetu ya kufundisha tufeni pote?

      11 Mara kwa mara, ‘mtumwa mwaminifu’ ameandaa vyombo vilivyokusudiwa wasikilizaji mahususi au fulani tu. Kwa kielelezo, namna gani watu ambao huenda wakahitaji msaada wa pekee kwa sababu ya malezi yao ya kitamaduni au ya kidini? Twaweza kuwasaidiaje wajifunze matakwa ya Mungu? Katika mwaka 1982 tulipokea tulichohitaji barabara—ile broshua ya kurasa 32 Furahia Milele Maisha Duniani! Kichapo hicho chenye picha nyingi kimekuwa chombo chenye matokeo katika kuwafundisha wale wasioweza kusoma wala kuandika au wale wasiojua kusoma vizuri. Kina utoaji sahili sana ulio rahisi kuelewa wa mafundisho ya Kimaandiko ya msingi. Tangu itolewe, broshua Maisha Duniani imechangia sana programu yetu ya kufundisha tufeni pote. Nakala zaidi ya 105,100,000 zimechapwa katika lugha 239, na kuifanya iwe kichapo chenye kutafsiriwa katika lugha nyingi kuliko kingine ambacho Watch Tower Society imetokeza hadi leo!

      12, 13. (a) Tangu mwaka 1990, ‘mtumwa mwaminifu’ ameandaa njia gani mpya ya kufikia wasikilizaji wengi? (b) Twaweza kutumiaje vidio za Sosaiti katika huduma yetu ya shambani? (c) Ni chombo gani kipya kilichoandaliwa hivi majuzi ili kusaidia katika kazi yetu ya kufanya wanafunzi?

      12 Kwa kuongezea vichapo vilivyochapwa, kuanzia mwaka 1990 ‘mtumwa mwaminifu’ ametuandalia njia ya kufundisha itoayo njia mpya ya kufikia wasikilizaji wengi—kaseti za vidio. Katika Oktoba mwaka huo, ile vidio ya dakika 55 Jehovah’s Witnesses—The Organization Behind the Name ilitolewa—vidio ya kwanza kupata kutolewa na Watch Tower Society. Huo utoaji mzuri wenye kuarifu, unaopatikana katika lugha 35, waonyesha tengenezo la ulimwenguni pote la watu wa Yehova wenye kujitoa wakitimiza amri ya Yesu ya kupiga mbiu ya habari njema katika dunia yote. Hiyo vidio imekusudiwa hasa kusaidia katika kazi yetu ya kufanya wanafunzi. Watangazaji wa Ufalme hawakupoteza wakati katika kukitumia chombo hicho kipya katika huduma ya shambani. Watangazaji fulani waliichukua katika mikoba yao ya vitabu, wakiwa tayari sikuzote kuionyesha au kuiazima kwa watu wanaopendezwa. Punde tu baada ya kutolewa kwayo, mwangalizi asafiriye aliandika hivi: “Vidio zimepata kuwa njia ya karne ya 21 ya kufikia akili na mioyo ya mamilioni ya watu, kwa hiyo ni tumaini letu kwamba vidio hii itakuwa ya kwanza tu kati ya vidio nyingi ambazo Sosaiti itatumia ili kuendeleza kazi ya Ufalme ulimwenguni pote.” Kwa kweli, vidio nyingine zimetolewa, kutia ndani ule mfululizo wenye sehemu tatu The Bible—A Book of Fact and Prophecy na Jehovah’s Witnesses Stand Firm Against Nazi Assault. Ikiwa vidio za Sosaiti zinapatikana katika lugha yako, je, umezitumia katika huduma yako ya shambani?a

      13 Hivi majuzi chombo kipya, ile broshua Mungu Anataka Tufanye Nini?, kiliandaliwa ili kusaidia katika kazi yetu ya kufanya wanafunzi. Kwa nini kilichapishwa? Chaweza kutumiwaje?

      Kukichunguza Chombo Kipya

      14, 15. Hiyo broshua mpya Anataka ilikusudiwa nani, nayo ina nini?

      14 Kichapo kipya Mungu Anataka Tufanye Nini? kimekusudiwa watu ambao tayari wana imani katika Mungu na wanaoistahi Biblia. Waangalizi wasafirio pamoja na wamishonari waliozoezwa Gileadi walio na uzoefu wa miaka mingi katika nchi zinazositawi walisaidia katika kuitayarisha broshua hii. Ina masomo mapana, yanayotia ndani mafundisho ya msingi ya Biblia. Maneno ni machangamfu, sahili, na ya moja kwa moja. Na wakati uleule, maandishi si sahili kupita kiasi. Haitoi “maziwa” tu bali pia “chakula kigumu” kutoka katika Neno la Mungu kwa njia ambayo watu walio wengi wataweza kuelewa.—Waebrania 5:12-14.

      15 Katika miaka ya majuzi watangazaji wa Ufalme katika nchi mbalimbali wameomba kichapo cha aina hiyo barabara. Kwa kielelezo, ofisi ya tawi Watch Tower Society katika Papua New Guinea iliandika hivi: “Watu wametatanishwa na mafundisho ya kidini yenye kupingana. Wanahitaji taarifa fupi za kweli, zinazotegemezwa na maandiko kadhaa ya Biblia ambayo wanaweza kuchunguza katika Biblia zao wenyewe. Wanahitaji utoaji ulio wazi na mahususi juu ya yale ambayo Mungu anataka Wakristo wa kweli wafanye na aina ya desturi na mazoea yasiyokubalika kwake.” Broshua Anataka ni kitu tunachohitaji barabara ili kuwasaidia watu hao wajifunze matakwa ya Mungu.

      16. (a) Ni nani hasa huenda wakanufaika kutokana na maelezo sahili katika hiyo broshua mpya? (b) Walio katika eneo lenu huenda wakanufaikaje kutokana na broshua Anataka?

      16 Waweza kukitumiaje chombo hiki kipya? Kwanza, chaweza kutumiwa ili kujifunza pamoja na watu ambao hawasomi vizuri au ambao huenda wasiwe na mwelekeo wa kusoma.b Watu hao huenda wakanufaika kutokana na maelezo sahili katika hiyo broshua. Baada ya kupitia nakala ya kichapo hicho iliyochapwa kimbele, ofisi za tawi za Watch Tower ziliandika yafuatayo: “Hii broshua itakuwa yenye kusaidia sana katika sehemu nyingi za nchi ambamo watu hawana mwelekeo wa kusoma sana.” (Brazili) “Kuna wahamiaji kadhaa ambao hawawezi kusoma lugha ya kwao na ambao bado hawasomi Kifaransa vizuri. Broshua hii yaweza kutumiwa kuwa msaada katika kujifunza pamoja na watu hao.” (Ufaransa) Je, waweza kufikiria watu katika eneo lenu ambao huenda wakanufaika kutokana na broshua Anataka?

      17. Katika nchi nyingi, broshua mpya huenda ikawa yenye mafaa katika njia ipi, na kwa nini?

      17 Pili, katika nchi nyingi hiyo broshua yaweza kutumiwa katika kuanzisha mafunzo ya Biblia pamoja na watu wenye kumhofu Mungu haidhuru ni kiasi gani cha elimu walicho nacho. Bila shaka, jitihada yapasa kufanywa ili kuanzisha funzo katika kitabu Ujuzi Uongozao Kwenye Uhai Udumuo Milele. Lakini katika hali fulani huenda ikawa rahisi zaidi kuanzisha funzo katika broshua. Kisha kwenye wakati ufaao, funzo lapasa kuhamishwa kwenye kitabu Ujuzi, msaada wetu mkuu wa funzo unaopendekezwa. Juu ya matumizi hayo ya broshua Anataka, ofisi za tawi za Watch Tower ziliandika hivi: “Broshua ya aina hii itakuwa na matokeo sana katika kuanzisha mafunzo mapya ya Biblia, ambayo yaweza kuendelezwa baadaye kwa kutumia kitabu Ujuzi.” (Italia) “Ingawa Wajapani ni wataalamu, wengi wana ujuzi mchache sana juu ya Biblia na mafundisho yayo ya msingi. Broshua hii itakuwa jiwe zuri la kukanyagia kuelekea kwenye kitabu Ujuzi.” (Japani) “Kuanzisha mafunzo ya Biblia ni jambo gumu, na fursa za kuanzisha funzo zaonekana kuwa afadhali wakati watangazaji waanzapo na broshua.”—Ujerumani.

      18. Twapaswa kukumbuka nini juu ya kutimiza matakwa ya Mungu?

      18 Ofisi za tawi za Sosaiti kotekote ulimwenguni ziliomba broshua hii, na ruhusa imetolewa ya kuitafsiri katika lugha 221. Kichapo hiki kipya na kithibitike kuwa chenye thamani katika kutusaidia kuwapa wengine msaada ili wajifunze yale ambayo Yehova Mungu anataka wafanye. Kwa upande wetu, acheni tukumbuke kwamba kutimiza matakwa ya Mungu, kutia na ile amri ya kuhubiri na kufanya wanafunzi, kunatupa sisi fursa yenye thamani ya kumwonyesha Yehova kadiri tunavyompenda. Ndiyo, yale ambayo Mungu anataka tufanye si mzigo wenye kulemea. Ni njia bora zaidi ya kuishi!—Zaburi 19:7-11.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki