Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Uhai Baada ya Kifo—Watu Huamini Nini?
    Mnara wa Mlinzi—1999 | Aprili 1
    • Uhai Baada ya Kifo—Watu Huamini Nini?

      “Mtu akifa, je! atakuwa hai tena?”—AYUBU 14:14.

      1, 2. Wengi hutafutaje faraja mpendwa wao anapokufa?

      KATIKA nyumba ya mazishi huko New York City, marafiki na familia watembea kimya-kimya kando ya jeneza lililo wazi la mvulana mwenye umri wa miaka 17 ambaye amekufa kutokana na kansa. Mama ya mvulana huyo aliyevunjika moyo arudia-rudia kwa machozi hivi: “Tommy ana furaha zaidi sasa. Mungu alitaka Tommy awe mbinguni naye.” Hivyo ndivyo amefundishwa kuamini.

      2 Kilometa 11,000 kutoka huko, katika Jamnagar, India, mwana mkubwa zaidi kati ya wana watatu awasha magogo moto mahali pa kuchomea maiti ya baba yao aliyekufa. Huku kelele ya moto ikiendelea, Brahman arudia-rudia maombi ya Kisanskriti hivi: “Nafsi isiyokufa kamwe na iendelee katika jitihada zake za kuwa sawa na nafsi kuu ya mwenyezi mungu.”

      3. Watu wamejiuliza maswali gani kwa enzi zilizopita?

      3 Uhalisi wa kifo watuzunguka. (Waroma 5:12) Ni jambo la kawaida kwetu kuwazia ikiwa kifo ndicho mwisho wa mambo yote. Akitafakari juu ya duru ya kawaida ya mimea, Ayubu, mtumishi mwaminifu wa Yehova Mungu wa kale, alionelea hivi: “Yako matumaini ya mti, ya kuwa ukikatwa utachipuka tena, wala machipukizi yake hayatakoma.” Vipi, basi, kuhusu wanadamu? “Mtu akifa, je! atakuwa hai tena?” Ayubu akauliza. (Ayubu 14:7, 14) Katika enzi zilizopita, watu katika kila jamii wametafakari maswali haya: Je, kuna uhai baada ya kifo? Ikiwa ndivyo, ni uhai wa aina gani? Basi, watu wameamini nini? Na kwa nini?

      Majibu Mengi, Kichwa Kilekile

      4. Watu wa dini mbalimbali huamini nini juu ya uhai baada ya kifo?

      4 Wakristo wengi wa jina tu huamini kwamba baada ya kifo, watu huenda mbinguni au motoni. Wahindu, nao, huamini katika kuzaliwa upya katika umbo jingine. Kulingana na itikadi za Kiislamu, kuna siku ya kiama baada ya kifo, wakati ambapo Allah atachanganua maisha ya kila mtu na kumpeleka kila mtu paradisoni au motoni. Katika nchi fulani, itikadi juu ya wafu ni mchanganyiko wa tamaduni za kienyeji na Ukristo wa jina. Kwa mfano, katika Sri Lanka, Wabudha na Wakatoliki huacha milango na madirisha yakiwa wazi mtu afapo nyumbani kwao, nao huweka jeneza miguu ya mfu ikielekeana na mlango wa mbele. Wao huamini kwamba kufanya hivyo hurahisisha kuondoka kwa roho, au nafsi, ya aliyekufa. Miongoni mwa Wakatoliki na Waprotestanti wengi wa Afrika Magharibi, kuna desturi ya kufunika vioo mtu afapo ili mtu yeyote asiangalie kioo na kuona roho ya mtu aliyekufa. Kisha, baada ya siku 40, familia na marafiki huadhimisha kupaa kwa nafsi kwenda mbinguni.

      5. Dini nyingi hukubaliana juu ya itikadi gani iliyo kuu?

      5 Yajapokuwa maoni hayo mengi, yaonekana kwamba dini nyingi hukubaliana angalau juu ya jambo moja. Huamini kwamba kitu fulani ndani ya mtu—kiwe chaitwa nafsi, roho, au mzuka—hakifi na huendelea kuishi baada ya mwili kufa. Karibu mamia yote ya dini na mafarakano ya Jumuiya ya Wakristo hutetea itikadi ya kwamba nafsi haiwezi kufa. Itikadi hiyo pia ni fundisho rasmi katika dini ya Kiyahudi. Ndilo msingi wenyewe wa fundisho la dini ya Hindu la kuzaliwa upya katika umbo jingine. Waislamu huamini kwamba nafsi huendelea kuishi baada ya mwili kufa. Wenyeji wa Australia, Waabudu-maumbile wa Afrika, Washinto, na hata Wabudha, wote hao hufundisha namna tofauti-tofauti za fundisho hilohilo.

      6. Wasomi fulani hulionaje lile wazo la kwamba nafsi haiwezi kufa?

      6 Kwa upande mwingine, kuna watu walio na maoni kwamba uhai wa kuweza kufahamu mambo huisha mtu anapokufa. Kwa maoni yao, lile wazo la kwamba uhai wa kihisia-moyo na wenye akili huendelea ukiwa nafsi isiyo na utu, iliyo kama kivuli ambayo imetengana na mwili, huonekana kuwa lisilopatana na akili. Mwandishi aliye pia msomi Mhispania wa karne ya 20, Miguel de Unamuno, aandika hivi: “Kuamini kwamba nafsi haiwezi kufa ni kutaka nafsi isiweze kufa, lakini ni kutaka sana iwe hivyo hivi kwamba kutaka huko kwamfanya mtu apuuze ukweli na asitumie akili.” Wengine wanaoamini hivyo hutia ndani watu wa namna mbalimbali kama vile Aristotle na Epikurasi, wanafalsafa wa kale wenye sifa, daktari Hipokrato, mwanafalsafa Mskoti David Hume, msomi Mwarabu Averroës, na aliyekuwa waziri mkuu wa kwanza wa India baada ya uhuru, Jawaharlal Nehru.

      7. Ni maswali gani muhimu juu ya itikadi inayohusu kutokufa kwa nafsi ambayo lazima yachunguzwe sasa?

      7 Tukiwa tunakabiliwa na mawazo na itikadi za aina hiyo zenye kupingana, lazima tuulize: Je, kweli tuna nafsi isiyoweza kufa? Ikiwa kweli nafsi yaweza kufa, basi fundisho hilo lisilo la kweli lingeweza kuwaje sehemu muhimu ya dini zilizo nyingi za leo? Wazo hilo lilianzia wapi? Ni lazima tupate majibu ya kweli na yenye kuridhisha kwa maswali hayo kwa kuwa wakati wetu ujao huyategemea. (1 Wakorintho 15:19) Lakini kwanza, acheni tuchunguze jinsi fundisho hilo la kwamba nafsi haiwezi kufa lilivyoanza.

      Jinsi Fundisho Hilo Lilivyoanza

      8. Socrates na Plato walitimiza fungu gani katika kuendeleza wazo la kwamba nafsi haiwezi kufa?

      8 Socrates na Plato, wanafalsafa Wagiriki wa karne ya tano K.W.K. waaminiwa kuwa miongoni mwa watu wa kwanza kuendeleza ile itikadi kwamba nafsi haiwezi kufa. Lakini, hawakuwa waanzilishi wa wazo hilo. Badala yake, walilirekebisha na kulibadili liwe fundisho la kifalsafa, hivyo, wakilifanya livutie zaidi watu wenye elimu wa siku yao na kuendelea. Ukweli ni kwamba Wazoroasta wa Uajemi ya kale na Wamisri waliokuwa kabla yao waliamini katika kutokufa kwa nafsi. Basi swali ni, Ni nini chanzo cha fundisho hilo?

      9. Ni nini kilichokuwa chanzo cha uvutano uliohusu tamaduni zote za kale za Misri, Uajemi, na Ugiriki?

      9 “Katika ulimwengu wa kale,” chasema kitabu The Religion of Babylonia and Assyria, “Misri, Uajemi, na Ugiriki zilipatwa na uvutano wa dini ya Kibabiloni.” Kuhusu itikadi za kidini za Kimisri, kitabu hicho chaendelea kusema hivi: “Kwa sababu ya ule uhusiano wa mapema kati ya Misri na Babilonia, kama ionyeshwavyo na yale mabamba ya El-Amarna, bila shaka kulikuwa na uwezekano mkubwa kwa maoni na desturi za Kibabiloni kupenya na kuingia katika madhehebu za Misri.”a Mambo hayohayo yaweza kusemwa kuhusu tamaduni za kale za Uajemi na Ugiriki.

      10. Maoni ya Wababiloni kuhusu uhai baada ya kifo yalikuwa nini?

      10 Lakini, je, Wababiloni wa kale waliamini katika kutokufa kwa nafsi? Kuhusu hoja hiyo, Profesa Morris Jastrow, Jr., wa Chuo Kikuu cha Pennsylvania, Marekani, aliandika hivi: “Wala watu wala viongozi wa kidini [wa Babilonia] hawakutarajia kamwe uwezekano wa kuangamizwa kabisa kwa uhai. [Kwa maoni yao] kifo kilikuwa kijia cha kuingia aina nyingine ya uhai, na kusema kwamba nafsi yaweza kufa [ya uhai wa sasa] kulikazia tu jinsi isivyowezekana kuponyoka badiliko katika maisha ambalo huletwa na kifo.” Ndiyo, Wababiloni waliamini kwamba uhai wa aina fulani, katika njia fulani, uliendelea baada ya kifo. Walionyesha hilo kwa kuzika vitu pamoja na wafu kwa matumizi katika uhai baada ya kifo.

      11, 12. Baada ya Furiko, ni nini kilichokuwa chanzo cha fundisho la kutokufa kwa nafsi ?

      11 Kwa wazi, fundisho la kwamba nafsi haiwezi kufa hurudi nyuma hadi Babiloni la kale. Je, hilo ni muhimu? Ndiyo, kwa sababu kulingana na Biblia, jiji la Babeli, au Babiloni, lilianzishwa na Nimrodi, kitukuu wa Noa. Baada ya Furiko katika siku ya Noa, watu wote walisema lugha moja na walikuwa na dini moja. Nimrodi alikuwa “katika kupingana na Yehova,” na pia yeye na wafuasi wake walitaka ‘kujifanyia jina.’ Hivyo, kwa kuanzisha jiji hilo na kujenga mnara huko, Nimrodi alianzisha dini tofauti.—Mwanzo 10:1, 6, 8-10, NW; 11:1-4.

      12 Mapokeo husema kwamba Nimrodi alikufa kifo cha jeuri. Kwa kupatana na akili, baada ya kifo chake, Wababiloni wangalielekea kumstahi sana akiwa mwanzilishi, mjenzi, na mfalme wa kwanza wa jiji lao. Kwa kuwa mungu Marduk (Merodaki) alionwa kuwa mwanzilishi wa Babiloni na idadi fulani ya wafalme wa Babiloni hata waliitwa jina lake, wasomi fulani wamedokeza kwamba Marduk huwakilisha Nimrodi aliyefanywa kuwa mungu. (2 Wafalme 25:27; Isaya 39:1; Yeremia 50:2) Ikiwa ndivyo ilivyo basi, lile wazo la kwamba mtu ana nafsi ambayo huendelea kuishi baada ya kifo lazima liwe lilikuwapo angalau kufikia wakati wa kifo cha Nimrodi. Kwa vyovyote, historia hufunua kwamba baada ya Furiko, chanzo cha fundisho la kwamba nafsi haiwezi kufa kilikuwa Babeli, au Babiloni.

      13. Fundisho la nafsi isiyoweza kufa lilieneaje usoni pa dunia yote, na tokeo lilikuwa nini?

      13 Biblia yaendelea kuonyesha kwamba Mungu alitatanisha juhudi za wajenzi wa mnara huko Babeli kwa kuchafua lugha yao. Wakiwa hawawezi kuwasiliana, waliacha mradi wao na wakatawanywa “kutoka huko . . . waende usoni pa nchi yote.” (Mwanzo 11:5-9) Lazima tukumbuke kwamba ingawa usemi wa hao walionuia kujenga mnara ulibadilishwa, njia yao ya kufikiri na dhana zao hazikubadilika. Likiwa tokeo, kokote walikoenda, walienda na mawazo yao ya kidini. Kwa njia hiyo, mafundisho ya kidini ya Kibabiloni—kutia ndani lile la kutokufa kwa nafsi—yalienea usoni pa dunia yote na kuwa msingi wa dini kubwa za ulimwengu. Hivyo, milki ya ulimwenguni pote ya dini isiyo ya kweli ikaanzishwa, ambayo yafafanuliwa ifaavyo katika Biblia kuwa “Babiloni Mkubwa, mama wa makahaba na wa mambo yenye kuchukiza sana ya dunia.”—Ufunuo 17:5.

      Milki ya Ulimwengu ya Dini Isiyo ya Kweli Yapanuka Kuelekea Mashariki

      14. Itikadi za kidini za Kibabiloni zilieneaje kuingia bara Hindi?

      14 Wanahistoria fulani husema kwamba zaidi ya miaka 3,500 iliyopita, mfululizo wa kuhama uliwaleta watu weupe, wa jamii ya Kiarya, kutoka kaskazini-magharibi kuingia Bonde la Indus, ambalo sasa limo hasa nchini Pakistan na India. Kutoka huko walisambaa kuingia katika nyanda za Mto Ganges na kuvuka India. Wataalamu fulani husema kwamba mawazo ya kidini ya wahamiaji hao yalitegemea mafundisho ya kale ya Wairani na Wababiloni. Basi, mawazo hayo ya kidini yakawa vyanzo vya dini ya Hindu.

      15. Lile wazo kuhusu nafsi isiyoweza kufa lilikujaje kuathiri dini ya Hindu ya leo?

      15 Katika India, lile wazo la kwamba nafsi haiwezi kufa lilibadilika na kuwa fundisho la kuzaliwa upya katika umbo jingine. Watu wenye hekima wa dini ya Hindu, waliokuwa waking’ang’ana na tatizo la ulimwenguni pote la uovu na kuteseka miongoni mwa wanadamu, walibuni ile iitwayo sheria ya Karma, sheria ya kwamba kila tokeo lina kisababishi. Wakiunganisha sheria hiyo na itikadi ya kwamba nafsi haiwezi kufa, walitokeza fundisho la kuzaliwa upya katika umbo jingine, ambamo mambo yastahiliyo na yasiyostahili yaliyofanywa katika uhai mmoja huthawabishwa au kuadhibiwa katika uhai unaofuata. Mradi wa waamini ni kufikia moksha, au kuwekwa huru kutokana na ule mzunguko wa kuzaliwa upya na kuwa kitu kimoja na yule aitwaye nafsi kuu au Nirvana. Kwa karne kadhaa, dini ya Hindu ilipokuwa ikienea, fundisho hilo la kuzaliwa upya katika umbo jingine lilienea pia. Na fundisho hilo limekuwa nguzo ya dini ya Hindu ya leo.

      16. Ni itikadi gani kuhusu uhai baada ya kifo iliyokuja kutawala fikira na mazoea ya idadi iliyo kubwa zaidi ya watu wa Asia Mashariki?

      16 Dini ya Hindu ilitokeza dini nyingine, kama vile Ubudha, Ujaini, na dini ya Sikh. Dini hizo huamini katika kuzaliwa upya katika umbo jingine. Isitoshe, Ubudha ulipokuwa ukipenya sehemu kubwa ya Asia Mashariki—China, Korea, Japani, na kwingineko—uliathiri sana tamaduni na dini za eneo hilo lote. Jambo hilo lilitokeza dini zenye mchanganyiko wa itikadi mbalimbali, zenye kuunga mkono mambo fulani ya Ubudha, ushirikina, na kuabudu wazazi wa kale waliokufa. Kati ya hizi, zile zenye uvutano mkubwa zaidi ni dini ya Tao, Ukonfyushasi, na dini ya Shinto. Hivyo, itikadi ya kwamba uhai huendelea kuwapo baada ya mwili kufa imekuja kutawala fikira za kidini na mazoea mbalimbali ya idadi kubwa zaidi ya watu katika eneo hilo la ulimwengu.

      Namna Gani Dini ya Kiyahudi, Jumuiya ya Wakristo, na Uislamu?

      17. Wayahudi wa kale waliamini nini kuhusu uhai baada ya kifo?

      17 Watu wanaofuata dini ya Kiyahudi, Jumuiya ya Wakristo, na Uislamu wanaamini nini kuhusu uhai baada ya kifo? Kati ya dini hizo, ile ya Kiyahudi ndiyo ya kale zaidi. Vyanzo vyake vinarudi nyuma miaka ipatayo 4,000 wakati wa Abrahamu—muda mrefu kabla Socrates na Plato kubuni wazo la kwamba nafsi haiwezi kufa. Wayahudi wa kale waliamini katika ufufuo wa wafu wala hawakuamini katika hali fulani ya kiasili ya kutoweza kufa kwa kibinadamu. (Mathayo 22:31, 32; Waebrania 11:19) Basi, fundisho la kwamba nafsi haiwezi kufa liliingiaje katika dini ya Kiyahudi? Historia yatoa jibu.

      18, 19. Fundisho la kutokufa kwa nafsi liliingiaje katika dini ya Kiyahudi?

      18 Mwaka wa 332 K.W.K., Aleksanda Mkubwa alishinda sehemu ya Mashariki ya Kati, kutia na Yerusalemu. Watawala waliotawala baada ya Aleksanda waliendeleza mipango yake ya kueneza Ugiriki katika milki hiyo, mchanganyiko wa tamaduni hizo mbili—wa Kigiriki na wa Kiyahudi—ukatukia. Punde si punde Wayahudi wakafahamu mawazo ya Kigiriki, hata baadhi yao wakawa wanafalsafa.

      19 Filo wa Aleksandria, wa karne ya kwanza W.K., alikuwa mmojawapo wa wanafalsafa hao Wayahudi. Filo alimstahi sana Plato na alijitahidi sana kufafanua dini ya Kiyahudi kwa kutumia maneno ya falsafa ya Kigiriki, hivyo akitayarisha njia kwa ajili ya Wayahudi wenye akili wa baadaye. Talmud—muhtasari ulioandikwa wa sheria za mdomo za marabi—iliathiriwa pia na wazo la Kigiriki. “Marabi wa Talmud,” chasema kichapo Encyclopaedia Judaica, “waliamini kwamba nafsi iliendelea kuishi baada ya kifo.” Baadaye, fasihi ya kifumbo ya Kiyahudi, Cabala, hata yafundisha juu ya kuzaliwa upya katika umbo jingine. Hivyo, wazo la kwamba nafsi haiwezi kufa lilipenya kisiri kupitia falsafa ya Kigiriki na kuingia dini ya Kiyahudi. Ni nini liwezalo kusemwa juu ya kuingia kwa fundisho hilo katika Jumuiya ya Wakristo?

      20, 21. (a) Ni upi uliokuwa msimamo wa Wakristo wa mapema kuhusu falsafa ya Plato, au falsafa ya Kigiriki? (b) Ni nini kilichosababisha kuchanganywa kwa mawazo ya Plato na mafundisho ya Kikristo?

      20 Ukristo wa kweli ulianza na Yesu Kristo. Miguel de Unamuno, aliyenukuliwa mapema, aliandika hivi kuhusu Yesu: “Aliamini hasa katika kufufuliwa kwa mwili, kulingana na njia ya Kiyahudi, wala hakuamini kwamba nafsi haiwezi kufa, kwa njia ya [Kigiriki] ya Plato.” Alimalizia kwa kusema hivi: “Kutoweza kufa kwa nafsi . . . ni fundisho la kipagani la kifalsafa.” Kwa kufikiria hilo, twaweza kuona ni kwa nini mtume Paulo aliwaonya vikali Wakristo wa karne ya kwanza dhidi ya “falsafa na udanganyo mtupu kulingana na mapokeo ya wanadamu, kulingana na mambo ya msingi ya ulimwengu na si kulingana na Kristo.”—Wakolosai 2:8.

      21 Hata hivyo, “fundisho [hilo] la kipagani la kifalsafa” lilipenya lini na jinsi gani katika Jumuiya ya Wakristo? Kichapo The New Encyclopædia Britannica chaeleza hivi: “Kuanzia katikati ya karne ya 2 [W.K.] Wakristo waliokuwa wamezoezwa falsafa ya Kigiriki kwa kiasi fulani walianza kuhisi uhitaji wa kueleza imani yao kwa kutumia maneno ya falsafa za Kigiriki, ili kujiridhisha wenyewe na ili kugeuza imani ya wapagani walioelimika. Falsafa iliyowafaa kabisa ilikuwa mafundisho ya Uplato.” Wanafalsafa wawili wa mapema walioathiri sana mafundisho ya Jumuiya ya Wakristo walikuwa Origen wa Aleksandria na Augustine wa Hippo. Wote wawili waliathiriwa sana na mawazo ya Plato nao waliyapenyeza katika mafundisho ya Kikristo.

      22. Fundisho la kutokufa kwa nafsi limebakije kuwa fundisho muhimu katika Uislamu?

      22 Ilhali wazo la kwamba nafsi haiwezi kufa katika dini ya Kiyahudi na katika Jumuiya ya Wakristo lilitokea kwa sababu ya uvutano wa Plato, dhana hiyo iliingizwa katika Uislamu tangu mwanzo wake. Korani, kitabu kitakatifu cha Waislamu, hufundisha kwamba mwanadamu ana nafsi ambayo huendelea kuishi baada ya kifo. Husema kwamba hatimaye nafsi itaishi katika shamba la paradiso ya kimbingu au kuadhibiwa motoni. Hilo halimaanishi kwamba wasomi Waarabu hawajajaribu kuunganisha mafundisho ya Kiislamu na falsafa ya Kigiriki. Kwa hakika, Waarabu waliathiriwa kwa kiasi fulani na maandishi ya Aristotle. Hata hivyo, Waislamu bado huamini katika kutokufa kwa nafsi.

      23. Ni maswali yapi ya lazima kuhusu uhai baada ya kifo yatakayochunguzwa katika makala inayofuata?

      23 Kwa wazi, dini ulimwenguni pote zimetokeza itikadi nyingi zenye kutatanisha juu ya uhai baada ya kifo, kwa kutegemea fundisho la kwamba nafsi haiwezi kufa. Na itikadi hizo zimeathiri, naam, hata kutawala na kufanya mabilioni ya watu kuwa watumwa. Tukabiliwapo na hayo yote, twalazimika kuuliza: Je, kweli yawezekana kujua ni nini hutupata tunapokufa? Je, kuna uhai baada ya kifo? Biblia husema nini kuhusu hilo? Tutachunguza hilo katika makala inayofuata.

      [Maelezo ya Chini]

      a El-Amarna ni mahali pa magofu ya Akhetaton, jiji la Misri, ambalo yadaiwa lilijengwa karne ya 14 K.W.K.

  • Uhai Baada ya Kifo—Biblia Husema Nini?
    Mnara wa Mlinzi—1999 | Aprili 1
    • Uhai Baada ya Kifo—Biblia Husema Nini?

      “U mavumbi wewe, nawe mavumbini utarudi.”—MWANZO 3:19.

      1, 2. (a) Kuna mawazo yapi mbalimbali kuhusu uhai baada ya kifo? (b)Twahitaji kuchunguza nini ili tutambue yale ambayo Biblia hufundisha kuhusu nafsi?

      “WAZO la kuteseka milele halipatani na itikadi ya kwamba Mungu anapenda vitu vilivyoumbwa. . . . Kuamini kwamba nafsi huadhibiwa milele kwa sababu ya makosa ya miaka michache, bila kuipatia fursa ya kurekebisha, kwapingana na akili timamu,” akaeleza mwanafalsafa Mhindu Nikhilananda.

      2 Leo, sawa na Nikhilananda, watu wengi hawastareheshwi na fundisho la kuteswa milele. Vivyo hivyo, watu wengine wanaona ugumu kuelewa dhana kama kule kufikia Nirvana na kuunganishwa na asili. Hata miongoni mwa wale wanaodai kwamba itikadi zao zinategemea Biblia, mna mawazo yenye kutofautiana juu ya nafsi ni nini nayo hupatwa na nini tunapokufa. Lakini kwa kweli Biblia hufundisha nini juu ya nafsi? Ili kupata jibu, twahitaji kuchunguza maana ya neno la Kiebrania na la Kigiriki, linalotafsiriwa “nafsi” katika Biblia.

      Nafsi Kulingana na Biblia

      3. (a) Ni neno gani hutafsiriwa “nafsi” katika Maandiko ya Kiebrania, na maana yake ya msingi ni nini? (b) Andiko la Mwanzo 2:7 lathibitishaje kwamba neno “nafsi” laweza kumaanisha mtu mzima?

      3 Neno la Kiebrania litafsiriwalo “nafsi” ni neʹphesh, nalo hupatikana mara 754 katika Maandiko ya Kiebrania. Neno neʹphesh humaanisha nini? Kulingana na kamusi The Dictionary of Bible and Religion, neno hilo “kwa kawaida hurejezea kiumbe chote kizima kilicho hai, mtu mzima.” Hilo lathibitishwa na ufafanuzi wa Biblia kuhusu nafsi kwenye Mwanzo 2:7: “BWANA Mungu akamfanya mtu kwa mavumbi ya ardhi, akampulizia puani pumzi ya uhai; mtu akawa nafsi hai.” Ona kwamba mtu wa kwanza “akawa” nafsi hai. Hiyo ni kusema, Adamu hakuwa na nafsi; yeye alikuwa nafsi—kama vile mtu awaye daktari ni daktari. Basi, neno “nafsi” hapa lafafanua mtu mzima.

      4. Ni neno gani hutafsiriwa “nafsi” katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, na maana ya msingi ya neno hilo ni nini?

      4 Neno litafsiriwalo “nafsi” (psy·kheʹ) lapatikana zaidi ya mara mia moja katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo. Sawa na neno neʹphesh, kwa kawaida neno hilo hurejezea mtu mzima. Kwa mfano, fikiria taarifa zifuatazo: “Nafsi yangu yataabika.” (Yohana 12:27) “Hofu ikaanza kuwa juu ya kila nafsi.” (Matendo 2:43) “Acheni kila nafsi iwe katika ujitiisho kwa mamlaka zilizo kubwa.” (Waroma 13:1) “Semeni kwa kuliwaza nafsi zilizoshuka moyo.” (1 Wathesalonike 5:14) “Watu wachache, yaani, nafsi nane, walichukuliwa salama kupitia maji.” (1 Petro 3:20) Kwa wazi, neno psy·kheʹ, sawa na neno neʹphesh, hurejezea mtu mzima. Kulingana na msomi Nigel Turner, neno hilo “humaanisha mtu hasa, mtu binafsi, mwili halisi ambao umepuliziwa rûa [roho] ya Mungu. . . . Mkazo watiwa kwenye mtu binafsi akiwa mzima.”

      5. Je, wanyama ni nafsi? Eleza.

      5 Kwa kupendeza, katika Biblia neno “nafsi” hutumika, si kwa wanadamu tu, bali pia kwa wanyama. Kwa mfano, likifafanua kuumbwa kwa viumbe wa baharini, andiko la Mwanzo 1:20 (NW), lasema kwamba Mungu aliamuru hivi: “Maji na yajawe na kundi la nafsi hai.” Na siku ya uumbaji iliyofuata, Mungu aliamuru hivi: “Dunia na itokeze nafsi hai kulingana na aina zake, wanyama wa nyumbani na wanyama watembeao na hayawani mwitu wa dunia kulingana na aina yake.”—Mwanzo 1:24, NW; linganisha Hesabu 31:28, NW.

      6. Ni nini linaloweza kusemwa kuhusu jinsi ambavyo Biblia hutumia neno “nafsi”?

      6 Hivyo, jinsi neno “nafsi” litumiwavyo katika Biblia hurejezea mtu au mnyama au uhai wa mtu au wa mnyama. (Ona sanduku hapo juu.) Fasili ya Biblia juu ya nafsi ni sahili, yenye upatano, na haina falsafa zenye kutatanisha na ushirikina wa watu. Mambo yakiwa hivyo, swali linalohitaji kuulizwa kwa haraka ni, Kulingana na Biblia, nafsi hupatwa na nini wakati wa kifo?

      Wafu Hawana Fahamu

      7, 8. (a) Maandiko hufunua nini juu ya hali ya wafu? (b) Toa mifano kutoka kwa Biblia ionyeshayo kwamba nafsi yaweza kufa.

      7 Hali ya wafu yaeleweshwa waziwazi kwenye Mhubiri 9:5, 10, ambapo twasoma hivi: “Wafu hawajui kitu . . . hakuna kazi, wala shauri, wala maarifa, wala hekima ndani ya kaburi.” (Zaire Swahili Bible) Kwa hiyo, kifo ni hali ya kutoendelea kuishi. Mtunga-zaburi aliandika kwamba mtu anapokufa, “huurudia udongo wake, siku hiyo mawazo yake yapotea.” (Zaburi 146:4) Wafu hawana fahamu, hawatendi.

      8 Alipokuwa akitangaza hukumu dhidi ya Adamu, Mungu alitaarifu hivi: “U mavumbi wewe, nawe mavumbini utarudi.” (Mwanzo 3:19) Kabla Mungu hajamwumba kutoka katika mavumbi ya ardhi na kumpa uhai, Adamu hakuwako. Alipokufa, alirudia hali hiyo. Adhabu yake ilikuwa kifo—wala si kuhamishwa hadi makao mengine. Basi, ni nini kilichoipata nafsi yake? Kwa kuwa katika Biblia neno “nafsi” mara nyingi hurejezea tu mtu mwenyewe, tusemapo kwamba Adamu alikufa, tunamaanisha kwamba nafsi iliyoitwa Adamu ilikufa. Huenda hilo likasikika kuwa jambo lisilo la kawaida kwa mtu ambaye huamini kwamba nafsi haiwezi kufa. Hata hivyo, Biblia hutaarifu hivi: “Nafsi inayofanya zambi, itakufa.” (Ezekieli 18:4, ZSB) Mambo ya Walawi 21:1 (NW), huzungumza juu ya “nafsi iliyokufa” (“maiti,” Biblia Habari Njema). Na Wanadhiri waliambiwa wasikaribie “nafsi yoyote iliyokufa” (“mwili mfu,” Lamsa).—Hesabu 6:6, NW.

      9. Biblia humaanisha nini inaposema kwamba “nafsi [ya Raheli] ilikuwa ikitoka”?

      9 Lakini vipi juu ya taarifa kwenye Mwanzo 35:18 inayohusu kifo chenye kuhuzunisha cha Raheli, kilichotukia alipokuwa akimzaa mwana wake wa pili? Hapo twasoma hivi: “Ikawa hapo katika kutoa roho [“nafsi,” NW] yake, maana alikufa, akamwita jina lake Benoni, lakini babaye alimwita Benyamini.” Je, fungu hilo ladokeza kwamba Raheli alikuwa na kitu fulani ndani yake chenye uhai kilichoondoka alipokuwa akifa? La hasha. Kumbuka kwamba, neno “nafsi” laweza pia kumaanisha uhai wa mtu. Kwa hiyo, katika kisa cha Raheli “nafsi” ilimaanisha tu “uhai” wake. Hiyo ndiyo sababu tafsiri nyingine za Biblia hutafsiri maneno “nafsi yake ilikuwa ikitoka” kuwa “uhai wake ulikuwa ukififia” (Knox), “alipumua kwa mara ya mwisho” (Jerusalem Bible), na “uhai wake ulimtoka” (Bible in Basic English). Hakuna dokezo lolote la sehemu fulani isiyoelezeka ya Raheli iliyoendelea kuishi baada ya kifo chake.

      10. Ni katika njia gani nafsi ya mwana aliyefufuliwa wa mjane ‘ilimrudia’?

      10 Ilikuwa vivyo hivyo kwa habari ya kufufuliwa kwa mwana wa mjane, kulikorekodiwa katika 1 Wafalme sura ya 17. Katika mstari wa 22 twasoma kwamba Eliya alisali kwa ajili ya mvulana huyo mchanga, “BWANA akaisikia sauti ya Eliya; roho [“nafsi,” NW] ya mtoto ikamrudia, akafufuka.” Mara nyingine tena, neno “nafsi” lamaanisha “uhai.” Kwa hiyo, New American Standard Bible husema hivi: “Uhai wa mtoto ukamrudia naye akafufuka.” Naam, uhai ndio uliomrudia mvulana huyo, wala si umbo fulani lililo kama kivuli. Hilo lapatana na mambo ambayo Eliya alimwambia mama ya mvulana huyo: “Tazama, mwanao yu hai.”—1 Wafalme 17:23.

      Vipi Kuhusu Roho?

      11. Kwa nini neno “roho” haliwezi kurejezea sehemu ya mtu iliyojitenga na mwili ambayo huendelea kuishi baada ya kifo?

      11 Biblia husema kwamba mtu anapokufa, “pumzi [“roho,” NW] yake hutoka, huurudia udongo wake.” (Zaburi 146:4) Je, hilo lamaanisha kwamba roho iliyojitenga na mwili huondoka kihalisi na kuendelea kuishi baada ya mtu kufa? Hilo halingewezekana, kwa sababu mtunga-zaburi afuatisha kusema: “Siku hiyo mawazo yake yapotea” (“mafikili yake yanapotea,” ZSB). Basi, roho ni nini, nayo ‘humtokaje’ mtu anapokufa?

      12. Maneno ya Kiebrania na Kigiriki ambayo yametafsiriwa “roho” katika Biblia yanamaanisha nini?

      12 Katika Biblia maneno yanayotafsiriwa “roho” (Kiebrania, ruʹach; Kigiriki, pneuʹma) hasa humaanisha “pumzi.” Hivyo, badala ya kusema “roho yake hutoka,” tafsiri ya Union Version husema “pumzi yake hutoka.” (Zaburi 145:4) Lakini neno “roho” humaanisha mengi zaidi ya lile tendo la kupumua. Kwa kielelezo, katika kufafanua kuangamizwa kwa uhai wa binadamu na wa wanyama wakati wa Gharika ya tufeni pote, Mwanzo 7:22 husema hivi: “Kila kitu chenye pumzi ya roho [au, “kani,” NW; Kiebrania, ruʹach] ya uhai puani mwake kikafa, kila kilichokuwako katika nchi kavu.” Kwa hiyo, “roho” yaweza kurejezea kani ya uhai itendayo katika viumbe vyote vyenye uhai, wanadamu na pia wanyama, ambayo huendelezwa kwa kupumua.

      13. Roho humrudiaje Mungu wakati mtu anapokufa?

      13 Basi, andiko la Mhubiri 12:7 lamaanisha nini linapotaarifu kwamba ‘roho humrudia Mungu aliyeitoa’? Je, hilo lamaanisha kwamba roho husafiri kihalisi kupitia angani kwenda alipo Mungu? La hasha. Kwa kuwa roho ndiyo kani ya uhai, hiyo ‘humrudia Mungu’ katika maana ya kwamba tumaini lolote la mtu huyo la wakati ujao humtegemea Mungu peke yake. Mungu tu ndiye awezaye kurudisha roho, au kani ya uhai, akimrudisha mtu kwenye uhai. (Zaburi 104:30) Lakini je, Mungu anakusudia kufanya hivyo?

      “Atainuka”

      14. Yesu alisema na kufanya nini ili kuwatuliza na kuwafariji dada za Lazaro baada ya kifo cha ndugu yao?

      14 Katika mji mdogo wa Bethania, karibu kilometa tatu mashariki ya Yerusalemu, Maria na Martha walikuwa wakiomboleza kifo cha mapema cha ndugu yao, Lazaro. Yesu alihuzunika pamoja nao, kwa kuwa alimpenda Lazaro na dada zake. Yesu angeweza kuwafariji dada hao namna gani? Si kwa kuwaambia hadithi fulani isiyoeleweka, bali kwa kuwaambia ukweli. Yesu alisema kisahili hivi: “Ndugu yako atainuka.” Kisha Yesu akaenda kaburini, naye akamfufua Lazaro—akiurudisha uhai katika mtu aliyekuwa amekufa kwa siku nne!—Yohana 11:18-23, 38-44.

      15. Martha aliitikiaje yale ambayo Yesu alisema na kufanya?

      15 Je, Martha alishangazwa na taarifa ya Yesu kwamba Lazaro “atainuka”? Yaonekana sivyo, kwa kuwa alijibu hivi: “Najua atafufuliwa katika ufufuo siku ya mwisho.” Tayari alikuwa na imani katika ahadi ya ufufuo. Kisha Yesu akamwambia hivi: “Mimi ndio ufufuo na uhai. Yeye ambaye hudhihirisha imani katika mimi, hata ingawa afa, atakuja kwenye uhai.” (Yohana 11:23-25) Muujiza wa kufufuliwa kwa Lazaro ulitia nguvu imani ya Martha na kutia wengine imani. (Yohana 11:45) Lakini neno “ufufuo” lamaanisha nini hasa?

      16. Neno “ufufuo” humaanisha nini?

      16 Neno “ufufuo” limetafsiriwa kutoka katika neno la Kigiriki a·naʹsta·sis, ambalo likitafsiriwa kihalisi, lamaanisha “kusimama tena.” Watafsiri wa Kiebrania waliotafsiri Kigiriki wametafsiri neno a·naʹsta·sis kwa fungu la maneno linalomaanisha “kufufuliwa kwa wafu” (Kiebrania, techi·yathʹ ham·me·thimʹ).a Kwa hiyo, ufufuo huhusisha kumwinua mtu kutoka katika hali isiyo na uhai ya kifo—kurudisha na kuanzisha tena uhai wa mtu.

      17. (a) Kwa nini kufufuliwa kwa watu mmoja-mmoja hakutasababisha ugumu kwa Yehova Mungu na Yesu Kristo? (b) Yesu alitoa ahadi gani kuhusu wale waliomo katika makaburi ya ukumbusho?

      17 Akiwa na hekima isiyo na kikomo na mwenye kumbukumbu kamilifu, Yehova Mungu aweza kumfufua mtu kwa urahisi. Si vigumu kwake kukumbuka maisha ya waliokufa—utu wao, historia yao ya kibinafsi, na mambo yote kuwahusu. (Ayubu 12:13; linganisha Isaya 40:26.) Isitoshe, kama vile kisa cha Lazaro kionyeshavyo, Yesu Kristo ana nia na anaweza kufufua wafu. (Linganisha Luka 7:11-17; 8:40-56.) Kwa hakika, Yesu Kristo alisema hivi: “Saa inakuja ambayo katika hiyo wote wale waliomo ndani ya makaburi ya ukumbusho watasikia sauti yake [Yesu] na kutoka.” (Yohana 5:28, 29) Ndiyo, Yesu Kristo aliahidi kwamba wote wale walio katika kumbukumbu ya Yehova watafufuliwa. Kwa wazi, kulingana na Biblia, nafsi hufa, na kitatuzi cha kifo ni ufufuo. Lakini mabilioni ya watu wameishi na kufa. Ni nani miongoni mwao walio katika kumbukumbu ya Mungu, wakisubiri ufufuo?

      18. Ni nani watakaofufuliwa?

      18 Wale ambao wamefuatia mwendo wa uadilifu wakiwa watumishi wa Yehova watafufuliwa. Lakini, mamilioni ya watu wengine wamekufa bila kuonyesha ikiwa wangejipatanisha na viwango vya uadilifu vya Mungu. Hawakujua matakwa ya Yehova au hawakuwa na wakati wa kufanya mabadiliko yaliyohitajiwa. Hao wengine pia wako katika kumbukumbu ya Mungu na hivyo watafufuliwa, kwa kuwa Biblia huahidi hivi: “Kutakuwa na ufufuo wa waadilifu na wasio waadilifu pia.”—Matendo 24:15.

      19. (a) Mtume Yohana aliona ono gani linalohusu ufufuo? (b) Ni nini ‘kinachovurumishwa ndani ya ziwa la moto,’ na usemi huo wamaanisha nini?

      19 Mtume Yohana aliona ono lenye kusisimua la waliofufuliwa wakiwa wamesimama mbele ya kiti cha enzi cha Mungu. Akifafanua hilo, aliandika hivi: “Bahari ikawatoa hao wafu waliokuwa ndani yayo, na kifo na Hadesi vikawatoa wafu ndani yavyo, nao walihukumiwa mmoja-mmoja kulingana na vitendo vyao. Na kifo na Hadesi vikavurumishwa ndani ya ziwa la moto. Hili humaanisha kifo cha pili, ziwa la moto.” (Ufunuo 20:12-14) Ebu fikiria hilo lamaanisha nini! Wafu wote walio katika kumbukumbu ya Mungu wataondolewa kutoka kwenye Hadesi, au Sheoli, kaburi la jumla la wanadamu. (Zaburi 16:10; Matendo 2:31) Kisha “kifo na Hadesi” vitatupwa katika lile liitwalo “ziwa la moto,” likifananisha uharibifu kamili. Kaburi la jumla la wanadamu litakoma kuwako.

      Tazamio la Pekee!

      20. Mamilioni ya watu ambao sasa wamekufa watafufuliwa katika mazingira ya aina gani?

      20 Mamilioni ya watu watakapofufuliwa, hawatarudi kwenye uhai katika dunia tupu. (Isaya 45:18) Wataamka kwenye mazingira mazuri yaliyoboreshwa nao watakuta kwamba wametayarishiwa makao, mavazi, na chakula kingi. (Zaburi 67:6; 72:16; Isaya 65:21, 22) Ni nani watakaofanya matayarisho yote hayo? Kwa wazi, lazima kutakuwa na watu watakaokuwa wakiishi katika ulimwengu mpya kabla ya ufufuo wa kidunia kuanza. Lakini hao watakuwa nani?

      21, 22. Ni tazamio gani la pekee linalowangojea wale wanaoishi katika “siku za mwisho”?

      21 Utimizo wa unabii wa Biblia huonyesha kwamba tunaishi katika “siku za mwisho” za mfumo huu wa mambo.b (2 Timotheo 3:1) Karibuni sana, Yehova Mungu ataingilia shughuli za wanadamu na kufutilia mbali uovu kutoka duniani. (Zaburi 37:10, 11; Mithali 2:21, 22) Wakati huo, ni nini kitakachowapata watu wanaomtumikia Mungu kwa uaminifu?

      22 Yehova hatawaharibu waadilifu pamoja na waovu. (Zaburi 145:20) Hajawahi kufanya jambo kama hilo, naye hatalifanya asafishapo ubaya wote kutoka duniani. (Linganisha Mwanzo 18:22, 23, 26.) Kwa hakika, kitabu cha mwisho cha Biblia husema juu ya “umati mkubwa, ambao hakuna mtu aliyeweza kuuhesabu, kutoka katika mataifa yote na makabila na vikundi vya watu na lugha,” ukitoka katika “dhiki kubwa.” (Ufunuo 7:9-14) Ndiyo, umati mkubwa wa watu wataokoka dhiki kubwa ambamo ulimwengu mbovu wa sasa utaishia, nao wataingia katika ulimwengu mpya wa Mungu. Humo, wanadamu watiifu wanaweza kunufaika kikamili kutokana na maandalizi ya ajabu ya Mungu ya kuwaondolea wanadamu dhambi na kifo. (Ufunuo 22:1, 2) Hivyo, “umati mkubwa” hawatahitaji kufa kamwe. Ni tazamio la pekee kama nini!

      Uhai Bila Kifo

      23, 24. Ni lazima ufanye nini ili ufurahie uhai bila kifo katika Paradiso duniani?

      23 Je, twaweza kuwa na uhakika katika tumaini hilo lenye kutokeza? Bila shaka! Yesu Kristo mwenyewe alionyesha kwamba kungekuwa na wakati ambapo watu wangeishi bila kufa kamwe. Kabla tu ya kumfufua rafiki yake Lazaro, Yesu alimwambia Martha hivi: “Kila mtu aliye hai na hudhihirisha imani katika mimi hatakufa hata kidogo kabisa.”—Yohana 11:26.

      24 Je, wataka kuishi milele katika Paradiso duniani? Je, watamani sana kuwaona tena wapendwa wako? “Ulimwengu unapitilia mbali na ndivyo na tamaa yao, lakini yeye ambaye hufanya mapenzi ya Mungu hudumu milele,” asema mtume Yohana. (1 Yohana 2:17) Sasa ndio wakati wa kujifunza mapenzi ya Mungu ni nini na kuazimia kuishi kupatana nayo. Ndipo wewe, pamoja na mamilioni ya wengine ambao tayari wanafanya mapenzi ya Mungu, mwaweza kuishi milele katika Paradiso duniani.

      [Maelezo ya Chini]

      a Ingawa neno “ufufuo” halionekani katika Maandiko ya Kiebrania, tumaini la ufufuo latajwa waziwazi kwenye Ayubu 14:13, Danieli 12:13, na Hosea 13:14.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki