-
Warusi Wathamini Sana Uhuru wa KuabuduAmkeni!—2000 | Februari 22
-
-
Tukio jingine kuu la mkusanyiko lilikuwa kupokea salamu kutoka Moscow, ambapo watu 15,108 walikusanyika kwa ajili ya mkusanyiko wao kwenye mwisho-juma huohuo. Wajumbe katika New York City walisisimuka kama nini kusikia tangazo kwamba watu 600 walikuwa wamebatizwa huko! Hiyo ilikuwa kweli hasa kwa sababu ya ripoti zenye kuogofya za magazeti na televisheni zilizokuwa zimeanza kutokea Marekani na kwingineko katika juma lililotangulia tarehe ya mkusanyiko.
Kilichokuwa Kikitokea Moscow
Katika Julai 21, 1999, Mashahidi walitia sahihi mkataba wa kutumia Stediamu ya Olympic iliyo karibu na sehemu ya kati ya Moscow karibu tu na kanisa kubwa la Othodoksi la Urusi. Lakini juma moja kabla ya mkusanyiko kuanza, ilikuwa dhahiri kwamba kungekuwa na upinzani. Kufikia Jumatano, Agosti 18, kibali cha kutumia stediamu hakikuwa kimepokewa bado, hata ingawa malipo yalikuwa yametolewa tayari. Maofisa walisaidiwa kuona kwamba, kama ionyeshwavyo na sanduku kwenye ukurasa wa 28, Mashahidi wa Yehova ni tengenezo la kidini linalotambuliwa kisheria nchini Urusi.
Kwa sababu karibu wajumbe 15,000 wa mkusanyiko walikuwa wakijitayarisha kuhudhuria Ijumaa asubuhi, wawakilishi wa Mashahidi walianza kuwa na wasiwasi. Wajumbe fulani walikuwa wakisafiri hadi Moscow kutoka majiji na miji iliyo umbali wa kilometa nyingi. Hatimaye, baada ya mazungumzo ya saa kadhaa, karibu saa 2:00 usiku, Alhamisi, Agosti 19, wasimamizi wa stediamu walifurahi kuwajulisha wawakilishi wa Mashahidi kwamba mkusanyiko huo unaweza kufanywa. Wasimamizi wa jiji walikuwa wamesema kwamba hawakupinga mkusanyiko huo.
Asubuhi iliyofuata maelfu walimiminika kwenye stediamu hiyo. Mashahidi wa kujitolea walikuwa wamefanya kazi usiku kucha ili kutayarisha kuwasili kwa wajumbe. Pia asubuhi hiyo ya kwanza waandishi wa habari walikuwepo, ambao mapema zaidi walikuwa wamearifiwa kuhusu upinzani wa kufanywa kwa mkusanyiko huo. “Pongezi!” mmoja wao akasema kwa mshangao. “Tunaterema kusikia kwamba mkusanyiko wenu utafanywa.”
Kielelezo cha Mwenendo Wenye Utaratibu
Wasimamizi wa stediamu waliona kwamba lingekuwa jambo la busara kuchukua hatua za usalama. Hivyo, walinda-usalama wakiwa na vifaa vya kugundua chuma kama vile vinavyotumiwa kuchunguza abiria kwenye viwanja vya ndege waliwekwa kwenye kila kiingilio. Pia polisi waliwekwa ndani ya stediamu yote. Mkusanyiko uliendelea kwa njia yenye utaratibu licha ya tisho kubwa.
Mnamo Jumamosi alasiri mtu fulani alipiga simu akidokeza kwamba bomu lilikuwa limetegwa kwenye stediamu hiyo. Tisho hilo lilipokewa muda mfupi kabla ya hotuba mbili za mwisho siku hiyo. Kwa hiyo, kwa ombi la idhini la wasimamizi wa stediamu hiyo, tangazo fupi lilitolewa watu watoke kwenye stediamu mara moja. Watu walipofanya hivyo kwa njia ya utaratibu, maofisa wa stediamu na mapolisi walishangaa. Hawakuwa wamepata kuona jambo kama hilo! Waliuliza kama jambo hilo lilikuwa limefanyiwa mazoezi.
Hakuna bomu lililopatikana, na siku iliyofuata programu ilirefushwa ili itie ndani hotuba ambazo hazikuwa zimetolewa Jumamosi. Wasimamizi wa stediamu walipendezwa na mkusanyiko huo.
-
-
Warusi Wathamini Sana Uhuru wa KuabuduAmkeni!—2000 | Februari 22
-
-
[Picha katika ukurasa wa 26, 27]
Zaidi ya watu 15,000 walikusanyika katika Stediamu ya Olympic ya Moscow
-