-
Kufanya Vitu Vyote Kuwa Vipya—Kama IlivyotabiriwaMnara wa Mlinzi—2000 | Aprili 15
-
-
13, 14. (a) Twapaswa kuchunguza andiko gani jingine ambapo usemi “mbingu mpya na dunia mpya” wapatikana? (b) Kwa nini unabii wa Petro utupendeze hasa wakati huu?
13 Angalia usije ukakosa kuelewa. Huku si kufasiri Biblia wala kutupia jicho historia ya kale tu. Waweza kuona hilo kwa kufungua andiko jingine ambapo usemi “mbingu mpya na dunia mpya” wapatikana. Katika 2 Petro sura ya 3, utapata usemi huo na kuona kwamba wakati wetu ujao wahusika.
14 Mtume Petro aliandika barua yake zaidi ya miaka 500 baada ya Wayahudi kurudi katika nchi yao. Akiwa mmoja wa mitume wa Yesu, Petro alikuwa akiwaandikia wafuasi wa Kristo, “Bwana” anayetajwa katika 2 Petro 3:2. Katika mstari wa 4, Petro ataja ‘kuwapo kulikoahidiwa’ kwa Yesu ambako kwafanya unabii huo uwe wa maana sana leo. Kuna uthibitisho wa kutosha unaoonyesha kwamba tangu Vita ya Ulimwengu ya Kwanza, Yesu amekuwapo katika maana ya kuwa na mamlaka akiwa Mtawala katika Ufalme wa kimbingu wa Mungu. (Ufunuo 6:1-8; 11:15, 18) Hilo lina maana ya pekee tufikiriapo jambo jingine ambalo Petro alitabiri katika sura hiyo.
15. Unabii wa Petro kuhusu “mbingu mpya” unatimizwaje?
15 Twasoma hivi kwenye 2 Petro 3:13: “Ziko mbingu mpya na dunia mpya ambazo tunangojea kulingana na ahadi yake, na katika hizo uadilifu utakaa.” Huenda tayari unajua kwamba Yesu ambaye yuko mbinguni ndiye Mtawala mkuu katika hizo “mbingu mpya.” (Luka 1:32, 33) Hata hivyo, maandiko mengine ya Biblia yanaonyesha kwamba hatawali akiwa peke yake. Yesu aliahidi kwamba mitume na watu wengine kama wao wangekuwa na sehemu mbinguni. Katika kitabu cha Waebrania, mtume Paulo aliwaeleza hao kuwa “washiriki wa mwito wa kimbingu.” Naye Yesu alisema kwamba wale wa kikundi hicho wangeketi katika viti vya enzi pamoja naye mbinguni. (Waebrania 3:1; Mathayo 19:28; Luka 22:28-30; Yohana 14:2, 3) Tunamaanisha kwamba watu wengine wanatawala pamoja na Yesu wakiwa sehemu ya mbingu mpya. Basi, Petro alimaanisha nini alipotumia usemi “dunia mpya”?
16. Ni “dunia [gani] mpya” iliyopo sasa?
16 Kama ilivyo katika utimizo wa kale—kurudi kwa Wayahudi katika nchi yao—utimizo wa sasa wa 2 Petro 3:13 wahusisha watu wanaojinyenyekeza chini ya utawala wa hizo mbingu mpya. Unaweza kuona mamilioni ya watu leo wanaojinyenyekeza kwa furaha chini ya utawala huo. Wananufaika kutokana na programu yake ya elimu na wanajitahidi kufuata sheria zake zipatikanazo katika Biblia. (Isaya 54:13) Hao ndio msingi wa “dunia mpya” katika maana ya kwamba wao ndio jamii ya ulimwenguni pote ya watu wa mataifa yote, lugha zote, na jamii zote, nao hufanya kazi pamoja wakijitiisha chini ya Mfalme anayetawala, Yesu Kristo. Jambo muhimu ni kwamba unaweza kuwa mmoja wao!—Mika 4:1-4.
17, 18. Kwa nini maneno yanayopatikana kwenye 2 Petro 3:13 yanatupa sababu ya kuutazamia wakati ujao?
17 Usidhani kwamba huo ndio mwisho wa mambo, kwamba hatujui barabara mambo yatakayotukia wakati ujao. Kwa kweli, ukichunguza muktadha wa 2 Petro sura ya 3 utaona mambo yanayodokeza kwamba badiliko kubwa litatukia. Katika mstari wa 5 na wa 6, Petro aandika juu ya Furiko la siku ya Noa, Gharika iliyokomesha ulimwengu mwovu wa wakati huo. Katika mstari wa 7, Petro ataja kwamba “mbingu na dunia zilizopo sasa,” mamlaka za utawala na watu pia, zimewekwa akiba kwa ajili ya “siku ya hukumu na ya uangamizo wa watu wasiomwogopa Mungu.” Hilo lathibitisha kwamba usemi “mbingu na dunia” haurejezei sayari yetu, ulimwengu halisi, bali wanadamu na mamlaka zao za utawala.
18 Petro aeleza katika mistari inayofuata kwamba siku ijayo ya Yehova itatokeza usafishaji mkubwa, ikifanya matayarisho kwa ajili ya mbingu mpya na dunia mpya zilizotajwa katika mstari wa 13. Ona mwisho wa mstari huo—“katika hizo uadilifu utakaa.” Je, hilo halidokezi kwamba mabadiliko makubwa mazuri lazima yatukie? Je, hilo halikuzi tazamio la mambo mapya kwelikweli, wakati ambapo wanadamu watafurahia zaidi maisha kuliko wanavyofanya leo? Ikiwa waweza kuelewa hilo, basi umepata kufahamu mambo ambayo Biblia hutabiri, ufahamu ambao ni watu wachache tu wanao.
19. Ni katika kikao gani kitabu cha Ufunuo chataja “mbingu mpya na dunia mpya” zitakazokuja?
19 Lakini acheni tulichunguze jambo hilo zaidi. Tumechunguza usemi “mbingu mpya na dunia mpya” katika Isaya sura ya 65 na pia katika 2 Petro sura ya 3. Sasa fungua Ufunuo sura ya 21, ambapo usemi huo wapatikana tena katika Biblia. Tena, kuelewa kikao kutatusaidia. Sura mbili kabla, katika Ufunuo sura ya 19, twaona vita ya ufananisho ikifafanuliwa kinaganaga—lakini si vita kati ya mataifa yenye uhasama. “Neno la Mungu” yuko kwenye upande mmoja wa vita. Yaelekea unatambua kwamba jina hilo lamrejezea Yesu Kristo. (Yohana 1:1, 14) Yeye yuko mbinguni, na katika ono hili, anaonekana akiwa na majeshi yake ya kimbingu. Akipigana na nani? Sura hiyo yataja “wafalme,” “makamanda wa kijeshi,” na watu wenye nyadhifa mbalimbali, “wadogo na wakubwa.” Pigano hilo lahusu siku ijayo ya Yehova, kuharibiwa kwa uovu. (2 Wathesalonike 1:6-10) Katika sura inayofuata, Ufunuo sura ya 20 yaanza kwa kueleza kuondolewa kwa yule “nyoka wa awali, aliye Ibilisi na Shetani.” Jambo hilo linatutayarisha kuchunguza Ufunuo sura ya 21.
20. Andiko la Ufunuo 21:1 laonyesha kutakuwa na badiliko gani muhimu wakati ujao?
20 Mtume Yohana aanza kwa maneno haya yenye kusisimua: “Nikaona mbingu mpya na dunia mpya; kwa maana mbingu ya kwanza na dunia ya kwanza zilikuwa zimepitilia mbali, na bahari haipo tena.” Kutokana na mambo ambayo tumeona katika Isaya sura ya 65 na 2 Petro sura ya 3, tuna hakika kwamba hilo halimaanishi kuziondoa mbingu halisi na sayari yetu pamoja na vilindi vyake vya maji. Kama vile sura zinazotangulia zilivyoonyesha, watu waovu na mamlaka zao za utawala, kutia ndani mtawala asiyeonekana, Shetani, wataondolewa. Naam, kinachoahidiwa hapa ni mfumo mpya wa mambo unaohusisha watu duniani.
21, 22. Yohana anatuhakikishia baraka gani, na kufutwa kwa machozi kwamaanisha nini?
21 Tunahakikishiwa jambo hilo tuchunguzapo unabii huu wa ajabu. Mwisho wa mstari wa 3 wazungumzia wakati ambapo Mungu atakuwa na wanadamu, akiwafikiria na kuwanufaisha watu wanaofanya mapenzi yake. (Ezekieli 43:7) Yohana aendelea kusema hivi katika mstari wa 4 na 5: “Naye [Yehova] atafuta kabisa kila chozi kutoka katika macho yao, na kifo hakitakuwapo tena, wala ombolezo wala kupaaza kilio wala umivu halitakuwapo tena kamwe. Mambo ya zamani yamepitilia mbali. Na Yeye aketiye juu ya kiti cha ufalme akasema: ‘Tazama! Mimi ninafanya vitu vyote kuwa vipya.’ Pia, husema: ‘Andika, kwa sababu maneno haya ni ya uaminifu na ya kweli.’” Ni unabii wenye kutia moyo kama nini!
22 Hebu tua ufurahie mambo ambayo Biblia inatabiri. ‘Mungu atafuta kabisa kila chozi katika macho yao.’ Hilo haliwezi kuwa larejezea machozi ya kawaida ambayo husafisha macho yetu yawezayo kudhuriwa kwa urahisi, wala haliwezi kuwa larejezea machozi ya furaha. La, Mungu atafuta kabisa machozi ambayo husababishwa na kuteseka, huzuni, kutamaushwa, kuumizwa, na maumivu makali. Twawezaje kuwa na uhakika? Ahadi hiyo ya Mungu yenye kutokeza yahusianisha kufuta kabisa machozi na ‘kutokuwepo tena kwa kifo, maombolezo, kupaaza kilio, na maumivu.’—Yohana 11:35.
23. Unabii wa Yohana watuhakikishia mwisho wa hali zipi?
23 Je, hilo halithibitishi kwamba kansa, ugonjwa wa ubongo usababishao kupooza, magonjwa ya moyo, na hata kifo zitakuwa zimeondolewa? Ni nani kati yetu ambaye hajafiwa na mpendwa kutokana na ugonjwa fulani, aksidenti, au msiba? Mungu anaahidi hapa kwamba kifo hakitakuwapo tena, jambo linalodokeza kwamba watoto wowote ambao huenda wakazaliwa wakati huo hawatalazimika kukua kisha kuzeeka na hatimaye kufa kutokana na uzee. Unabii huo pia wamaanisha kwamba ugonjwa wa kupungua akili hautakuwapo tena, wala kudhoofika kwa mifupa, magonjwa ya mji wa mimba, magonjwa ya macho—magonjwa ambayo watu huugua sana uzeeni.
24. ‘Mbingu mpya na dunia mpya’ zitakuwaje baraka, na ni nini ambacho bado tutachunguza?
24 Bila shaka, ungekubali kwamba maombolezo na kupaaza kilio kungepungua iwapo kifo, uzee, na maradhi yangeondolewa. Hata hivyo, vipi juu ya ufukara, kuwadhulumu watoto, na ubaguzi wenye uonevu kwa sababu ya malezi au rangi ya ngozi? Kama mambo hayo—yaliyo ya kawaida sana leo—yangeendelea, bado maombolezo na kupaaza kilio zingekuwako. Kwa hiyo, maisha katika “mbingu mpya na dunia mpya” hayataharibiwa na mambo yanayosababisha huzuni leo. Ni badiliko lililoje!
-
-
Je, Utakuwepo Katika Ulimwengu Mpya?Mnara wa Mlinzi—2000 | Aprili 15
-
-
2. Unatazamia mambo gani?
2 Katika makala iliyotangulia, tulichunguza matabiri matatu kati ya manne ambapo Biblia hutabiri juu ya “mbingu mpya na nchi [“dunia,” NW] mpya.” (Isaya 65:17) Utabiri mmoja kati ya matabiri hayo yenye kutegemeka umerekodiwa kwenye Ufunuo 21:1. Mistari inayofuata inataja wakati ambapo Mungu Mweza Yote atabadili kabisa hali duniani ziwe bora. Atafuta machozi ya huzuni. Watu hawatakufa tena kutokana na uzee, ugonjwa, au aksidenti. Maombolezo, kilio, na maumivu yatatoweka. Ni matazamio yenye kupendeza kama nini! Lakini tunaweza kuwa na hakika kwamba matazamio hayo yatatimizwa, nayo yaweza kuwa na matokeo gani juu yetu wakati huu?
Sababu za Kuwa na Uhakika
3. Kwa nini twaweza kutumaini ahadi za Biblia kuhusu wakati ujao?
3 Ona jinsi Ufunuo 21:5 linavyoendelea kusema. Lamnukuu Mungu, aketiye katika kiti chake cha ufalme mbinguni akitangaza hivi: “Tazama! Mimi ninafanya vitu vyote kuwa vipya.” Ahadi hiyo ya Mungu ni bora kuliko tangazo lolote la kitaifa la uhuru, kuliko sheria yoyote ya leo ya haki za binadamu, au lengo lolote la wanadamu la wakati ujao. Ni tangazo linalotegemeka kabisa kutoka kwa Mmoja ambaye Biblia husema ‘hawezi kusema uwongo.’ (Tito 1:2) Inaeleweka kwamba huenda ukahisi hakuna kitu kingine kinachohitajiwa ila kuendelea tu kufurahia matazamio hayo mazuri sana na kumtumaini Mungu. Lakini si lazima tukomee hapo. Kuna mengi bado tuwezayo kujifunza juu ya wakati wetu ujao.
4, 5. Ni unabii gani mbalimbali wa Biblia tuliochunguza tayari ambao waweza kuimarisha tumaini letu juu ya mambo yatakayotukia wakati ujao?
4 Fikiria mambo ambayo makala iliyotangulia ilithibitisha kuhusu ahadi za Biblia juu ya mbingu mpya na dunia mpya. Isaya alitabiri mfumo huo mpya, na unabii wake ulitimizwa Wayahudi waliporudi katika nchi yao na kuanzisha tena ibada ya kweli. (Ezra 1:1-3; 2:1, 2; 3:12, 13) Hata hivyo, je, unabii wa Isaya ulirejezea tukio hilo tu? Bila shaka la! Mambo aliyotabiri yangetimizwa pia katika njia kubwa zaidi muda mrefu baadaye. Kwa nini tukate kauli hiyo? Kwa sababu ya mambo tusomayo katika 2 Petro 3:13 na Ufunuo 21:1-5. Maandiko hayo yarejezea mbingu mpya na dunia mpya zitakazowanufaisha Wakristo ulimwenguni pote.
5 Kama ilivyotajwa awali, Biblia hutumia usemi “mbingu mpya na dunia mpya” mara nne. Tumechunguza semi tatu kati ya hizo nne nasi tumekata kauli yenye kutia moyo sana. Biblia hutabiri waziwazi kwamba Mungu ataondoa uovu na mambo mengine yanayosababisha kuteseka na kwamba atazidi kuwabariki wanadamu katika mfumo wake mpya ulioahidiwa.
6. Unabii wa nne unaotaja “mbingu mpya na dunia mpya” watabiri nini?
6 Sasa na tuchunguze usemi unaosalia wa “mbingu mpya na dunia mpya,” kwenye Isaya 66:22-24: “Kama vile mbingu mpya na nchi [“dunia,”NW] mpya, nitakazofanya, zitakavyokaa mbele zangu, asema BWANA, ndivyo uzao wenu na jina lenu litakavyokaa. Na itakuwa, mwezi mpya hata mwezi mpya, na sabato hata sabato, wanadamu wote watakuja kuabudu mbele zangu, asema BWANA. Nao watatoka nje na kuitazama mizoga ya watu walioniasi; maana funza wao hatakufa, wala moto wao hautazimika nao watakuwa chukizo machoni pa wote wenye mwili.”
7. Kwa nini tufikie mkataa wa kwamba andiko la Isaya 66:22-24 litatimizwa wakati ujao?
7 Unabii huo ulitimizwa miongoni mwa Wayahudi waliorudishwa katika nchi yao, lakini kungekuwa na utimizo mwingine. Lazima utimizo huo ungetokea baadaye sana, baada ya barua ya pili ya Petro na Ufunuo kuandikwa, kwa kuwa barua hizo zataja ‘mbingu na dunia mpya’ za wakati ujao. Twaweza kutarajia utimizo huo mkubwa na ulio kamili katika mfumo mpya. Fikiria baadhi ya mambo tuwezayo kutazamia kufurahia.
8, 9. (a) Ni katika maana gani watu wa Mungu wataendelea ‘kukaa’? (b) Ni nini maana ya unabii kwamba watumishi wa Yehova wataabudu “mwezi mpya hata mwezi mpya, na sabato hata sabato”?
8 Andiko la Ufunuo 21:4 laonyesha kwamba kifo hakitakuwapo tena kamwe. Maneno ya Isaya sura ya 66 yakubaliana na ahadi hiyo. Twaweza kuona kuanzia mstari wa 22 kwamba Yehova anajua ya kwamba mbingu mpya na dunia mpya hazitakuwa za muda mfupi tu. Isitoshe, watu wake watadumu; wataendelea ‘kukaa’ mbele zake. Yale ambayo tayari Mungu amewafanyia wateule wake yatupa uhakika. Wakristo wa kweli wamekabili mnyanyaso mkali, hata wamekabili jitihada za kishupavu za kuwaangamiza. (Yohana 16:2; Matendo 8:1) Lakini, hata maadui wenye nguvu sana wa watu wa Mungu, kama vile Maliki Nero wa Roma na Adolf Hitler, hawajaweza kuwaondolea mbali waaminifu-washikamanifu wa Mungu, wanaoitwa kwa jina lake. Yehova amehifadhi kutaniko la watu wake, nasi tuna hakika kwamba anaweza kuendelea kulifanya likae hata milele.
9 Vivyo hivyo, wakiwa mtu mmoja-mmoja, wale walio waaminifu kwa Mungu, wakiwa sehemu ya dunia mpya, jamii ya waabudu wa kweli katika ulimwengu mpya, watakaa daima kwa kuwa watakuwa wakimtolea Muumba wa vitu vyote ibada safi. Ibada hiyo haitakuwa ya pindi kwa pindi au isiyo na utaratibu. Sheria ya Mungu, ambayo Waisraeli walipewa kupitia Musa, ilitaka matendo fulani ya ibada yafanywe kila mwezi, uliotiwa alama na mwezi mpya, na kila juma, lililotiwa alama na siku ya Sabato. (Mambo ya Walawi 24:5-9; Hesabu 10:10; 28:9, 10; 2 Mambo ya Nyakati 2:4) Kwa hiyo, Isaya 66:23 lataja ibada ya kawaida na yenye kuendelea ya Mungu, juma baada ya juma, mwezi baada ya mwezi. Kutoamini kuwepo kwa Mungu na unafiki wa kidini hazitakuwako wakati huo. “Wanadamu wote watakuja kuabudu mbele” za Yehova.
10. Kwa nini unaweza kuwa na hakika kwamba ulimwengu mpya hautaharibiwa daima na waovu?
10 Isaya 66:24 latuhakikishia kwamba amani na uadilifu za dunia mpya hazitakuwa hatarini kamwe. Waovu hawataiharibu dunia kamwe. Kumbuka kwamba andiko la 2 Petro 3:7 lasema kwamba tunangojea “siku ya hukumu na ya uangamizo wa watu wasiomwogopa Mungu.” Watakaoharibiwa ni watu wasiomwogopa Mungu. Hakuna madhara yatakayowapata wasio na hatia, tofauti na vile itukiavyo mara nyingi katika vita vya wanadamu, ambapo majeruhi walio raia huwa wengi kuliko askari. Hakimu Mkuu atuhakikishia kwamba siku yake itakuwa ya kuangamiza watu wasiomwogopa Mungu.
11. Isaya anaonyesha ni nini kitampata yeyote anayekataa Mungu na ibada yake?
11 Waokokaji waadilifu wataona kwamba neno la Mungu la kiunabii ni la kweli. Mstari wa 24 hutabiri kwamba ‘mizoga ya watu waliomwasi’ Yehova itakuwa uthibitisho wa hukumu yake. Huenda maneno ya waziwazi ambayo Isaya alitumia yakawa yenye kushtua. Hata hivyo, yanapatana na jambo hakika la kihistoria. Nje ya kuta za Yerusalemu la kale kulikuweko mahali mbalimbali pa kutupa takataka na, pindi kwa pindi, mizoga ya wahalifu walioonekana kuwa hawastahili mazishi ya heshima.a Huko funza na moto mkali zingemaliza upesi takataka hizo na mizoga hiyo. Kwa wazi, mfano wa Isaya waonyesha mfano wa hukumu ya Yehova dhidi ya waasi ambayo haiwezi kubadilishwa.
Mambo Ambayo Ameahidi
12. Isaya atoa madokezo gani zaidi kuhusu maisha katika ulimwengu mpya?
12 Ufunuo 21:4 latuambia mambo ambayo hayatakuwapo katika mfumo mpya ujao. Hata hivyo, ni mambo gani yatakayokuwapo wakati huo? Maisha yatakuwaje? Je, twaweza kupata madokezo yoyote yenye kutegemeka? Ndiyo. Isaya sura ya 65 yafafanua kiunabii hali tutakazofurahia iwapo tutakubaliwa na Yehova kuishi wakati aumbapo hatimaye mbingu mpya na dunia mpya. Waliobarikiwa kuishi daima katika dunia mpya hawatazeeka kisha wafe. Isaya 65:20 latuhakikishia hivi: “Hatakuwapo tena mtoto wa siku chache, wala mzee asiyetimia siku zake; kwa maana mtoto atakufa mwenye umri wa miaka mia; bali mtenda dhambi mwenye umri wa miaka mia atalaaniwa.”
13. Isaya 65:20 latuhakikishiaje kwamba watu wa Mungu watakuwa salama?
13 Unabii huo ulipotimizwa mara ya kwanza kwa watu wa Isaya, ulimaanisha kwamba watoto wa nchi hiyo walikuwa salama. Hakuna adui waliokuwa wakiwajia, kama vile Wababiloni walivyofanya pindi moja, ili kunyakua watoto wanyonyao au kuangamiza wanaume wenye nguvu. (2 Mambo ya Nyakati 36:17, 20) Katika ulimwengu mpya ujao, watu watakuwa salama salimini nao wataweza kufurahia maisha. Iwapo mtu ataamua kumwasi Mungu, hataruhusiwa kuendelea kuishi. Mungu atamwondoa. Itakuwaje ikiwa mtenda-dhambi huyo mwasi ana umri wa miaka mia moja? Atakufa akiwa “mtoto wa siku chache” ikilinganishwa na kufurahia maisha yasiyo na kikomo.—1 Timotheo 1:19, 20; 2 Timotheo 2:16-19.
14, 15. Ni utendaji gani wenye kuthawabisha uwezao kutarajia kulingana na Isaya 65:21, 22?
14 Badala ya kuzungumzia sana jinsi mtenda-dhambi wa kukusudia awezavyo kuondolewa, Isaya afafanua hali za maisha zitakazokuwapo katika ulimwengu mpya. Jiwazie ukiwa katika hali hizo. Huenda mambo uwezayo kuwazia kwanza yakawa yale unayopenda sana. Isaya azungumzia mambo hayo katika mstari wa 21 na 22: “Watajenga nyumba, na kukaa ndani yake; watapanda mizabibu, na kula matunda yake. Hawatajenga, akakaa mtu mwingine ndani yake; hawatapanda, akala mtu mwingine; maana kama siku za mti ndivyo zitakavyokuwa siku za watu wangu, na wateule wangu wataifurahia kazi ya mikono yao muda wa siku nyingi.”
15 Ikiwa bado hujapata ujuzi wa kujenga au kulima, unabii wa Isaya wadokeza kwamba utaelimishwa. Hata hivyo, je, ungetaka kujifunza ukisaidiwa na wafunzi wenye uwezo, labda majirani wenye fadhili wanaofurahia kukusaidia? Isaya hakusema ikiwa nyumba yako itakuwa na madirisha makubwa yenye pazia na yasiyo na vioo ili kukuwezesha kufurahia kupunga upepo, au madirisha yenye vioo ambavyo kupitia hivyo waweza kuona majira yenye kubadilika-badilika. Je, utajenga nyumba yako ikiwa na paa yenye kuinama ili mvua na theluji zitiririke? Au tabia ya nchi ya kwenu itahitaji paa tambarare—kama mojawapo ya zile za Mashariki ya Kati—paa ambayo wewe na familia yako mwaweza kukusanyikia ili kula milo mizuri na kuwa na mazungumzo yenye kupendeza?—Kumbukumbu la Torati 22:8; Nehemia 8:16.
16. Kwa nini unaweza kutarajia ulimwengu mpya uwe wenye kuridhisha daima?
16 Jambo la maana zaidi kuliko kujua mambo hayo madogo-madogo ni kwamba utakuwa na makao yako mwenyewe. Yatakuwa yako—si kama vile leo uwezavyo kujitahidi kujenga kisha mtu mwingine akanufaika. Isaya 65:21 pia lasema kwamba utapanda na kula matunda. Ni wazi kwamba hilo laonyesha jinsi hali itakavyokuwa kwa ujumla. Utaridhishwa sana na jitihada zako, matokeo ya jasho lako mwenyewe. Nawe utaweza kufanya hivyo kwa muda mrefu—“kama siku za mti.” Bila shaka hilo lapatana na ufafanuzi wa “vitu vyote kuwa vipya”!—Zaburi 92:12-14.
17. Wazazi watatiwa moyo hasa na ahadi gani?
17 Ikiwa wewe ni mzazi, maneno haya yatakugusa moyo: “Hawatajitaabisha kwa kazi bure, wala hawatazaa kwa taabu; kwa sababu wao ni wazao wa hao waliobarikiwa na BWANA, na watoto wao pamoja nao. Na itakuwa ya kwamba, kabla hawajaomba, nitajibu; na wakiwa katika kunena, nitasikia.” (Isaya 65:23, 24) Je, unajua maumivu ya ‘kuzaa kwa taabu’? Hatuhitaji kuorodhesha matatizo yawezayo kuwapata watoto ambayo huwataabisha wazazi na watu wengine. Kuhusiana na hilo, sote tumeona wazazi ambao hujishughulisha sana na kazi, utendaji, au anasa zao wenyewe hivi kwamba hawana wakati wa kutosha kwa watoto wao. Tofauti na hao, Yehova anatuhakikishia kwamba atasikia na kutosheleza mahitaji yetu, hata atayatarajia.
18. Kwa nini waweza kutarajia kufurahia wanyama katika ulimwengu mpya?
18 Ufikiriapo mambo uwezayo kufurahia katika ulimwengu mpya, wazia mandhari ambayo neno la Mungu la kiunabii lataja: “Mbwa-mwitu na mwana-kondoo watalisha pamoja, na simba atakula majani kama ng’ombe; na mavumbi yatakuwa chakula cha nyoka. Hawatadhuru wala kuharibu katika mlima wangu mtakatifu wote, asema BWANA.” (Isaya 65:25) Wasanii wamejaribu kuchora mandhari hiyo, lakini hiyo si mchoro wa kuwaziwa tu usioonyesha mambo kihalisi. Mandhari hiyo itakuwa halisi. Amani itaenea miongoni mwa wanadamu na pia kati yao na wanyama. Wataalamu wengi wa wanyama na watu wengi wanaopenda wanyama hutumia miaka mingi zaidi maishani mwao wakijifunza juu ya aina chache za wanyama au hata mnyama mmoja tu. Tofauti na hilo, hebu wazia mambo utakayoweza kujifunza wakati ambapo wanyama hawatakuwa wakiwaogopa wanadamu. Ndipo utakapoweza kuwakaribia hata ndege na viumbe wadogo ambao hukaa msituni—naam, uwatazame, ujifunze, na kuwafurahia. (Ayubu 12:7-9) Utaweza kufanya hivyo ukiwa salama salimini, bila hatari yoyote kutokana na mwanadamu au mnyama. Yehova asema: “Hawatadhuru wala kuharibu katika mlima wangu mtakatifu wote.” Litakuwa badiliko lililoje tofauti na hali zilizoko leo!
-