Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Nchi Ambazo Zilikuwa Sehemu ya Yugoslavia
    2009 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
    • Mwanamke mmoja kijana Mromani alijifunza kweli akiwa mtoto kutoka kwa mashangazi wake walioishi katika nchi nyingine. Kizuizi kimoja alichohitaji kushinda ni kujua kusoma na kuandika. Akichochewa na upendo kwa Yehova, alijifunza kusoma na kuandika katika muda wa miaka mitatu aliyokuwa akijifunza Biblia. Kizuizi cha pili kilikuwa babu yake, ambaye aliishi naye. Mwanamke huyo anasema hivi: “Nilijificha nilipokuwa nikienda kwenye mikutano.” Lakini babu yake aliporudi, alimpiga. Anasema hivi: “Niliteseka sana kimwili kwa sababu ya kweli, lakini sikukata tamaa. Nilitafakari kuhusu mateso yote ya mwanamume mwaminifu Ayubu. Nilimpenda sana Yehova, na niliazimia kutoacha kujifunza.” Hivi sasa anatumikia akiwa painia, naye anajifunza Biblia pamoja na wasichana wawili wasiojua kusoma na kuandika. Ingawa hakuenda katika shule ya kilimwengu, anathamini jinsi ambavyo Shule ya Huduma ya Kitheokrasi imemzoeza kuwafundisha wengine.

  • Nchi Ambazo Zilikuwa Sehemu ya Yugoslavia
    2009 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
    • “Ninaweza Kuwapata Wapi Watu Hawa?”

      AGRON BASHOTA

      ALIZALIWA 1973

      ALIBATIZWA 2002

      MAELEZO MAFUPI KUMHUSU Alikuwa mwanajeshi katika Jeshi la Ukombozi la Kosovo na sasa anatumika akiwa painia wa kawaida na mtumishi wa huduma.

      NILIPOONA mambo mabaya sana yaliyofanywa wakati wa vita, kama vile kuwaua watoto wadogo, nilikata kauli kwamba hakuna Mungu. Nilifikiri hivi: ‘Ikiwa yupo, kwa nini hakomeshi mateso haya yote?’ Imani yangu ilidhoofika zaidi nilipoona jinsi viongozi wa dini ya Kiislamu walivyounga mkono vita dhidi ya Waserbia. Kabla ya vita, nilikuwa Mwislamu, hata hivyo, vita vilipokwisha, sikuamini tena kwamba kuna Mungu, na nilijiunga na Jeshi la Ukombozi la Kosovo. Ingawa nilikuwa katika jeshi hilo kwa muda mfupi tu, niliheshimiwa sana na nilipata mapendeleo mengi. Hilo lilinifanya niwe mkali na mwenye kiburi kwa sababu watu walifanya nilivyoagiza.

      Inasikitisha kwamba nilimtendea mke wangu kwa njia hiyohiyo. Nilifikiri kwamba anapaswa kufanya kila jambo ninalomwambia na kutii maagizo yangu yote. Mke wangu, Merita, alikuwa amekutana na Mashahidi wakati wa vita na alikuwa na vitabu vyao vichache. Usiku mmoja kabla ya kwenda kulala, alisema hivi: “Chukua vitabu hivi usome. Vina habari kumhusu Mungu.” Nilikasirika kwamba alifikiri angenifundisha kumhusu Mungu. Ili kuepuka ugomvi, Merita alienda kulala.

      Nilibaki na vitabu hivyo, nikaamua kusoma broshua Mungu Anataka Tufanye Nini? Kisha nikasoma kijitabu Sasa Ndio Wakati wa Kumtii Mungu Kweli Kweli. Nikiwa Mwislamu, nilishangaa kuona kwamba kilinukuu Kurani. Halafu nikasoma magazeti kadhaa ya Mnara wa Mlinzi na Amkeni! Baadaye usiku huohuo, nilienda katika chumba cha kulala na kumwamsha mke wangu. Nilimuuliza: “Ni nani aliyekupa vitabu hivi? Ninaweza kuwapata wapi watu hawa?”

      Niliguswa moyo sana na mambo niliyosoma, lakini mke wangu alikuwa na shaka na aliogopa kwa kuwa hakujua nilichokusudia kufanya. Hata hivyo, usiku huo tulimpigia simu Shahidi mmoja, akatujulisha wakati na mahali ambapo wangefanyia mkutano wao. Asubuhi iliyofuata tulihudhuria mkutano huo. Nilivutiwa sana kuona jinsi ndugu walivyotukaribisha kwa fadhili! Sikufikiri kamwe kwamba kuna watu kama hao duniani. Niliona wazi kwamba walikuwa tofauti. Wakati wa mkutano nilikuwa na swali ambalo nilitaka sana lijibiwe, hata niliinua mkono wangu ili niulize swali hilo. Wazee walikuwa na wasiwasi kidogo kwa sababu hawakujua kwa nini nilitaka sana kuzungumza nao. Bila shaka, walifurahi sana walipotambua kwamba nilitaka tu kujua nilichopaswa kufanya ili niwe Shahidi wa Yehova.

      Nilianza kujifunza Biblia siku hiyohiyo. Nilitaka kuboresha sana utu wangu, na haingekuwa rahisi kufanya hivyo. Nilitaka kuacha kuvuta sigara, na nilihisi kwamba nilihitaji kuvunja uhusiano na marafiki wangu wa zamani. Kusali na kuhudhuria mikutano kwa ukawaida kulinisaidia kutubu mwenendo wangu wa zamani wa maisha na kuvaa utu mpya. Kweli imebadili kabisa maisha yangu na ya familia yangu! Sasa mimi na mke wangu tunatumikia tukiwa mapainia wa kawaida, na mwaka wa 2006, niliwekwa rasmi kuwa mtumishi wa huduma. Sasa ninaweza kuwasaidia wengine kuelewa kwa nini watu wanateseka na jinsi Yehova atakavyotatua matatizo yetu yote hivi karibuni.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki