Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Nchi Ambazo Zilikuwa Sehemu ya Yugoslavia
    2009 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
    • Historia ya Kisasa ya Kosovo

      Chuki kati ya Waserbia na Waalbania huko Kosovo miaka ya 1980 ilisababisha vita vikali katika miaka ya 1990, na watu waliteseka sana na kuumia. Chini ya hali hiyo, ndugu na dada zetu waliwaonyesha waamini wenzao wa makabila yote “upendo wa kindugu usio na unafiki.” (1 Pet. 1:22) Kwa kuongezea, wametii amri ya Kristo ya ‘kuwapenda adui zao na kusali kwa ajili ya wale wanaowatesa.’ (Mt. 5:43-48) Hata hivyo, nyakati nyingine imekuwa vigumu kufanya hivyo.

      Saliu Abazi, anayezungumza Kialbania, na ambaye alikuwa Mwislamu zamani anasema: “Ndugu waliokuwa Waislamu zamani hawatendewi sikuzote kwa fadhili na Waislamu, na watu wa familia zetu wanafikiri kimakosa kwamba tumewaacha kwa sababu tumechagua dini nyingine. Pia, kwa sababu ya chuki ya kikabila kati ya Waalbania na Waserbia, mara nyingi inakuwa vigumu kwa wale waliokuwa Waislamu kuwahubiria Waserbia.”

      Hata hivyo, kikundi cha watu 30 wa makabila mbalimbali kilikuwa kikikutana katika nyumba ya Saliu. “Katika miaka hiyo,” anakumbuka Saliu, “mikutano ilifanywa katika Kiserbia, na tulipata vitabu kutoka Belgrade. Siku moja polisi walikuja kwa ghafula katika nyumba yangu. Wakati huo akina ndugu kutoka Belgrade walikuwa tu wameleta vitabu, na sote tulikuwa tukifurahia ushirika. Nilipowaambia polisi kwamba hao walikuwa ndugu zangu, hawangeweza kuelewa jinsi Waserbia na Waalbania wanavyoweza kuwa ndugu.” Mwaka wa 1998, kikundi hicho cha wahubiri kilikodi mahali pa kutumia kama Jumba la Ufalme, katika mji mkubwa zaidi wa Kosovo, Priština.

      Katika majira ya masika ya 1999, chuki ya kikabila na roho ya utaifa ilipamba moto sana. Saliu anasema: “Jirani yangu alitisha kwamba ikiwa mimi na mwanangu hatungeshiriki katika vita, nyumba yetu ingeteketezwa kabisa. Hali ya kisiasa iliwachochea vibaya watu. Kwa sababu watu walipinga serikali iliyokuwa ikitawala Serbia, sheria hazingeweza kutekelezwa, watu walikuwa wajeuri, nao walifanya walichotaka.”

      Waserbia walioishi Kosovo walikabili hali ngumu zaidi kadiri hali ya kisiasa ilivyozidi kuzorota. Katika vita vya mwaka wa 1999, maelfu ya Waserbia na Waalbania walilazimika kukimbilia nchi nyingine jirani. Hata hivyo, ingawa kulikuwa na chuki kali sana ya kikabila, Saliu alihatarisha uhai wake kwa kuwaruhusu ndugu zake Waserbia wakimbilie katika nyumba yake.

      KUFINYANGWA NA MAONI YA YEHOVA

      Dada mmoja alisema hivi: “Chuki kati ya Waserbia na Waalbania ilikuwa kali sana. Tulijifunza kuwachukia tangu utotoni. Si rahisi kuacha chuki hiyo hata baada ya kujifunza kweli. Wengi wetu tulilazimika kufanya mabadiliko makubwa ili tufuate maoni ya Yehova. Kwa sababu ya chuki hiyo, hata nilipokuwa nikijifunza kwamba Yehova ni upendo, nilikuwa nikimwepuka dada fulani katika kutaniko kwa sababu tu ni Mserbia. Hata hivyo, nilipoendelea kujifunza nilianza kutambua kwamba kweli ya Neno la Yehova inawaunganisha watu, lakini mafundisho ya dini nyingine yanawagawanya watu.” Je, nguvu za Neno la Mungu za kuwabadili watu zimemsaidia dada huyo kuvaa utu mpya wa Kikristo? Anasema hivi: “Sasa, ninafurahi kutumikia katika kutaniko moja na ndugu na dada zangu Waserbia.”—Kol. 3:7-11; Ebr. 4:12.

      Umoja wa kweli wa Kikristo unaonekana wazi katika ulimwengu huu uliogawanyika kidini. Wakati watu walipokuwa wakiteketeza nyumba na kurusha guruneti kwa sababu ya roho ya utaifa, ndugu zetu walikuwa wakisafiri kwenda Belgrade, Serbia, kwa ajili ya kusanyiko mwezi wa Julai 1998. Waalbania, Wakroatia, Wamakedonia, na Waromani walisafiri pamoja katika mabasi kwa amani. Dashurie Gashi, ambaye alikuwa akienda kubatizwa kwenye kusanyiko hilo, anasema hivi: “Askari-jeshi walipolisimamisha basi, nyuso zao zilionyesha kwamba walikuwa wameshtuka. Hata ingawa kulikuwa na chuki kali ya kikabila katika nchi hizo, tulikuwa kikundi kimoja chenye umoja—watu wa Yehova.”

      Mwanamke mmoja kijana Mromani alijifunza kweli akiwa mtoto kutoka kwa mashangazi wake walioishi katika nchi nyingine. Kizuizi kimoja alichohitaji kushinda ni kujua kusoma na kuandika. Akichochewa na upendo kwa Yehova, alijifunza kusoma na kuandika katika muda wa miaka mitatu aliyokuwa akijifunza Biblia. Kizuizi cha pili kilikuwa babu yake, ambaye aliishi naye. Mwanamke huyo anasema hivi: “Nilijificha nilipokuwa nikienda kwenye mikutano.” Lakini babu yake aliporudi, alimpiga. Anasema hivi: “Niliteseka sana kimwili kwa sababu ya kweli, lakini sikukata tamaa. Nilitafakari kuhusu mateso yote ya mwanamume mwaminifu Ayubu. Nilimpenda sana Yehova, na niliazimia kutoacha kujifunza.” Hivi sasa anatumikia akiwa painia, naye anajifunza Biblia pamoja na wasichana wawili wasiojua kusoma na kuandika. Ingawa hakuenda katika shule ya kilimwengu, anathamini jinsi ambavyo Shule ya Huduma ya Kitheokrasi imemzoeza kuwafundisha wengine.

      Adem Grajçevci alikuwa Mwislamu kabla ya kujifunza kweli mwaka wa 1993 huko Ujerumani. Kisha mwaka wa 1999, alirudi katika nchi yao ya Kosovo na kama Mashahidi wengine wapya, alikabiliana na chuki na upinzani kutoka kwa watu wa jamaa yake. Adem anakumbuka hivi: “Nilipokuwa nikijifunza kweli, nilifurahi sana kujua kwamba Shetani ndiye mtawala wa ulimwengu na kwamba ndiye anayesababisha jeuri yote iliyopo.” Baba ya Adem hakupendezwa na imani mpya ya Kikristo ya mwana wake, hivyo akamwambia achague kati ya Yehova na familia yao. Adem alimchagua Yehova, akaendelea kufanya maendeleo ya kiroho, na sasa anatumikia akiwa mzee Mkristo. Inafurahisha kwamba baada ya miaka mingi kupita, baba ya Adem hana chuki tena, naye sasa anaheshimu zaidi uamuzi ambao Adem alifanya.

      Adnan, mwana wa Adem, hakupendezwa hata kidogo na dini alipokuwa mtoto. Alijihusisha sana na mchezo fulani kama wa karate na wenzake walimbandika jina, Muuaji. Hata hivyo, mwishowe kweli ilipogusa moyo wake aliacha kabisa mchezo huo. Alifanya maendeleo makubwa naye akabatizwa. Alisema hivi: “Muda mfupi baada ya kubatizwa nililazimika kufanya uamuzi. Nilikuwa na kazi nzuri, na vilevile pesa nyingi. Lakini nilikuwa mgonjwa kiroho na sikuwa na wakati wa kuhubiri. Niliamua kufanya mabadiliko, hivyo niliacha kazi yangu.” Alianza kufanya upainia, akawekwa kuwa mtumishi wa huduma, na baadaye akaalikwa kuhudhuria darasa la kwanza la Shule ya Mazoezi ya Kihuduma huko Albania. Sasa, Adnan ni mzee wa kutaniko, naye ni painia wa pekee pamoja na mke wake, Hedije. Anahisi namna gani kuhusu uamuzi aliofanya? Anasema: “Nimepata furaha isiyo na kifani. Sijuti kamwe kwamba nilichagua huduma ya wakati wote.”

      UMOJA KATIKA IBADA NA MAFUNDISHO

      Leo makutaniko yote sita nchini Kosovo yamekodi majengo ya kutumia kama Majumba ya Ufalme. Makutaniko mengine ni madogo, kama lile lililo katika mji wa Peć, ambalo lina wahubiri 28. Kwa kuwa kuna upungufu wa ndugu waliowekwa rasmi, makutaniko fulani hayawezi kuwa na hotuba ya watu wote kila juma. Hata hivyo, kama ndugu na dada zao wa mji wa Peć, wanakutana kwa uaminifu kila juma kwa ajili ya Funzo la Mnara wa Mlinzi na mikutano mingine ya kutaniko.

      Kwa miaka mingi Halmashauri ya Nchi ya Serbia iliwafanyia uchungaji wenye upendo ndugu wa Kosovo walipokuwa wakikabili hali ngumu sana. Ili kutimiza mahitaji yanayobadilika ya ndugu hao, Baraza Linaloongoza lilichagua ofisi ya tawi ya Albania isimamie kazi ya kuhubiri nchini Kosovo kuanzia mwaka wa 2000.

      Kwa muda mrefu, Mashahidi wengi wa Yehova nchini Kosovo walikuwa Waserbia, kwa hiyo mikutano ilifanywa katika Kiserbia, na ndugu walifurahi kuwasaidia watu waliozungumza Kialbania kuelewa mikutano. Sasa hali imebadilika. Ndugu wengi nchini Kosovo ni Waalbania. Makutaniko yote yanatumia Kialbania isipokuwa kutaniko moja ndilo linalotumia Kiserbia, na ndugu wanafurahi kutafsiri hotuba ili ndugu Waserbia waelewe mikutano. Makusanyiko yote yanafanywa katika lugha zote mbili. Kwa mfano, programu yote ya kusanyiko la wilaya la 2008 ilifanywa katika Kialbania na ikatafsiriwa katika Kiserbia, na hotuba kuu zilitolewa katika Kiserbia na wazee wa Kosovo. Ndugu mmoja anaeleza hivi: “Ingawa watu wengine wanachukiana huko nje, ndani ya jumba sisi ni familia moja.”

      Ijapokuwa watu wengi huko Kosovo ni Waislamu, wanaiheshimu Biblia, na wengi wao wako tayari kuzungumzia mambo ya dini. Ndugu wa Kosovo walifurahi sana kupata kilele kipya cha wahubiri 164 katika 2008. Huku wakimtegemea Yehova kikamili, wameazimia kuendelea kujitahidi kabisa kuhubiri eneo lao, na kuwatangazia watu wa mataifa yote habari njema.

  • Nchi Ambazo Zilikuwa Sehemu ya Yugoslavia
    2009 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
    • [Sanduku/Picha katika ukurasa wa 236, 237]

      “Ninaweza Kuwapata Wapi Watu Hawa?”

      AGRON BASHOTA

      ALIZALIWA 1973

      ALIBATIZWA 2002

      MAELEZO MAFUPI KUMHUSU Alikuwa mwanajeshi katika Jeshi la Ukombozi la Kosovo na sasa anatumika akiwa painia wa kawaida na mtumishi wa huduma.

      NILIPOONA mambo mabaya sana yaliyofanywa wakati wa vita, kama vile kuwaua watoto wadogo, nilikata kauli kwamba hakuna Mungu. Nilifikiri hivi: ‘Ikiwa yupo, kwa nini hakomeshi mateso haya yote?’ Imani yangu ilidhoofika zaidi nilipoona jinsi viongozi wa dini ya Kiislamu walivyounga mkono vita dhidi ya Waserbia. Kabla ya vita, nilikuwa Mwislamu, hata hivyo, vita vilipokwisha, sikuamini tena kwamba kuna Mungu, na nilijiunga na Jeshi la Ukombozi la Kosovo. Ingawa nilikuwa katika jeshi hilo kwa muda mfupi tu, niliheshimiwa sana na nilipata mapendeleo mengi. Hilo lilinifanya niwe mkali na mwenye kiburi kwa sababu watu walifanya nilivyoagiza.

      Inasikitisha kwamba nilimtendea mke wangu kwa njia hiyohiyo. Nilifikiri kwamba anapaswa kufanya kila jambo ninalomwambia na kutii maagizo yangu yote. Mke wangu, Merita, alikuwa amekutana na Mashahidi wakati wa vita na alikuwa na vitabu vyao vichache. Usiku mmoja kabla ya kwenda kulala, alisema hivi: “Chukua vitabu hivi usome. Vina habari kumhusu Mungu.” Nilikasirika kwamba alifikiri angenifundisha kumhusu Mungu. Ili kuepuka ugomvi, Merita alienda kulala.

      Nilibaki na vitabu hivyo, nikaamua kusoma broshua Mungu Anataka Tufanye Nini? Kisha nikasoma kijitabu Sasa Ndio Wakati wa Kumtii Mungu Kweli Kweli. Nikiwa Mwislamu, nilishangaa kuona kwamba kilinukuu Kurani. Halafu nikasoma magazeti kadhaa ya Mnara wa Mlinzi na Amkeni! Baadaye usiku huohuo, nilienda katika chumba cha kulala na kumwamsha mke wangu. Nilimuuliza: “Ni nani aliyekupa vitabu hivi? Ninaweza kuwapata wapi watu hawa?”

      Niliguswa moyo sana na mambo niliyosoma, lakini mke wangu alikuwa na shaka na aliogopa kwa kuwa hakujua nilichokusudia kufanya. Hata hivyo, usiku huo tulimpigia simu Shahidi mmoja, akatujulisha wakati na mahali ambapo wangefanyia mkutano wao. Asubuhi iliyofuata tulihudhuria mkutano huo. Nilivutiwa sana kuona jinsi ndugu walivyotukaribisha kwa fadhili! Sikufikiri kamwe kwamba kuna watu kama hao duniani. Niliona wazi kwamba walikuwa tofauti. Wakati wa mkutano nilikuwa na swali ambalo nilitaka sana lijibiwe, hata niliinua mkono wangu ili niulize swali hilo. Wazee walikuwa na wasiwasi kidogo kwa sababu hawakujua kwa nini nilitaka sana kuzungumza nao. Bila shaka, walifurahi sana walipotambua kwamba nilitaka tu kujua nilichopaswa kufanya ili niwe Shahidi wa Yehova.

      Nilianza kujifunza Biblia siku hiyohiyo. Nilitaka kuboresha sana utu wangu, na haingekuwa rahisi kufanya hivyo. Nilitaka kuacha kuvuta sigara, na nilihisi kwamba nilihitaji kuvunja uhusiano na marafiki wangu wa zamani. Kusali na kuhudhuria mikutano kwa ukawaida kulinisaidia kutubu mwenendo wangu wa zamani wa maisha na kuvaa utu mpya. Kweli imebadili kabisa maisha yangu na ya familia yangu! Sasa mimi na mke wangu tunatumikia tukiwa mapainia wa kawaida, na mwaka wa 2006, niliwekwa rasmi kuwa mtumishi wa huduma. Sasa ninaweza kuwasaidia wengine kuelewa kwa nini watu wanateseka na jinsi Yehova atakavyotatua matatizo yetu yote hivi karibuni.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki