“Pata Baraka Kupitia Mfalme Anayeongozwa na Roho”
◼ “Mwanadamu amemtawala mwanadamu kwa kumuumiza.” Maneno hayo yanayopatikana katika Mhubiri 8:9, yanafafanua vizuri historia ya utawala wa wanadamu. Je, kuna tumaini? Au je, hali ya zamani inaonyesha jinsi hali itakavyokuwa wakati ujao? Maswali hayo yatazungumziwa katika hotuba ya watu wote itakayotolewa kwenye Makusanyiko ya Wilaya ya Mashahidi wa Yehova ya 2008/2009 ya “Kuongozwa na Roho ya Mungu.” Hotuba hiyo yenye kichwa “Pata Baraka Kupitia Mfalme Anayeongozwa na Roho,” itakazia uangalifu mtu mmoja ambaye atatawala kwa haki ya kweli na upendo na ambaye alitoa uhai wake kwa ajili yetu, yaani, Yesu Kristo.—Mathayo 20:28.
Ni nini kinachomfanya Yesu awe tofauti na watawala wengine wote? Isaya, nabii wa Mungu anajibu hivi: “Roho ya Yehova [Mungu] itatua juu yake, roho ya hekima na ya uelewaji, roho ya shauri na ya nguvu, roho ya ujuzi na ya kumwogopa Yehova; naye atakuwa na shangwe katika kumwogopa Yehova. Na hatahukumu kulingana na sura inayoonekana kwa macho yake tu, wala kukaripia kulingana tu na jambo lililosikiwa na masikio yake. Naye atawahukumu kwa uadilifu watu wa hali ya chini, atakaripia kwa unyoofu kwa ajili ya watu wapole wa dunia.”—Isaya 11:2-4.
Je, ufafanuzi huo unakupendeza? Ikiwa ndivyo, unakaribishwa kuhudhuria hotuba ya watu wote katika moja ya mamia ya makusanyiko ya wilaya ambayo yatafanywa ulimwenguni pote kuanzia mwezi huu. Ukipenda kujua kusanyiko lililo karibu nawe litafanyika wapi, unaweza kuwasiliana na Mashahidi wa Yehova katika eneo lenu au kuwaandikia barua wachapishaji wa gazeti hili kwa kutumia anwani zilizoonyeshwa katika ukurasa wa 5. Gazeti la Mnara wa Mlinzi la Machi 1, 2008 (1/3/2008), lina orodha ya mahali ambapo makusanyiko yote yatafanywa nchini Burundi, Kenya, Kongo (Kinshasa), Rwanda, Tanzania, na Uganda.