-
Mwige Yehova Unapowazoeza Watoto WakoMnara wa Mlinzi—2001 | Oktoba 1
-
-
Fanya Mazungumzo ya Familia Yapendeze
18. Wazazi wanawezaje kutenga wakati kwa ajili ya funzo la Biblia la familia la kawaida?
18 Miongoni mwa njia bora zaidi za kufundisha watoto wako ni kuwa na funzo la Biblia la familia kwa ukawaida na kuzungumzia Andiko kila siku. Funzo la familia huwa na matokeo sana linapofanywa kwa ukawaida. Yaelekea halitakuwa la kawaida lisipopangiwa wakati hususa wa kufanywa. Kwa hiyo lazima wazazi ‘wanunue wakati’ kwa ajili ya funzo. (Waefeso 5:15-17) Laweza kuwa jambo gumu kuchagua wakati hususa utakaowafaa wote. Baba mmoja aliona kwamba kadiri watoto walivyokua, ratiba zao zilitofautiana na ikawa vigumu kukusanya familia yote pamoja. Hata hivyo, washiriki wote wa familia hiyo walikuwepo sikuzote za mikutano ya jioni. Kwa hiyo baba huyo alipanga kufanya funzo la familia katika mojawapo ya jioni hizo. Mpango huo ukawa na matokeo. Sasa watoto wote watatu ni watumishi wa Yehova waliobatizwa.
19. Wazazi wanawezaje kumwiga Yehova wanapoongoza funzo la familia?
19 Hata hivyo, haitoshi kusoma habari fulani za Kimaandiko kijuujuu tu wakati wa funzo. Waisraeli waliorudishwa walifundishwa na Yehova kupitia makuhani ambao ‘walieleza maana ya’ Sheria “hata wakayafahamu yaliyosomwa.” (Nehemia 8:8) Kabla ya funzo la familia baba mmoja aliyefanikiwa kusaidia watoto wake wote saba wampende Yehova, alikuwa akienda chumbani mwake na kutayarisha kimbele habari ambayo itafaa mahitaji ya kila mtoto. Alifanya funzo lipendeze watoto wake. “Tulifurahia funzo sikuzote,” asema mmoja wa wanawe ambaye sasa ni mtu mzima. “Iwapo tungeitwa tulipokuwa tukicheza mpira uwanjani ili tukafanye funzo la familia, tungeacha kucheza mara moja na kukimbia tukajifunze. Siku ya funzo ilikuwa mojawapo ya jioni zenye kufurahisha zaidi ya zote katika juma.”
-
-
Unaweza Kumsaidiaje Mtoto “Mpotevu”?Mnara wa Mlinzi—2001 | Oktoba 1
-
-
6, 7. Wazazi wanaweza kuwasaidiaje watoto wao wasitawishe tamaa ya Neno la Mungu?
6 Ni muhimu kama nini wazazi wawasaidie watoto wao kusitawisha tamaa ya Neno la Mungu! Licha ya kuwa na funzo la familia la kawaida, msichana mmoja tineja alishirikiana na wahuni. Asema hivi kuhusu funzo lao la familia: “Baba alipouliza maswali, nilisoma tu majibu, bila hata kumwangalia uso.” Badala ya kupitia kijuujuu tu habari wakati wa funzo la familia, wazazi wenye hekima hutumia ustadi wa kufundisha. (2 Timotheo 4:2) Ili kijana afurahie funzo, ni lazima ahusishwe kwenye funzo hilo. Kwa nini usiulize maswali ya maoni na kumwacha ajieleze? Mtie moyo mtoto aeleze jinsi yeye binafsi anavyoweza kutumia habari inayozungumziwa.a
7 Isitoshe, fanya mazungumzo ya Kimaandiko yawe yenye kuchangamsha. Inapofaa, waambie watoto waigize matukio na drama za Biblia. Mnapozungumzia matukio fulani, wasaidie watoto wapige picha akilini ya nchi ambako mambo hayo yalitukia na mandhari yake pia. Huenda ikasaidia kutumia ramani na chati. Naam, kwa kuwa mbunifu, funzo la familia laweza kufanywa kwa njia mbalimbali zenye kuchangamsha. Wazazi pia wanapaswa kuchunguza uhusiano wao na Yehova. Wanapokuwa na uhusiano wa karibu na Yehova, wanaweza kuwasaidia watoto wao wafanye hivyo.—Kumbukumbu la Torati 6:5-7.
-