-
Je, Maisha Yana Maana Yoyote?Mnara wa Mlinzi—2011 | Julai 1
-
-
Je, Maisha Yana Maana Yoyote?
“JE, MAISHA yana maana yoyote?” Watu wengi wameuliza swali hilo. Jambo la kusikitisha ni kwamba hata wawe na maoni gani kuhusu maisha, wengi wao hawawezi kuepuka kile mtaalamu wa mfumo wa neva kutoka Australia, Viktor E. Frankl, anaeleza kuwa “hali ya kuhisi kwamba maisha hayana maana na ni ubatili.”
Kwa nini watu wengi wanahisi hivyo? Sababu moja ni kwamba mamilioni ya watu kotekote ulimwenguni wanaishi katika hali mbaya sana na zenye kusikitisha. Kila siku wanakabili umaskini, magonjwa, jeuri isiyo na sababu, na ukandamizaji. Kwa kweli, wanahisi kwamba maisha yao ‘yamejaa msukosuko,’ kama Ayubu wa kale alivyosema kuhusu mateso ya wanadamu. (Ayubu 14:1) Hangaiko lao kuu katika maisha ni kupata mahitaji yao ya siku baada ya siku.
Wakati huohuo, mamilioni ya wengine wanafurahia utajiri na usalama wa kadiri fulani. Inaonekana kwamba wana kila kitu kinachohitajika ili kuwa na furaha maishani. Lakini sivyo ilivyo kwa wengi. Kwa nini? Kwa sababu mara kwa mara, “taabu na mambo yenye kuumiza”—matatizo ya kifedha yasiyotazamiwa au misiba yenye kuumiza kama vile kifo cha mtoto—hukatiza matumaini na ndoto zao.—Zaburi 90:10.
Kuna jambo lingine linalofanya watu wahisi kwamba maisha “hayana maana na ni ubatili.” Ni jambo gani hilo? Ufupi wa maisha. Kwa wengi, ni jambo lisilopatana na akili kwamba wanadamu wanaishi maisha mafupi sana ingawa wana uwezo wa kutimiza mambo mengi makubwa. Hawawezi kuelewa ukweli ambao sote tunakabili: Hata kama tutaepuka misiba mikubwa inayowapata wanadamu, mwishowe tutakufa tu.—Mhubiri 3:19, 20.
Je, Maisha Yatakosa Maana Sikuzote?
Mfalme Sulemani wa Israeli la kale alieleza waziwazi jambo hilo. Alitazama jinsi watu katika siku zake walivyofanya kazi kwa bidii wakitumia vipawa na uwezo wao katika kupanda mashamba yao, kupalilia, kujenga, na kutunza familia zao, kama vile tu tunavyofanya leo. Hivyo, akauliza, ‘Watu wanapata faida gani?’ Alifikia mkataa wa kwamba kila kitu ambacho watu wanafanya ni “ubatili na kufuatilia upepo.”—Mhubiri 2:17.
Lakini, je, Mfalme Sulemani aliamini kwamba kila kitu ambacho wanadamu wanafanya kingekuwa “ubatili na kufuatilia upepo” sikuzote? Hapana. Alikuwa tu akieleza mambo halisi yanayotokea maishani katika ulimwengu huu. Hata hivyo, Neno la Mungu lililoongozwa na roho yake linatuhakikishia kwamba maisha hayataendelea kuwa jinsi yalivyo sasa!
Unaweza kupata uhakika huo jinsi gani? Tafadhali soma makala mbili zinazofuata. Zinaweza kukusaidia kuelewa kwa nini maisha yaonekana kuwa yasiyo na maana, jinsi hali hiyo itakavyorekebishwa, na unayoweza kufanya ili maisha yako yawe na maana hata sasa.
-
-
Kwa Nini Maisha Yanaonekana Kama Hayana Maana Yoyote?Mnara wa Mlinzi—2011 | Julai 1
-
-
Kwa Nini Maisha Yanaonekana Kama Hayana Maana Yoyote?
KWA nini uamini kwamba sikuzote maisha hayatakuwa tu “mafupi yasiyo na faida” ambayo “hupita kama kivuli,” kama Mfalme Sulemani anavyoeleza? (Mhubiri 6:12, Biblia Habari Njema) Biblia, Neno la Mungu lililoongozwa na roho yake, ambayo ni chanzo cha habari kinachotegemeka, inaahidi kuwa wakati ujao maisha yatakuwa na maana kwelikweli.—2 Timotheo 3:16, 17.
Biblia inatueleza Mungu alikuwa na kusudi gani mwanzoni alipoiumba dunia. Pia inaeleza kwa nini dunia imejaa ukosefu wa haki, ukandamizaji, na kuteseka. Kwa nini ni muhimu tuelewe mambo hayo? Kwa sababu jambo kuu linalowafanya watu wafikiri kuwa maisha hayana maana yoyote ni kwamba hawajui—au wanaamua kupuuza—kusudi la Mungu kuelekea dunia na wanadamu wanaoishi juu yake.
Mungu Ana Kusudi Gani Kuelekea Dunia?
Yehova Mungua aliiumba dunia ikiwa paradiso kamilifu—mahali ambapo wanaume na wanawake wangefurahia milele maisha kamili wakiwa wanadamu wakamilifu. Ukweli huo muhimu unapingana kabisa na wazo linalokubaliwa na wengi lakini lisilopatana na Maandiko kwamba Mungu aliiumba dunia iwe mahali ambapo angewajaribu wanadamu ili kuona kama wanastahili kuishi maisha yenye maana zaidi katika ulimwengu wa roho.—Ona sanduku “Je, Ni Lazima Tuondoke Duniani Ili Kufurahia Maisha Yenye Maana?” katika ukurasa wa 6.
Mungu alimuumba mwanamume na mwanamke kwa mfano wake, na kuwapa uwezo wa kuiga sifa zake nzuri. (Mwanzo 1:26, 27) Aliwaumba wakiwa wakamilifu. Walikuwa na kila kitu walichohitaji ili kufurahia maisha mazuri na yenye maana milele. Hilo lingetia ndani kuijaza dunia, kuitiisha, na kuibadilisha yote kuwa paradiso kama tu bustani ya Edeni.—Mwanzo 1:28-31; 2:8, 9.
Ni Nini Kilichotokea?
Bila shaka, kuna tatizo lililotokea. Wanadamu kwa ujumla hawaigi sifa nzuri za Mungu. Nayo dunia si paradiso. Basi, ni nini kilichotokea? Wazazi wetu wa kwanza, Adamu na Hawa, walitumia vibaya uhuru wao wa kuchagua. Walitaka kuwa “kama Mungu,” wakijiamulia “mema na mabaya.” Kwa kufanya hivyo waliiga uasi wa Shetani Ibilisi.—Mwanzo 3:1-6.
Hivyo basi, uovu si hali isiyoeleweka, iliyopangwa mapema na Mungu. Uovu ulianza wakati Shetani na baadaye Adamu na Hawa, walipoasi utawala wa Mungu. Matokeo ya uasi huo yalifanya wazazi wetu wa kwanza wapoteze Paradiso na ukamilifu, wakajiletea dhambi na kifo wao wenyewe, na pia wazao wao, yaani, wanadamu wote. (Mwanzo 3:17-19; Waroma 5:12) Uasi huo ndio uliosababisha hali zinazofanya maisha yaonekane kuwa bila maana yoyote.
Kwa Nini Mungu Hakuondoa Uovu Mara Moja?
Watu fulani hujiuliza, ‘Kwa nini Mungu hakuondoa uovu mara moja kwa kumharibu Shetani na waasi wengine kisha kuanzisha maisha upya?’ Je, hilo lingekuwa jambo la busara? Ungehisi jinsi gani ikiwa ungesikia kwamba kuna serikali fulani yenye nguvu ambayo humuua mara moja mtu yeyote anayeipinga? Bila shaka, jambo kama hilo lingewafanya watu walio na usawaziko wajitenge na serikali hiyo. Pia, haingekuwa ikiwawekea raia wake mfano unaofaa kuhusu viwango vya mema na mabaya.
Mungu aliamua kutowaondoa waasi hao mara moja. Kwa busara, aliruhusu wakati upite ili masuala ambayo yalizushwa katika Edeni kuhusu njia yake ya kutawala, yatatuliwe milele.
Uovu Wote Utaondolewa
Jambo muhimu la kukumbuka ni: Mungu ameruhusu uovu uendelee kwa muda fulani tu. Amefanya hivyo akijua kuwa ana uwezo wa kuondoa matokeo mabaya ya uovu huo. Atafanya hivyo wakati ambapo masuala yaliyozushwa na uasi dhidi ya utawala wake yatakapotatuliwa.
Kusudi la Mungu kuelekea dunia na wanadamu halijabadilika. Kupitia nabii Isaya, Yehova anatuhakikishia kuwa Yeye ndiye Mtengenezaji wa dunia, “ambaye hakuiumba tu bila sababu, ambaye aliiumba ili ikaliwe na watu.” (Isaya 45:18) Hivi karibuni, atairudisha dunia katika hali kamilifu aliyokusudia mwanzoni. Baada ya kuthibitisha kuwa njia yake ya kutawala ndiyo ya haki, atakuwa na sababu ya kutumia nguvu zake zisizo na kipimo kutimiza mapenzi yake na kuuondoa uovu wote. (Isaya 55:10, 11) Katika sala ya mfano, Yesu Kristo alimwomba Mungu achukue hatua hiyo. Yesu alitufundisha tusali hivi: “Mapenzi yako na yatendeke duniani kama ilivyo mbinguni.” (Mathayo 6:9, 10) Hayo yanatia ndani nini?
Mapenzi ya Mungu Kuelekea Dunia
Kati ya baraka nyingine nyingi, “wapole wataimiliki dunia.” (Zaburi 37:9-11, 29; Methali 2:21, 22) Yesu Kristo “atamkomboa maskini anayelilia msaada, pia mwenye kuteseka.” Atawakomboa kutoka katika “ukandamizaji na katika jeuri.” (Zaburi 72:12-14) Hakutakuwa na vita tena; wala kifo, machozi, maumivu, au kuteseka. (Zaburi 46:9; Ufunuo 21:1-4) Maelfu ya watu ambao wamekufa wakati huu ambapo Mungu ameruhusu uovu uwepo, watafufuliwa waishi hapa duniani, na watakuwa na nafasi ya kufaidika na baraka hizo na nyinginezo.—Yohana 5:28, 29.
Kwa kweli, Yehova ataondoa madhara yoyote ambayo yamesababishwa na uasi wa Shetani. Yehova atayaondoa kabisa hivi kwamba “taabu za zamani [mambo yote yanayosababisha majonzi na maumivu] kwa kweli zitasahauliwa.” (Isaya 65:16-19) Hatuna shaka yoyote kuhusu wakati huo ujao. Mungu hasemi uwongo. Ahadi zake zote zinatimia. Maisha hayatakuwa tena “ubatili na kufuatilia upepo.” (Mhubiri 2:17) Badala yake yatakuwa na maana tele.
Lakini namna gani wakati huu? Je, kujua yale ambayo Biblia inafundisha na kuelewa kusudi la Mungu kuelekea dunia kunaweza kufanya maisha yako yawe na maana zaidi? Makala ya mwisho katika mfululizo huu inazungumzia swali hilo.
[Maelezo ya Chini]
a Katika Biblia, jina la kibinafsi la Mungu ni Yehova.
[Sanduku katika ukurasa wa 6]
Je, Ni Lazima Tuondoke Duniani ili Kufurahia Maisha Yenye Maana?
Kwa miaka mingi, watu wasiojua kusudi la Mungu kuelekea dunia, wamefundisha kwamba ni lazima tuondoke duniani ili tuweze kufurahia maisha yenye maana.
Wengine wamesema kwamba nafsi, ambazo haziwezi kufa, “zilifurahia maisha bora kabla ya kuingia ndani ya miili ya wanadamu.” (New Dictionary of Theology) Nao wengine wamesema kwamba nafsi hizo “zimefungwa ndani ya mwili ili kuadhibiwa kwa dhambi zilizofanya zilipokuwa mbinguni.”—Cyclopedia of Biblical, Theological, and Ecclesiastical Literature.
Wanafalsafa Wagiriki, kama Sokratesi na Plato, walifundisha hivi: Wakati nafsi inapotoka kwenye mwili wa mwanadamu ndipo tu “inapoacha upumbavu, woga, kutangatanga, tamaa mbaya, na maovu mengine yanayompata mwanadamu,” kisha inaenda kuishi “pamoja na miungu milele.”—Plato’s Phaedo, 81, A.
Baadaye wale wanaoitwa viongozi wa Kikristo waliingiza katika mafundisho yao “wazo hilo la kutokufa kwa nafsi” lililofundishwa na wanafalsafa hao Wagiriki.—Christianity—A Global History.
Linganisha mambo hayo na mafundisho matatu ya msingi yaliyo katika Biblia:
1. Kusudi la Mungu kwa dunia ni kwamba iwe makao ya kudumu ya wanadamu, bali si mahali pa muda pa kuwajaribu wanadamu ili kuona kama wanastahili kuishi pamoja naye mbinguni. Kama Adamu na Hawa wangemtii Mungu, bado wangekuwa hai hapa duniani katika paradiso.—Mwanzo 1:27, 28; Zaburi 115:16.
2. Ingawa dini nyingi zinafundisha kwamba mwanadamu ana nafsi isiyoweza kufa, yaani, kitu fulani kinachokaa ndani yake, Biblia inafundisha jambo tofauti na rahisi kueleweka. Mwanadamu ni “nafsi hai” aliyeumbwa kutokana na “mavumbi ya nchi.” (Mwanzo 2:7) Biblia haisemi kamwe kwamba nafsi haiwezi kufa. Inasema kuwa nafsi inaweza kuuawa au kuharibiwa, na hivyo kufanya isiwepo kabisa. (Zaburi 146:4; Mhubiri 9:5, 10; Ezekieli 18:4, 20) Adamu, aliyekuwa nafsi ya kwanza, alikufa hakika na kurudi mavumbini ambako alitoka. Alirudia hali ya kutokuwapo.—Mwanzo 2:17; 3:19.
3. Wakati ujao wa mwanadamu hautegemei kuwa na nafsi isiyoweza kufa ambayo huondoka na kwenda katika makao fulani ya roho, badala yake inategemea ahadi ya Mungu ya kuwafufua watu waishi katika dunia paradiso.—Danieli 12:13; Yohana 11:24-26; Matendo 24:15.
-
-
Maisha Yenye Maana Sasa na MileleMnara wa Mlinzi—2011 | Julai 1
-
-
Maisha Yenye Maana Sasa na Milele
MAISHA yako yanaweza kuwa na maana hata sasa. Jinsi gani? Kwa kufuata kanuni zenye hekima zinazopatikana katika Neno la Mungu, Biblia. Acheni tuchunguze baadhi ya kanuni hizo.
KANUNI YA BIBLIA: “Hakuna jambo bora,” akaandika Mfalme Sulemani, kuliko kwamba mwanadamu “ale, naam, anywe na kuifanya nafsi yake ione mema kwa sababu ya kazi yake ngumu.”—MHUBIRI 2:24.
Tuliumbwa tukiwa na tamaa ya kuridhika na kazi inayofaa. Hata unapokabili hali ngumu, unaweza kuridhika kwa kiasi fulani sasa kwa kufanya kazi kwa bidii na kwa unyofu.
KANUNI YA BIBLIA: “Kuna furaha zaidi katika kutoa kuliko ilivyo katika kupokea.”—MATENDO 20:35.
Watu wengi wametambua kwamba kuwasaidia wengine, yaani, kutumia wakati na nguvu zao ili kuwasaidia walio katika hali ngumu, ni jambo linalothawabisha na kuongeza maana katika maisha yao. Mfalme Sulemani aliandika: “Usiwanyime watu mema wanayostahili, mkono wako ukiwa na uwezo wa kuyafanya.”—Methali 3:27.
Fikiria kisa cha Ralph. Baada ya kustaafu, alijiunga na mke wake katika utumishi wa Kikristo wa wakati wote. Wanajitolea kutumia saa kadhaa kila mwezi katika utumishi huo, ili kuwafundisha wengine Biblia. Ralph anasema, “Tunapofika nyumbani jioni, huwa tumechoka kwa sababu ya kutumia nguvu zetu zote katika kumtumikia Baba yetu wa mbinguni, bali si kwa sababu tu ya uzee. Inafurahisha kuchoka kwa ajili ya kazi njema!” Yeye na mke wake wana furaha kwa sababu wanatumia wakati wao mwingi kuwasaidia wengine.
KANUNI YA BIBLIA: “Rafiki wa kweli anapenda nyakati zote, naye ni ndugu aliyezaliwa kwa ajili ya wakati wa taabu.”—METHALI 17:17.
Inaweza kuwa rahisi kukabiliana na matatizo unapokuwa na marafiki. Mwanafalsafa Mwingereza Francis Bacon aliandika kwamba kwa wale wasiokuwa na marafiki wa kweli, “dunia ni kama nyika.” Kuwa na marafiki wa kweli na kuwa rafiki mzuri, ni mambo yanayoweza kukusaidia ukabiliane na hali ngumu na kufanya maisha yawe yenye kupendeza na kuridhisha.
KANUNI YA BIBLIA: “Wenye furaha ni wale wanaotambua uhitaji wao wa kiroho.”—MATHAYO 5:3.
Hivyo, Yesu alitaja jambo muhimu unalopaswa kufanya ili kufurahia kutimizwa kwa ahadi za Mungu. Jambo hilo ni kutambua na kutosheleza ‘uhitaji wako wa kiroho.’ Tofauti na wanyama, sisi tuna tamaa ya kiasili ya kujua maana na kusudi la uhai. Ni Yehova Mungu pekee anayeweza kututimizia uhitaji huo, na anafanya hivyo kupitia Neno lake, Biblia. Kama tulivyoona katika makala iliyotangulia, Biblia inafunua kusudi la Mungu kuelekea dunia. Inatueleza kwa nini tupo hapa, kwa nini watu wanateseka sana, na mambo ambayo Mungu anatazamia tufanye. Kuelewa kweli hizo za Kimaandiko ni muhimu ikiwa tunataka kuishi maisha yenye maana na yenye kuridhisha. Wale wanaotenga wakati wa kusoma Biblia na kufuata yale wanayojifunza, wanakuwa na furaha. Kwa nini? Kwa sababu kwa kufanya hivyo, wanajenga uhusiano mzuri na Muumba wetu, “Mungu mwenye furaha,” Yehova.—1 Timotheo 1:11.
KANUNI YA BIBLIA: “Mkumbuke, sasa, Muumba wako . . . kabla siku zenye msiba hazijaja na miaka iwe imekaribia utakaposema: ‘Sioni maana ya maisha.’”—MHUBIRI 12:1, THE NEW ENGLISH BIBLE.
Shauri la Mfalme Sulemani kwa vijana, ambao wakati wa ujana wao huenda wakakosa kutambua kwamba hatimaye maisha yanaweza kuwa yenye misiba, linatuhusu sote. Acha lengo lako maishani liwe kumtumikia Muumba wako. Hilo litafanya maisha yako yawe na kusudi halisi. Kataa kabisa mtazamo huu: “Tule na tunywe, kwa maana kesho tutakufa.” (1 Wakorintho 15:32) Ikiwa utamtanguliza Mungu kwanza mambo ‘yatakuendea vyema,’ linasema andiko la Mhubiri 8:12.
Msichana anayeitwa Wendi alithibitisha jambo hilo kuwa kweli. Alipokuwa kijana, yeye na dada yake walijifunza Kihispania ili waweze kuhamia Jamhuri ya Dominika, ambako kulikuwa na uhitaji mkubwa wa wahubiri wa habari njema za Biblia. “Tulijidhabihu sana ili kutumika katika eneo lenye uhitaji wa wahubiri, lakini tulifurahia sana. Hakuna jambo lingine bora kuliko hilo ambalo ningefanya katika hiyo miezi sita! Baraka tulizopata zilikuwa nyingi zaidi kuliko mambo tuliyodhabihu.”
Ushikamanifu kwa Mungu Hufanya Maisha Yawe na Maana
Kusitawisha uhusiano mzuri na Yehova kunaweza kufanya maisha yako yawe na maana zaidi kwa njia ya pekee sana. Jinsi gani? Shetani hakuwadanganya Adamu na Hawa waasi utawala wa Mungu tu, bali pia alidai kuwa hakuna mwanadamu anayeweza kuendelea kuwa mshikamanifu kwa Mungu anapojaribiwa. (Ayubu 1:9-11; 2:4) Unaweza kusaidia kuthibitisha kwamba Shetani ni mwongo! Jinsi gani? Kwa kuendelea kuwa mshikamanifu kwa Mungu, kwa kutii kanuni zake, na kwa kuonyesha kwamba unatambua kuwa Yehova ana haki kamili ya kutuamulia lililo jema na lililo baya.—Ufunuo 4:11.
Nyakati nyingine huenda tukalazimika kuvumilia hali ngumu ikiwa tunataka kufuata njia inayofaa maishani. Je, hali hizo zitafanya maisha yetu yakose maana? Hebu wazia kwamba adui mkatili anasema mambo ya uwongo kumhusu rafiki yetu au mtu wetu wa ukoo. Ikiwa kukabiliana na adui huyo ili kututetea jina la rafiki huyo kutatuingiza katika matatizo, je, jambo hilo lingefanya maisha yetu yakose maana? Bila shaka, hapana! Tungekuwa tayari kukabiliana na hali hiyo ili kutetea jina zuri la rafiki yetu. Kuwa mshikamanifu kwa Mungu kunaweza kumaanisha hivyo pia. Kwa kweli, tunapoendelea kuwa washikamanifu chini ya hali hizi ngumu tunaufurahisha moyo wa Mungu.—Methali 27:11.
Maisha Yenye Maana Milele
Fanya yote unayoweza ili kujifunza kumhusu Mungu na kusudi lake. Yesu Kristo mwenyewe alisema: “Uzima wa milele ndio huu, waendelee kupata ujuzi juu yako wewe, Mungu wa pekee wa kweli, na juu ya yule uliyemtuma, Yesu Kristo.” (Yohana 17:3) Mungu atakapotimiza kusudi lake la awali kuelekea dunia, wanadamu waaminifu watafurahia yale ambayo Yehova alikusudia wafurahie tangu mwanzo, yaani, “uzima wa milele” katika dunia paradiso. Kisha, maisha yatakuwa yenye maana na yenye kuridhisha kwelikweli.—Zaburi 145:16.
Unaweza kupata wapi ujuzi ambao Yesu alizungumzia? Katika Biblia, Neno la Mungu lililoongozwa na roho yake. Ikiwa ungependa kupata msaada wa kujifunza Biblia, usisite kuwaandikia wachapishaji wa gazeti hili. Watafurahi kufanya mpango ili mtu akutembelee na kukusaidia kujifunza yale ambayo Biblia inafundisha hasa.
-