Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • “Kujawa na Shangwe na Roho Takatifu”
    “Kutoa Ushahidi Kamili” Kuhusu Ufalme wa Mungu
    • SURA YA 11

      “Kujawa na Shangwe na Roho Takatifu”

      Paulo anatuwekea mfano mzuri wa kushughulika na watu wakali, wasiotaka kusikiliza

      Matendo 13:1-52

      1, 2. Safari ya Barnaba na Sauli ina tofauti gani na zile safari nyingine za umishonari, na safari hiyo itasaidiaje kutimiza andiko la Matendo 1:8?

      NI SIKU ya shangwe sana katika kutaniko la Antiokia. Kati ya manabii na walimu wote, Barnaba na Sauli ndio waliochaguliwa na roho takatifu kwenda kutangaza habari njema katika sehemu za mbali.a (Mdo. 13:1, 2) Ni kweli kwamba wanaume wanaostahili walitumwa wakati uliopita. Hata hivyo, wakati huo wamishonari hao walienda maeneo ambayo Ukristo ulikuwa umetia mizizi. (Mdo. 8:14; 11:22) Sasa, Barnaba na Sauli—pamoja na Yohana Marko, atakayewahudumia—wanatumwa nchi ambazo watu wengi hawajasikia kamwe habari njema.

      2 Miaka 14 hivi iliyopita, Yesu aliwaambia wafuasi wake: “Mtakuwa mashahidi wangu katika Yerusalemu, katika Yudea yote na Samaria, na mpaka sehemu ya mbali zaidi ya dunia.” (Mdo. 1:8) Kuwekwa rasmi kwa Barnaba na Sauli kuwa wamishonari kutachangia sana kutimizwa kwa unabii huo wa Yesu!b

      ‘Wawekeni kando kwa Ajili ya Kazi’ (Mdo. 13:1-12)

      3. Kwa nini haikuwa rahisi kusafiri katika karne ya kwanza?

      3 Kuna maendeleo mengi sana katika ulimwengu wa leo. Kwa muda wa saa moja au mbili, watu wanaweza kusafiri mbali sana kwa kutumia magari na ndege. Hali hii ni tofauti na ile ya karne ya kwanza W.K. Siku hizo, watu walitembea kwa miguu katika barabara mbaya. Kwa siku nzima mtu angeweza kusafiri kilomita 30 hivi, na safari hiyo ilikuwa yenye kuchosha sana.c Ingawa Barnaba na Sauli walitazamia kwa hamu kwenda kwenye mgawo wao, bila shaka walijua kwamba watalazimika kufanya jitihada nyingi na kujinyima mengi.​—Mt. 16:24.

      SAFARI KATIKA SIKU ZA MITUME

      Zamani, kusafiri kwa kutumia barabara kulichukua muda mrefu, kulichosha, na kugharimu pesa nyingi kuliko kusafiri kwa mashua. Hata hivyo, ili kufika sehemu nyingi, njia pekee ilikuwa kutembea kwa miguu.

      Msafiri angeweza kutembea kilomita 30 hivi kwa siku. Angekumbana na hali ngumu kama vile jua kali, mvua, baridi, au kushambuliwa na wezi. Mtume Paulo alisema kwamba aliposafiri, ‘mara nyingi alikabili hatari za kutokana na mito, hatari za kutokana na wezi.’​—2 Kor. 11:26.

      Milki ya Roma ilikuwa na barabara nyingi nzuri za mawe. Kando ya barabara kuu, kulikuwa na nyumba za wageni kila baada ya umbali wa safari ya siku moja hivi kwa miguu. Karibu nusu ya safari, kulikuwa na hoteli ambazo mtu angeweza kupata chakula au mahitaji mengine ya msingi. Waandishi wa enzi hizo walitaja kwamba hoteli na nyumba hizo za wageni zilikuwa chafu, zilijaa watu, viroboto na zilikuwa na joto sana. Hazikuheshimika na zilipendwa na watu wanaotenda mambo mabaya. Mara nyingi, wahudumu wa sehemu hizo waliwaibia wasafiri na walitoa huduma za ukahaba.

      Bila shaka Wakristo waliepuka sehemu hizo kadiri walivyoweza. Hata hivyo, waliposafiri kwenda sehemu ambazo hawakuwa na watu wa ukoo au marafiki, walilazimika kukaa humo.

      4. (a) Barnaba na Sauli walichaguliwaje, na waabudu wenzao waliitikiaje? (b) Tunawezaje kuwaunga mkono wale wanaopewa mapendeleo ya kitheokrasi?

      4 Lakini, kwa nini roho takatifu iliagiza moja kwa moja Barnaba na Sauli wawekwe kando ‘kwa ajili ya kazi’? (Mdo. 13:2) Biblia haisemi. Hata hivyo, tunajua kwamba roho takatifu ilielekeza wanaume hao wachaguliwe. Hatusomi popote kwamba manabii na walimu huko Antiokia walipinga uamuzi huo bali waliunga mkono kabisa uamuzi huo. Wazia jinsi Barnaba na Sauli walivyohisi wakati ndugu zao wa kiroho bila wivu wowote ‘walipofunga na kusali na kuweka mikono juu yao, na kuwaacha waende.’ (Mdo. 13:3) Sisi pia, tunapaswa kuwaunga mkono wale wanaopata mapendeleo ya kitheokrasi, kutia ndani wanaume wanaowekwa rasmi kuwa waangalizi katika kutaniko. Badala ya kuwaonea wivu, tunapaswa ‘kuwafikiria kwa njia inayozidi ile ya kawaida katika upendo kwa sababu ya kazi yao.’​—1 The. 5:13.

      5. Eleza jinsi kisiwa cha Kipro kilivyohubiriwa.

      5 Baada ya kutembea hadi Seleukia, bandari iliyokuwa karibu na Antiokia, Barnaba na Sauli walisafiri kwa mashua hadi kisiwa cha Kipro, umbali wa kilomita 200 hivi.d Kwa kuwa alikuwa mzaliwa wa Kipro, bila shaka Barnaba alikuwa na hamu kubwa ya kutangaza habari njema katika eneo la nyumbani kwao. Walipofika Salami, jiji lililokuwa kwenye ufuo wa mashariki wa kisiwa hicho, wanaume hao hawakupoteza wakati wowote. Mara moja, “wakaanza kulitangaza neno la Mungu katika masinagogi ya Wayahudi.”e (Mdo. 13:5) Barnaba na Sauli walisafiri kutoka upande mmoja hadi upande wa pili wa Kipro, wakihubiri katika majiji makubwa yaliyokuwa njiani. Ikitegemea barabara waliyopitia, huenda wamishonari hao walitembea kilomita 160 hivi!

      MASINAGOGI YA WAYAHUDI

      Neno “sinagogi” linamaanisha “kukusanya pamoja.” Mwanzoni, neno hilo lilimaanisha kusanyiko au kutaniko la Wayahudi na baadaye likapata maana mpya yaani mahali au jengo lililotumiwa kwa ajili ya kusanyiko hilo.

      Inaaminika kwamba masinagogi yalianza kutumiwa wakati wa ile miaka 70 Wayahudi walipokuwa uhamishoni Babiloni au muda mfupi baada ya kutoka huko. Masinagogi yalikuwa mahali pa kutoa elimu, kuabudu, kusoma na kufafanua Maandiko, na kuchochea watu kiroho. Katika karne ya kwanza W.K., kila mji katika maeneo ya Palestina ulikuwa na sinagogi. Majiji makubwa, kama Yerusalemu, yalikuwa na masinagogi kadhaa.

      Hata hivyo, si Wayahudi wote waliorudi Palestina baada ya uhamisho wa Babiloni. Wengi walihamia nchi nyingine ili kufanya biashara. Kufikia karne ya tano hivi K.W.K., Wayahudi walikuwa wakiishi katika wilaya zote 127 za Milki ya Uajemi. (Esta 1:1; 3:8) Baada ya muda, wakaanza kuishi katika majiji yaliyozunguka Bahari ya Mediterania. Wayahudi hao walioishi katika maeneo hayo wakaanza kujenga masinagogi.

      Katika masinagogi, Sheria ilisomwa na kufafanuliwa kila Sabato. Kulikuwa na jukwaa la kusomea lililozungukwa na viti katika pande tatu. Mwanamume yeyote Myahudi aliyekuwa mwamini angeweza kusoma, kuhubiri, au kuwahimiza wengine katika sinagogi.

      6, 7. (a) Sergio Paulo ni nani, na kwa nini Bar-Yesu alijaribu kumzuia asisikilize habari njema? (b) Sauli alishughulikiaje upinzani wa Bar-Yesu?

      6 Katika karne ya kwanza, ibada ya uwongo ilikuwa imeenea sana Kipro. Hilo lilionekana wazi Barnaba na Sauli walipofika Pafo, kwenye ufuo wa magharibi wa kisiwa hicho. Huko walikutana “na mwanamume Myahudi aliyeitwa Bar-Yesu, ambaye alikuwa mlozi na nabii wa uwongo, [naye] alikuwa pamoja na liwali Sergio Paulo, mwanamume mwenye akili.”f Katika karne ya kwanza, Waroma wengi wenye kuheshimika—hata ‘wanaume wenye akili,’ kama Sergio Paulo—waliwaendea walozi au wanajimu kutafuta msaada wa kufanya maamuzi mazito. Hata hivyo, Sergio Paulo alivutiwa sana na ujumbe wa Ufalme naye “alitamani kulisikia neno la Mungu.” Hilo halikumpendeza Bar-Yesu, ambaye jina lake la cheo lilikuwa Elima, yaani, “Mlozi.”​—Mdo. 13:6-8.

      7 Bar-Yesu aliupinga ujumbe wa Ufalme. Njia pekee ambayo angeweza kutumia ili kudumisha cheo chake kikubwa akiwa mshauri wa Sergio Paulo ilikuwa ni kwa “kumzuia yule liwali asiwe mwamini.” (Mdo. 13:8) Hata hivyo, Sauli hakumruhusu mlozi huyo amkengeushe Sergio Paulo. Alifanya nini? Masimulizi yanasema: “Sauli, aitwaye pia Paulo, akiwa amejaa roho takatifu, akamtazama kwa makini [Bar-Yesu] na kumwambia: “Ewe mtu uliyejaa kila aina ya upunjaji na kila aina ya ulaghai, wewe mwana wa Ibilisi, wewe adui wa kila jambo la uadilifu, je, hutaacha kuzipotosha njia za Yehova zilizo sawa? Tazama! mkono wa Yehova uko juu yako, nawe utakuwa kipofu, hutaona nuru ya jua kwa kipindi fulani.” Mara moja akaangukiwa na ukungu mzito na giza, naye akazunguka akitafuta mtu wa kumshika mkono ili amwongoze.”g Matokeo? “Yule liwali alipoona jambo lililotokea, akawa mwamini kwa sababu alistaajabishwa na fundisho la Yehova.”​—Mdo. 13:9-12.

      Ndugu ameshika Biblia iliyofunguliwa, akitetea kweli mbele ya hakimu mahakamani.

      Kama Paulo, tunaitetea kweli kwa ujasiri hata tukikabili upinzani

      8. Tunawezaje kuiga ujasiri wa Paulo?

      8 Paulo hakumwogopa Bar-Yesu. Vivyo hivyo, hatupaswi kuogopa wapinzani wanapojaribu kuvuruga imani ya wale wanaopendezwa na ujumbe wa Ufalme. Ni kweli kwamba maneno yetu yanapaswa kuwa “yenye neema sikuzote, yaliyokolezwa chumvi.” (Kol. 4:6) Hata hivyo, hatuwezi kuacha hali ya kiroho ya mtu anayependezwa iwe hatarini kwa sababu tu tunataka kuepuka ubishi. Wala hatupaswi kuogopa kufichua dini za uwongo kama za Bar-Yesu, ambazo zinaendelea ‘kupotosha njia za Yehova zilizo sawa.’ (Mdo. 13:10) Kama Paulo, na tuendelee kutangaza kweli kwa ujasiri na kuichochea mioyo ya watu wanyoofu. Ingawa huenda tusione waziwazi utegemezo wa Mungu, kama ilivyokuwa katika kisa cha Paulo, tuna uhakika kwamba Yehova atatumia roho yake takatifu kuwavuta watu wanaostahili kwenye ile kweli.​—Yoh. 6:44.

      ‘Neno la Kitia Moyo’ (Mdo. 13:13-43)

      9. Paulo na Barnaba waliweka mfano gani mzuri unaoweza kuigwa na wale wanaosimamia kutaniko leo?

      9 Inaonekana kulikuwa na badiliko fulani wanaume hao walipoondoka Pafo kuelekea Perga, pwani ya Asia Ndogo, umbali wa kilomita 250 hivi kupitia baharini. Katika Matendo 13:13 kikundi hicho, kinaitwa cha “Paulo na wenzake.” Inaonekana tangu wakati huo, Paulo ndiye aliyesimamia kikundi hicho. Hata hivyo, hakuna jambo lolote linaloonyesha kwamba Barnaba alianza kumwonea wivu Paulo. Badala yake, wanaume hao wawili waliendelea kumtumikia Mungu bega kwa bega. Paulo na Barnaba wanawawekea mfano mzuri wale wanaosimamia kutaniko leo. Badala ya kujitafutia makuu, Wakristo wanakumbuka maneno haya ya Yesu: “[Ninyi] nyote ni ndugu.” Pia alisema: “Yeyote anayejiinua atanyenyekezwa, na yeyote anayejinyenyekeza atainuliwa.”​—Mt. 23:8, 12.

      10. Eleza jinsi safari ya kutoka Perga kuelekea Antiokia ya Pisidia ilivyokuwa.

      10 Walipofika Perga, Yohana Marko aliwaacha Paulo na Barnaba, akarudi Yerusalemu. Haieleweki kwa nini aliondoka. Paulo na Barnaba waliendelea na safari kutoka Perga hadi Antiokia ya Pisidia, jiji lililokuwa katika wilaya ya Galatia. Safari hiyo haikuwa rahisi, kwa kuwa Antiokia ya Pisidia iko mita 1,100 juu ya usawa wa bahari. Mara nyingi njia za milimani zilikuwa na wanyang’anyi. Isitoshe, huenda Paulo alikuwa na matatizo ya afya pia.h

      11, 12. Alipotoa hotuba katika sinagogi huko Antiokia ya Pisidia, Paulo alitumia njia gani ili kuwavutia wasikilizaji wake?

      11 Wakiwa Antiokia ya Pisidia, Paulo na Barnaba waliingia katika sinagogi siku ya Sabato. Masimulizi hayo yanasema: “Baada ya kusoma hadharani Sheria na Manabii, maofisa wasimamizi wa sinagogi wakawatuma watu kwao, wakisema: ‘Wanaume, akina ndugu, ikiwa mna neno lolote la kuwatia moyo watu, lisemeni.’” (Mdo. 13:15) Basi Paulo akasimama na kuanza kuzungumza.

      12 Paulo alianza hotuba yake kwa kusema: “Wanaume, Waisraeli nanyi wengine mnaomwogopa Mungu.” (Mdo. 13:16) Watu hao waliomsikiliza Paulo walikuwa Wayahudi na wageuzwa imani. Paulo alitumia njia gani ili kuwavutia watu hao ambao hawakutambua jukumu la Yesu katika kusudi la Mungu? Paulo alianza kwa kusimulia historia ya Wayahudi. Alieleza jinsi Yehova ‘alivyowainua watu hao walipokuwa wakiishi wakiwa wageni katika nchi ya Misri’ na jinsi ambavyo baada ya kuachiliwa huru, Mungu ‘aliwavumilia huko nyikani’ kwa miaka 40. Pia, Paulo alisimulia jinsi Waisraeli walivyomiliki Nchi ya Ahadi na jinsi ambavyo Yehova ‘aliwapa nchi yao iwe urithi wao.’ (Mdo. 13:17-19) Inasemekana kwamba Paulo alikuwa akirejelea Maandiko fulani yaliyokuwa yamesomwa kwa sauti muda mfupi uliopita kulingana na desturi za Sabato. Ikiwa ndivyo, huo ni mfano mzuri unaoonyesha kwamba Paulo alijua jinsi ya kuwa “mambo yote kwa watu wa namna zote.”​—1 Kor. 9:22.

      13. Tunaweza kufanya nini ili kuwavutia watu tunaowahubiria?

      13 Sisi pia tunapaswa kujitahidi kuwavutia watu tunaowahubiria. Kwa mfano, kujua dini ya mtu kunaweza kutusaidia kuchagua habari zitakazompendeza. Pia, tunaweza kunukuu Maandiko ambayo huenda mtu huyo anajua. Huenda tukapata matokeo mazuri kwa kumwomba mtu huyo asome Biblia yake mwenyewe. Jitahidi kuchochea mioyo ya watu unaozungumza nao.

      14. (a) Paulo alianza kuzungumzia habari njema kuhusu Yesu jinsi gani, naye alitoa onyo gani? (b) Umati ulifanya nini baada ya kusikia maneno ya Paulo?

      14 Kisha, Paulo akazungumzia ukoo wa wafalme wa Israeli uliomtokeza “mwokozi, yaani, Yesu” ambaye alitayarishiwa njia na Yohana Mbatizaji. Halafu akaeleza jinsi Yesu alivyouawa na kufufuliwa. (Mdo. 13:20-37) “Acheni ijulikane kwenu,” Paulo akasema, “kwamba kupitia mtu huyo mnatangaziwa msamaha wa dhambi . . . kila mtu anayeamini anatangazwa kuwa bila hatia kupitia mtu huyu.” Naye akawaonya: “Jihadharini ili msipatwe na mambo haya yanayosemwa katika Manabii: ‘Tazameni, ninyi wenye dharau, na mshangae na kuangamia, kwa sababu ninafanya kazi fulani katika siku zenu, kazi ambayo hamtaiamini kamwe hata mtu yeyote akiwaeleza kirefu.’” Matokeo yalikuwa yenye kushangaza. Biblia inasema: “Watu wakawasihi wazungumzie mambo hayo Sabato iliyofuata.” Isitoshe, baada ya kusanyiko la sinagogi kumalizika, “Wayahudi wengi na wageuzwa imani waliomwabudu Mungu wakawafuata Paulo na Barnaba.”​—Mdo. 13:38-43.

      “Tunawageukia Mataifa” (Mdo. 13:44-52)

      15. Baada ya Paulo kutoa hotuba, ni nini kilichotokea Sabato iliyofuata?

      15 Sabato iliyofuata, “karibu jiji lote” lilikusanyika ili kumsikiliza Paulo. Hilo halikuwafurahisha Wayahudi fulani, nao wakaanza “kupinga wakikufuru mambo ambayo Paulo alikuwa akisema.” Paulo na Barnaba wakawaambia hivi kwa ujasiri: “Ilikuwa lazima neno la Mungu lihubiriwe kwenu kwanza. Kwa kuwa mnalikataa na kujiona hamstahili uzima wa milele, tazameni! tunawageukia mataifa. Kwa maana Yehova ametuamuru kwa maneno haya: ‘Nimewachagua muwe nuru ya mataifa, na muwe wokovu mpaka miisho ya dunia.’”​—Mdo. 13:44-47; Isa. 49:6.

      Paulo na Barnaba wakitupwa nje ya jiji la Antiokia ya Pisidia na wapinzani wenye hasira.

      “Wakaanza kuwatesa Paulo na Barnaba . . .  Nao wanafunzi wakaendelea kujawa na shangwe na roho takatifu.”—Matendo 13:50-52

      16. Wayahudi walifanya nini waliposikia maneno makali ya wamishonari hao, nao Paulo na Barnaba walifanya nini upinzani ulipotokea?

      16 Watu wa Mataifa waliokuwa wakisikiliza walishangilia, na “wote waliokuwa na mwelekeo unaofaa kwa ajili ya uzima wa milele wakawa waamini.” (Mdo. 13:48) Baada ya muda mfupi, neno la Yehova likaenea nchini kote. Hata hivyo, Wayahudi waliitikia kwa njia tofauti. Wamishonari hao waliwaambia kwamba ingawa walikuwa wa kwanza kutangaziwa Neno la Mungu, walimkataa Masihi na hivyo hawangeweza kuepuka hukumu kali ya Mungu. Wayahudi hao wakawachochea wanawake mashuhuri na wakuu wa jiji hilo, “nao wakaanza kuwatesa Paulo na Barnaba na kuwatupa nje ya mipaka yao.” Paulo na Barnaba walifanya nini? “Wakawakung’utia mavumbi yaliyokuwa kwenye miguu yao na kwenda Ikoniamu.” Je, huo ndio mwisho wa Ukristo katika Antiokia ya Pisidia? Hapana! Wanafunzi waliobaki “wakaendelea kujawa na shangwe na roho takatifu.”​—Mdo. 13:50-52.

      17-19. Tunawezaje kuiga mfano mzuri uliowekwa na Paulo na Barnaba, na ni kwa njia gani kufanya hivyo kutatuletea shangwe?

      17 Tunaweza kujifunza jambo muhimu kutokana na hatua ambayo wanaume hao walichukua upinzani ulipotokea. Hatuachi kamwe kuhubiri, hata wakati watu mashuhuri ulimwenguni wanapojaribu kutuzuia tusitangaze ujumbe wetu. Pia, kumbuka kwamba watu wa Antiokia walipoukataa ujumbe, Paulo na Barnaba ‘walikung’uta mavumbi kutoka miguuni mwao.’ Hawakufanya hivyo kwa sababu ya hasira, bali walitaka kuonyesha kwamba hawana lawama. Wamishonari hao walitambua kwamba hawangeweza kuwalazimisha watu wakubali ujumbe wao. Hata hivyo, watu hao hawangeweza kuwazuia kuhubiri. Paulo na Barnaba hawakupunguza bidii yao badala yake walienda Ikoniamu, na kuendelea kuhubiri!

      18 Namna gani wanafunzi waliobaki Antiokia? Ni kweli kwamba lilikuwa eneo gumu. Hata hivyo, shangwe yao haikutegemea matokeo waliyopata. Yesu alisema: “Wenye furaha ni wale wanaolisikia neno la Mungu na kulishika!” (Luka 11:28) Hivyo ndivyo wanafunzi waliobaki Antiokia ya Pisidia walivyofanya.

      19 Kama walivyofanya Paulo na Barnaba, na tukumbuke kwamba jukumu letu ni kuhubiri habari njema, iwe watu watasikiliza au la. Hata ikiwa watu tunaowahubiria hawapendezwi, tusisahau jinsi hali ilivyokuwa katika karne ya kwanza. Tukiithamini kweli tuliyo nayo, na kukubali kuongozwa na roho takatifu, sisi pia tunaweza kuwa na shangwe, hata tukikabili upinzani.​—Gal. 5:18, 22.

      BARNABA—“MWANA WA FARAJA”

      Yosefu, Mlawi, mzaliwa wa Kipro, alijulikana sana katika kutaniko la Yerusalemu. Mitume walimpatia jina lingine, lililopatana na utu wake. Walimwita Barnaba, yaani, “Mwana wa Faraja.” (Mdo. 4:36) Barnaba alipoona waamini wenzake wana uhitaji fulani, hakusita kuwasaidia.

      Barnaba akitoa mchango wa mifuko miwili ya sarafu.

      Siku ya Pentekoste, mwaka wa 33 W.K., wanafunzi wapya 3,000 walibatizwa. Inawezekana wengi kati yao walisafiri kwenda Yerusalemu kwa ajili ya sherehe hiyo na hawakupanga kukaa katika jiji hilo kwa muda mrefu. Kutaniko lilihitaji pesa na vitu vingine ili kuhudumia umati huo. Kwa hiyo, Barnaba akauza sehemu ya shamba na kuwaletea mitume mchango wa pesa.​—Mdo. 4:32-37.

      Barnaba alikuwa mwangalizi Mkristo mkomavu, na sikuzote alikuwa tayari kuwasaidia wengine. Wanafunzi wengine wote walipomwogopa Sauli wa Tarso aliyejulikana kuwa mtesaji, Barnaba alimsaidia. (Mdo. 9:26, 27) Barnaba alikubali kwa unyenyekevu Paulo alipompa shauri zito yeye na Petro kuhusu jinsi Wakristo Wayahudi na wa Mataifa wanavyopaswa kujiendesha. (Gal. 2:9, 11-14) Mifano hiyo michache inaonyesha kwamba kwa kweli Barnaba aliishi kulingana na jina lake, yaani “Mwana wa Faraja.”

      a Ona Sanduku lenye kichwa “Barnaba—‘Mwana wa Faraja.’”

      b Kufikia wakati huo, makutaniko yalikuwa yameenea sehemu za mbali sana kama vile Antiokia ya Siria—lililokuwa kilomita 550 hivi kaskazini mwa Yerusalemu.

      c Ona sanduku lenye kichwa “safari katika siku za mitume.”

      d Katika karne ya kwanza, meli zingeweza kusafiri kilomita 150 hivi kwa siku ikitegemea upepo. Safari hiyo ingechukua muda mrefu zaidi ikiwa hali ya hewa ni mbaya.

      e Ona Sanduku lenye kichwa “Masinagogi ya Wayahudi.”

      f Kisiwa cha Kipro kilikuwa chini ya utawala wa Roma. Mkuu wa kisiwa hicho alikuwa liwali.

      g Tangu wakati huo na kuendelea, Sauli alianza kuitwa Paulo. Watu fulani husema kwamba alijipa jina hilo la Kiroma kwa heshima ya Sergio Paulo. Hata hivyo, kwa kuwa aliendelea kuitwa Paulo hata alipoondoka Kipro, lazima kulikuwa na sababu nyingine, kwamba Paulo, “mtume wa mataifa,” aliamua kwamba tangu wakati huo na kuendelea atatumia jina lake la Kiroma. Huenda pia alitumia jina Paulo kwa sababu matamshi ya Kigiriki ya jina lake la Kiebrania, Sauli, yanafanana sana na neno la Kigiriki lenye maana mbaya.​—Rom. 11:13.

      h Miaka kadhaa baadaye Paulo aliwaandikia barua Wagalatia. Katika barua hiyo, Paulo alisema: “kwa sababu ya ugonjwa wa kimwili kwamba nilipata nafasi yangu ya kwanza ya kuwatangazia habari njema.”​—Gal. 4:13.

  • “Wakizungumza kwa Ujasiri kwa Mamlaka ya Yehova”
    “Kutoa Ushahidi Kamili” Kuhusu Ufalme wa Mungu
    • SURA YA 12

      “Wakizungumza kwa ujasiri kwa mamlaka ya Yehova”

      Paulo na Barnaba waonyesha unyenyekevu, uvumilivu, na ujasiri

      Matendo 14:1-28

      1, 2. Ni mambo gani yanayotokea, Paulo na Barnaba wakiwa Listra?

      KUNA vurugu jijini Listra. Mwanamume aliyezaliwa kilema anarukaruka kwa shangwe baada ya kuponywa na watu wawili asiowajua. Watu wanastaajabishwa na jambo hilo, na kuhani wa Zeu anawaletea mashada ya maua watu hao wawili ambao umati unaamini kuwa ni miungu. Ng’ombe-dume wanavuta pumzi kwa nguvu na kutoa mlio huku kuhani huyo akiwa tayari kuwachinja. Mara moja Paulo na Barnaba wanamkataza asifanye hivyo. Wanayararua mavazi yao, wanaruka ndani ya umati na kuwasihi sana wasiwaabudu.

      2 Kisha, Wayahudi wapinzani kutoka Antiokia ya Pisidia na Ikoniamu wakafika. Wakawachongea kwa chuki na kuwapotosha watu wa Listra. Umati huohuo, uliotaka kumwabudu Paulo, sasa ukamzunguka na kumpiga kwa mawe mpaka akapoteza fahamu. Baada ya hasira yao kupoa, wanamburuta Paulo, wanamtoa nje ya malango ya jiji, na kumwacha afe.

      3. Tutazungumzia maswali gani katika sura hii?

      3 Ni nini kilichosababisha vurugu hiyo? Wahubiri wa habari njema leo wanaweza kujifunza nini kutokana na matukio hayo? Wazee Wakristo wanawezaje kuiga mfano wa Barnaba na Paulo ambao walivumilia katika huduma yao, na ‘kuzungumza kwa ujasiri kwa mamlaka ya Yehova?’​—Mdo. 14:3.

      “Umati Mkubwa . . . Wakawa Waamini” (Mdo. 14:1-7)

      4, 5. Kwa nini Paulo na Barnaba walienda Ikoniamu, na ni nini kilichotokea huko?

      4 Siku chache zilizotangulia, Paulo na Barnaba walikuwa wametupwa nje ya jiji la Antiokia ya Pisidia baada ya Wayahudi wapinzani kuwachochea watu wawatese. Lakini, badala ya kuvunjika moyo, wanaume hao wawili “wakawakung’utia mavumbi yaliyokuwa kwenye miguu yao” wakaaji wa jiji hilo walioukataa ujumbe wao. (Mdo. 13:50-52; Mt. 10:14) Paulo na Barnaba wakaondoka kwa amani na kuacha mambo mikononi mwa Mungu. (Mdo. 18:5, 6; 20:26) Wamishonari hao wawili hawakupoteza shangwe yao, bali waliendelea na safari yao ya kuhubiri. Wakasafiri karibu kilomita 150 kuelekea upande wa kusini-mashariki na kufika nchi tambarare yenye rutuba iliyo katikati ya safu za milima ya Taurus na Sultan.

      5 Mwanzoni, Paulo na Barnaba waliamua kukaa Ikoniamu. Jiji hilo lenye utamaduni wa Kigiriki ni mojawapo ya majiji ya mkoa wa Galatia, katika milki ya Roma.a Jiji hilo lilikuwa na Wayahudi wengi mashuhuri na idadi kubwa ya wageuzwa imani wasio Wayahudi. Kulingana na desturi yao, Paulo na Barnaba waliingia ndani ya sinagogi na kuanza kuhubiri. (Mdo. 13:5, 14) “Wakazungumza vizuri hivi kwamba umati mkubwa wa Wayahudi na pia Wagiriki wakawa waamini.”​—Mdo. 14:1.

      IKONIAMU—JIJI LA WAFRIGIA

      Jiji la Ikoniamu lilikuwa kwenye eneo tambarare, lenye maji ya kutosha na rutuba. Jiji hilo lilikuwa kwenye makutano ya njia muhimu ya biashara iliyounganisha Siria na Roma, Ugiriki, na mkoa wa Asia wa Roma.

      Waikoniamu waliabudu Cybele, mungu wa uzazi wa Frigia, na ibada hiyo ilihusisha mambo fulani yaliyotokana na ibada ya Wagiriki wakati wa enzi za utawala wa Wagiriki. Jiji hilo lilichukuliwa na Roma mwaka wa 65 K.W.K., na katika karne ya kwanza W.K., likawa kituo chenye ufanisi cha biashara na kilimo. Ingawa Wayahudi mashuhuri waliishi Ikoniamu, inaonekana jiji hilo lilidumisha utamaduni wa Kigiriki. Masimulizi ya kitabu cha Matendo yanasema kwamba Wayahudi na “Wagiriki” waliishi huko.​—Mdo. 14:1.

      Jiji la Ikoniamu lilikuwa katikati ya Likaonia na Frigia, katika maeneo ya Galatia. Waandishi fulani wa zamani, kutia ndani Cicero na Strabo, walisema kwamba Ikoniamu lilikuwa jiji la Likaonia, na inaonekana kwamba jiji hilo lilikuwa katika eneo la Likaonia. Hata hivyo, kulingana na masimulizi ya kitabu cha Matendo jiji la Ikoniamu ni tofauti na Likaonia, ambapo “lugha ya Kilikaonia” ilizungumzwa. (Mdo. 14:1-6, 11) Kwa sababu hiyo, wachambuzi hudai kwamba kitabu cha Matendo si sahihi. Hata hivyo, mwaka wa 1910, wachimbuzi wa vitu vya kale walipata maandishi katika jiji hilo yanayoonyesha kwamba Kifrigia ndiyo lugha iliyozungumzwa Ikoniamu kwa karne mbili baada ya Paulo na Barnaba kutembelea jiji hilo. Hivyo, mwandikaji wa kitabu cha Matendo hakukosea kwa kutofautisha Ikoniamu na majiji ya Likaonia.

      6. Kwa nini Paulo na Barnaba walipata matokeo mazuri, nasi tunawezaje kuwaiga?

      6 Kwa nini Paulo na Barnaba walipata matokeo mazuri? Paulo aliyajua Maandiko vizuri. Aliyahusianisha kwa ustadi na historia, unabii, na Sheria ya Musa ili kuthibitisha kwamba Yesu ndiye Masihi aliyeahidiwa. (Mdo. 13:15-31; 26:22, 23) Barnaba aliwajali sana watu. (Mdo. 4:36, 37; 9:27; 11:23, 24) Wanaume hao hawakutegemea uelewaji wao wenyewe bali walizungumza “kwa mamlaka ya Yehova.” Unawezaje kuwaiga wamishonari hao unapohubiri? Kwa kufanya mambo yafuatayo: Lijue kabisa Neno la Mungu. Chagua Maandiko yatakayowavutia wasikilizaji wako. Tafuta njia za kuwafariji wale unaowahubiria. Na sikuzote mafundisho yako yategemee mamlaka ya Neno la Yehova, bali si hekima yako.

      7. (a) Habari njema huwa na matokeo gani? (b) Ikiwa familia yenu imegawanyika kwa sababu ya habari njema, unapaswa kukumbuka nini?

      7 Hata hivyo, si kila mtu jijini Ikoniamu aliyefurahi kusikia ujumbe wa Paulo na Barnaba. Luka anasema hivi: “Wayahudi ambao hawakuamini wakawachochea watu wa mataifa na kuwafanya wawachukie akina ndugu.” Paulo na Barnaba waliamua kukaa huko na kutetea habari njema, na “wakatumia muda mrefu wakizungumza kwa ujasiri.” Hata hivyo, “umati wa jiji ulikuwa umegawanyika; baadhi yao walikuwa upande wa Wayahudi lakini wengine upande wa mitume.” (Mdo. 14:2-4) Ndivyo ilivyo leo, ujumbe wa habari njema huleta umoja kwa watu fulani, lakini kwa wengine huleta mgawanyiko. (Mt. 10:34-36) Ikiwa familia yenu imegawanyika kwa sababu ya habari njema, kumbuka kwamba mara nyingi upinzani hutokea kwa sababu ya uchongezi au uvumi usio na msingi. Mwenendo wako unaweza kubadili mtazamo wa wale wanaokupinga.​—1 Pet. 2:12; 3:1, 2.

      8. Kwa nini Paulo na Barnaba waliondoka Ikoniamu, nasi tunaweza kujifunza nini?

      8 Baada ya muda, wapinzani huko Ikoniamu wakapanga njama ya kuwapiga mawe Paulo na Barnaba. Wamishonari hao wawili walipopata habari, waliamua kwenda kuhubiri katika eneo lingine. (Mdo. 14:5-7) Leo, wahubiri wa Ufalme hutumia busara. Tunaposhambuliwa kwa maneno, sisi huendelea kuhubiri kwa ujasiri. (Flp. 1:7; 1 Pet. 3:13-15) Lakini tukiona kwamba kuna uwezekano wa kutendewa kwa jeuri, tunaepuka kufanya jambo la kipumbavu linaloweza kuhatarisha uhai wetu au wa waabudu wenzetu.​—Met. 22:3.

      “Mgeuke . . . Mje kwa Mungu Aliye Hai” (Mdo. 14:8-19)

      9, 10. Jiji la Listra lilikuwa wapi, na ni mambo gani tunayojua kuhusu wenyeji wake?

      9 Paulo na Barnaba wakaelekea Listra, eneo la milki ya Roma lililokuwa kilomita 30 hivi kusini-magharibi mwa Ikoniamu. Jiji la Listra lilikuwa na uhusiano wa karibu sana na Antiokia ya Pisidia, lakini jiji hilo halikuwa na Wayahudi wengi maarufu. Ingawa wenyeji walizungumza Kigiriki, lugha yao ya asili ilikuwa Kilikaonia. Paulo na Barnaba walianza kuhubiri katika eneo la umma huenda kwa sababu jiji hilo halikuwa na sinagogi. Petro alimponya mtu aliyezaliwa kilema jijini Yerusalemu. Paulo pia alimponya mtu aliyezaliwa kilema jijini Listra. (Mdo. 14:8-10) Kwa sababu ya muujiza ambao Petro alifanya, umati mkubwa wa watu ukaamini. (Mdo. 3:1-10) Lakini muujiza ambao Paulo alifanya ulikuwa na matokeo tofauti kabisa.

      10 Kama tulivyoona mwanzoni mwa sura hii, yule mtu aliyekuwa kilema aliporuka na kuanza kutembea, mara moja umati wa wapagani huko Listra ukafikiri kwamba wao ni miungu. Walimwita Barnaba Zeu, mkuu wa miungu, naye Paulo wakamwita Herme, mwana wa Zeu na msemaji wa miungu. (Ona sanduku lenye kichwa “Jiji la Listra na Madhehebu ya Zeu na Herme.”) Hata hivyo, Barnaba na Paulo waliazimia kuusadikisha umati kwamba wanazungumza na kutenda kwa mamlaka ya Yehova, Mungu wa kweli, bali si kwa mamlaka ya miungu ya kipagani.​—Mdo. 14:11-14.

      JIJI LA LISTRA NA MADHEHEBU YA ZEU NA HERME

      Jiji la Listra lilikuwa katika bonde lililokuwa mbali na barabara kuu. Kaisari Augusto aliliteka jiji hilo na kulifanya kuwa sehemu ya milki ya Roma na kuliita Julia Felix Gemina Lustra. Kikosi cha jeshi cha jiji hilo kilitumiwa kulinda mkoa wa Galatia dhidi ya mashambulizi kutoka kwa makabila ya watu walioishi milimani. Jiji hilo lilitawaliwa kulingana na utaratibu wa Kiroma, na maofisa wa jiji hilo walikuwa na majina ya cheo ya Kilatini. Hata hivyo, jiji la Listra liliendelea kudumisha utamaduni wake wa Kilikaonia kuliko utamaduni wa Kiroma. Ndio sababu watu wa Listra wanaotajwa katika kitabu cha Matendo walizungumza Kilikaonia.

      Kati ya vitu vya kale vilivyopatikana karibu na jiji la Listra ni maandishi yanayowataja “makuhani wa Zeu” na sanamu ya mungu Herme. Hekalu la Zeu na Herme lilipatikana katika eneo hilo pia.

      Hadithi za kale zilizoandikwa na Ovid, mshairi Mroma (43 K.W.K. hadi 17 W.K.) zinatupatia habari zaidi kuhusu masimulizi ya kitabu cha Matendo. Kulingana na Ovid, Jupiter na Mercury, miungu wa Kiroma wanaoitwa Zeu na Herme katika Kigiriki, walitembelea Frigia wakiwa na umbo la wanadamu. Walienda katika nyumba elfu moja, lakini hakuna mtu hata mmoja aliyewakaribisha isipokuwa Philemon na Baucis, wenzi wa ndoa waliozeeka, ambao waliwakaribisha katika nyumba yao duni. Ili kuonyesha shukrani zao, Zeu na Herme walibadili nyumba hiyo na kuwa hekalu lililojengwa kwa marumaru na dhahabu, na kuwafanya Philemon na Baucis kuwa makuhani. Kisha wakaharibu nyumba za watu wote ambao hawakuwakaribisha. Kitabu kimoja kinasema hivi: “Iwapo watu wa Listra walikumbuka hadithi hiyo walipowaona Paulo na Barnaba wakimponya mtu aliyekuwa mlemavu, huenda ndio sababu walitaka kuwakaribisha na kuwatolea dhabihu.”​—The Book of Acts in Its Graeco-Roman Setting.

      Paulo na Barnaba wakikataa kusifiwa na umati jijini Listra. Watu hao wanacheza muziki, wanatayarisha dhabihu na kuinama mbele yao.

      “Mgeuke kutoka katika mambo haya ya bure mje kwa Mungu aliye hai, aliyeumba mbingu na dunia.”—Matendo 14:15

      11-13. (a) Paulo na Barnaba waliwaambia nini wenyeji wa Listra? (b) Tunaweza kujifunza nini kutokana na maneno ya Paulo na Barnaba?

      11 Licha ya mambo hayo yote, Paulo na Barnaba walijitahidi kufikia mioyo ya wasikilizaji wao kwa njia bora zaidi. Katika kisa hiki, Luka anaeleza njia yenye mafanikio iliyotumiwa kuwahubiria wapagani habari njema. Ona jinsi Paulo na Barnaba walivyowasihi wasikilizaji wao: “Wanaume, kwa nini mnafanya mambo haya? Sisi pia ni wanadamu tulio na udhaifu kama wenu. Nasi tunawatangazia habari njema, ili mgeuke kutoka katika mambo haya ya bure mje kwa Mungu aliye hai, aliyeumba mbingu na dunia na bahari na vitu vyote vilivyomo. Katika vizazi vilivyopita aliruhusu watu wa mataifa yote waendelee kutembea katika njia zao, ingawa hakujiacha bila ushahidi kwa kuwa alitenda mema, akiwapa ninyi mvua kutoka mbinguni na majira ya mavuno, akiwashibisha kwa chakula na kuijaza mioyo yenu furaha.”​—Mdo. 14:15-17.

      12 Tunaweza kujifunza nini kutokana na maneno hayo yenye kuchochea? Kwanza, Paulo na Barnaba hawakujiona kuwa bora kuliko wasikilizaji wao. Hawakujifanya kuwa watu wenye uwezo wa pekee. Badala yake, walikubali kwamba walikuwa na udhaifu uleule kama wa wapagani waliowasikiliza. Ni kweli kwamba Paulo na Barnaba walikuwa wamepokea roho takatifu na kuwekwa huru kutokana na utumwa wa mafundisho ya uwongo. Pia, walikuwa na tumaini la pekee la kutawala pamoja na Kristo. Hata hivyo, walijua kwamba watu wa Listra wangeweza kupata zawadi hizohizo ikiwa wangemtii Kristo.

      13 Tunawaonaje wale tunaowahubiria? Je, tunaona wako sawa na sisi? Tunapowasaidia wengine kujifunza kweli za Neno la Mungu, je, tunawaiga Paulo na Barnaba kwa kuepuka kujitafutia sifa? Charles Taze Russell, mwalimu stadi aliyeongoza kazi ya kuhubiri mwishoni mwa karne ya 19 na mwanzoni mwa karne ya 20, aliweka mfano mzuri. Aliandika: ‘Hatujitafutii sifa wala heshima kwa sababu ya habari tunazoandika; wala hatutaki kuitwa Viongozi au Marabi.’ Ndugu Russell alikuwa mnyenyekevu kama Paulo na Barnaba. Vivyo hivyo, tunapohubiri, kusudi letu ni kuwasaidia watu wamgeukie “Mungu aliye hai” si kujitafutia utukufu.

      14-16. Ni masomo gani mengine tunayojifunza kutokana na mambo ambayo Paulo na Barnaba waliwaambia watu wa Listra?

      14 Jambo la pili tunaloweza kujifunza kutokana na mazungumzo hayo ni; Paulo na Barnaba walibadilika kulingana na hali. Wayahudi na wageuzwa imani waliokuwa Ikoniamu walijua mengi kuhusu Maandiko au jinsi Mungu alivyoshughulika na taifa la Israeli, lakini watu wa Listra walijua mambo machache au hawakujua kabisa mambo hayo. Hata hivyo, wale waliowasikiliza Paulo na Barnaba walikuwa wakulima. Jiji la Listra lilikuwa na hali nzuri ya hewa na mashamba yenye rutuba. Watu hao wangeweza kuona uthibitisho wa kutosha wa sifa za Muumba kupitia mambo kama vile majira ya mavuno, na wamishonari hao walitumia jambo hilo kama msingi wa kuwahubiria.​—Rom. 1:19, 20.

      15 Je, sisi pia tunaweza kubadilika kulingana na hali? Ingawa mkulima anaweza kupanda mbegu ileile katika mashamba tofauti, anahitaji kutumia mbinu tofauti za kuutayarisha udongo. Huenda udongo fulani ukawa laini na tayari kwa ajili ya kupanda mbegu, lakini udongo mwingine ukahitaji matayarisho zaidi. Vivyo hivyo, tunapanda mbegu ileile, yaani, ujumbe wa Ufalme unaopatikana katika Neno la Mungu. Hata hivyo, kama Paulo na Barnaba, tutajitahidi kutambua hali na dini za watu tunaowahubiria. Jambo hilo litatusaidia kuwahubiria ujumbe wa Ufalme kulingana na hali zao.​—Luka 8:11, 15.

      16 Tunaweza kujifunza jambo la tatu kutokana na masimulizi kuhusu Paulo, Barnaba, na watu wa Listra. Licha ya jitihada zetu, wakati mwingine mbegu tunazopanda zinanyakuliwa au kuanguka kwenye miamba. (Mt. 13:18-21) Jambo hilo likitokea, usikate tamaa. Kama Paulo alivyowakumbusha wanafunzi huko Roma, “kila mmoja wetu [kutia ndani kila mtu tunayezungumza naye Neno la Mungu] atatoa hesabu kwa Mungu kwa ajili yake mwenyewe.”​—Rom. 14:12.

      “Wakawakabidhi kwa Yehova” (Mdo. 14:20-28)

      17. Baada ya kuondoka Derbe, Paulo na Barnaba walienda wapi, na kwa nini?

      17 Paulo alipoburutwa na kutolewa nje ya jiji la Listra akiwa mahututi, wanafunzi walimzunguka, akasimama, akaingia jijini na kukaa hapo usiku kucha. Siku iliyofuata, Paulo na Barnaba wakaanza safari ya kilomita 100 kwenda Derbe. Wazia maumivu makali ambayo Paulo alikuwa nayo wakati wa safari hiyo, kwani saa chache zilizopita alikuwa amepigwa mawe! Hata hivyo, yeye na Barnaba walivumilia, na walipofika Derbe, wakafanya “watu wengi kuwa wanafunzi.” Kisha, badala ya kwenda nyumbani kwao huko Antiokia ya Siria, “wakarudi Listra, Ikoniamu, na Antiokia [ya Pisidia].” Kwa nini? Ili kuwatia nguvu “wanafunzi na kuwatia moyo wabaki katika imani.” (Mdo. 14:20-22) Waliweka mfano mzuri sana! Walitanguliza mahitaji ya kutaniko badala ya starehe zao. Waangalizi wanaosafiri na wamishonari wa siku zetu wanaiga mfano wao.

      18. Wanaume wazee huwekwa rasmi jinsi gani?

      18 Zaidi ya kuwatia nguvu wanafunzi kwa maneno na mfano wao, Paulo na Barnaba waliwaweka rasmi “wazee kwa ajili yao katika kila kutaniko.” Ingawa Paulo na Barnaba ‘walitumwa na roho takatifu’ katika safari hiyo ya umishonari, walisali na kufunga, nao “wakawakabidhi [wazee hao] kwa Yehova.” (Mdo. 13:1-4; 14:23) Ndivyo ilivyo leo. Kabla ya mapendekezo, baraza la wazee husali na kuchanganua ili kutambua ikiwa ndugu anatimiza sifa za Kimaandiko. (1 Tim. 3:1-10, 12, 13; Tito 1:5-9; Yak. 3:17, 18; 1 Pet. 5:2, 3) Jambo kuu si muda ambao amekuwa Mkristo. Badala yake, maneno na mwenendo wake unapaswa kuonyesha wazi kwamba roho takatifu inafanya kazi katika maisha yake. Mtu anastahili kutumikia akiwa mwangalizi ikiwa anatimiza sifa zilizo katika Maandiko. (Gal. 5:22, 23) Mwangalizi wa mzunguko huwaweka rasmi wazee na watumishi wa huduma.​—Linganisha 1 Timotheo 5:22.

      19. Wazee wanawajibika kwa nani, na wanawaigaje Paulo na Barnaba?

      19 Wazee waliowekwa rasmi wanajua kwamba wanawajibika mbele za Mungu. (Ebr. 13:17) Kama walivyofanya Paulo na Barnaba, wazee wanaongoza katika kazi ya kuhubiri. Wanawatia nguvu Wakristo wenzao kwa maneno yao. Wanatanguliza faida za kutaniko badala ya starehe zao.​—Flp. 2:3, 4.

      20. Tunanufaikaje tunaposoma ripoti kuhusu kazi ya uaminifu ya ndugu zetu?

      20 Mwishowe Paulo na Barnaba waliporudi kwenye makao yao huko Antiokia ya Siria, walisimulia “mambo mengi ambayo Mungu alikuwa amefanya kupitia kwao, na kwamba alikuwa amewafungulia mataifa mlango wa kuingia kwenye imani.” (Mdo. 14:27) Tunaposoma kuhusu kazi ya uaminifu ya ndugu zetu Wakristo na jinsi ambavyo Yehova amebariki jitihada zao, tunatiwa moyo kuendelea ‘kuzungumza kwa ujasiri kwa mamlaka ya Yehova.’

      a Ona sanduku lenye kichwa “Ikoniamu—Jiji la Wafrigia.”

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki