-
Kitabu cha Biblia Namba 58—Waebrania“Kila Andiko, Lenye Pumzi ya Mungu, Lafaa”
-
-
13. (a) Ni jinsi gani Kristo alivyopata kuwa “kuhani milele,” mwenye daraka la kuleta wokovu wa milele? (b) Kwa nini Paulo awahimiza Waebrania wasonge mbele kwenye ukomavu?
13 Maoni ya ukomavu juu ya ubora wa ukuhani wa Kristo (4:14–7:28). Paulo awahimiza Waebrania washikilie kumwungama Yesu, Kuhani Mkuu aliye mkubwa ambaye amepita katika mbingu, ili waweze kupata rehema. Kristo hakujitukuza, bali Baba ndiye aliyesema hivi: “Ndiwe kuhani milele kwa mfano wa Melkizedeki.” (Ebr. 5:6; Zab. 110:4) Kwanza, Kristo alikamilishwa kwa ajili ya cheo cha kuhani mkuu kwa kujifunza utii kupitia kuteseka, ili awe na daraka la kuwaletea wokovu wa milele wale wanaomtii. Paulo ‘ana maneno mengi ya kunena ambayo ni shida kuyaeleza,’ lakini Waebrania wangali watoto wachanga wenye kuhitaji maziwa, hali, kwa uhakika, wapaswa kuwa walimu. “Chakula kigumu ni cha watu wazima, ambao akili zao, kwa kutumiwa, zimezoezwa kupambanua mema na mabaya.” Mtume awahimiza ‘wakaze mwendo ili waufikilie utimilifu.’—Ebr. 5:11, 14; 6:1.
14. Ni jinsi gani waamini waweza kuirithi ahadi, na tumaini lao limethibitishwaje?
14 Haiwezekani wale ambao wamelijua neno la Mungu na ambao wameanguka, wakatendeshwa tena waje kwenye toba “kwa sababu wao wamtundika Mwana wa Mungu upya kwa ajili yao wenyewe na kumfunua wazi kwenye aibu ya peupe.” Ni kupitia imani na saburi tu kwamba waamini waweza kuirithi ahadi iliyofanywa kwa Abrahamu—ahadi iliyohakikishwa na kuimarishwa na mambo mawili yasiyobadilika: neno la Mungu na kiapo chake. Tumaini lao, ambalo ni “nanga kwa ajili ya nafsi, ikiwa hakika na imara pia,” limethibitishwa na kuingia kwa Yesu “ndani ya pazia” akiwa Mtangulizi na Kuhani Mkuu kulingana na namna ya Melkizedeki.—6:6, 19, NW.
15. Ni nini huonyesha kwamba ukuhani wa Yesu, ulio kulingana na namna ya Melkizedeki, ungekuwa bora kuliko wa Lawi?
15 Melkizedeki huyu alikuwa “mfalme wa Salemu” na pia “kuhani wa Mungu aliye juu.” Hata Abrahamu kichwa cha familia alimlipa zaka (sehemu ya kumi), na kupitia yeye Lawi akafanya hivyo, akiwa bado katika viuno vya Abrahamu. Hivyo baraka ya Melkizedeki kwa Abrahamu ilinyooka ikamfikia Lawi asiyezaliwa, na hiyo ilionyesha kwamba ukuhani wa Kilawi ulikuwa hafifu kwa ule wa Melkizedeki. Zaidi ya hilo, ikiwa ukamilifu ulikuja kupitia ukuhani wa Kilawi wa Haruni, je! kungekuwa na uhitaji wa kuhani mwingine “kwa mfano wa Melkizedeki”? Zaidi ya hilo, kwa kuwa kuna badiliko la ukuhani, “hapana budi sheria nayo ibadilike.”—7:1, 11, 12.
16. Kwa nini ukuhani wa Yesu ni bora kuliko ukuhani chini ya Sheria?
16 Kwa uhakika, Sheria haikukamilisha chochote bali ilithibitika kuwa dhaifu na isiyo na matokeo. Makuhani wayo walikuwa wengi kwa sababu waliendelea kufa, lakini Yesu kwa “kuwa akaa milele, anao ukuhani wake usioondoka. Naye, kwa sababu hii, aweza kuwaokoa kabisa wao wamjiao Mungu kwa yeye; maana yu hai sikuzote ili awaombee.” Huyu Kuhani Mkuu, Yesu, ni “mtakatifu, asiyekuwa na uovu, asiyekuwa na waa lo lote, aliyetengwa na wakosaji,” hali makuhani wakuu waliowekwa na Sheria ni dhaifu, wakilazimika kwanza kutoa dhabihu kwa ajili ya dhambi zao wenyewe kabla hawajaweza kuombea wengine. Kwa hiyo neno la kiapo cha Mungu ‘limemweka Mwana, aliyekamilika hata milele.’—7:24-26, 28.
-
-
Kitabu cha Biblia Namba 58—Waebrania“Kila Andiko, Lenye Pumzi ya Mungu, Lafaa”
-
-
25. Paulo anaonyesha matumizi gani ya Maandiko ya Kiebrania yanayoelimisha?
25 Kuongezea hayo, kaitka barua ya Paulo kwa Waebrania, tunaona ushuhuda wenye kusisimua moyo kwamba unabii mbalimbali ulioandikwa zamani za kale katika Maandiko ya Kiebrania ulitimizwa baadaye katika njia ya ajabu. Wote huo ni kwa kutuagiza na kutufariji leo. Kwa kielelezo, katika Waebrania, mara tano Paulo anatumia maneno ya unabii wa Ufalme kwenye Zaburi 110:1 kwa Yesu Kristo akiwa Mbegu ya Ufalme, ambaye “ameketi mkono wa kuume wa kiti cha enzi cha Mungu” ili asubiri “adui zake wawekwe kuwa chini ya miguu yake.” (Ebr. 12:2; 10:12, 13; 1:3, 13; 8:1) Zaidi ya hilo, Paulo anukuu Zaburi 110:4 katika kueleza umaana wa cheo cha Mwana wa Mungu akiwa “kuhani milele kwa mfano wa Melkizedeki.” Kama vile Melkizedeki wa kale, ambaye katika maandishi ya Biblia “hana baba, hana mama, hana wazazi, hana mwanzo wa siku zake, wala mwisho wa uhai wake,” Yesu ni Mfalme na pia “adumu kuhani milele” ili kuleta mafaa za milele za dhabihu yake ya ukombozi kwa wote wanaojiweka chini ya utawala wake kwa utiifu. (Ebr. 5:6, 10; 6:20; 7:1-21) Ni kwa Mfalme-Kuhani uyo huyo ambaye Paulo arejezea katika kunukuu Zaburi 45:6, 7: “Mungu ni kiti cha enzi chako milele na milele, na fimbo ya ufalme wako ni fimbo ya unyoofu. Ulipenda uadilifu, na ulichukia uhalifu wa sheria. Ndiyo sababu Mungu, Mungu wako, amekupaka mafuta ya shangwe zaidi ya wenzi wako.” (Ebr. 1:8, 9, NW) Kwa kadiri Paulo anavyonukuu Maandiko ya Kiebrania na kuonyesha utimizo wayo katika Kristo Yesu, twaona sehemu-sehemu za vigezo vya kimungu vikiingia mahali pavyo na kutuelimisha.
-