Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Msifuni Kristo​—Mfalme Mtukufu!
    Mnara wa Mlinzi—2014 | Februari 15
    • MFALME APANDA “KWA KUTETEA KWELI”

      11. Kristo anapanda “kwa kutetea kweli” jinsi gani?

      11 Soma Zaburi 45:4. Mfalme huyo Shujaa hapigani vita vya ushindi ili kumiliki nchi mbalimbali na kuwatiisha watu. Anapigana vita vya uadilifu kwa makusudi yafaayo. Anapanda “kwa kutetea kweli na unyenyekevu na uadilifu.” Kweli muhimu zaidi ambayo ni lazima itetewe inahusu enzi kuu ya Yehova ya ulimwengu mzima. Shetani alipomwasi Yehova, alitilia shaka haki ya Yehova ya kutawala. Tangu wakati huo, kweli hiyo ya msingi imepingwa na roho waovu na wanadamu pia. Sasa, wakati umefika wa Mfalme aliyetiwa mafuta na Yehova kupanda ili kutetea kweli kuhusu enzi kuu ya Yehova kwa umilele wote.

      12. Mfalme anapandaje ‘kwa kutetea unyenyekevu’?

      12 Mfalme huyo anapanda pia ‘kwa kutetea unyenyekevu.’ Akiwa Mwana mzaliwa-pekee wa Mungu, ameweka mfano bora sana kwa kuwa mnyenyekevu na kujitiisha kwa ushikamanifu chini ya enzi kuu ya Baba yake. (Isa. 50:4, 5; Yoh. 5:19) Raia wote washikamanifu wa Mfalme huyo ni lazima waige mfano wake, na kujitiisha kwa unyenyekevu chini ya enzi kuu ya Yehova katika mambo yote. Ni wale tu wanaofanya hivyo watakaoruhusiwa kuishi katika ulimwengu mpya alioahidi Mungu.—Zek. 14:16, 17.

      13. Kristo anapandaje ‘kwa kutetea uadilifu’?

      13 Kristo pia anapanda ‘kwa kutetea uadilifu.’ Uadilifu anaotetea Mfalme huyo ni “uadilifu wa Mungu,” yaani, viwango vya Yehova vya mambo yanayofaa na yasiyofaa. (Rom. 3:21; Kum. 32:4) Isaya alitabiri hivi kumhusu Mfalme Yesu Kristo: “Mfalme atatawala kwa ajili ya uadilifu.” (Isa. 32:1) Utawala wa Yesu utaleta “mbingu mpya” na “dunia mpya” zilizoahidiwa, ambamo “uadilifu utakaa.” (2 Pet. 3:13) Kila mkaaji wa ulimwengu huo mpya atahitaji kutii viwango vya Yehova.—Isa. 11:1-5.

      MFALME ANATIMIZA “MAMBO YENYE KUOGOPESHA”

      14. Mkono wa kuume wa Kristo utatimizaje “mambo yenye kuogopesha”? (Tazama picha kwenye ukurasa wa 3.)

      14 Mfalme huyo anayepanda amejifunga upanga kwenye paja lake. (Zab. 45:3) Lakini, wakati utafika wa kuchukua upanga huo na kuushika kwa mkono wake wa kuume. Mtunga-zaburi alitabiri hivi: “Mkono wako wa kuume utakufundisha mambo yenye kuogopesha.” (Zab. 45:4) Yesu Kristo atakapopanda ili kutekeleza hukumu za Yehova katika Har–Magedoni, atatimiza “mambo yenye kuogopesha” dhidi ya adui zake. Hatujui atatumia njia gani kuuharibu mfumo wa Shetani. Lakini, hatua hiyo itawatia woga wakaaji wa dunia ambao hawajatii onyo la Mungu la kujitiisha chini ya utawala wa Mfalme huyo. (Soma Zaburi 2:11, 12.) Katika unabii wake kuhusu siku za mwisho, Yesu alisema kwamba watu ‘wangezimia kwa woga na tarajio la mambo yanayokuja juu ya dunia inayokaliwa; kwa maana nguvu za mbingu zitatikiswa.’ Kisha akasema hivi: “Na ndipo watakapomwona Mwana wa binadamu akija katika wingu akiwa na nguvu na utukufu mwingi.”—Luka 21:26, 27.

      15, 16. “Majeshi” yanayomfuata Kristo vitani yatatia ndani nani?

      15 Kitabu cha Ufunuo kinatangaza kuja kwa Mfalme “akiwa na nguvu na utukufu mwingi” kwa kusema hivi: “Nikaona mbingu imefunguliwa, na, tazama! farasi mweupe. Na yeye aliyeketi juu yake anaitwa Mwaminifu na wa Kweli, naye anahukumu na kufanya vita kwa uadilifu. Pia, majeshi yaliyokuwa mbinguni yalikuwa yakimfuata juu ya farasi weupe, nayo yalikuwa yamevikwa kitani bora cheupe, safi. Na upanga mrefu mkali unachomoza kutoka kinywani mwake, ili ayapige mataifa nao, naye atawachunga kwa fimbo ya chuma. Yeye anakanyaga pia shinikizo la divai ya hasira ya ghadhabu ya Mungu Mweza-Yote.”—Ufu. 19:11, 14, 15.

      16 “Majeshi” ya mbinguni yanayomfuata Kristo vitani yanatia ndani nani? Yesu aliandamana na “malaika zake” alipojifunga upanga kwa mara ya kwanza ili kumfukuza Shetani na roho wake waovu kutoka mbinguni. (Ufu. 12:7-9) Ni jambo linalopatana na akili kufikia mkataa wa kwamba katika vita vya Har–Magedoni, majeshi ya Kristo yatatia ndani malaika watakatifu. Ni nani wengine walio katika majeshi hayo? Yesu aliwaahidi hivi ndugu zake watiwa-mafuta: “Yeye atakayeshinda na kushika matendo yangu mpaka mwisho nitampa mamlaka juu ya mataifa, naye atawachunga watu kwa fimbo ya chuma hivi kwamba watavunjwa vipande-vipande kama vyombo vya udongo, kama vile nilivyopokea kutoka kwa Baba yangu.” (Ufu. 2:26, 27) Hivyo, majeshi ya Kristo ya mbinguni yatatia ndani pia ndugu zake watiwa-mafuta, na watakuwa wamepata thawabu yao mbinguni wakati huo. Watawala hao watiwa-mafuta watakuwa pamoja na Kristo atakapotimiza “mambo yenye kuogopesha” huku akiwachunga mataifa kwa fimbo ya chuma.

  • Msifuni Kristo​—Mfalme Mtukufu!
    Mnara wa Mlinzi—2014 | Februari 15
    • 19. Kristo ‘ataendelea mpaka afanikiwe’ na kukamilisha ushindi wake jinsi gani?

      19 Baada ya kuuharibu mfumo mwovu wa Shetani duniani, Kristo ‘ataendelea mpaka afanikiwe katika fahari yake.’ (Zab. 45:4) Atakamilisha ushindi wake kwa kumtupa Shetani na roho wake waovu ndani ya abiso kwa Miaka Elfu Moja. (Ufu. 20:2, 3) Ibilisi na malaika zake wakiwa katika hali ya kutotenda kama ya wafu, wakaaji wa dunia hawatakuwa tena chini ya uvutano wa kishetani nao watajitiisha kikamili chini ya Mfalme wao mshindi na mwenye utukufu. Hata hivyo, kabla ya kuona dunia nzima ikigeuzwa hatua kwa hatua kuwa paradiso, watakuwa na sababu nyingine ya kushangilia pamoja na Mfalme wao na watawala wenzake. Makala inayofuata itazungumzia tukio hilo lenye shangwe.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki