-
Zawadi Zilizofaa MfalmeMnara wa Mlinzi—2015 | Machi 1
-
-
Zawadi Zilizofaa Mfalme
“Wanajimu kutoka sehemu za Mashariki . . . wakafungua hazina zao na kumtolea zawadi—dhahabu na ubani na manemane.”—Mathayo 2:1, 11.
UNGEPENDA kumpa zawadi gani mtu aliye muhimu sana kwako? Katika nyakati za Biblia baadhi ya vikolezo vilikuwa na thamani kama dhahabu—thamani kubwa sana iliyomfaa mfalme.a Hii ndiyo sababu vikolezo vyenye harufu nzuri vilikuwa miongoni mwa zawadi ambazo wanajimu walileta kwa “mfalme wa wayahudi.”—Mathayo 2:1, 2, 11.
Mafuta ya zeri
Biblia inasema hivi pia kuhusu malkia wa Sheba alipofunga safari kumtembelea Mfalme Sulemani: “Ndipo akampa mfalme talanta 120 za dhahabu, na mafuta ya zeri kwa wingi sana, na mawe ya thamani; na kulikuwa hakujapata kuwa na mafuta ya zeri kama yale ambayo malkia wa Sheba alimpa Mfalme Sulemani.”b (2 Mambo ya Nyakati 9:9) Pia wafalme walimpelekea Sulemani mafuta ya zeri ili kumtakia mema.—2 Mambo ya Nyakati 9:23, 24.
Kwa nini vikolezo hivyo na vitu vilivyotengenezwa kwa vikolezo hivyo, vilikuwa vyenye thamani na gharama kubwa sana katika nyakati za Biblia? Kwa sababu vilitumiwa katika urembo, dini, na mazishi. (Tazama sanduku “Matumizi ya Vikolezo Vyenye Harufu Nzuri Katika Nyakati za Biblia.”) Mbali na kwamba vikolezo hivyo vilihitajiwa sana, viliuzwa bei ghali kwa sababu ya gharama za usafirishaji na upatikanaji.
KUVUKA JANGWA LA ARABIA
Kida
Katika nyakati za Biblia, baadhi ya mimea ya vikolezo ilisitawi kwenye Bonde la Yordani. Hata hivyo, vikolezo vingine vililetwa kutoka nchi nyingine. Biblia imetaja vikolezo vya aina mbalimbali. Vikolezo vinavyotajwa vinatia ndani waridi, udi, mafuta ya zeri, mdalasini, ubani, na manemane. Zaidi ya hayo, kulikuwa na vikolezo vingine vya chakula kama vile bizari, mnanaa, na dili.
Vikolezo hivyo vilitoka wapi? Udi, kida, na mdalasini vilipatikana katika nchi za leo za China, India, na Sri Lanka. Vikolezo kama vile ubani na manemane vilitokana na miti na mimea ambayo ilisitawi katika maeneo ya jangwa kuanzia Arabia kusini hadi Somalia iliyo Afrika. Nardo, kilikuwa kikolezo cha pekee kilichotoka India katika maeneo ya Himalaya.
Zafarani
Ili kufika Israeli, vikolezo vingi vilisafirishwa kupitia Arabia. Kwa sababu hiyo, katika milenia ya kwanza na ya pili K.W.K., Arabia ilikuja kuwa “msambazaji mkuu wa bidhaa hizo kati ya Mashariki na Magharibi,” kikasema kitabu The Book of Spices. Miji ya kale, ngome, na vituo vya safari vilivyo katika eneo la Negev kusini mwa Israel vinaonyesha njia walizotumia wafanyabiashara wa vikolezo hivyo. Shirika la World Heritage Centre la UNESCO liliripoti kwamba makazi hayo “yalichangia faida kubwa ya biashara hiyo . . . kutoka Arabia kusini hadi Mediterania.”
“Kiwango kidogo kiliuzwa kwa bei ghali, na kwa kuwa watu wengi walivipenda sana, vikolezo vilitumiwa kufanya biashara.” —The Book of Spices
Kwa kawaida msafara uliobeba vikolezo hivyo vyenye harufu nzuri ulisafiri umbali wa kilometa 1,800 hivi ukipitia Arabia. (Ayubu 6:19) Biblia inataja msafara wa wafanyabiashara Waishmaeli waliokuwa wamebeba “ubani mweusi na zeri na gome lenye utomvu” kutoka Gileadi hadi Misri.” (Mwanzo 37:25) Wana wa Yakobo walimuuza ndugu yao Yosefu awe mtumwa kwa wafanyabiashara hao.
-