Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Siri Takatifu Yakunjuka
    Mnara wa Mlinzi—1990 | Januari 15
    • Siri Takatifu Yakunjuka

      “Siri takatifu ya huu ujitoaji kimungu ni kubwa bila shaka.”​—1 TIMOTHEO 3:16, NW.

      1. Ni siri gani yenye kuelezwa kwenye 1 Timotheo 3:16?

      JE! MAFUMBO hukuvutia wewe? Je! wewe huona shangwe kuchunguza siri? Walio wengi kati yetu hufanya hivyo! Basi, jiunge nasi tuchunguzapo moja ya siri zilizo kubwa kupita zote​—siri iliyofungwa kufuli ndani ya Neno la Mungu kwa maelfu ya miaka. Siri takatifu hii huathiri sana maisha zetu, za wakati uliopo na wakati ujao. Hiyo ni ‘ile siri takatifu ya ujitoaji kimungu,’ ambayo twaelezwa kwenye 1 Timotheo 3:16, NW. Lo, jinsi twapasWa kuwa wenye shukrani kwa Yehova, “afunuaye siri,” kwa kutujulisha kwa neema siri hii tukufu mno na fasiri yayo!​—Danieli 2:28, 29.

      2. (a) Ni lini Yehova aliponena kwanza juu ya siri takatifu, na aliahidi nini wakati huo? (b) Ni maswali gani ambayo yataka kujibiwa?

      2 Yehova alinena kwanza juu ya siri takatifu baada ya Nyoka kuwa amemdanganya Hawa, na Adamu akawa amemfuata katika uasi. Ndipo Mungu akaahidi kwamba “mbegu,” au uzao, ungeponda kichwa cha Nyoka. (Mwanzo 3:15, NW) Ni nani Mbegu huyu? Angeshindaje Nyoka? Je! yeye angetetea ukweli wa Mungu na kusudi Lake kuelekea dunia hii?

      3. Unabii wa kimungu uliandaa vidokezi gani juu ya utambulisho na utendaji wa yule Mbegu?

      3 Kwa wakati wake, unabii wa kimungu ulifunua vidokezi kuhusu utambulisho na utendaji wa Mbegu huyo wakati ujao. Yeye angekuwa mzao wa Abrahamu, angerithi ufalme wa Daudi, na angeitwa Mwana-Mfalme wa Amani. ‘Kwa wingi wa utawala wake wa kimwana-mfalme na kwa amani kutakuwa hakuna mwisho.’ (Isaya 9:6, 7, NW; Mwanzo 22:15-18; Zaburi 89:35-37) Lakini kama vile Warumi 16:25 hutaarifu, siri takatifu hiyo ‘ilisitirika kwa zamani za milele.’

      Kutatua Lile Fumbo

      4. Siri takatifu ilianzaje kukunjuka katika 29 W.K.?

      4 Mwishowe, baada ya mileani nne, mnurisho ulitokea ghafula! Katika njia gani? Katika 29 W.K., Yohana alibatiza Yesu wa Nazareti katika Mto Yordani, na kutoka mbinguni sauti ya Mungu ikajulisha wazi hivi: “Huyu ni Mwanangu, mpendwa wangu, ninayependezwa naye.” (Mathayo 3:17) Ah, huyu hatimaye akawa ndiye yule Mbegu aliyeahidiwa! Ile siri takatifu ilikuwa imeanza kukunjuka katika nyuso zayo zote zilizo tukufu, kutia na lile jambo la ujitoaji kimungu.

      5. “Ujitoaji kimungu” ni nini, nao huathirije wale wanaouzoea?

      5 Sisi twaelewaje “ujitoaji kimungu”? Katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, usemi huu wapatikana mara 20 tu, zaidi ya nusu ya mara hizo katika barua mbili za Paulo kwa Timotheo. Kichapo Insight on the Scriptures hueleza maana ya “ujitoaji kimungu” kuwa “kicho, ibada, na utumishi kwa Mungu, pamoja na uaminifu-mshikamanifu kwa enzi kuu yake ya ulimwengu wote mzima.” Kicho hutoka ndani ya moyo wenye kukaribia Mungu, kwa hofu nyingi ya kustahi fahari yake, umilele wake, na wingi wa uumbaji wake mtukufu, pamoja na ushukuru kwa ajili ya zawadi za kiroho na kimwili ambazo humimina juu ya wanadamu wenye kuthamini. Kweli kweli, kila mmoja wetu ambaye huzoea ujitoaji kimungu aweza kusema, kama vile mtunga zaburi kwenye Zaburi 104:1: ‘Ee nafsi yangu, umhimidi Bwana [Yehova, NW]. Wewe, Bwana [Yehova, NW], Mungu wangu, umejifanya mkuu sana; umejivika heshima na adhama.”

      6. (a) Waabudu wa Yehova watofautianaje na wakaa-vitini wa Jumuiya ya Wakristo? (b) Paulo alisema nini kwenye Warumi 11:33, 34, na hivyo ni maswali gani yenye kutokezwa?

      6 Ujitoaji wetu kwa Mungu ni lazima ujionyeshe, nao hufanya hivyo kupitia vitendo. Kwa habari hii, waabudu wa Mungu wa kweli, Yehova, ni tofauti sana na wakaa-vitini wa makanisa yenye kufifia ya Jumuiya ya Wakristo. Kwa watu wengi duniani, dini​—ikiwa wangali wana dini​—ni kawaida tu, kisetiri ambacho huvaliwa kuwafanya waonekane watakatifu huku wakiishi maisha yenye upatano na ulimwengu mfisadi uwazungukao. Hata hawajui Mungu ni nani. Kwa uhakika, watu kama hao wahitaji kutii maneno ya Paulo kwenye Matendo 17:23, NW, aliposema hivi kwa Waathene walioheshimu mno ‘Mungu Asiyejulikana’: “Kile mnachotolea ujitoaji kimungu bila kujua, hicho ndicho mimi nawatangazia nyinyi.” Kuhusu Mungu huyo mkuu, Paulo apaaza sauti hivi kwenye Warumi 11:33, 34, NW: “O kina cha mali ya Mungu na hekima na maarifa! Jinsi hukumu zake hazichunguziki na zenye kupita uwezo wa kuchunguza ni njia zake! Kwa maana ‘ni nani amepata kujua akili ya Yehova, au ni nani amekuwa mshauri wake?’ “Basi, ni jinsi gani sisi huja kujua njia za Mungu? Ni kupitia kujifunza ile ‘siri takatifu ya ujitoaji kimungu.’ Lakini twafanyaje hivyo?

      7. Kwa nini yaweza kusemwa kwamba “siri takatifu ya huu ujitoaji kimungu ni kubwa bila shaka”?

      7 Kwenye 1 Timotheo sura ya 3, mtume Paulo atoa kwanza muhtasari wa mambo yatakwayo kwa watumishi katika nyumba ya Mungu, ambayo yaelezwa katika 1Ti 3 mstari wa 15, NW, kuwa “kundi la Mungu aliye hai, nguzo na tegemezo la ukweli.” Halafu Paulo aongeza hivi, katika 1Ti 3 mstari 16, NW: “Siri takatifu ya huu ujitoaji kimungu ni kubwa bila shaka.” Kubwa kweli kweli kwa sababu Yehova alituma Mwana wake mzaliwa pekee duniani ili afungue kufuli ya siri hii, kuonyesha ujitoaji kimungu ni nini kikweli na jinsi ulivyo wa maana sana, tegemeo la ibada ya kweli. Siri takatifu ya huu ujitoaji kimungu yadhihirishwa na mwendo wa maisha ya Yesu hapa duniani. Ni lazima wote wapendao Yehova wajenge imani yao na maisha zao juu ya Kristo, aliyetoa kielelezo cha ujitoaji kimungu. Basi, ni jinsi gani Yesu alionyesha wazi siri takatifu ya ujitoaji kimungu?

      Nyuso Sita

      8. (a) Ni nini zile nyuso sita za siri takatifu ambayo Paulo aeleza kwenye 1 Timotheo 3:16? (b) “Yeye” ambaye adhihirishwa ni nani?

      8 Kwa uvuvio wa kimungu, Paulo ajibu swali hilo. Kwenye 1 Timotheo 3:16, NW, yeye aeleza nyuso sita za siri takatifu hii, akisema hivi: “Yeye [1] alidhihirishwa katika mnofu, [2] alijulishwa wazi kuwa mwadilifu katika roho, [3] aliwatokea malaika, [4] alihubiriwa kote miongoni mwa mataifa, [5] aliaminiwa katika ulimwengu, [6] alipokewa juu katika utukufu.” Ni nani “Yeye” huyu mwenye kudhihirishwa? Kwa uwazi, “Yeye” ni yule Mbegu aliyeahidiwa, Yesu, aliyekuja kufanya mapenzi ya Mungu. Yeye ni kitovu cha siri takatifu, akiifanya iwe “kubwa” kweli kweli.

      9. Kuna uthibitisho gani kwamba 1 Timotheo 3:16 haipasi kusomwa hivi: ‘Mungu alidhihirika katika mnofu’?

      9 Wanautatu hujaribu kuchafua uelewevu wa siri takatifu hii kwa kusema kwamba “Yeye” kwenye 1 Timotheo 3:16, NW, ni Mungu mwenyewe. Wao hufanya msingi wa kusema hivyo uwe Biblia ya King James, ambayo husomwa kwamba, “Mungu alikuwa dhahiri katika mnofu.” Hata hivyo, hati za Kigiriki zenye kutegemeka zaidi husema nini? Kwa upatani, hizo hutumia kijina “Yeye” badala ya “Mungu.” Sasa wachambuzi wa maandishi wakubali kwamba kuingizwa kwa “Mungu” katika andiko hili ni kosa la waandishi. Hivyo, tafsiri za karibuni zaidi, kama vile American Standard Version, The New English Bible, na New World Translation, husomwa kwa usahihi hivi: ‘Yeye [au, Yeye ambayej alidhihirishwa katika mnofu.’ Si Mungu mwenyewe aliyetokea “katika mnofu,” hapana. Bali, ni Mwana wake mpendwa aliye kiumbe wa kwanza, ambaye kwa habari zake mtume Yohana aliandika hivi: “Naye Neno alifanyika mwili, akakaa kwetu; nasi tukauona utukufu wake, utukufu kama wa Mwana pekee atokaye kwa Baba; amejaa neema [fadhili zisizostahilika, NW] na kweli.”​—Yohana 1:14.

      ‘Kadhihirishwa Katika Mnofu’

      10. (a) Sehemu ya kwanza ya ile siri takatifu ilikujaje kuonekana wazi kwenye ubatizo wa Yesu? (b) Kwa nini Yesu akawa “Adamu wa mwisho”?

      10 Sehemu ya kwanza ya siri takatifu ilikuja kuwa wazi kwenye ubatizo wa Yesu: Yesu “alidhihirishwa katika mnofu” akiwa Mwana wa Mungu mpakwa-mafuta. Yehova Mungu alikuwa amehamisha uhai wa Mwana wake kutoka mbinguni akautia katika tumbo-uzazi la Mariamu ili Yesu aweze kuzaliwa katika mnofu akiwa binadamu mkamilifu. Hivyo, kama vile 1 Wakorintho 15:45-47 huonyesha, Yesu akawa Adamu wa pili, au “wa mwisho,” nafsi kamilifu ya kibinadamu yenye kulingana barabara na Adamu wa kwanza. Kwa kusudi gani? Timotheo wa Kwanza 2 5, 6 humtaja “Adamu wa mwisho” kuwa “Mwanadamu, Kristo Yesu; ambaye alijitoa mwenyewe kuwa ukombozi kwa ajili ya wote.” Kwa msingi huu wa kisheria wa dhabihu kamilifu ya kibinadamu, Yesu hupatanisha lile agano jipya kuelekea wanadamu 144,000 ambao huwa warithi washirika pamoja naye katika Ufalme wake.​—Ufunuo 14:1-3.

      11. Manufaa za dhabihu ya ukombozi ya Yesu zanyooka kufikia nani?

      11 Je! wengine pia wangenufaika na kifo cha Yesu cha dhabihu? Ndiyo bila shaka! Yohana wa Kwanza 2:2 hutaarifu kwamba Yesu Kristo “ni [dhabihu ya] kipatanisho kwa dhambi zetu [yaani, dhambi za Wakristo wapakwa-mafuta kama Yohana]; wala si kwa dhambi zetu tu, bali na kwa dhambi za ulimwengu wote.” Hivyo manufaa za ukombozi wa Yesu huenea kufika mbali kupita Wakristo wapakwa-mafuta 144,000 kufikia ulimwengu wote wa aina ya binadamu. “Umati mkubwa” ambao wako hai sasa na maelfu ya mamilioni watakaofufuliwa katika dunia Paradiso watapokea uhai wa milele kwa msingi wa imani yao katika dhabihu ya ukombozi ya Yesu. Tayari, kama ilivyosemwa kwa unabii kwenye Ufunuo 7:9, 10, umati mkubwa umeosha majoho yao na kuyafanya meupe kwa kujizoeza imani katika damu iliyomwagwa ya Mwana-Kondoo, Yesu Kristo. Wao wahesabiwa kuwa waadilifu kwa habari ya urafiki pamoja na Mungu. Kwa shangwe, wao wajifunza zile nyuso mbalimbali za siri takatifu na kuonyesha ujitoaji kimungu kupatana na kielelezo cha Yesu!

      Nyuso Nyingine

      12. Ni jinsi gani Yesu “alijulishwa wazi kuwa mwadilifu katika roho”?

      12 Sasa, namna gani sehemu ya pili iliyo kwenye 1 Timotheo 3:16, NW? Yesu “alijulishwa wazi kuwa mwadilifu katika roho.” Lakini jinsi gani? Ni kwa Yehova kuinua Mwanaye mshika-uaminifu-maadili kutoka kwa wafu akawe na uhai wa roho. Hiyo ilikuwa sawa na Yehova kujulisha wazi kwamba Yesu alikuwa mwadilifu kabisa na mwenye kustahiki migawo zaidi iliyotukuka. Kama vile Warumi 1:4 yaeleza jambo hilo, Yesu ‘alijulishwa wazi kuwa Mwana wa Mungu kulingana na roho ya utakatifu kwa njia ya ufufuo kutoka kwa wafu.” Akithibitisha hilo, Petro atuambia hivi katika barua yake ya kwanza, sura ya 3, mstari wa 18, NW: “Kristo alikufa mara moja kwa wakati wote kwa habari ya dhambi, mtu mwadilifu kwa ajili ya wasio waadilifu, kwamba awaongoze nyinyi kwa Mungu, akiuawa katika mnofu, bali akafanywa kuwa hai katika roho.” Je! kielelezo cha Yesu cha ujitoaji kimungu kinakuongoza wewe kwa Mungu?

      13. Yesu aliyefufuliwa aliwatokea malaika gani, na ni ujumbe wa aina gani ambao aliwahubiria?

      13 Akiendelea na 1 Timotheo 3:16, NW, ndipo Paulo arejezea sehemu ya tatu ya siri takatifu, akisema kwamba Yesu “aliwatokea malaika.” Malaika hao wangeweza kuwa nani? Kuhusu Yesu, sasa ‘akiwa amefanywa kuwa hai katika roho,’ Petro aandika hivi kwenye 1 Petro 3:19, 20, NW: “Katika hali hii pia alikwenda zake na kuwahubiri roho walio gerezani, ambao hapo kwanza walikuwa wasiotii wakati saburi ya Mungu ilipokuwa ikingojea katika siku za Noa.” Kulingana na Yuda 6, roho hao walikuwa “malaika wasioilinda enzi yao wenyewe, lakini wakayaacha makao yao yaliyowahusu” katika mbingu. Walivaa miili ya kimnofu ili wapate shangwe ya ngono isiyo halali pamoja na wanawake. Gharika ilipolazimisha malaika hao kurudi katika makao ya kiroho, walitupwa katika Tartaro, hali ya kushushwa kabisa. (2 Petro 2:4) Yesu aliyefufuliwa aliwahubiri. Lakini je! huo ulikuwa ujumbe wa wokovu? Sivyo kabisa! Bali, Yesu alishutumu uovu wao kuwa kinyume kabisa cha ujitoaji kimungu. Wowote wa watu wa Mungu ambao huchezea ukosefu wa adili kingono leo wapaswa wapate onyo kutokana na hukumu iliyotangazwa juu ya malaika hao!

      14. Ilikuwaje hata habari njema zikaanza ‘kuhubiriwa miongoni mwa mataifa’?

      14 Sehemu ya nne ya 1 Timotheo 3:16 ni kwamba Yesu “alihubiriwa miongoni mwa mataifa.” Hilo limetimizwaje? Kabla tu ya kukamatwa kwake, Yesu aliwaambia mitume hivi: “Amin, Amin, nawaambieni, Yeye aniaminiye mimi, kazi nizifanyazo mimi, yeye naye atazifanya; naam, na kubwa kuliko hizo atafanya, kwa kuwa mimi naenda kwa Baba.” (Yohana 14:12) Muda mfupi baada ya hapo, kwenye Pentekoste 33 W.K., Yesu alimimina roho takatifu juu ya wanafunzi wake, na zile habari zenye kugutusha za kwamba “Yesu huyo Mungu alimfufua” zikaanza kuhubiriwa kwa Wayahudi. Baadaye, Wasamaria pia walikubali neno la Mungu na wakaanza kupokea roho takatifu. (Matendo 2:32; 8:14-17) Kisha, katika 36 W.K., Petro akahubiria Kornelio na wengine waliokusanyika katika nyumba yake. Hivyo, habari njema zikaanza ‘kuhubiriwa miongoni mwa mataifa,’ yaani, miongoni mwa wasio Wayahudi, ambao pia walipakwa mafuta kwa roho takatifu.

      15. Ni nini chenye kuthibitisha kwamba Wakristo wa kame ya kwanza walikuwa wamejifunza vizuri ile siri takatifu ya ujitoaji kimungu?

      15 Kama ilivyoripotiwa kwenye Matendo 12:24, “neno la Bwana [Yehova, NW] likazidi na kuenea.” Matendo 17:6 yasimulia kwamba kaskazini mwa Ugiriki wapinzani walipaaza sauti, kama vile wafanyavyo huko hata leo hii: “Watu hawa walioupindua ulimwengu wamefika huku nako.” Katika muda wa miaka 30 tangu hapo, Paulo angeweza kuandika akiwa Roma kwamba habari njema zilikuwa ‘zimehubiriwa katika uumbaji wote ulio chini ya mbingu.’ (Wakolosai 1:23, NW) Wakristo wa wakati huo walikuwa wamejifunza vizuri ile siri takatifu ya ujitoaji kimungu. Lo, waliitumia kwa bidii iliyoje! Sisi pia na tujifunze siri hiyo na kuitumia katika siku hii ya upeo wa kuhubiri Ufalme!

      16. Sehemu ya tano ya ile siri takatifu ilikuwa nini, na ni utendaji gani uliofanya ionekane wazi?

      16 Kwa kuitikia kuhubiri huko kwa karne ya kwanza, sehemu ya tano ya siri takatifu ya 1 Timotheo 3:16 ikaonekana wazi sana. Yesu sasa “aliaminiwa ulimwenguni.” Hiyo ilitokea kwa sababu ya ujitoaji kimungu ulio kama wa Kristo wa wamisionari wenye bidii, kutia na Paulo na Timotheo. Walipeleka habari njema ndani ya Esia Ndogo na Ulaya, labda hata mbali kufikia Hispania, na ndani ya Afrika Mashariki kwa kinywa cha Mwethiopia aliyebatizwa, huku Petro akitumikia katika Babuloni.

      17. Kwa nini Yesu aaminiwa kotekote katika ulimwengu wa ki-siku-hizi?

      17 Namna gani siku yetu? Tangu 1919 mabaki wapakwa-mafuta wamekuwa wakionyesha ujitoaji kimungu ulio kielelezo chema. Wapakwa-mafuta hao wamejenga imara juu ya msingi wa imani uliowekwa na Yesu. Hasa tangu 1935 wamechukua hatua zaidi ya kukusanya umati mkubwa, ambao washangilia tazamio la kupita “dhiki kubwa” na kuona shangwe ya uhai wa milele katika dunia paradiso. (Ufunuo 7:9, 14) Hivyo, zile habari njema zenye kuelekeza fikira kwa Yesu zaaminiwa kotekote katika ulimwengu wa ki-siku-hizi. Sasa Mashahidi wa Yehova zaidi ya 3,700,000 wanahubiri na kusitawi kuzunguka tufe lote wakiwa katika ujitoaji kimungu!

      18. Ni jinsi gani Yesu ‘alipokewa juu katika utukufu’?

      18 Uso mmoja zaidi wa siri takatifu hiyo wabakia, ule wa sita: Yesu “alipokewa juu katika utukufu.” Wakati wa zile siku 40 baada ya kuhuishwa katika roho, Yesu alijivika-vika miili ya kimnofu, akiwatokea wanafunzi wake na kuwaambia “mambo yaliyouhusu ufalme wa Mungu.” Halafu akapaa mbinguni. (Matendo 1:3, 6-9) Hivyo sala yake, iliyoandikwa kwenye Yohana 17:1-5, ilijibiwa: “Baba, . . . mtukuze Mwanao, ili Mwana wako naye akutukuze wewe . . . Mimi nimekutukuza duniani . . . Na sasa, Baba, unitukuze mimi pamoja nawe, kwa utukufu ule niliokuwa nao pamoja nawe kabla ya ulimwengu kuwako.”

      19. Ni lazima iwe ilitokeaje Yesu aliporudi mbinguni?

      19 Ni lazima iwe kulikuwa na ushangilio mkubwa sana Yesu aliporudi mbinguni! Mapema zaidi, wakati Yehova alipoweka misingi ya dunia, ‘wana wote wa Mungu walipiga kelele kwa furaha.’ (Ayubu 38:7) Ni lazima vikosi hivyo vya malaika viwe vilijawa na shangwe nyingi mno kumpokea tena miongoni mwao Bingwa huyo mwenye kutetea enzi kuu ya Yehova kwa uaminifu-mshikamanifu!

      20. Kwa nini Yesu amerithi jina tukufu jinsi hiyo, naye alifanya nini alipokuwa angali duniani?

      20 Kwenye Waebrania 1:3, 4, Paulo asema hivi juu ya Yesu mwenye ushindi: “Akiisha kufanya utakaso wa dhambi, aliketi mkono wa kuume wa Ukuu huko juu; amefanyika bora kupita malaika, kwa kadiri jina alilolirithi lilivyo tukufu kuliko lao.” Kristo alipokea iina hilo kwa sababu ya kushinda kwake ukosefu wa uadilifu. Mwana huyu wa Mungu alikuwa ameanzisha kweli kweli kijia cha ujitoaji kimungu hapa duniani. Pia alikuwa ameweka kigezo kwa wengine wote watakaofikia uhai wa milele. Yesu akiwa ametukuzwa kwenye mkono wa kuume wa Mungu katika mbingu, siri takatifu ya huu ujitoaji kimungu ilifunuliwa katika sehemu zayo zote.

  • Kujifunza Siri Takatifu ya Ujitoaji Kimungu
    Mnara wa Mlinzi—1990 | Januari 15
    • Kujifunza Siri Takatifu ya Ujitoaji Kimungu

      “Hata Kristo aliteseka kwa ajili ya nyinyi, akiachia nyinyi kiolezo ili mfuate kwa ukaribu hatua zake.”​—1 PETRO 2:21, NW.

      1. Kusudi la Yehova limekuwa nini kuhusu ‘siri takatifu ya ujitoaji kimungu’?

      “SIRI takatifu ya huu ujitoaji kimungu” si siri tena! (1 Timotheo 3:16, NW) Hiyo ni tofauti kama nini na siri za dini bandia, kama Utatu wa kifumbo, ambazo hubaki zikiwa siri! Hakuna mtu awezaye kuzielewa. Badala ya kuwa hivyo, Yehova amekusudia kwamba siri takatifu iliyofunuliwa katika mtu Yesu Kristo itangazwe kwa mapana kwa kadiri iwezekanavyo. Yesu mwenyewe akawa ndiye kielelezo chenye kutokeza cha mpiga mbiu mwenye bidii wa Ufalme wa Mungu. Sisi twaweza kujifunza mengi kutoka ujumbe wake na njia ya kuhubiri, kama tutakavyoona sasa.

      2. Kwa nini kuhudumu kwa Yesu kwawekwa mbele ya ukombozi? (Mathayo 20:28)

      2 Basi, acheni tumfikirie Yesu zaidi akiwa ‘amedhihirishwa katika mnofu.’ (1 Timotheo 3:16, NW) Kwenye Mathayo 20:28, NW, twasoma kwamba Yesu ‘alikuja, si kuhudumiwa, bali kuhudumu na kutoa nafsi yake iwe ukombozi badala ya wengi.’ Hii hata yaweka kuhudumu kwake mbele ya ukombozi. Kwa nini iwe hivyo? Basi, nyuma katika Edeni yule Nyoka mwenye hila alikuwa ametokeza ubishi juu ya uhalali wa enzi kuu ya Yehova juu ya aina ya binadamu, akidokeza kwamba uumbaji wa Mungu ulikuwa wenye waa na kwamba hakuna mwanadamu ambaye akiwa chini ya mtihani angeweza kushika uaminifu wa kimaadili kwa Aliye Juu Zaidi. (Linganisha Ayubu 1:6-12; 2:1-10.) Huduma ya Yesu isiyo na waa akiwa mwanadamu mkamilifu, “Adamu wa mwisho,” ilimwonyesha Shetani mfanya-madai kuwa mwongo mwovu. (1 Wakorintho 15:45) Zaidi ya hilo, Yesu alithibitisha kikamili sifa zake za kutumikia akiwa “Wakili Mkuu [wa Mungu] na Mwokozi,” na za ‘kuihukumu kwa uadilifu dunia yote yenye kukaliwa’ ili kutetea enzi kuu ya Yehova.​—Matendo 5:31; 17:31, NW.

      3. Ni jinsi gani Yesu alikanusha kabisa dai la Shetani?

      3 Yesu alikanusha kabisa dai la Shetani lenye dhihaka kali! Katika historia yote, hakuna mwanadamu juu ya dunia hii aliyetumikia Mungu kwa ujitoaji hivyo​—kujapokuwa na mizaha, mapigo ya mijeledi, na mateso ya kimwili na ya kiakili. Kristo alilazimika kuvumilia masuto yenye kukufuru kuwa kwake Mwana wa Mungu. Kwa kupita katika yote hayo​—hata mpaka kifo chenye maumivu makali sana na aibu​—yeye alikuwa imara, asiyeondoleka katika uaminifu-mshikamanifu kwa Baba yake. Kwenye Wafilipi 2:8, 9, NW, Paulo aandika kwamba kwa sababu Yesu alitii ‘mpaka kifo, ndiyo, kifo juu ya mti wa mateso, Mungu alimkweza na kumpa jina lililo juu ya kila jina jingine.’ Yesu alimfichua Shetani akaonekana wazi kama alivyo hasa, mwongo mwenye sumu ya nyoka!

      4. Kwa nini Yesu angeweza kuambia Pilato kwamba yeye alikuwa ameingia ndani ya ulimwengu kutoa ushahidi kwa ule ukweli?

      4 Hivyo, kwenye umalizio wa miaka michache tu ya kuhubiri kwa bidii nyingi, Yesu angeweza kushuhudia kijasiri hivi kwa Pontio Pilato: “Wewe mwenyewe unasema kwamba mimi ni mfalme. Kwa ajili ya hili mimi nimezaliwa, na kwa ajili ya hili mimi nimekuja ndani ya ulimwengu, ili kwamba nipaswe kutoa ushahidi kwa ule ukweli. Kila mmoja aliye upande wa ukweli husikiliza sauti yangu.” (Yohana 18:37, NW) Yesu alikuwa ameonyesha ujitoaji kimungu ulio bora kabisa katika kupiga mbiu ya ukweli wa Ufalme wa Mungu kotekote katika Palestina. Alizoeza wanafunzi wake wawe wahubiri wenye bidii pia. Lo, kielelezo chake hutuchochea kama nini tufuate hatua zake leo!

      Kujifunza Kutokana na Kielelezo Wetu 6 kwa njia ya ujitoaji kimungu tulio nao

      5. Twaweza kujifunza nini kuhusu ujitoaji kimungu kwa kumtazama Yesu tukiwa tumemkazia macho?

      5 Kwa njia ya ujitoaji kimungu tulio nao katika kufanya mapenzi ya Yehova, sisi pia twaweza kuthibitisha Ibilisi kuwa mwongo. Hata tupatwe na majaribu gani, hakuna yoyote ya hayo yatapata kamwe kuwa sawa na maumivu makali na matendo ya kuvunjiwa heshima yaliyompata Yesu. Basi, acheni sisi tujifunze kutokana na Kielelezo wetu. Kama vile Waebrania 12:1, 2, NW, yatuhimiza, sisi na tupige mbio kwa uvumilivu “huku tukimtazama kwa kumkazia macho Wakili Mkuu na Mkamilishaji wa imani yetu, Yesu.” Tofauti na Adamu, aliyeshindwa alipotahiniwa kuhusu ujitoaji kimungu, Yesu alipata kuwa ndiye mwanadamu mmoja duniani aliyekabili mitihani yote kikamilifu. Moja kwa moja hadi kifo, yeye alithibitika kuwa “mwaminifu-mshikamanifu, asiye na ujanja, asiyechafuliwa, aliyetengwa na wenye dhambi.” (Waebrania 7:26, NW) Akiwa na uaminifu wa maadili yasiyo na waa, yeye angeweza kusema hivi kwa adui zake: “Ni nani miongoni mwenu anishuhudiaye ya kuwa nina dhambi?” Yesu alivurumisha dai la Shetani likamrudia yeye mwenyewe, akijulisha wazi hivi: “Mtawala wa ulimwengu . . . hana uwezo juu yangu.” Na katika kumalizia hotuba yake ya mwisho kwa wanafunzi wake kabla ya kusalitiwa na kukamatwa, aliwaambia hivi: “Jipeni moyo; mimi nimeushinda ulimwengu.”​—Yohana 8:46; 14:30; 16:33, NW.

      6. (a) Kwa nini Yesu ajua aina ya burudisho ambalo lahitajiwa na aina ya binadamu? (b) Yesu alionyesha hofu ya Mungu kwa kadiri gani?

      6 Alipokuwa katika mnofu hapa duniani, Yesu alijionea mwenyewe vile mambo huwa mtu akiwa mwanadamu, “mdogo punde kuliko malaika.” (Waebrania 2:7) Alipata kujulia unyonge mbalimbali wa kibinadamu na kwa hiyo ana matayarisho ya kutosha ili atumikie akiwa Mfalme na Hakimu wa aina ya binadamu kwa miaka elfu moja. Huyu Mwana wa Mungu, aliyesema, “Njoni kwangu, nyinyi nyote mnaomenyeka na kulemewa na mizigo, nami nitawaburudisha nyinyi,” ajua ni burudisho la aina gani ambalo lahitajiwa na aina ya binadamu. (Mathayo 11:28, NW) Waebrania 5:7-9 yatuambia hivi: “Siku hizo za mwili wake, alimtolea yule, awezaye kumwokoa na kumtoa katika mauti, maombi na dua pamoja na kulia sana na machozi, akasikilizwa kwa jinsi alivyokuwa mcha Mungu; na, ingawa ni Mwana, alijifunza kutii kwa mateso hayo yaliyompata; naye alipokwisha kukamilishwa [katika utii], akawa sababu ya wokovu wa milele kwa watu wote wanaomtii.” Yesu hakuyumba-yumba, hata ingawa alilazimika kuvumilia kufikia hatua ya kupata umo kali la kifo cha kibinadamu katika kupokea ‘jeraha la kisigino’ kutoka kwa yule Nyoka mwenye chuki. (Mwanzo 3:15) Kama Yesu, sisi na tuonyeshe hofu ya kimungu sikuzote, hata kufikia kifo ikiwa yahitajiwa iwe hivyo, huku tukiwa na uhakika kwamba Yehova Mungu atasikia dua zetu na kutupa wokovu.

      “Kuishi Kwenye Uadilifu”

      7. Kulingana na 1 Petro 2:21-24, Kristo alituachia kiolezo gani, na mwendo wake wapasa kutuathiri jinsi gani?

      7 Alipokuwa angali dhahiri katika mnofu, kwa uaminifu mshikamanifu Yesu alifungua ile shela yenye kuifunika siri takatifu ya ujitoaji kimungu. Twasoma hivi kwenye 1 Petro 2:21-24, NW: “Hata Kristo aliteseka kwa ajili ya nyinyi, akiachia nyinyi kiolezo ili mfuate kwa ukaribu hatua zake. Yeye hakufanya dhambi, wala udanganyifu haukupatikana katika kinywa chake. Alipokuwa akitukanwa, yeye hakurudisha kutukana. Alipokuwa akiteswa, yeye hakutisha, bali aliendelea kujikabidhi mwenyewe kwa yeye anayehukumu kwa uadilifu. Yeye mwenyewe alichukua dhambi zetu katika mwili wake mwenyewe juu ya mti, ili tupate kuondolewa dhambi na kuishi kwenye uadilifu.” Sisi tuwapo tukitafakari mwendo wa Yesu, lo, huo watutia moyo kama nini tufuate ujitoaji kimungu, tushike uaminifu wa maadili, na tuishi kwenye uadilifu kama alivyofanya!

      8. Sisi twaweza kuishije kwenye uadilifu kama Yesu?

      8 Yesu aliishi kikweli kwenye uadilifu. Zaburi 45:7, NW, ilitoa unabii hivi juu yake: “Umependa uadilifu na ukachukia uovu.” Akitumia maneno hayo kwa Yesu, mtume Paulo alisema hivi kwenye Waebrania 1:9, NW: “Ulipenda uadilifu, na ulichukia kutotii sheria.” Kulingana na nuru ya uelewevu wetu kuhusu ile siri takatifu ya huu ujitoaji kimungu, sikuzote sisi na tupende uadilifu na kuchukia ubaya kama Yesu. Katika maadili ya Kikristo, ambayo leo yashambuliwa vikali sana na ulimwengu wa Shetani, na katika mishughuliko yetu yote pamoja na wale walio ndani na nje ya tengenezo la Mungu, acheni sisi tuazimie kuishi kwenye uadilifu, tukitegemeza kanuni za haki za Yehova. Na acheni tuendelee kula karamu ya Neno la Mungu ili tuwe na muono-ndani ambao wahitajiwa sana ili kukinza Ibilisi na njama zake!

      9. Ni nini kilichoongezea bidii ya Yesu katika huduma, na jambo hilo lilihusisha nini kwa habari ya wachungaji wa dini bandia?

      9 Jambo fulani zaidi lilimsukuma Yesu awe mwenye bidii katika huduma yake. Jambo gani? Kwenye Mathayo 9:36 twasoma hivi: “Alipowaona makutano, aliwahurumia, kwa sababu walikuwa wamechoka na kutawanyika kama kondoo wasio na mchungaji.” Kwa hiyo Yesu “akaanza kuwafundisha mambo mengi.” (Marko 6:34) Kwa lazima, hiyo ilihusu kufunua uovu na kutotii sheria kwa wachungaji bandia wa kidini. Kulingana na Mathayo 15:7-9, Yesu alisema hivi kwa baadhi ya hawa: “Enyi wanafiki, ni vema alivyotabiri Isaya kwa habari zenu, akisema, Watu hawa huniheshimu kwa midomo; ila mioyo yao iko mbali nami. Nao waniabudu bure, wakifundisha mafundisho yaliyo maagizo ya wanadamu.”

      Fumbo Lenye Kuleta Masikitiko Makubwa

      10. Leo, “fumbo la huku kutotii sheria” lakaza fikira juu ya nani, nao wana hatia ya nini?

      10 Kama vile Yesu alivyonena dhidi ya viongozi wa dini bandia, ndivyo sisi leo twaona masikitiko makubwa kuhusu fumbo moja ambalo latofautiana sana na ile siri takatifu ya ujitoaji kimungu. Kwenye 2 Wathesalonike 2:7, NW, Paulo aliliita “fumbo la huku kutotii sheria.” Lilikuwa fumbo katika karne ya kwanza W.K. kwa sababu halingefunuliwa shela yenye kulifunika mpaka muda mwingi upite baada ya kifo cha mitume. Leo, fumbo hilo lakaza fikira juu ya makasisi wa Jumuiya ya Wakristo, ambao hupendezwa zaidi na siasa kuliko kujulisha wazi habari njema za Ufalme wa Mungu wenye uadilifu. Unafiki ni tele miongoni mwao. Waevanjeli wa mafarakano ya Kiprotestanti ya Jumuiya ya Wakristo ambao huhubiri katika televisheni ni kielelezo cha wazi sana kuhusu jambo hilo: walaghai wenye kunyoa mali za makundi yao ya kondoo, kujenga makao makubwa mno ya mamilioni ya dola, kushirikiana na malaya, kulia machozi bandia kama mamba wakati wafichuliwapo, na kuendelea kuomba-omba pesa, saa zote pesa zaidi. Vatikani ya Roma Katoliki ina hali kama hiyo ya kuchukiza sana, ikijihusisha katika mambo ya siasa bila kusumbuliwa na dhamiri, ikiwa na majionyesho ya nje-nje, na mazoea ya ufisadi katika shughuli za benki.

      11. Ni jambo gani litapata makasisi wa Jumuiya ya Wakristo na sehemu yote ya Babuloni Mkubwa?

      11 Si ajabu kwamba jamii ya makasisi wa Jumuiya ya Wakristo yaweza kutambulishwa kuwa “mtu wa kuasi [sheria]”! (2 Wathesalonike 2:3) Sehemu hii ambayo ndiyo kubwa zaidi ya Babuloni Mkubwa itafichuliwa wazi kwa ukamili na kuteketezwa, pamoja na dini nyingine yote ya dini bandia. Kama vile tusomavyo kwenye Ufunuo 18:9-17, wanasiasa na wanabiashara (na wanabenki wao) wataomboleza hivi wakati huo: “Ole, ole, mji ule ulio mkuu!” Babuloni Mkubwa na mafumbo yake yatakuwa yamefunuliwa wazi yakawa utupu, kwa kutofautiana kabisa na mambo yote yenye kuimulikia nuru ile siri takatifu ya ujitoaji kimungu.

      12. Upendo wa Yesu kwa uadilifu ulimwongoza kufanya nini?

      12 Kupenda kwa Yesu uadilifu na kuchukia kutotii sheria kulimwongoza afanye jitihada ya kujikaza kabisa kwa ajili ya ibada ya kweli. Katika ziara yake ya kwanza ya kwenda Yerusalemu akiwa Mwana mpakwa-mafuta wa Mungu, alifukuza wafanya biashara na wabadili fedha watoke ndani ya hekalu, akijulisha wazi hivi: “Yaondoeni haya; msiifanye nyumba ya Baba yangu kuwa nyumba ya biashara!” (Yohana 2:13-17) Katika ziara ya baadaye kwenye hekalu, Yesu aliwaambia hivi Wayahudi wenye kupinga: “Ninyi ni wa baba yenu, Ibilisi, na tamaa za baba yenu ndizo mpendazo kuzitenda. Yeye alikuwa mwuaji tangu mwanzo; wala hakusimama katika kweli, kwa kuwa hamna hiyo kweli ndani yake. Asemapo uongo, husema yaliyo yake mwenyewe; kwa sababu yeye ni mwongo, na baba wa huo [uongo].” (Yohana 8:44) Yesu alionyesha ujasiri ulioje kuwaambia kinagaubaga wanadini hao kwamba ni waongo na ni wana wa Ibilisi!

      13. (a) Ni wapi hasa ambapo chuki ya Yesu kwa ukosefu wa kutii sheria yaonyeshwa? (b) Kwa nini makasisi wasiotii sheria wastahili hukumu yenye kufanana na ile iliyotamkwa na Yesu juu ya waandishi na Mafarisayo?

      13 Mahali ambapo chuki ya Yesu juu ya kutotii sheria yaonyeshwa vizuri kuliko mahali pengine popote ni katika shutumu lake lenye kuwachoma vikali waandishi na Mafarisayo wenye sumu ya vipiri, kama ilivyoandikwa katika Mathayo sura ya 23. Humo yeye hutamka “ole” wa mara saba, akiwalinganisha na ‘makaburi yaliyopakwa chokaa​—yaliyojaa kila namna ya uchafu, unafiki, na uasi [kutotii sheria].’ Lo, jinsi Yesu alivyotamani sana kukomboa watu walioonewa watoke kwenye ukosefu huo wa kutii sheria! “Yerusalemu, Yerusalemu,” yeye akapaaza kilio, “ni mara ngapi nimetaka kuwakusanya pamoja watoto wako, kama vile kuku avikusanyavyo pamoja vifaranga vyake chini ya mabawa yake, lakini hamkutaka! Angalieni, nyumba yenu mmeachiwa hali ya ukiwa.” (Mt 23 Mistari 37, 38) Makasisi wasiotii sheria wa siku yetu wastahili hukumu kama hiyo kwa sababu, katika maneno ya 2 Wathesalonike 2:12, NW, ‘hawaamini ukweli bali wao huona raha katika ukosefu wa uadilifu.’ Ukosefu wao wa kutii sheria ndicho kinyume kabisa cha ujitoaji kimungu ambao Yesu alionyesha sana kwa uaminifu-mshikamanifu alipokuwa hapa duniani.

      Kujulisha Wazi Hukumu za Mungu

      14. Uthamini kwa ile siri takatifu ya ujitoaji kimungu wapasa kutusukuma tufanye nini?

      14 Uthamini wetu wa siri takatifu ya ujitoaji kimungu wapasa utuongoze sikuzote tufuate hatua za Yesu kwa ukaribu. Kama yeye, sisi twapaswa kuwa wenye bidii katika kupiga mbiu ya kile ambacho Isaya 61:2, NW, hukieleza kuwa “siku ya nia njema upande wa Yehova na siku ya kisasi upande wa Mungu wetu.” Na tufanye kwa bidii sehemu yetu “kufariji wote wanaoomboleza.” Kama vile ilivyokuwa Yesu akiwa duniani, leo moyo mkuu huhitajiwa ili kujulisha wazi hukumu za Yehova, kutia na zile jumbe thabiti zilizo katika makala zenye kutoboa mambo wazi katika Mnara wa Mlinzi na katika kile kitabu Revelation​—Its Grand Climax At Hand! Ni lazima tuhubiri kwa ujasiri na busara, semi zetu zikiwa ‘zimekolezwa munyu’ ili ziwe zenye ladha kwa wale wenye mbetuko wa kuelekea uadilifu. (Wakolosai 4:6) Tukiwa tumekwisha kujifunza kutokana na kielelezo cha Yesu cha ujitoaji kimungu, sisi na tuweze kuripoti wakati uwadiapo kwamba tumemaliza kazi ambayo Yehova alitupa tuifanye.​—Mathayo 24:14; Yohana 17:4.

      15. Kwa habari ya siri takatifu ya Mungu, ni jambo gani limetukia tangu 1914?

      15 Alipokuwa dhahiri katika mnofu, Yesu alikuwa Kielelezo kizuri kama nini! Lo, jinsi siri takatifu ya ujitoaji kimungu ilivyotimizwa katika yeye! Lo, jinsi alivyokuza jina la Yehova kwa ujasiri! Na lo, jinsi Baba ya Yesu alivyomthawabisha ajabu kwa ajili ya mwendo wake wa kushika uaminifu wa maadili! Lakini bado kuna zaidi kuhusu siri takatifu ya Mungu. Tangu 1914 tumekuwa tukiishi katika “siku ya Bwana.” (Ufunuo 1:10) Kama vile Ufunuo 10:7, NW, wataarifu, ni wakati wa ‘kuleta tamati ya siri takatifu ya Mungu kulingana na habari njema.’ Sasa sauti za kimbingu zimepiga mbiu hivi: “Ufalme wa ulimwengu ulipata kuwa ufalme wa Bwana yetu [Yehova] na wa Kristo wake, na yeye atatawala akiwa mfalme milele na milele.” (Ufunuo 11:15, NW) Yehova ametawaza Mfalme wa Kimesiya, Yesu Kristo, juu ya kiti chake cha ufalme chenye utukufu awe mtawala-mwenzi pamoja na Yeye!

      16. Mfalme aliyepewa kiti cha ufalme karibuni, Yesu Kristo, alionyeshaje upesi kwamba yeye hujali kuwako kwa hofu ya kumcha Mungu mbinguni?

      16 Akiwa mtawala-mwenzi pamoja na Mungu katika Ufalme uliozaliwa karibuni, Yesu aitwa Mikaeli pia (ikimaanisha “Ni Nani Aliye Kama Mungu?”). Hakuna mwasi yeyote aweza kamwe kufanikiwa kuwa kama Mungu, na Mfalme aliyepewa kiti cha ufalme karibuni alionyesha hivyo upesi kwa kuvurumisha Nyoka wa awali, Shetani, na malaika zake chini duniani. (Ufunuo 12:7-9) Ndiyo, Yesu hujali kuwako kwa hofu ya kumcha Mungu mbinguni, sawa na vile alivyoonyesha ujitoaji kimungu akiwa duniani. Yesu Kristo aliyetukuzwa hatapumzika mpaka atokomeze dini bandia na kufutilia mbali tengenezo la Shetani, lenye kuonekana na lisiloonekana.

      17. Tangu 1914, ni jambo gani limekuwa likitukia kwa utimizo wa Mathayo 25:31-33?

      17 Tangu 1914 utimizo wa unabii wa Yesu mwenyewe kwenye Mathayo 25:31-33 umemulika nuru nyangavu kwenye ile siri takatifu ya Mungu. Hapo Yesu ajulisha wazi hivi: “Hapo atakapokuja Mwana wa Adamu katika utukufu wake, na malaika watakatifu wote pamoja naye, ndipo atakapoketi katika kiti cha utukufu wake; na mataifa yote watakusanyika mbele zake; naye atawabagua kama vile mchungaji abaguavyo kondoo na mbuzi; atawaweka kondoo mkono wake wa kuume, na mbuzi mkono wake wa kushoto.” Akiwa katika mbingu katika mahali pafaapo sana kuona mambo, Mfalme, Hakimu, na Mteteaji mtukufu huyu wa ujitoaji kimungu ataleta kisasi, kwanza juu ya “mtu wa kuasi [sheria]” na matangukano mengine ya Babuloni Mkubwa, kisha juu ya wote wenye kubakia wakiwa viasili vya tengenezo ovu la Shetani la kidunia na wenye kuliunga mkono wakiwa kama mbuzi. Ndipo Shetani atatiwa ndani ya abiso. (Ufunuo 20:1-3, NW) Lakini “waadilifu” walio kama kondoo wataondoka wakaingie ndani ya uhai wa milele. (Mathayo 25:46, NW) Wewe na uwe katika kikundi hicho kinyoofu kwa kufuatia ujitoaji kimungu!

      18. Sisi tuna pendeleo gani lenye shangwe kuhusiana na ile siri takatifu ya ujitoaji kimungu?

      18 Ufunuo 19:10, NW, watutia moyo ‘tuabudu Mungu.’ Na kwa nini? Andiko laendelea kusema: “Kwa kuwa kutoa ushahidi kwa Yesu ndiko kunakovuvia kutoa unabii.” Mwingi sana wa unabii uliovuviwa wa nyakati za kale ulitoa ushahidi kwa Yesu! Na kwa kadiri unabii huo umetimizwa, ile siri takatifu ya Mungu imekuwa wazi kabisa. Kwa hiyo, sisi twashangilia kujua kwamba ile siri takatifu ya huu ujitoaji kimungu ilikuja kudhihirishwa katika utu wa Yesu. Sisi tumependelewa kiajabu kufuata katika hatua zake tukiwa wahudumu wanyenyekevu wa Ufalme wa Mungu. Ndiyo, tumestahishwa heshima ya kushiriki kuelewa na kupiga mbiu juu ya kadiri yote ya siri takatifu ya Mungu kulingana na zile habari njema!

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki