-
ParadisoKutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko
-
-
Maandiko hayo yalielekeza kwenye kurudishwa kwa Paradiso hapa duniani. Andiko la Danieli 7:13, 14 lilikuwa limetabiri kwamba wakati “utawala na heshima na ufalme” vitakabidhiwa Masihi, ‘vikundi vyote vya watu, vya mataifa na lugha vitamtumikia yeye.’ Raia hao wa Ufalme watakuwa hapa duniani. Kutokana na yale aliyomwambia Yesu, inaonekana yule mtenda-maovu alikuwa akionyesha tumaini la kwamba Yesu atamkumbuka wakati huo utakapofika.
Basi, Yesu atakuwa pamoja na mtenda-maovu jinsi gani? Kwa kumfufua kutoka kwa wafu, kumwandalia mahitaji yake ya kimwili, na kumpa nafasi ya kujifunza na kujipatanisha na matakwa ya Yehova ili apate uzima wa milele. (Yoh. 5:28, 29) Yesu aliona kwamba mtenda-maovu huyo ana mtazamo wa toba na heshima, na mtazamo huo ukawa msingi wa kumweka kati ya mabilioni ya watu watakaofufuliwa waishi duniani na kupata nafasi ya kuthibitisha kuwa wanastahili kuishi milele katika Paradiso.
Mtenda-maovu huyo atakuwa katika Paradiso wakati gani?
Kituo kinachotumiwa katika andiko la Luka 23:43 kinaweza kuathiri uelewaji wa mtu. Hati za kwanza za Kigiriki za Biblia hazikuwa na vituo. The Encyclopedia Americana (1956, Buku la 23, uku. 16) inasema hivi: “Inaonekana Wagiriki hawakutumia vituo katika hati na maandishi yao ya zamani.” Vituo hivyo vilianza kutumiwa katika karne ya 9 W.K. Je, andiko la Luka 23:43 linapaswa kuandikwa, “Kweli ninakuambia, Leo utakuwa pamoja nami katika Paradiso” (ZSB), au linapaswa kuwa, ‘Kweli ninakuambia leo, Utakuwa pamoja nami katika Paradiso’? Mafundisho ya Kristo na sehemu nyingine za Biblia zinapaswa kuwa msingi wa kufanya uamuzi, wala si kituo kilichotiwa katika maandishi karne nyingi baada ya Yesu kusema maneno hayo.
The Emphasised Bible iliyotafsiriwa na J. B. Rotherham inapatana na kituo kilicho katika Tafsiri ya Ulimwengu Mpya. Katika kielezi-chini kuhusu Luka 23:43, L. Reinhardt, mtafsiri wa Biblia Mjerumani anasema hivi: “Kituo kinachotumiwa sasa [na watafsiri walio wengi] katika mstari huu bila shaka si cha kweli nacho kinapingana na maoni yote ya Kristo na yule mtenda-maovu. . . . [Kristo] kwa hakika hakuelewa paradiso kuwa ni sehemu fulani ya makao ya wafu, bali badala yake aliielewa kuwa ni kurudishwa kwa paradiso duniani.”
Yesu ‘ataingia katika ufalme wake’ wakati gani na kutimiza kusudi la Baba yake kuifanya dunia iwe paradiso? Kitabu cha Ufunuo, kilichoandikwa miaka 63 hivi baada ya kusemwa kwa maneno yaliyoandikwa katika Luka 23:42, 43, kinaonyesha kwamba matukio hayo yalikuwa bado ya wakati ujao. (Ona ukurasa wa 397-400, chini ya “Vipindi vya Wakati,” pia kichwa “Siku za Mwisho.”)
-
-
RohoKutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko
-
-
Roho
Maana: Neno hili la Kiebrania ruʹach na la Kigiriki pneuʹma, ambayo mara nyingi hutafsiriwa “roho,” yana maana kadhaa. Yote yanamaanisha kitu ambacho hakionekani kwa macho ya wanadamu na ambacho ni nguvu zinazotenda. Maneno hayo ya Kiebrania na Kigiriki yanatumiwa kuhusu (1) upepo, (2) nguvu za utendaji zilizo katika viumbe vya duniani, (3) nguvu zinazotoka katika moyo wa mfano wa mtu na ambazo humfanya aseme na kutenda mambo katika njia fulani, (4) maneno yanayotoka katika chanzo kisichoonekana, (5) watu wa roho, na (6) nguvu za utendaji za Mungu, au roho takatifu. Matumizi kadhaa kama hayo yanazungumziwa hapa kuhusiana na masuala ambayo huenda yakazuka katika huduma ya shambani.
Roho takatifu ni nini?
Kulinganisha maandishi ya Biblia yanayotaja roho takatifu huonyesha kwamba inasemekana kuwa ‘inajaza’ watu; wanaweza ‘kubatizwa’ nayo; na wanaweza ‘kutiwa mafuta’ nayo. (Luka 1:41; Mt. 3:11; Mdo 10:38) Hakuna lolote kati ya hayo ambalo lingefaa ikiwa roho takatifu ingekuwa mtu.
Pia Yesu aliita roho takatifu kuwa “msaidizi” (Kigiriki, pa·raʹkle·tos), naye alisema kwamba msaidizi huyo ‘atafundisha,’ ‘atatoa ushahidi,’ ‘atasema,’ na ‘atasikia.’ (Yoh. 14:16, 17, 26; 15:26; 16:13) Mara nyingine vitu hupewa utu katika Maandiko. Kwa mfano, hekima inasemwa kuwa ina “watoto.” (Luka 7:35) Dhambi na kifo huitwa wafalme. (Rom. 5:14, 21) Ijapokuwa maandiko fulani yanasema kwamba roho ‘ilisema,’ maandiko mengine huonyesha wazi kwamba hilo lilifanywa kupitia malaika au wanadamu. (Mdo. 4:24, 25; 28:25; Mt. 10:19, 20; linganisha Matendo 20:23 na 21:10, 11.) Katika andiko la 1 Yohana 5:6-8, si roho peke yake bali pia “maji na damu” husemwa kuwa ‘vinatoa ushahidi.’ Kwa hiyo, hakuna neno lolote linalopatikana katika maandiko hayo ambalo linathibitisha kwamba roho takatifu ni mtu.
Utambulisho sahihi wa roho takatifu ni lazima upatane na maandiko yote yanayotaja roho hiyo. Kutokana na hayo, ni jambo linalopatana na akili kukata shauri kwamba roho takatifu ni nguvu za utendaji za Mungu. Hiyo si mtu bali ni nguvu ambazo Mungu hutoa ili kutimiza mapenzi yake matakatifu.—Zab. 104:30; 2 Pet. 1:21; Mdo. 4:31.
Ona pia ukurasa wa 368, 369, chini ya kichwa “Utatu.”
Ni nini kinachoonyesha kwamba mtu kweli ana roho takatifu?
Luka 4:18, 31-35: “[Yesu alisoma katika kitabu cha kukunjwa cha nabii Isaya:] ‘Roho ya Yehova iko juu yangu, kwa sababu alinitia mafuta kuwatangazia maskini habari njema’ . . . Naye akashuka kwenda Kapernaumu, jiji moja la Galilaya. Naye alikuwa akiwafundisha siku ya sabato; nao wakastaajabishwa na njia yake ya kufundisha, kwa sababu maneno yake yalikuwa yenye mamlaka. Basi katika sinagogi kulikuwa na mtu mwenye roho, roho mwovu, mchafu, naye akapaaza sauti . . . Lakini Yesu akamkemea, akisema: ‘Nyamaza, na umtoke.’ Kwa hiyo, baada ya kumwangusha mtu huyo chini katikati yao, yule roho mwovu akamtoka bila kumuumiza.” (Ni nini kilichoonyesha kwamba Yesu ana roho ya Mungu? Masimulizi hayo hayasemi kwamba alitetemeka au alipaaza sauti au aliruka-ruka. Badala yake, yanasema kwamba yeye alisema akiwa na mamlaka. Hata hivyo, inafaa kuangaliwa kwamba katika pindi hiyo roho mwovu alimchochea mtu apaaze sauti na kuanguka chini.)
Andiko la Matendo 1:8 linasema kwamba wakati wafuasi wa Yesu wangepokea roho takatifu wangekuwa mashahidi wake. Kulingana na Matendo 2:1-11, wakati walipopokea roho hiyo, watazamaji walivutiwa na uhakika wa kwamba, ingawa wale waliokuwa wakisema wote walikuwa watu wa Galilaya, walikuwa wakisema mambo matukufu ya Mungu katika lugha ambazo wageni wengi waliokuwapo walizijua. Lakini habari hiyo haisemi kwamba wale waliopokea roho hiyo walipaaza sauti na kuruka-ruka.
-