-
Matangulizi ya Kutumia Katika Huduma ya ShambaniKutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko
-
-
● ‘Habari. Jina langu ni ——. Kusudi langu la kuja hapa ni kuongea nawe baraka za Ufalme wa Mungu na jinsi tunavyoweza kuzipata. Lakini naona kwamba una shughuli nyingi (au, unataka kuondoka). Je, nikueleze jambo fupi tu?’
KATIKA ENEO LINALOHUBIRIWA MARA NYINGI
● ‘Nimefurahi kukukuta nyumbani. Tunafanya ziara ya kila juma katika mtaa huu, nasi tuna jambo zaidi la kushiriki pamoja nawe kuhusu mambo mazuri ajabu ambayo Ufalme wa Mungu utawafanyia wanadamu.’
● ‘Hujambo. Nimefurahi kukuona tena. . . . Je, kila mtu nyumbani ni mzima? . . . Nimepitia kidogo hapa ili nishiriki pamoja nawe wazo fulani kuhusu . . . ’
● ‘Habari ya asubuhi. . . . Nimekuwa nikitafuta nafasi nyingine ya kuongea na wewe. (Kisha taja jambo hususa unalotaka kuzungumzia.)’
-
-
Jinsi Unavyoweza Kujibu Vizuia-Mazungumzo VikitokeaKutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko
-
-
Jinsi Unavyoweza Kujibu Vizuia-Mazungumzo Vikitokea
Maelezo: Matarajio ya watu ya uzima hutegemea mtazamo wao kwa Yehova Mungu na Ufalme wake mikononi mwa Kristo Yesu. Ujumbe wa Ufalme wa Mungu unavutia, nao unaelekeza kwenye tumaini pekee linalotegemeka kwa ajili ya wanadamu. Ni ujumbe unaobadili maisha. Tunataka kila mtu ausikie. Tunafahamu kwamba ni wachache tu watakaoupokea na kuuthamini, lakini tunajua kwamba angalau watu wanahitaji kuusikia ili wafanye uchaguzi wa jambo wanalojua. Hata hivyo, si kila mtu aliye tayari kusikiliza, nasi hatujaribu kumlazimisha. Lakini tukiwa na utambuzi mara nyingi inawezekana kuvigeuza vizuia-mazungumzo viwe nafasi za mazungumzo zaidi. Hii ni mifano ambayo baadhi ya Mashahidi wenye uzoefu wametumia wakijitahidi kutafuta wanaostahili. (Mt. 10:11) Hatupendekezi kwamba ukariri moyoni lolote la majibu haya bali uweke wazo akilini, ulitie katika maneno yako mwenyewe na kulieleza kwa njia inayoonyesha kwamba unapendezwa kikweli na mtu unayesema naye. Unapofanya hivyo, unaweza kuwa na uhakika kwamba wale ambao mioyo yao ina mwelekeo unaofaa watasikiliza na kuthamini yale ambayo Yehova anafanya ili kuwavuta kwenye maandalizi yake ya upendo ya kupata uzima.—Yoh. 6:44; Mdo. 16:14.
‘MIMI SIPENDEZWI’
● ‘Hebu nikuulize, Unamaanisha kwamba hupendezwi na Biblia, au hupendezwi na dini kwa ujumla? Nauliza hivyo kwa sababu tumekutana na watu wengi ambao wakati mmoja walikuwa watu wa dini lakini hawaendi tena kanisani kwa sababu wanaona unafiki mwingi katika makanisa (au, wanaona kwamba dini ni biashara tu; au, hawaoni inafaa dini kujiingiza katika siasa; n.k.). Biblia pia haikubali matendo hayo, nayo huandaa msingi pekee unaotuwezesha kuutazamia wakati ujao tukiwa na uhakika.’
● ‘Ikiwa unamaanisha kwamba hupendezwi na dini nyingine, ninaelewa hilo. Lakini inaelekea unapendezwa na wakati ujao tunaoweza kutazamia kwa sababu ya hatari ya vita vya nyukilia (au, jinsi tunavyoweza kuwalinda watoto wetu ili wasitumie vibaya dawa za kulevya; au linaloweza kufanywa kuhusu uhalifu ili tusiogope kutembea barabarani; n.k.). Je, unaona kuna tarajio lolote la kupata utatuzi wa kweli?’
● ‘Je, ni kwa sababu tayari una dini . . . Hebu niambie, Je, unafikiri kuna wakati ambapo watu wote watakuwa katika dini moja? . . . Ni nini kinachozuia jambo hilo lisitendeke? . . . Ili hilo lifaulu, ni msingi gani unaohitajiwa?’
● ‘Ninaweza kuelewa jambo hilo. Miaka michache iliyopita nilikuwa na maoni kama hayo. Lakini nilisoma jambo fulani katika Biblia lililonisaidia niwe na maoni tofauti. (Mwonyeshe mtu huyo lilikuwa nini.)’
● ‘Ungependa nikuonyeshe katika Biblia jinsi unavyoweza kuwaona tena wapendwa wako waliokufa (au, kusudi la kweli la maisha; au, jinsi inavyoweza kutusaidia kuziunganisha familia zetu; n.k.)?’
● ‘Ikiwa unamaanisha kwamba hupendi kununua kitu, hebu nikutulize akili. Mimi sifanyi biashara. Lakini je, unapenda kuwa na nafasi ya kuishi katika paradiso duniani, bila magonjwa na uhalifu, ukiwa na jirani wanaokupenda kwelikweli?’
● ‘Je, wewe hujibu hivyo sikuzote Mashahidi wa Yehova wanapokutembelea? . . . Je, umewahi kujiuliza kwa nini tunaendelea kuwatembelea watu au jambo tunalotaka kusema? . . . Kwa ufupi, sababu ya kuja kukuona ni kwamba ninajua jambo fulani ambalo wewe unapaswa kulijua pia. Kwa nini usisikilize mara hii tu?’
‘SIPENDEZWI NA DINI’
● ‘Ninaelewa maoni yako. Kusema kweli, makanisa hayaufanyi ulimwengu huu kuwa mahali salama zaidi pa kuishi, sivyo? . . . Hebu nikuulize, Umekuwa na maoni hayo sikuzote? . . . Lakini unamwamini Mungu?’
● ‘Kuna watu wengi walio na maoni kama yako. Dini haijawasaidia kamwe. Hiyo ni moja ya sababu ambazo zinafanya tukutembelee—kwa sababu makanisa hayajawaambia watu ukweli kumhusu Mungu na kusudi lake zuri ajabu kwa wanadamu.’
● ‘Lakini nina uhakika kwamba unapendezwa na maisha yako ya baadaye. Je, unajua kwamba Biblia ilitabiri hali zilizo ulimwenguni leo? . . . Nayo inaonyesha yatakayotokea baadaye.’
● ‘Je, umekuwa na maoni hayo sikuzote? . . . Una maoni gani kuhusu wakati ujao?’
‘MIMI SIPENDEZWI NA MASHAHIDI WA YEHOVA’
● ‘Watu wengi hutuambia hivyo. Je, umewahi kujiuliza kwa nini watu kama mimi hujitolea kuwatembelea watu hata ingawa tunajua kwamba huenda watu wengi wasitukaribishe? (Taja mambo makuu katika Ezekieli 9:1-11, ukieleza kwamba, ikitegemea jinsi watu wanavyoitikia ujumbe wa Ufalme, kila mtu ‘anatiwa alama’ ili aje kuokolewa katika dhiki kuu au aje kuharibiwa na Mungu.)’
● ‘Ninaelewa jambo hilo, kwa sababu mimi pia nilikuwa na maoni hayo. Lakini, bila kupendelea, nikaamua kumsikiliza mmoja wao. Ndipo nikagundua kwamba sikuwa nimeambiwa ukweli kuwahusu. (Taja shtaka moja la uwongo ambalo watu wengi hutumia kisha ueleze tunayoamini.)’
● ‘Muda mfupi uliopita nilimwambia jambo hilohilo Shahidi mmoja aliyekuja kunitembelea. Lakini kabla hajaondoka niliuliza swali ambalo niliamini kwamba hawezi kulijibu. Ungependa kulijua swali hilo? . . . (Kwa mfano: Kaini alitoa wapi mke wake?)’ (Pendekezo hili litumiwe tu na wale ambao walipatwa na jambo hilo.)
● ‘Ikiwa wewe ni mtu wa dini, ninaelewa unachomaanisha. Bila shaka dini yako ni muhimu kwako. Lakini nafikiri utakubali kwamba sote tunapendezwa na (taja kichwa kinachofaa).’
● ‘Basi bila shaka una dini yako mwenyewe. Tafadhali, ungependa kuniambia ni dini gani hiyo? . . . Sisi hufurahia kuzungumza na watu wa dini yako. Una maoni gani kuhusu (taja kichwa chako cha mazungumzo)?’
● ‘Ndiyo, naelewa hilo. Tumekutembelea kwa sababu tungependa kuona watu wakiishi pamoja kwa amani. Tumechoka kusikia kila siku habari za vita na kuteseka. Nadhani wewe pia unahisi hivyo. . . . Lakini ni nini kinachoweza kuleta mabadiliko yanayohitajiwa? . . . Tumepata kitia-moyo katika ahadi za Biblia.’
● ‘Asante kwa kunijulisha maoni yako. Tafadhali unaweza kuniambia jambo linalofanya usipendezwe nasi? Je, ni yale tunayokuonyesha katika Biblia, au ni kwa sababu tumekuja kukutembelea?’
‘NINA DINI YANGU MWENYEWE’
● ‘Hebu niambie, Je, dini yako inafundisha kwamba kuna wakati ambapo watu wanaopenda mema wataishi milele duniani? . . . Hilo ni jambo lenye kuvutia, sivyo? . . . Limo humu katika Biblia. (Zab. 37:29; Mt. 5:5; Ufu. 21:4)’
● ‘Ninakubali kwamba kila mtu anapaswa kujifanyia uamuzi kuhusiana na jambo hili. Lakini je, unajua kwamba Mungu mwenyewe anatafuta watu wa aina fulani ili wawe waabudu wake wa kweli? Ona hapa katika Yohana 4:23, 24. Inamaanisha nini kumwabudu Mungu “kwa kweli”? . . . Mungu ametupa msaada gani ili tuweze kujua lililo kweli na lisilo kweli? . . . (Yoh. 17:17) Hebu ona jinsi ilivyo muhimu kwetu binafsi. (Yoh. 17:3)’
● ‘Je, umekuwa mtu wa dini maisha yako yote? Unafikiri wanadamu watapata kuungana katika dini moja? . . . Nimefikiria jambo hilo sana kwa sababu ya maneno yaliyoandikwa katika Ufunuo 5:13. . . . Tunahitaji kufanya nini ili tupatane na jambo hilo?’
● ‘Nilikuwa nikitumaini kumwona mtu kama wewe anayependezwa na mambo ya kiroho. Watu wengi leo hawapendi mambo ya kiroho. Una maoni gani kuhusu ahadi ya Biblia kwamba Mungu ataondoa uovu wote na kuifanya dunia hii iwe mahali ambapo watu wanaopenda uadilifu peke yao wataishi? Je, jambo hilo ni zuri kwako?’
● ‘Je, unajihusisha sana na mambo ya kanisa? . . . Je, siku hizi kanisa hujaa watu wakati wa ibada? . . . Je, unaona kwamba wafuasi wengi wanaonyesha tamaa ya moyo mnyoofu ya kutumia Neno la Mungu katika maisha ya kila siku? (Au, Je, unaona kwamba washiriki wana maoni yanayolingana kuhusu utatuzi wa matatizo yanayoukabili ulimwengu?) Sisi tumeona kwamba kuna faida ya kujifunza Biblia nyumbani.’
● ‘Inaonekana umeridhika na dini yako. Lakini watu wengi hawaridhiki na hali zilizo ulimwenguni. Labda wewe pia unaona hivyo, sivyo? . . . Ulimwengu unaelekea wapi?’
● ‘Je, wewe hupenda kusoma Biblia? . . . Je, unapata wakati wa kuisoma kwa ukawaida?’
● ‘Asante kwa kuniambia hivyo. Ninaamini utakubali kwamba, hata tuwe wa dini gani, sote tunapendezwa sana na amani ya ulimwengu (au, njia za kuwalinda watoto wetu wasipatwe na mavutano mabaya; au kuwa na ujirani ambamo watu wanapendana kikweli; au, kuwa na uhusiano mzuri pamoja na watu wengine, na hilo linaweza kutokeza tatizo wakati kila mtu anahisi yuko chini ya mkazo).’
● ‘Ninafurahi kujua kwamba unapenda dini. Watu wengi leo hawachukui dini kwa uzito. Hata wengine hufikiri hakuna Mungu. Lakini, kulingana na yale ambayo umefundishwa, unafikiri Mungu ni mtu wa aina gani? . . . Ona kwamba Biblia inatuonyesha jina lake. (Kut. 6:3; Zab. 83:18)’
● ‘Yesu alipowatuma wanafunzi wake wakahubiri, aliwaambia waende katika kila sehemu ya dunia, na hivyo wangewakuta watu wengi ambao wana dini tofauti. (Mdo. 1:8) Lakini alijua kwamba wale walio na njaa na kiu ya uadilifu wangesikiliza. Ni ujumbe gani hasa ambao alisema ungetangazwa wakati wetu? (Mt. 24:14) Ufalme huo unamaanisha nini kwetu?’
‘TAYARI SISI NI WAKRISTO HAPA KWETU’
● ‘Ninafurahi kusikia hivyo. Basi bila shaka unajua kwamba Yesu mwenyewe alifanya kazi kama hii, akiwatembelea watu katika nyumba zao, naye aliwaagiza wanafunzi wake pia wafanye hivyo. Unajua habari walizohubiri? . . . Hizo ndizo habari ambazo tumekuja kuzungumzia leo. (Luka 8:1; Dan. 2:44)’
● ‘Basi nina hakika utaona uzito wa mambo ambayo Yesu alisema hapa katika Mahubiri ya Mlimani. Alitaja mambo waziwazi lakini pia alionyesha upendo aliposema . . . (Mt. 7:21-23) Basi, tunahitaji kujiuliza hivi, Nayajua kadiri gani mapenzi ya Baba wa mbinguni? (Yoh. 17:3)’
‘NINA SHUGHULI’
● ‘Basi nitasema kwa ufupi sana. Nilikuja kuzungumza nawe jambo moja tu muhimu. (Eleza mambo makuu ya mazungumzo yako ukitumia sentensi mbili hivi.)’
● ‘Ni sawa. Nitapenda kukutembelea wakati mwingine ambao unakufaa zaidi. Lakini kabla sijaondoka, ningependa kusoma andiko moja tu linalotupatia jambo muhimu la kufikiria.’
● ‘Ninaelewa. Mimi pia ni mama (au, mfanyakazi; au mwanafunzi) nami nina shughuli nyingi. Kwa hiyo nitasema kwa ufupi. Sote tunakabiliwa na hali nzito. Biblia inaonyesha kwamba tunakaribia sana wakati ambapo Mungu atauharibu mfumo wa mambo wa sasa ulio mbovu. Lakini kuna watu watakaookoka. Swali ni, Mimi na wewe tunapaswa kufanya nini ili tuwe kati yao? Biblia inajibu swali hilo. (Sef. 2:2, 3)’
● ‘Hiyo ndiyo sababu hasa iliyonifanya nikutembelee. Sote tuna shughuli nyingi sana hivi kwamba nyakati nyingine mambo muhimu kwelikweli maishani hupuuzwa, sivyo? . . . Nitasema kwa ufupi, lakini naamini utapendezwa na andiko hili moja tu. (Luka 17:26, 27) Sote hatutaki kujikuta katika hali hiyo, kwa hiyo tunahitaji kutafuta wakati katika maisha yetu yenye shughuli nyingi ili tufikirie mambo ambayo Biblia inasema. (Toa kichapo.)’
● ‘Je, itakufaa zaidi tukirudi baada ya nusu saa hivi, baada ya kuwatembelea jirani zako?’
● ‘Basi sitachukua muda mrefu. Labda nitakutembelea siku nyingine. Lakini kabla sijaondoka, ningependa nikupe kichapo hiki. (Mpe toleo la mwezi huo.) Kichapo hiki kina masomo yatakayokufahamisha majibu ya Biblia kwa maswali kama (taja swali moja au mawili tu).’
● ‘Pole kwa kuwa nimekutembelea wakati usiofaa. Labda unajua kwamba mimi ni mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Nilitaka kuzungumza na wewe jambo muhimu kutoka katika Biblia. Lakini kwa kuwa huna wakati wa kusikiliza sasa, ningependa kukupa trakti hii, inayozungumzia (taja kichwa). Itakuchukua muda mfupi tu kuisoma trakti hii, lakini itakupendeza sana.’
● ‘Ninaelewa jambo hilo. Inaonekana hakuna wakati wa kutosha kufanya kila jambo. Lakini umepata kujiuliza jinsi ambavyo maisha yangekuwa tofauti ikiwa ungeishi milele? Najua jambo hili huenda likasikika kuwa geni. Lakini acha nikuonyeshe andiko moja tu la Biblia linaloeleza jinsi jambo hilo linavyowezekana. (Yoh. 17:3) Kwa hiyo, jambo tunalohitaji kufanya sasa ni kupata ujuzi huu kumhusu Mungu na Mwana wake. Ndiyo sababu tunawaachia watu vichapo hivi.’
‘KWA NINI MNAWATEMBELEA WATU MARA NYINGI?’
● ‘Kwa sababu tunaamini kwamba tunaishi katika siku za mwisho zinazotajwa katika Biblia. Tunaona kwamba ni muhimu kwetu sote kufikiria yatakayotokea baada ya hizi hali za sasa. (Taja jambo moja au mawili yaliyotukia hivi karibuni au hali za sasa.) Swali ni, tunahitaji kufanya nini ikiwa tunataka kuuokoka mwisho wa mfumo huu wa mambo?’
● ‘Kwa sababu tunampenda Mungu na jirani zetu. Sote tunapaswa kufanya hivyo, sivyo?’
‘TAYARI NAIJUA VIZURI KAZI YENU’
● ‘Ninafurahi sana kusikia hivyo. Je, una mtu wa ukoo au rafiki ambaye ni Shahidi? . . . Hebu nikuulize: Unaamini tunayofundisha kutoka katika Biblia, yaani, kwamba tunaishi katika “siku za mwisho,” kwamba hivi karibuni Mungu atawaharibu waovu, na kwamba dunia hii itakuwa paradiso ambamo watu wanaweza kuishi milele wakiwa na afya kamilifu katikati ya jirani wanaopendana kwelikweli?’
‘HATUNA PESA’
● ‘Sisi hatuombi pesa. Lakini tunawatolea watu funzo la Biblia nyumbani bila malipo. Moja la masomo hayo ni (tumia kichwa cha sura fulani kutoka katika kichapo kinachotolewa wakati huu). Je, nitumie dakika chache niwaonyeshe jinsi linavyofanywa? Haitawagharimu hata shilingi moja.’
-