-
Kwa Nini Kujivika Unyenyekevu?Mnara wa Mlinzi—1991 | Julai 15
-
-
shauri la Paulo: “Msinie yaliyo makuu, lakini mkubali kushughulishwa na mambo manyonge.” (Warumi 12:16) Lakini, unyenyekevu waweza kunufaishaje sisi na wengineo?
Manufaa za Unyenyekevu
Faida moja ya unyenyekevu ni kwamba inatuzuia tusijigambe juu ya sisi wenyewe. Hivyo hatuwaudhi wengine na tunaepuka aibu ya kibinafsi kama hawapati mshangao kwa ajili ya vitendo vyetu. Twapaswa kujigamba juu ya Yehova, si juu ya sisi wenyewe.—1 Wakorintho 1:31.
Unyenyekevu unatusaidia kupata mwelekezo wa kimungu. Yehova alituma malaika kwa Danieli akiwa na njozi kwa sababu nabii huyo alikuwa amejinyenyekeza mbele ya Mungu alipokuwa akitafuta-tafuta mwelekezo na ufahamu. (Danieli 10:12) Ezra alipokuwa karibu kuongoza watu wa Yehova nje ya Babuloni wakiwa na dhahabu na fedha nyingi ya kurembesha hekalu katika Yerusalemu, alitangaza kufunga ili waweze kujinyenyekeza mbele za Mungu. Tokeo likawa nini? Yehova aliwalinda juu ya shambulio la kiadui pindi ya ile safari ya hatari. (Ezra 8:1-14, 21-32) Kama Danieli na Ezra, na tuonyeshe unyenyekevu na kutafuta mwelekezo wa Yehova badala ya kujaribu kutimiza majukumu yenye kutolewa na Mungu katika hekima na uwezo wetu wenyewe.
Kama tumejivika vazi la unyenyekevu, tutawastahi (tutawaheshimu) wengine. Kwa mfano, watoto walio na unyenyekevu huwastahi na kuwatii wazazi wao. Wakristo wanyenyekevu huwastahi waamini wenzao wa mataifa, rangi, na malezi mengineyo, kwa kuwa unyenyekevu unatufanya tusipendelee.—Matendo 10:34, 35; 17:26.
Unyenyekevu unaendeleza upendo na amani. Mtu mnyenyekevu hapigani na waamini wenzake kwa juhudi ya kuimarisha haki zake zenye kudhaniwa. Paulo alifanya tu mambo yaliyokuwa yenye kujenga na hangesumbua dhamiri ya ndugu. (Warumi 14:19-21; 1 Wakorintho 8:9-13; 10:23-33) Unyenyekevu unatusaidia pia kuendeleza upendo na amani kwa kuwasamehe wengine kwa ajili ya dhambi zao dhidi yetu. (Mathayo 6:12-15; 18:21, 22) Unatusukuma kumwendea mtu aliyeudhiwa, kukiri kosa letu, kumwomba msamaha wake, na kufanya tuwezavyo ili kusahihisha kosa lolote ambalo huenda ikawa tumelifanya. (Mathayo 5:23, 24; Luka 19:8) Ikiwa mtu aliyeudhiwa anatukaribia, unyenyekevu unatuchochea kusuluhisha mambo kwa amani katika roho ya upendo.—Mathayo 18:15; Luka 17:3.
Ukombozi unategemea kuonyesha unyenyekevu. Kwa mfano, kuhusu Mungu, inasemwa hivi: “Watu wanaoonewa [wanyenyekevu, NW] wewe utawaokoa; ila macho yako ni juu ya wenye kiburi, uwadhili.” (2 Samweli 22:28) Mfalme Yesu Kristo ‘apandaye katika kusudi la ukweli na unyenyekevu na uadilifu,’ atawaokoa wale wanaojinyenyekeza mbele yake na mbele ya Baba yake. (Zaburi 45:4, NW) Wale waonyeshao unyenyekevu waweza kupata faraja katika maneno haya: “Mtafuteni BWANA [Yehova, NW], enyi nyote mlio wanyenyekevu wa dunia, ninyi mliozitenda hukumu zake; itafuteni haki, utafuteni unyenyekevu; huenda mtafichwa katika siku ya hasira ya BWANA [Yehova, NW].”—Sefania 2:3.
Unyenyekevu na Tengenezo la Mungu
Unyenyekevu unaongoza watu wa Mungu kuthamini tengenezo lake na kukaa pamoja nalo wakiwa washika uaminifu wa maadili. (Linganisha Yohana 6:66-69.) Ikiwa hatupewi pendeleo la utumishi tulilokuwa tukitazamia kupokea, unyenyekevu utatusaidia tushirikiane pamoja na wale wenye daraka ndani ya kundi. Na ushirikiano wetu wenye unyenyekevu unaweka mfano mzuri.
Kwa upande mwingine, unyenyekevu unatuzuia kutokana na kuonyesha majivuno kuhusu mapendeleo yetu ya utumishi miongoni mwa watu wa Yehova. Unatuzuia kutokana na kutafuta sifa kwa kazi ambayo tumependelewa kufanya katika tengenezo la Mungu. Tena, ikiwa tunatumikia tukiwa wazee, unyenyekevu unatusaidia kutendea kundi la Mungu kwa wororo.—Matendo 20:28, 29; 1 Petro 3:8.
Unyenyekevu na Nidhamu
Vazi la unyenyekevu linatusaidia kupokea nidhamu. Watu wanyenyekevu hawako kama Mfalme Uzia wa Yuda, ambaye moyo wake ulikuja kuwa wenye kujigamba sana hivi kwamba alijitwalia bila haki majukumu ya kikuhani. Yeye ‘alimwasi Yehova, Mungu wake; kwani aliingia hekaluni mwa Yehova, ili afukize uvumba juu ya madhabahu ya kufukizia.’ Uzia alipowaghadhibikia makuhani kwa kumsahihisha, alipatwa na ukoma. Lo! ni bei iliyoje kulipa kwa ajili ya kukosa unyenyekevu! (2 Nyakati 26:16-21; Mithali 16:18) Usiwe kamwe kama Uzia na kuacha kiburi kikuzuie kukubali nidhamu kutoka kwa Mungu kupitia Neno na tengenezo Lake.
Kuhusu hilo Paulo aliwaambia Wakristo Waebrania waliopakwa mafuta: “Mmeyasahau yale maonyo, yasemayo nanyi kama kusema na wana, Mwanangu, usiyadharau marudia ya Bwana [nidhamu kutoka kwa Yehova, NW], wala usizimie moyo ukikemewa naye; maana yeye ambaye Bwana [Yehova, NW] ampenda, humrudi, naye humpiga kila mwana amkubaliye. . . . Kila adhabu wakati wake haionekani kuwa kitu cha furaha, bali cha huzuni; lakini baadaye huwaletea wao waliozoezwa nayo matunda ya haki yenye amani.” (Waebrania 12:5-11) Pia, kumbuka kwamba “maonyo ya kumwadilisha mtu ni njia ya uzima.”—Mithali 6:23.
Baki Ukiwa Umejivika Unyenyekevu
Ni muhimu kama nini Wakristo wajivike vazi la unyenyekevu sikuzote! Linatusukuma kuvumilia tukiwa wahubiri wa Ufalme, tukitoa ushahidi kwa unyenyekevu kutoka nyumba kwa nyumba katika kutafuta-tafuta wale walio na “mwelekeo wenye kufaa kwa ajili ya uhai wa milele.” (Matendo 13:48, NW; 20:20) Kwa kweli, unyenyekevu unatusaidia kuendelea kumtii Mungu katika mambo yote, ingawa wapinzani wenye kiburi huchukia mwendo wetu wenye uadilifu.—Zaburi 34:21.
Kwa sababu unyenyekevu unatusukuma ‘kumtumaini Yehova kwa moyo wetu wote,’ anafanya mapito yetu yanyoke. (Mithali 3:5, 6) Kwa hakika, tunaweza kutembea pamoja na Mungu na kuonea shangwe upendeleo na baraka yake ikiwa tumejivika tu sifa hiyo nzuri. Kama vile mwanafunzi Yakobo alivyoandika: “Nyenyekeeni mbele ya Bwana [Yehova, NW], naye atawainueni.” (Yakobo 4:10, HNWW) Acheni basi tujivike unyenyekevu, lile vazi lenye urembo lililobuniwa na Yehova Mungu.
-
-
Mkutano Wa Kila Mwaka Oktoba 5, 1991Mnara wa Mlinzi—1991 | Julai 15
-
-
Mkutano Wa Kila Mwaka Oktoba 5, 1991
MKUTANO WA KILA MWAKA wa washiriki wa Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania utafanywa siku ya October 5, 1991, kwenye Jumba la Makusanyiko la Mashahidi wa Yehova, 2932 Kennedy Boulevard, Jersey City, New Jersey. Mkutano wa utangulizi wa washirika peke yao utafanywa saa 3.30 asubuhi, ukifuatwa na ule mkutano wa ujumla wa kila mwaka saa 4.00 asubuhi.
Washirika wa Shirika hilo wanapaswa kuijulisha Ofisi ya Mwandishi sasa juu ya badiliko lolote lililotokea mwaka uliopita katika anwani zao za barua ili barua zile za kawaida za ujulisho na uwakilishaji ziweze kuwafikia muda mfupi baada ya Agosti 1.
Barua za uwakilishaji, watakazopelekewa washiriki pamoja na ujulisho wa mkutano wa kila mwaka, zinapasa kurudishwa ili ziifikie Ofisi ya Mwandishi wa Sosaiti si baada ya Agosti 15. Inampasa kila mshiriki ajaze mambo yote yaliyo katika barua ya uwakilishaji na kuirudisha haraka, akitaarifu kama atakuwapo ama hatakuwapo mkutanoni yeye binafsi. Habari zenye kutajwa katika kila barua ya uwakilishaji zinapasa kusema jambo hilo waziwazi, kwa kuwa ndizo zitakazotegemewa katika kujua ni akina nani watakaokuwapo binafsi.
Inatarajiwa kwamba kipindi kizima, kutia ndani mkutano ule rasmi wa kishughuli na ripoti mbalimbali, kitamalizwa ifikapo saa 7.00 alasiri au muda mfupi baada ya hapo. Hakutakuwa na kipindi cha alasiri. Kwa sababu nafasi ni ndogo, itawezekana kuingia kwa kuwa na tikiti tu. Hakutakuwa na mipango ya kuunganisha mahali pengine-pengine kwa kamba za simu ili kuusikia mkutano wa kila mwaka.
-