-
Kiongozi Ni Nani?2015 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
Donald Nowills, aliyepewa mgawo wa kusimamia kazi katika ofisi ya tawi baada ya wamishonari kufukuzwa, alikuwa na umri wa miaka 20, na miaka minne tu ilikuwa imepita tangu abatizwe. Ingawa alikuwa ametumikia akiwa mwangalizi wa mzunguko kwa miezi michache, kazi ya ofisini ilikuwa mpya kwake. Ndugu Nowills alikuwa na ofisi ndogo katika nyumba yake, ambayo ilikuwa imejengwa kwa mbao, bati na sakafu ya udongo. Ilikuwa huko Gualey, eneo hatari sana la Ciudad Trujillo. Akisaidiwa na Félix Marte, alichapisha nakala za Mnara wa Mlinzi kwa ajili ya nchi nzima.
Gazeti Mnara wa Mlinzi la mwaka wa 1958 lililonakiliwa kwa mashine
Mary Glass, ambaye mume wake, Enrique, alikuwa amefungwa wakati huo, alimsaidia Ndugu Nowills. Anaeleza hivi: “Ningemaliza kazi yangu saa 11:00 jioni na kwenda kwenye ofisi ya Ndugu Nowills kuchapa magazeti ya Mnara wa Mlinzi. Halafu Ndugu Nowills angepiga fotokopi kwa mashine ndogo. Baadaye, dada kutoka Santiago tuliyemwita ‘malaika,’ angeweka magazeti hayo ndani ya debe tupu la mafuta ya kupikia. Kisha alifunika machapisho hayo kwa kitambaa, halafu akaweka mihogo, viazi, au majimbi (nduma) juu yake. Kisha angefunika kwa gunia. Halafu angesafiri kwa basi kuelekea kaskazini mwa nchi na kuliachia kila kutaniko nakala moja. Kila familia ingejifunza nakala hiyo na kisha kuipa familia nyingine.”
Mary anaongezea hivi: “Tulihitaji kuwa macho, kwa kuwa barabara zilikuwa na maofisa wa serikali waliokuwa wakipeleleza mahali ambako magazeti ya Mnara wa Mlinzi yalikuwa yakichapishwa. Hata hivyo hawakufanikiwa. Yehova alitulinda sikuzote.”
-
-
Hatari ya Kukamatwa2015 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
JAMHURI YA DOMINIKA
Hatari ya Kukamatwa
“Wenye Kujihadhari Kama Nyoka na Hata Hivyo Wasio na Hatia Kama Njiwa”
Ilikuwa muhimu kwa watumishi waaminifu wa Yehova kuendelea kupata chakula cha kiroho wakati wa marufuku, lakini ulikuwa wakati hatari sana kwa waabudu wa kweli. Wakati huo, ndugu wengi walikamatwa na kufungwa mara kwa mara gerezani.
Juanita Borges anaeleza hivi: “Nilipojifunza kweli mwaka wa 1953, nilijua vizuri kwamba nikiwa Shahidi wa Yehova, ningekabili hatari ya kukamatwa. Ndivyo ilivyotokea. Novemba 1958, nilipokuwa nikimtembelea Dada Eneida Suárez, polisi wapelelezi walitukamata kwa tuhuma ya kufanya mikutano. Tulifungwa miezi mitatu gerezani, na kila mmoja wetu alitozwa faini ya pesos 100, ambazo wakati huo zilikuwa sawa na dola 100 za Marekani.”
Polisi wapelelezi walikuwa na orodha zenye habari kuhusu ndugu na dada zetu.
Serikali ilitumia mbinu mbalimbali kuwazuia Mashahidi kukusanyika pamoja, hata hivyo akina ndugu hawakukata tamaa. Lakini walipaswa kuwa “wenye kujihadhari kama nyoka na hata hivyo wasio na hatia kama njiwa.” (Mt. 10:16) Andrea Almánzar anakumbuka hivi: “Ili kuhudhuria mikutano, kila mtu alipaswa kuwasili wakati tofauti. Mara nyingine tuliondoka usiku ili tusitambuliwe.”
Jeremías Glass alipozaliwa, baba yake León, alikuwa gerezani. Jeremías alianza kuhubiri mwaka wa 1957 akiwa na umri wa miaka saba. Anakumbuka mikutano iliyofanywa kwa siri nyumbani kwao na tahadhari waliyochukua ili wasigunduliwe. Jeremías anaeleza hivi: “Kila mtu aliyehudhuria alipewa ubao mdogo wenye namba iliyoonyesha utaratibu wa kuondoka. Mkutano ulipoisha, baba yangu angenipeleka mlangoni kukagua namba kwenye vibao hivyo na kuwaelekeza watu waondoke wawili-wawili bila kupita njia moja.”
Tahadhari nyingine ilikuwa kupanga mikutano wakati ambapo uwezekano wa kukamatwa ulikuwa mdogo. Kwa mfano, Mercedes García alijifunza kweli kutoka kwa mjomba wake, Pablo González. Akiwa na umri wa miaka saba, mama yake alikufa na baba yake alifungwa gerezani, na kuacha watoto kumi wa kiume na wa kike, kutia ndani Mercedes. Mercedes alibatizwa mwaka wa 1959 akiwa na umri wa miaka tisa. Ili wasikamatwe, hotuba ya ubatizo ilitolewa saa tisa na nusu usiku. Hotuba hiyo ilitolewa katika nyumba ya ndugu, kisha ubatizo ukafanywa katika Mto Ozama, unaopita katikati ya mji mkuu. Mercedes anasema, “Tulikuwa njiani tukirudi nyumbani saa kumi na moja na nusu alfajiri watu walipokuwa wakiamka.”
-