-
Mkumbuke Mke wa LotiMasomo Unayoweza Kujifunza Katika Biblia
-
-
SOMO LA 10
Mkumbuke Mke wa Loti
Loti aliishi na Abrahamu mjomba wake, katika nchi ya Kanaani. Hatimaye, Abrahamu na Loti wakawa na mifugo mingi hivi kwamba hakukuwa na eneo la kutosha kwa ajili ya wanyama wao. Abrahamu alimwambia Loti: ‘Hatuwezi kuendelea kuishi pamoja katika eneo hili. Tafadhali, chagua upande utakaopenda kwenda nami nitaenda upande ule mwingine.’ Bila shaka Abrahamu hakuwa mbinafsi, sivyo?
Loti aliona sehemu ya nchi iliyo nzuri sana karibu na jiji la Sodoma. Kulikuwa na maji mengi na nyasi mbichi. Kwa hiyo akachagua eneo hilo na kuhamia yeye na familia yake.
Watu walioishi katika jiji la Sodoma na jiji jirani la Gomora walikuwa wabaya sana. Kwa kweli, walikuwa wabaya sana hivi kwamba Yehova aliamua kuharibu majiji hayo. Lakini Yehova alitaka kumwokoa Loti na familia yake, kwa hiyo aliwatuma malaika wawili wamwambie Loti hivi: ‘Ondokeni haraka mahali hapa, kwa sababu Yehova ataliangamiza jiji hili!’
Loti hakuondoka mara moja. Alichelewa. Kwa hiyo malaika walimchukua Loti, mke wake, na binti zake wawili na kuwatoa nje ya jiji, kisha wakawaambia hivi: ‘Kimbieni ili kuokoa uhai wenu! Msitazame nyuma, mkitazama nyuma mtakufa!’
Walipofika katika jiji la Soari, Yehova alinyesha mvua ya moto na kiberiti katika majiji ya Sodoma na Gomora. Majiji hayo mawili yaliharibiwa kabisa. Mke wa Loti alipokosa kumtii Yehova na kutazama nyuma akawa nguzo ya chumvi! Lakini Loti na binti zake walikuwa salama kwa sababu walimtii Yehova. Walihuzunika sana kwa sababu mke wa Loti hakumtii Yehova. Hata hivyo, walifurahi kwa kuwa walisikiliza maagizo ya Yehova.
“Mkumbukeni mke wa Loti.”—Luka 17:32
-
-
Jaribu la ImaniMasomo Unayoweza Kujifunza Katika Biblia
-
-
SOMO LA 11
Jaribu la Imani
Abrahamu alimfundisha mwana wake Isaka kumpenda Yehova na kutumaini ahadi zake. Hata hivyo, Isaka alipokuwa na umri wa miaka 25, Yehova alimwambia Abrahamu afanye jambo fulani ambalo lilikuwa gumu sana. Jambo gani?
Mungu alimwambia Abrahamu: ‘Tafadhali, mchukue mwana wako wa pekee na umtoe akiwa dhabihu kwenye mlima katika nchi ya Moria.’ Abrahamu hakujua ni kwa nini Yehova alimwomba afanye jambo hilo. Hata hivyo, alimtii Yehova.
Asubuhi na mapema siku iliyofuata, Abrahamu, Isaka na watumishi wake wawili walianza safari ya kwenda Moria. Baada ya kusafiri kwa siku tatu, waliiona milima kwa mbali. Abrahamu aliwaambia watumishi wake wabaki, ili yeye na Isaka waende wakatoe dhabihu. Abrahamu alichukua kisu naye Isaka alibeba kuni. Isaka alimuuliza baba yake hivi: ‘Mnyama wa dhabihu yuko wapi?’ Abrahamu akamjibu: ‘Mwanangu, Yehova ataandaa.’
Walipofika mlimani walijenga madhabahu. Kisha, Abrahamu akamfunga Isaka mikono na miguu na kumweka juu ya madhabahu.
Abrahamu akainua kisu. Mara moja, malaika wa Yehova akaita kutoka mbinguni akisema: ‘Abrahamu! Usimchinje mwana wako! Sasa ninajua kwamba una imani katika Mungu kwa sababu ulikuwa tayari kumtoa mwana wako kuwa dhabihu.’ Kisha, Abrahamu akamwona kondoo akiwa amejinasa kwenye kichaka. Bila kukawia alimfungua Isaka na kutoa dhabihu ya kondoo.
Kuanzia siku hiyo, Yehova alimwita Abrahamu kuwa rafiki yake. Je, unajua ni kwa nini? Abrahamu alifanya kila kitu ambacho Yehova alimwagiza, hata ingawa nyakati fulani hakuelewa sababu za kufanya hivyo.
Yehova alirudia ahadi yake kwa Abrahamu: ‘Nitakubariki nami nitafanya watoto wako wawe wengi.’ Hilo lilimaanisha kwamba Yehova angewabariki watu wote wema kupitia familia ya Abrahamu.
“Mungu aliupenda ulimwengu sana hivi kwamba akamtoa Mwana wake mzaliwa pekee, ili kila mtu anayemwamini asiangamizwe bali awe na uzima wa milele.”—Yohana 3:16
-