Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Yakobo Alipewa Urithi
    Masomo Unayoweza Kujifunza Katika Biblia
    • Yakobo akimpa Esau bakuli la mchuzi ili apewe haki ya kuwa mzaliwa wa kwanza

      SOMO LA 12

      Yakobo Alipewa Urithi

      Isaka na Rebeka wakiwa na watoto wao mapacha Yakobo na Esau

      Isaka alikuwa na umri wa miaka 40 alipomwoa Rebeka. Alimpenda sana. Baada ya muda walipata watoto wawili mapacha.

      Mtoto wa kwanza aliitwa Esau, na mdogo wake aliitwa Yakobo. Esau alipenda kuwinda, naye alikuwa mwindaji hodari. Lakini, Yakobo alipenda kazi za nyumbani.

      Wakati huo, mtoto wa kwanza alipewa vitu vingi vya baba yake, yaani, mali na shamba baba yake alipokufa. Vitu hivyo viliitwa urithi. Katika familia ya Isaka, urithi ulitia ndani kuwa sehemu ya ahadi ambazo Mungu alimwahidi Abrahamu. Esau hakuthamini ahadi hizo, lakini Yakobo alizithamini sana.

      Yakobo na Esau

      Siku moja, Esau alirudi kutoka mawindoni akiwa amechoka sana. Yakobo alikuwa akipika chakula kizuri, Esau akamwambia: ‘Nina njaa sana! Tafadhali, nipe mchuzi huo mwekundu!’ Yakobo akamjibu: ‘Nitakupa, lakini niapie kwanza kwamba utanipa urithi wako!’ Esau akamwambia: ‘Urithi hauna maana kwangu! Uchukue. Nipe chakula nile.’ Je, unafikiri Esau alifanya jambo la hekima? Hapana. Esau alimpa Yakobo kitu chenye thamani sana ili apewe tu mchuzi wa dengu.

      Isaka alipozeeka, wakati wa kumbariki mtoto wake wa kwanza ulifika. Hata hivyo, Rebeka alimsaidia Yakobo, mtoto wake wa pili kupata baraka. Esau alipojua jambo hilo, alikasirika sana na akapanga kumuua ndugu yake. Isaka na Rebeka walitaka kumlinda Yakobo, hivyo wakamwambia hivi: ‘Ondoka, nenda ukaishi na Labani, mjomba wako, mpaka ghadhabu ya Esau itulie.’ Yakobo alisikiliza ushauri wa wazazi wake, naye akakimbia ili aokoe uhai wake.

      “Mtu atapata faida gani akiupata ulimwengu wote kisha apoteze uhai wake? Kwa kweli, mtu anaweza kutoa nini ili abadilishane na uhai wake?”​—Marko 8:36, 37

      Maswali: Esau alipenda kufanya nini? Yakobo alipenda kufanya nini? Kwa nini Yakobo alibarikiwa badala ya Esau?

      Mwanzo 25:20-34; 27:1–28:5; Waebrania 12:16, 17

  • Yakobo na Esau Wafanya Amani
    Masomo Unayoweza Kujifunza Katika Biblia
    • Yakobo anainama na Esau anakimbia kumwelekea

      SOMO LA 13

      Yakobo na Esau Wafanya Amani

      Yehova alimwahidi Yakobo kwamba atamlinda kama alivyofanya kwa Abrahamu na Isaka. Yakobo aliishi katika eneo lililoitwa Harani. Alioa, akapata watoto na kuwa tajiri sana.

      Baadaye, Yehova alimwambia Yakobo hivi: ‘Rudi katika nchi ya baba zako.’ Hivyo, Yakobo na familia yake walianza safari ndefu ya kurudi Kanaani. Wakiwa njiani, watu fulani walimjia Yakobo na kumwambia: ‘Ndugu yako Esau yuko njiani anakuja, akiwa pamoja na wanaume 400!’ Yakobo aliogopa kwamba huenda Esau angemshambulia yeye na familia yake. Alisali hivi kwa Yehova: ‘ Tafadhali nilinde dhidi ya ndugu yangu.’ Siku iliyofuata, Yakobo alituma zawadi nyingi kwa Esau, yaani, kondoo, mbuzi, ng’ombe, ngamia na punda.

      Usiku huo, Yakobo alipokuwa peke yake alimwona malaika! Malaika alianza kupigana naye. Walipigana mweleka hadi asubuhi. Ingawa Yakobo aliumizwa, hakuacha kupigana. Kisha malaika akamwambia: ‘Niache niende.’ Lakini Yakobo akamjibu: ‘Sitakuacha mpaka unibariki.’

      Mwishowe malaika akambariki Yakobo. Sasa Yakobo alijua kwamba Yehova atamlinda ili Esau asimshambulie.

      Asubuhi, Yakobo alimwona kwa mbali Esau akija na wanaume 400. Yakobo alimkaribia Esau ndugu yake na kuinama chini mara saba. Esau alimkimbilia Yakobo na kumkumbatia. Wakalia pamoja na kufanya amani. Unafikiri Yehova alihisije Yakobo alipofanya amani na ndugu yake?

      Baadaye, Esau alirudi kwake, na Yakobo akaendelea na safari. Yakobo alikuwa na watoto wa kiume 12. Watoto hao ni Rubeni, Simeoni, Lawi, Yuda, Dani, Naftali, Gadi, Asheri, Isakari, Zabuloni, Yosefu, na Benjamini. Mmoja wa watoto hao, yaani, Yosefu—alitumiwa na Yehova kuwakomboa watu Wake. Je, unajua alifanya hivyo jinsi gani? Acheni tuone.

      “Endeleeni kuwapenda adui zenu na kusali kwa ajili ya wale wanaowatesa ninyi, ili mpate kuwa wana wa Baba yenu aliye mbinguni.”​—Mathayo 5:44, 45

      Maswali: Kwa nini Yakobo alibarikiwa? Yakobo alifanyaje amani na Esau?

      Mwanzo 28:13-15; 31:3, 17, 18; 32:1-29; 33:1-18; 35:23-26

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki