Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Mtumwa Aliyemtii Mungu
    Masomo Unayoweza Kujifunza Katika Biblia
    • Yosefu akimkimbia mke wa Potifa

      SOMO LA 14

      Mtumwa Aliyemtii Mungu

      Yosefu alikuwa mmoja wa wana wa mwisho wa Yakobo. Kaka zake waliona kuwa Yosefu ndiye aliyependwa zaidi na baba yao. Unafikiri jambo hilo lilifanya wahisije? Walianza kumwonea Yosefu wivu na kumchukia. Yosefu alipopata ndoto zisizo za kawaida, aliwaambia kuhusu ndoto hizo. Kaka zake walifikiri ndoto hizo zilimaanisha kwamba siku moja wangemwinamia. Sasa walimchukia hata zaidi!

      Kaka za Yosefu wakimtupa ndani ya shimo

      Siku moja, kaka za Yosefu walikuwa wakichunga kondoo karibu na jiji la Shekemu. Yakobo alimtuma Yosefu akaone wanaendeleaje. Kwa mbali walimwona Yosefu akija, nao wakaambiana hivi: ‘Yule mwota-ndoto anakuja. Basi na tumuue!’ Hivyo, wakamchukua na kumtupa ndani ya shimo refu. Lakini Yuda, mmoja wa kaka zake, akasema hivi: ‘Msimuue! Badala yake, tumuuze akawe mtumwa.’ Kwa hiyo, wakamuuza Yosefu kwa wafanyabiashara Wamidiani waliokuwa wakielekea Misri kwa vipande 20 vya fedha.

      Kisha, kaka za Yosefu wakachovya vazi lake ndani ya damu ya mbuzi, wakalipeleka kwa baba yao na kusema: ‘Je, hili si vazi la mwanao?’ Hivyo, Yakobo alifikiri kwamba mnyama-mwitu alikuwa amemwua Yosefu. Yakobo alivunjika moyo sana. Hakuna mtu aliyeweza kumfariji.

      Yosefu akiwa gerezani

      Alipofika Misri, Yosefu aliuzwa akiwa mtumwa kwa ofisa mwenye cheo cha juu aliyeitwa Potifa. Lakini Yehova alikuwa pamoja na Yosefu. Potifa aliona kwamba Yosefu alifanya kazi vizuri na angeweza kumtumaini. Baada ya muda mfupi, Potifa alimweka Yosefu juu ya mali zake zote.

      Mke wa Potifa akatambua kwamba Yosefu alikuwa na sura ya kupendeza na mwenye umbo zuri. Siku baada siku alikuwa akimwambia Yosefu alale naye. Yosefu angefanya nini? Alikataa na kusema: ‘Hapana! Ni kosa kufanya hivyo. Bwana wangu ananitumaini, na wewe ni mke wake. Nikilala nawe, nitamtendea Mungu dhambi!’

      Siku moja, mke wa Potifa alijaribu kumlazimisha Yosefu alale naye. Alishika vazi lake, lakini Yosefu akakimbia. Potifa aliporudi nyumbani, mke wake alimwambia kwamba Yosefu alimshambulia. Alikuwa akisema uwongo. Potifa alikasirika sana na kumfunga Yosefu gerezani. Lakini Yehova hakumsahau Yosefu.

      “Kwa hiyo, jinyenyekezeni chini ya mkono wenye nguvu wa Mungu, ili awainue kwa wakati unaofaa.”​—1 Petro 5:6

      Maswali: Kaka za Yosefu walimtendeaje? Kwa nini Yosefu alifungwa gerezani?

      Mwanzo 37:1–36; 39:1-23; Matendo 7:9

  • Yehova Hakumsahau Yosefu Kamwe
    Masomo Unayoweza Kujifunza Katika Biblia
    • Yosefu anamwelezea Farao maana ya ndoto zake

      SOMO LA 15

      Yehova Hakumsahau Yosefu Kamwe

      Yosefu alipokuwa gerezani, Farao mfalme wa Misri aliota ndoto ambazo hakuna mtu aliyeweza kueleza maana yake. Mtumishi mmoja alimwambia Farao kwamba Yosefu angeweza kumweleza maana ya ndoto zake. Mara moja, Farao akaagiza Yosefu aletwe.

      Farao akamwuliza hivi: ‘Unaweza kunieleza maana ya ndoto zangu?’ Yosefu akamwambia Farao hivi: ‘Nchi ya Misri itakuwa na chakula kingi kwa miaka saba, lakini miaka saba itakayofuata kutakuwa na njaa. Chagua mtu mwenye hekima ahifadhi chakula ili watu wako wasife njaa.’ Farao akajibu hivi: ‘Ninakuchagua wewe! Utakuwa mtu wa pili kwa mamlaka nchini Misri!’ Yosefu alijuaje maana ya ndoto za Farao? Yehova alimsaidia Yosefu.

      Yosefu anawaagiza watu wahifadhi chakula

      Kwa miaka saba iliyofuata, Yosefu alihifadhi chakula. Na kama ambavyo Yosefu alikuwa amesema, kukawa na njaa duniani pote. Watu walitoka maeneo mbalimbali kuja kununua chakula kutoka kwa Yosefu. Yakobo, baba ya Yosefu, alisikia kwamba kuna chakula nchini Misri, kwa hiyo akawatuma wana wake kumi waende huko kununua chakula.

      Wana wa Yakobo walienda kwa Yosefu, naye akawatambua mara moja. Lakini wao hawakumtambua Yosefu. Wakamwinamia kama alivyokuwa ameota akiwa mdogo. Yosefu alitaka kujua ikiwa kaka zake bado walikuwa na chuki. Kwa hiyo, akawaambia hivi: ‘Ninyi ni wapelelezi. Mnataka kuchunguza udhaifu wa nchi yetu.’ Wakasema, ‘Hapana! Tulizaliwa kaka 12 nchini Kanaani. Ndugu yetu mmoja amekufa, na yule mdogo zaidi yuko na baba yetu.’ Kisha Yosefu akawaambia hivi: ‘Nileteeni ndugu yenu mdogo, nami nitawaamini.’ Kwa hiyo wakarudi nyumbani kwao.

      Chakula kilipoisha, Yakobo aliwatuma tena wana wake waende Misri. Pindi hii, walisafiri pamoja na Benjamini, ndugu yao mdogo. Ili kuwajaribu ndugu zake, Yosefu alificha kikombe cha fedha kwenye mfuko wa Benjamini na kusema kwamba walikuwa wamekiiba. Watumishi wa Yosefu walipopata kikombe hicho kwenye mfuko wa Benjamini, ndugu zake walishtuka. Wakamwomba Yosefu awaadhibu wao badala ya Benjamini.

      Sasa Yosefu akatambua kwamba ndugu zake walikuwa wamebadilika. Yosefu akashindwa kujizuia. Akabubujikwa na machozi na kusema hivi: ‘Mimi ni ndugu yenu, Yosefu. Je, baba yangu yuko hai?’ Ndugu zake walishangaa sana. Akawaambia hivi: ‘Msihuzunike kwa sababu ya kile mlichonifanyia. Mungu alinituma huku ili niwaokoe. Sasa harakisheni mwende mkamlete baba yangu.’

      Wakarudi nyumbani kumwambia baba yao habari hizo njema, na baadaye wakamleta Misri. Sasa Yosefu na baba yake wakakutana tena baada ya miaka mingi.

      Yosefu akimsalimu baba yake, Yakobo

      “Msipowasamehe watu makosa yao, naye Baba yenu hatawasamehe makosa yenu.”—Mathayo 6:15

      Maswali: Yehova alimsaidiaje Yosefu? Yosefu alionyeshaje kwamba alikuwa amewasamehe kaka zake?

      Mwanzo 40:1–45:28; 46:1-7, 26-34; Zaburi 105:17-19; Matendo 7:9-15

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki