Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Ayubu Alikuwa Nani?
    Masomo Unayoweza Kujifunza Katika Biblia
    • Wanaume watatu walikuja kumwona Ayubu ambaye alikuwa na majipu mwili mzima

      SOMO LA 16

      Ayubu Alikuwa Nani?

      Katika nchi ya Usi, kulikuwa na mtu aliyemwabudu Yehova. Aliitwa Ayubu. Alikuwa tajiri sana na alikuwa na familia kubwa. Alikuwa mwenye fadhili, aliwasaidia maskini, wanawake ambao waume zao walikuwa wamekufa, na watoto ambao hawakuwa na wazazi. Lakini, kwa sababu tu alifanya yaliyo sawa, je, hilo lilimaanisha kwamba hangepatwa na matatizo yoyote?

      Shetani Ibilisi

      Ayubu hakujua kwamba Shetani Ibilisi alikuwa akimchunguza. Yehova alimwambia hivi Shetani: ‘Je, umemwona mtumishi wangu Ayubu? Hakuna yeyote aliye kama yeye duniani. Ananisikiliza na kufanya mambo mazuri.’ Shetani akamjibu hivi: ‘Ni kweli kwamba Ayubu anakutii. Unamlinda na kumbariki. Umempa mali na mifugo. Ukichukua vitu hivyo vyote, ataacha kukuabudu.’ Yehova akasema hivi: ‘Unaweza kumjaribu Ayubu. Lakini usimwue.’ Kwa nini Yehova alimruhusu Shetani amjaribu Ayubu? Alikuwa na uhakika kwamba Ayubu angeendelea kuwa mwaminifu.

      Shetani alianza kumjaribu Ayubu kwa kumletea misiba mbalimbali. Kwanza, aliwatuma watu fulani walioitwa Wasabea waibe ng’ombe na punda za Ayubu. Kisha, moto ukawateketeza kondoo wote wa Ayubu. Watu wengine walioitwa Wakaldayo, wakaiba ngamia zake. Watumishi waliokuwa wakitunza mifugo hiyo, waliuawa. Kisha Ayubu akapata msiba mbaya zaidi. Watoto wote wa Ayubu walikufa walipoangukiwa na nyumba waliyokuwa wakifanyia sherehe. Ayubu alivunjika moyo, lakini hakuacha kumwabudu Yehova.

      Shetani alitaka Ayubu ateseke hata zaidi, kwa hiyo, akamletea Ayubu majipu mwili mzima. Ayubu alikuwa na maumivu makali sana. Hakujua kwa nini alikuwa akipatwa na mambo yote hayo. Hata hivyo, bado Ayubu aliendelea kumwabudu Yehova. Mungu aliona jinsi Ayubu alivyotenda na akafurahi sana.

      Kisha, Shetani akatuma wanaume watatu waende kumjaribu Ayubu. Walimwambia hivi: ‘Lazima uwe umefanya dhambi na unajaribu kuificha. Sasa Mungu anakuadhibu.’ Ayubu alisema hivi: ‘Sijafanya kosa lolote.’ Lakini akaanza kufikiri kwamba Yehova ndiye aliyemletea matatizo hayo, na akasema kwamba Mungu hakuwa akimtendea kwa haki.

      Kijana mmoja aliyeitwa Elihu alikuwa akisikiliza mazungumzo hayo kimyakimya. Kisha akasema hivi: ‘Mambo yote mliyosema si ya kweli. Yehova ni mkuu kuliko tunavyoweza kufikiri. Hawezi kamwe kufanya mambo maovu. Anaona kila jambo, naye huwasaidia watu wanapokuwa na matatizo.’

      Ayubu pamoja na mke wake na mtoto mchanga

      Kisha Yehova akazungumza na Ayubu na kumwambia hivi: ‘Ulikuwa wapi nilipokuwa nikiumba mbingu na dunia? Kwa nini unasema kwamba sitendi kwa haki? Unazungumza, lakini hujui kwa nini mambo fulani hutukia.’ Ayubu alikubali kosa lake na kusema hivi: ‘Nilikosea. Nilisikia habari zako, lakini sasa nimekujua. Hakuna jambo lolote linaloweza kukushinda. Ninaomba msamaha kwa mambo niliyosema.’

      Majaribu yake yalipoisha, Yehova alimponya Ayubu na kumpa mali nyingi kuliko zile alizokuwa nazo mwanzoni. Ayubu aliishi kwa miaka mingi akiwa mwenye furaha. Yehova alimbariki Ayubu kwa sababu ya kumtii hata ilipokuwa vigumu kufanya hivyo. Je, utamwiga Ayubu kwa kuendelea kumwabudu Yehova hata inapokuwa vigumu kufanya hivyo?

      “Mmesikia kuhusu uvumilivu wa Ayubu na mmeona matokeo ambayo Yehova alileta.”​—Yakobo 5:11

      Maswali: Shetani alimjaribu Ayubu jinsi gani? Yehova alimbariki Ayubu jinsi gani?

      Ayubu 1:1–3:26; 4:7; 32:1-5; 34:5, 21; 35:2; 36:15, 26; 38:1-7; 40:8; 42:1-17

  • Musa Aliamua Kumwabudu Yehova
    Masomo Unayoweza Kujifunza Katika Biblia
    • Binti ya Farao anampata mtoto Musa huku Miriamu akiwatazama kwa karibu

      SOMA 17

      Musa Aliamua Kumwabudu Yehova

      Katika nchi ya Misri, watu wa familia ya Yakobo walikuja kuitwa Waisraeli. Baada ya Yakobo na Yosefu kufa, Farao mwingine alianza kutawala. Aliogopa kwamba Waisraeli wangekuwa wengi na hivyo kuwa na nguvu kuliko Wamisri. Kwa hiyo, Farao huyo aliwafanya Waisraeli kuwa watumwa. Aliwalazimisha kutengeneza matofali na kufanya kazi ngumu kwenye mashamba. Lakini kadiri Wamisri walivyowalazimisha wafanye kazi ngumu, ndivyo walivyozidi kuongezeka. Kwa kuwa Farao hakufurahia jambo hilo, aliagiza wavulana wote Waisraeli wauawe mara tu wanapozaliwa. Je, unaweza kuwazia jinsi Waisraeli walivyoogopa?

      Mwanamke Mwisraeli aliyeitwa Yokebedi, alijifungua mtoto wa kiume mwenye sura nzuri. Kwa sababu alitaka kumwokoa, aliamua kumweka ndani ya kikapu, na kumficha kwenye matete yaliyo kandokando ya Mto Nile. Miriamu, dada ya mtoto huyo, alikaa karibu ili aone kitakachotokea.

      Binti ya Farao alienda kuoga mtoni na akaona kikapu hicho. Ndani ya kikapu hicho, aliona mtoto akilia, naye akamsikitikia. Miriamu akamwuliza: ‘Ungependa nikutafutie mwanamke atakayemnyonyesha mtoto huyu kwa niaba yako?’ Binti ya Farao alipokubali, Miriamu akamleta Yokebedi, mama yake. Binti ya Farao akamwambia hivi: ‘Mchukue mtoto huyu uninyonyeshee, halafu nitakulipa.’

      Musa akikimbia

      Mtoto alipokuwa mkubwa, Yokebedi akamleta kwa binti ya Farao, naye akamwita Musa na kumlea kama mtoto wake. Musa alilelewa kama mtoto wa mfalme na angeweza kupata chochote alichotaka. Lakini Musa hakumsahau Yehova. Alijua kwamba yeye alikuwa Mwisraeli, si Mmisri. Na aliamua kumtumikia Yehova.

      Alipokuwa na umri wa miaka 40, Musa aliamua kuwasaidia Waisraeli wenzake. Alipomwona Mmisri akimpiga mtumwa Mwisraeli, Musa alimpiga kwa nguvu Mmisri huyo na kumuua. Halafu akamficha ndani ya mchanga. Farao alipogundua jambo hilo, alijaribu kumuua Musa. Lakini Musa akakimbilia nchi ya Midiani. Yehova alimtunza alipokuwa huko.

      “Kwa imani, Musa . . alikataa kuitwa mwana wa binti ya Farao, akachagua kuteswa pamoja na watu wa Mungu.”​—Waebrania 11:24, 25

      Maswali: Waisraeli walitendewaje walipokuwa Misri? Kwa nini Musa alikimbia kutoka Misri?

      Mwanzo 49:33; Kutoka 1:1-14, 22; 2:1-15; Matendo 7:17-29; Waebrania 11:23-27

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki