-
Kichaka Kinachowaka MotoMasomo Unayoweza Kujifunza Katika Biblia
-
-
SOMO LA 18
Kichaka Kinachowaka Moto
Musa aliishi Midiani kwa miaka 40. Alioa na kupata watoto. Siku moja alipokuwa akichunga kondoo karibu na Mlima Sinai, aliona kitu chenye kustaajabisha. Kichaka kilikuwa kikiwaka moto lakini hakikuteketea! Alipokikaribia ili aone kwa nini hakikuwa kikiteketea, alisikia sauti kutoka kwenye kichaka hicho ikisema: ‘Musa! Usikaribie zaidi. Vua viatu vyako kwa sababu mahali ambapo umesimama ni ardhi takatifu.’ Yehova ndiye aliyekuwa akizungumza kupitia malaika.
Musa aliogopa, kwa hiyo akauficha uso wake. Sauti hiyo ilisema hivi: ‘Nimeyaona mateso ya Waisraeli. Nitawakomboa kutoka kwa Wamisri na kuwapeleka kwenye nchi nzuri. Wewe ndiye utakayewaongoza watu wangu kutoka Misri.’ Je, unafikiri jambo hilo lilimshangaza Musa?
Musa akauliza hivi: ‘Watu wakiniuliza ni nani aliyenituma, niwaambie nini?’ Mungu akamjibu hivi: ‘Waambie kwamba Yehova, Mungu wa Abrahamu, Mungu wa Isaka, na Mungu wa Yakobo amekutuma.’ Kisha Musa akasema hivi: ‘Vipi ikiwa watu hao hawatanisikiliza?’ Yehova alimpa Musa uthibitisho kwamba atamsaidia. Alimwambia Musa atupe fimbo yake chini, nayo ikawa nyoka! Musa alipomkamata nyoka huyo kwenye mkia, akageuka kuwa fimbo. Yehova akasema hivi: ‘Ukiwafanyia muujiza huu, utathibitisha kwamba nimekutuma.’
Musa akasema: ‘Mimi si msemaji mzuri.’ Yehova akamwahidi hivi: ‘Nitakufundisha mambo unayopaswa kusema, nami nitamtuma Haruni, ndugu yako, ili akusaidie.’ Akiwa na uhakika kwamba Yehova alikuwa pamoja naye, Musa akamchukua mke na watoto wake, na kurudi Misri.
“Msihangaike kuhusu jambo mtakalosema au jinsi mtakavyolisema, kwa sababu mtapewa jambo la kusema katika saa hiyo.”—Mathayo 10:19
-
-
Mapigo Matatu ya KwanzaMasomo Unayoweza Kujifunza Katika Biblia
-
-
SOMO LA 19
Mapigo Matatu ya Kwanza
Waisraeli walilazimishwa kufanya kazi ngumu wakiwa watumwa. Yehova aliwatuma Musa na Haruni wamwambie hivi Farao: ‘Waruhusu watu wangu waondoke ili wakaniabudu huko nyikani.’ Kwa kiburi, Farao akasema hivi: ‘Mimi sijali Yehova anasema nini, na sitawaruhusu Waisraeli waondoke.’ Kisha Farao akawalazimisha wafanye kazi ngumu hata zaidi. Yehova angemfundisha Farao somo. Unajua alifanya nini? Alileta Mapigo Kumi juu ya Misri. Yehova alimwambia hivi Musa: ‘Farao amekataa kunisikiliza. Kesho asubuhi atakuwa kwenye Mto Nile. Nenda ukamwambie, kwa kuwa amekataa kuwaruhusu watu wangu waondoke, maji yote ya Mto Nile yatageuka kuwa damu.’ Musa alitii na akaenda kwa Farao. Farao alimwona Haruni akipiga maji ya Mto Nile kwa fimbo yake, nayo yakageuka kuwa damu. Samaki wakafa, mto ukaanza kunuka, na hakukuwa na maji safi ya kunywa kutoka kwenye Mto Nile. Lakini bado Farao alikataa kuwaruhusu Waisraeli waondoke.
Baada ya siku saba, Yehova alimtuma tena Musa kwa Farao akamwambie hivi: ‘Usipowaruhusu watu wangu waondoke, vyura watajaa katika nchi yote ya Misri.’ Haruni akainua fimbo yake na vyura wakaanza kujaa na kuifunika nchi. Kulikuwa na vyura katika nyumba za watu, vitandani, na kwenye vyombo. Vyura walikuwa kila mahali! Farao alimwambia Musa amwombe Yehova akomeshe pigo hilo. Akaahidi kwamba angewaruhusu Waisraeli waende. Kisha Yehova akakomesha pigo hilo, na Wamisri wakawakusanya vyura hao mafungu-mafungu. Nayo nchi ikaanza kunuka. Lakini kwa mara nyingine tena, Farao hakuwaruhusu Waisraeli waondoke.
Baada ya hapo, Yehova akamwambia Musa hivi: ‘Mwambie Haruni apige mavumbi ya dunia kwa fimbo yake, nayo yatakuwa mbu, au wadudu wadogo wanaouma.’ Papo hapo, mbu wakajaa kila mahali. Baadhi ya watu wa Farao walimwambia hivi: ‘Pigo hili limetoka kwa Mungu.’ Lakini bado Farao hakuwaruhusu Waisraeli waondoke.
“Nitawafanya wajue nguvu zangu na uwezo wangu, nao watalazimika kujua kwamba jina langu ni Yehova.”—Yeremia 16:21
-