-
Mapigo Sita YaliyofuataMasomo Unayoweza Kujifunza Katika Biblia
-
-
SOMO LA 20
Mapigo Sita Yaliyofuata
Musa na Haruni walienda kumwambia Farao ujumbe huu kutoka kwa Mungu: ‘Ikiwa hutawaruhusu watu wangu waende zao, nitatuma nzi juu ya nchi yako.’ Makundi makubwa ya nzi yakaanza kuvamia nyumba za Wamisri, matajiri kwa maskini. Nchi yote ikajaa nzi. Lakini katika eneo la Gosheni, ambako Waisraeli walikuwa wanaishi, hakukuwa na nzi. Pigo la nne na yale yaliyofuata yaliwapata Wamisri peke yao. Farao akamsihi hivi Musa: ‘Mwombe Yehova kwa niaba yangu aondoe nzi hao, kisha watu wako wanaweza kuondoka.’ Hata hivyo, Yehova alipowaondoa nzi, Farao alibadili mawazo yake. Unafikiri Farao angejifunza kutii?
Yehova alisema hivi: ‘Ikiwa Farao ataendelea kukataa kuwaruhusu watu wangu waende zao, mifugo ya Wamisri itapatwa na ugonjwa na kufa.’ Siku iliyofuata, mifugo ikaanza kufa. Lakini mifugo ya Waisraeli haikufa. Lakini bado Farao aliendelea kuwa na moyo mgumu na hakutaka kuwaruhusu waondoke.
Kisha Yehova akamwambia Musa arudi kwa Farao na kurusha majivu angani. Majivu hayo yakawa vumbi na kujaza nchi yote na kuwafunika Wamisri. Mavumbi hayo yakasababisha majipu juu ya Wamisri na wanyama wao wote. Ingawa hivyo, Farao alikataa kuwaruhusu Waisraeli waondoke.
Yehova akamtuma tena Musa kwa Farao amwambie hivi: ‘Bado unakataa kuwaruhusu watu wangu waondoke? Kesho mvua kubwa sana ya mawe itanyesha juu ya nchi.’ Siku iliyofuata, Yehova akafanya mvua kubwa ya mawe inyeshe, pia kukawa na ngurumo, na moto. Wamisri hawakuwa wamewahi kuona mvua kubwa kama hiyo. Miti yote na mimea iliharibiwa isipokuwa katika eneo la Gosheni. Farao akasema: ‘Msihi Yehova ili mvua iache kunyesha! Kisha nitawaruhusu mwende.’ Hata hivyo, mara tu mvua ilipoacha kunyesha, Farao alibadili mawazo yake tena.
Kisha Musa akasema hivi: ‘Sasa nzige watakula mimea yote iliyobaki baada ya mvua ya mawe kunyesha.’ Makundi ya nzige wengi wakala kila kitu kilichobaki shambani na kwenye miti. Farao akamsihi Musa hivi: ‘Mwombe Yehova awaondoe nzige hawa.’ Lakini hata baada ya Yehova kuwaondoa nzige, bado Farao aliendelea kuwa na moyo mgumu.
Yehova akamwambia Musa hivi: ‘Nyoosha mkono wako kuelekea angani.’ Papo hapo, giza zito likatokea katika nchi yote. Kwa siku tatu, Wamisri hawakuweza kuona kitu chochote. Waisraeli tu ndio waliokuwa na mwangaza katika nyumba zao.
Farao akamwambia Musa: ‘Wewe na watu wako mnaweza kwenda. Lakini waacheni wanyama wenu.’ Musa akasema: ‘Lazima twende na wanyama ili tukamtolee Mungu wetu dhabihu.’ Farao alikasirika sana. Akamwambia hivi Musa kwa hasira: ‘Toka hapa! Nikikuona tena nitakuua!’
“Nanyi mtaona tena tofauti kati ya mtu mwadilifu na mtu mwovu, kati ya yule anayemtumikia Mungu na yule asiyemtumikia.”—Malaki 3:18
-
-
Pigo la KumiMasomo Unayoweza Kujifunza Katika Biblia
-
-
SOMO LA 21
Pigo la Kumi
Musa alimwahidi Farao kwamba hangeenda kumwona tena. Lakini kabla hajaondoka, alimwambia Farao hivi: ‘Katikati ya usiku, kila mzaliwa wa kwanza nchini Misri, kuanzia mzaliwa wa kwanza wa Farao mpaka mzaliwa wa kwanza wa watumwa, atakufa.’
Yehova aliwaambia Waisraeli watayarishe mlo wa pekee. Alisema hivi: ‘Chinjeni kondoo dume au mbuzi wa mwaka mmoja, kisha mpake damu yake kwenye mlango wa nyumba zenu. Chomeni nyama hiyo na kuila pamoja na mkate usiotiwa chachu. Vaeni nguo na viatu na muwe tayari kuondoka. Nitawakomboa usiku wa leo.’ Hebu wazia jinsi Waisraeli walivyofurahi!
Katikati ya usiku, malaika wa Yehova alienda katika kila nyumba nchini Misri. Mzaliwa wa kwanza katika nyumba yoyote ambayo haikuwa imepakwa damu mlangoni, alikufa. Lakini malaika huyo alipita nyumba zilizokuwa zimepakwa damu. Kila mzaliwa wa kwanza alikufa katika familia zote nchini Misri, iwe ni za matajiri au maskini. Lakini hakuna mtoto hata mmoja wa Mwisraeli aliyekufa.
Hata mwana wa Farao mwenyewe alikufa. Farao hangeweza kuvumilia tena. Papo hapo akawaambia Musa na Haruni hivi: ‘Simameni. Ondokeni hapa. Nendeni mkamwabudu Mungu wenu. Chukueni wanyama wenu na mwende!’
Usiku huo, kukiwa na mwezi mpevu, Waisraeli waliondoka Misri wakiwa wamepangwa kulingana na familia na makabila yao. Kulikuwa na wanaume Waisraeli 600,000, pamoja na wanawake wengi na watoto. Pia, watu wengine wengi waliambatana nao ili wamwabudu Yehova. Hatimaye, Waisraeli walikuwa huru!
Ili kukumbuka jinsi ambavyo Yehova aliwakomboa, kila mwaka wangetayarisha mlo huo wa pekee. Mlo huo uliitwa Pasaka.
“Kwa sababu hii nimekuacha ubaki: ili nionyeshe nguvu zangu kuhusiana na wewe na ili jina langu litangazwe katika dunia yote.”—Waroma 9:17
-