-
Walivunja Ahadi YaoMasomo Unayoweza Kujifunza Katika Biblia
-
-
SOMO LA 24
Walivunja Ahadi Yao
Yehova alimwambia Musa hivi: ‘Njoo kwangu juu mlimani. Nitaandika sheria yangu juu ya mabamba ya mawe halafu nitakupa.’ Musa akapanda juu mlimani na kukaa huko kwa siku 40. Alipokuwa huko, Yehova akaandika zile Amri Kumi juu ya mabamba mawili ya mawe na kumpa Musa mabamba hayo.
Baada ya muda, Waisraeli wakafikiri kwamba Musa alikuwa amewaacha. Wakamwambia Haruni hivi: ‘Tunataka mtu wa kutuongoza. Tutengenezee mungu!’ Haruni akasema: ‘Nipeni dhahabu yenu.’ Akaiyeyusha dhahabu na kuifanya kuwa sanamu ya ndama. Watu wakasema hivi: ‘Huyu ndiye Mungu aliyetutoa Misri.’ Wakaanza kuabudu ndama huyo wa dhahabu na wakafanya sherehe. Je, hilo lilikuwa kosa? Ndiyo, kwa kuwa watu hao walikuwa wameahidi kumtumikia Yehova peke yake. Lakini sasa walikuwa wanavunja ahadi hiyo.
Yehova aliona kilichokuwa kikitendeka, naye akamwambia Musa hivi: ‘Shuka urudi kwa watu. Wameacha kunitii na wanaabudu mungu wa uwongo.’ Musa akashuka haraka kutoka mlimani, akiwa amebeba yale mabamba mawili.
Alipoikaribia kambi, Musa akawasikia watu wakiimba. Kisha akawaona wakicheza dansi na kuiinamia sanamu ya ndama. Musa akakasirika sana. Akatupa yale mabamba mawili chini, nayo yakavunjika vipande-vipande. Akaiharibu sanamu hiyo mara moja. Kisha akamuuliza Haruni hivi: ‘Watu hawa walikuambia nini ili ukubali kufanya jambo hili baya?’ Haruni akasema: ‘Usikasirike. Wewe unajua jinsi watu hawa walivyo. Walitaka niwatengenezee mungu, kwa hiyo nikatupa dhahabu yao ndani ya moto na sanamu hiyo ya ndama ikatokea!’ Haruni hakupaswa kufanya hivyo. Musa akarudi juu mlimani na kumsihi Yehova awasamehe watu hao.
Yehova aliwasamehe wale waliokuwa tayari kumtii. Je, umeona kwa nini ilikuwa muhimu kwa Waisraeli kufuata uongozi wa Musa?
“Wakati wowote unapoweka nadhiri kwa Mungu, usikawie kuitimiza, kwa maana hapendezwi na wapumbavu. Unapoweka nadhiri, itimize.”—Mhubiri 5:4
-
-
Maskani ya IbadaMasomo Unayoweza Kujifunza Katika Biblia
-
-
SOMO LA 25
Maskani ya Ibada
Musa alipokuwa kwenye Mlima Sinai, Yehova alimwambia ajenge hema la pekee linaloitwa maskani, ambapo Waisraeli wangemwabudu Mungu. Wangeweza kuibeba maskani waliposafiri.
Yehova alisema hivi: ‘Waambie watu watoe michango ya kujenga maskani.’ Waisraeli wakatoa dhahabu, fedha, shaba, mawe yenye thamani, na vito. Pia, walitoa sufu, vitambaa vya kitani, ngozi za wanyama, na vitu vingine vingi. Walitoa kwa ukarimu sana hivi kwamba Musa akalazimika kuwaambia hivi: ‘Tumepata michango ya kutosha! Msilete zaidi.’
Wanaume na wanawake wengi wenye ustadi walisaidia kujenga maskani. Yehova aliwapa hekima ili waweze kufanya kazi hiyo. Wengine walisokota nyuzi, wakatengeneza mavazi, au wakafanya kazi ya kutarizi. Wengine walifanya kazi kwa kutumia mawe, dhahabu, na mbao.
Watu wakajenga maskani kama tu Yehova alivyokuwa amewaambia. Wakaweka pazia maridadi ili kutenganisha maskani katika sehemu mbili, Patakatifu na Patakatifu Zaidi. Katika Patakatifu Zaidi kulikuwa na sanduku la agano lililotengenezwa kwa mbao za mshita na dhahabu. Katika Patakatifu kulikuwa na kinara cha taa cha dhahabu, meza, na madhabahu ya kufukiza uvumba. Katika ua kulikuwa na beseni ya shaba na madhabahu kubwa. Sanduku la agano liliwakumbusha Waisraeli kuhusu ahadi yao ya kumtii Yehova. Je, unajua agano ni nini? Ni ahadi ya pekee sana.
Yehova aliwachagua Haruni na wanawe wafanye kazi kwenye maskani wakiwa makuhani. Walipaswa kuitunza na kumtolea Yehova dhabihu. Ni Haruni peke yake ambaye aliruhusiwa kuingia Patakatifu Zaidi kwa kuwa yeye ndiye aliyekuwa kuhani mkuu. Aliingia humo mara moja kwa mwaka ili kutoa dhabihu kwa ajili ya dhambi zake, dhambi za familia yake, na dhambi za taifa lote la Israeli.
Waisraeli walikamilisha ujenzi wa maskani mwaka mmoja baada ya kutoka Misri. Sasa walikuwa na mahali pa kumwabudu Yehova.
Yehova akaijaza maskani utukufu wake na akafanya wingu litande juu yake. Wingu lilipoendelea kukaa juu ya maskani, Waisraeli hawakuondoka mahali walipokuwa wamepiga kambi. Lakini wingu lilipoinuka, walijua ni wakati wa kuondoka. Wangebomoa maskani na kufuata wingu hilo.
“Ndipo nikasikia sauti kubwa kutoka katika kile kiti cha ufalme ikisema: ‘Tazama! Hema la Mungu liko pamoja na wanadamu, naye atakaa pamoja nao, nao watakuwa watu wake. Na Mungu mwenyewe atakuwa pamoja nao.’”—Ufunuo 21:3
-