-
Wale Wapelelezi Kumi na WawiliMasomo Unayoweza Kujifunza Katika Biblia
-
-
SOMO LA 26
Wale Wapelelezi Kumi na Wawili
Waisraeli waliondoka Mlima Sinai na kusafiri kwenye nyika ya Parani hadi eneo linaloitwa Kadeshi. Wakiwa huko, Yehova akamwambia Musa hivi: ‘Tuma watu 12, mmoja kutoka kila kabila, wakaipeleleze nchi ya Kanaani, nchi nitakayowapa Waisraeli.’ Kwa hiyo, Musa akachagua watu 12 na kuwaambia hivi: ‘Nendeni kwenye nchi ya Kanaani mkachunguze kama inafaa kwa ajili ya kupanda chakula. Angalieni kama watu wa nchi hiyo ni dhaifu au wana nguvu na kama wanaishi katika mahema au majiji.’ Wapelelezi hao 12, kutia ndani Yoshua na Kalebu, wakaenda Kanaani.
Baada ya siku 40, wapelelezi hao wakarudi, wakiwa na tini, makomamanga, na zabibu. Wapelelezi hao wakasema hivi: ‘Ni nchi nzuri, lakini watu wanaokaa katika nchi hiyo ni wenye nguvu na majiji yake yana kuta ndefu sana.’ Naye Kalebu akasema hivi: ‘Tunaweza kuwashinda. Twendeni mara moja!’ Je, unajua kwa nini Kalebu alisema hivyo? Ni kwa sababu yeye na Yoshua walimtegemea Yehova. Lakini wale wapelelezi wengine kumi wakasema: ‘Hapana! Watu hao ni wakubwa sana, kama majitu! Sisi tulikuwa kama panzi tulipojilinganisha nao.’
Waisraeli walivunjika moyo. Wakaanza kulalamika na kuambiana hivi: ‘Tuchague kiongozi mwingine ili turudi Misri. Kwa nini twende kwenye nchi hiyo halafu tuuawe?’ Yoshua na Kalebu wakasema hivi: ‘Msimwasi Yehova, wala msiogope. Yehova atatulinda.’ Lakini Waisraeli hawakusikiliza. Hata walitaka kuwaua Yoshua na Kalebu!
Yehova alifanya nini? Alimwambia Musa hivi: ‘Ingawa nimewafanyia Waisraeli mambo mengi, bado hawanitii. Kwa sababu hiyo watakaa katika nyika hii kwa miaka 40, nao watakufa hapa. Watoto wao, Yoshua, na Kalebu ndio tu watakaoishi katika nchi niliyoahidi kuwapa.’
“Kwa nini mnaogopa sana, ninyi wenye imani ndogo?”—Mathayo 8:26
-
-
Walimwasi YehovaMasomo Unayoweza Kujifunza Katika Biblia
-
-
SOMO LA 27
Walimwasi Yehova
Muda fulani baadaye Waisraeli walipokuwa bado nyikani, Kora, Dathani, Abiramu, na watu wengine 250 walimwasi Musa. Walimwambia hivi: ‘Imetosha! Kwa nini wewe uwe kiongozi wetu na Haruni awe kuhani mkuu? Yehova yuko katikati yetu sisi sote, si wewe na Haruni tu.’ Jambo hilo halikumfurahisha Yehova. Aliona kwamba walikuwa wakimwasi yeye!
Musa akamwambia Kora na watu waliokuwa wakimuunga mkono hivi: ‘Kesho njooni kwenye maskani, na mje na vyetezo vilivyojaa uvumba. Yehova atatuonyesha amemchagua nani.’
Siku iliyofuata, Kora na wale wanaume 250 wakaenda kukutana na Musa kwenye maskani. Wakafukiza uvumba kana kwamba wao walikuwa makuhani. Yehova akamwambia Musa na Haruni: ‘Jitengeni na Kora na wanaume hawa.’
Ingawa Kora alikuwa ameenda kukutana na Musa kwenye maskani, Dathani, Abiramu, na familia zao walikataa kwenda. Yehova akawaambia Waisraeli wajitenge na mahema ya Kora, Dathani, na Abiramu. Mara moja, Waisraeli wakajitenga nao. Dathani, Abiramu, na familia zao wakasimama nje ya mahema yao. Ghafla nchi ikapasuka na kuwameza! Kwenye maskani, moto ukashuka na kumteketeza Kora na wale wanaume 250 waliokuwa pamoja naye.
Kisha Yehova akamwambia Musa hivi: ‘Chukua fimbo moja kutoka kwa kiongozi wa kila kabila, na uandike jina lake juu ya fimbo hiyo. Lakini kwenye fimbo ya kabila la Lawi, uandike jina la Haruni. Uziweke ndani ya maskani, na fimbo ya mtu nitakayemchagua itachipuka maua.’
Siku iliyofuata, Musa akatoa nje fimbo zote na kuwaonyesha viongozi. Fimbo ya Haruni ilikuwa na maua yanayomea na lozi zilizoiva. Kwa njia hiyo, Yehova akathibitisha kwamba alikuwa amemchagua Haruni kuwa kuhani mkuu.
“Watiini wale wanaoongoza kati yenu na mnyenyekee.”—Waebrania 13:17
-