Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Rahabu Awaficha Wapelelezi
    Masomo Unayoweza Kujifunza Katika Biblia
    • Rahabu anawalinda wapelelezi kwa kuwaelekeza askari upande mwingine

      SOMO LA 30

      Rahabu Awaficha Wapelelezi

      Wapelelezi Waisraeli walipoenda kwenye jiji la Yeriko, walikaa katika nyumba ya mwanamke aliyeitwa Rahabu. Mfalme wa Yeriko akatambua jambo hilo na kuwatuma askari kwenye nyumba ya Rahabu. Lakini Rahabu akawaficha wapelelezi hao wawili kwenye dari la nyumba yake na kuwaelekeza askari upande mwingine. Kisha Rahabu akawaambia wapelelezi hao hivi: ‘Nitawasaidia kwa sababu ninajua kwamba Yehova yuko upande wenu na kwamba mtaishinda nchi hii. Tafadhali mniahidi kwamba mtaiokoa familia yangu.’

      Wapelelezi wakamwambia Rahabu hivi: ‘Tunaahidi kwamba hakuna mtu ndani ya nyumba yako atakayeumia.’ Walimwambia hivi: ‘Funga kamba nyekundu dirishani, na watu wa familia yako wataokolewa.’

      Nyumba ya Rahabu, ikiwa na kamba nyekundu iliyofungwa dirishani, inaendelea kusimama huku kuta za Yeriko zikianguka

      Rahabu akawashusha wapelelezi hao kwa kamba kupitia dirisha lake. Wakaenda milimani na kujificha kwa siku tatu kabla ya kurudi kwa Yoshua. Kisha Waisraeli wakavuka Mto Yordani na kujitayarisha kuishinda nchi. Yeriko lilikuwa jiji la kwanza walilolishinda. Yehova aliwaambia walizunguke jiji mara moja kila siku kwa siku sita. Siku ya saba, walilizunguka jiji mara saba. Kisha makuhani wakapiga tarumbeta, nao askari wakapaaza sauti kwa kelele kadiri walivyoweza. Kuta za jiji hilo zikaanguka chini! Lakini nyumba ya Rahabu, ambayo ilikuwa kwenye ukuta, ikaendelea kusimama. Rahabu na familia yake wakaokolewa kwa sababu alimtegemea Yehova.

      “Vivyo hivyo, je, Rahabu . . . hakutangazwa pia kuwa mwadilifu kwa matendo, baada ya kuwakaribisha wale wajumbe na kuwatoa nje kupitia njia nyingine?”​—Yakobo 2:25

      Maswali: Kwa nini Rahabu aliwasaidia wapelelezi? Waisraeli walishambuliaje jiji la Yeriko? Ni nini kilichompata Rahabu na familia yake?

      Yoshua 2:1-24; 6:1-27; Waebrania 11:30, 31; Yakobo 2:24-26

  • Yoshua na Wagibeoni
    Masomo Unayoweza Kujifunza Katika Biblia
    • Wagibeoni walimwendea Yoshua na jeshi lake wakiwa wamevalia mavazi yaliyochakaa

      SOMO LA 31

      Yoshua na Wagibeoni

      Habari kuhusu kuanguka kwa Yeriko zilienea katika mataifa mengine ya Kanaani. Wafalme wao wakaamua kuungana ili wapigane na Waisraeli. Lakini Wagibeoni wakaamua kufanya jambo tofauti. Wakiwa wamevalia mavazi yaliyochakaa wakamwendea Yoshua na kusema hivi: ‘Tumetoka nchi ya mbali sana. Tumesikia kumhusu Yehova na yote aliyowafanyia mlipokuwa Misri na Moabu. Tunaomba mtuahidi kwamba hamtatushambulia, nasi tutakuwa watumishi wenu.’

      Yoshua aliwaamini na akawaahidi kwamba hatawashambulia. Siku tatu baadaye, akagundua kwamba hawakuwa wametoka nchi ya mbali. Walikuwa wakaaji wa nchi ya Kanaani. Yoshua akawauliza Wagibeoni hivi: ‘Kwa nini mlitudanganya?’ Wakamjibu: ‘Tuliogopa! Tunajua kwamba Yehova Mungu wenu anawapigania. Tafadhali msituue.’ Yoshua akatimiza ahadi yake na kuwaacha waendelee kuishi.

      Baada ya muda mfupi, wafalme watano Wakanaani na majeshi yao wakatishia kuwashambulia Wagibeoni. Yoshua na jeshi lake wakatembea usiku mzima ili kuwaokoa Wagibeoni. Vita vikaanza mapema asubuhi siku iliyofuata. Wakanaani wakaanza kukimbia kuelekea pande zote. Kila mahali walipokimbilia Yehova aliangusha mvua ya mawe makubwa juu yao. Kisha Yoshua akamwomba Yehova alifanye jua lisimame tuli. Kwa nini Yoshua amwombe Yehova afanye hivyo wakati jua halikuwahi kusimama tuli kabla ya hapo? Kwa sababu Yoshua alimwamini Yehova. Jua halikutua kwa siku nzima hadi Waisraeli walipowashinda wafalme Wakanaani na majeshi yao.

      Yoshua anatazama juu mbinguni na kumwomba Yehova afanye jua lisimame tuli

      “‘Ndiyo’ yenu imaanishe ndiyo, na ‘Siyo’ yenu, siyo, kwa maana linalozidi hayo linatoka kwa yule mwovu.”​—Mathayo 5:37

      Maswali: Wagibeoni walifanya nini ili kujilinda? Yehova aliwasaidiaje Waisraeli?

      Yoshua 9:1–10:15

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki