-
Rahabu Awaficha WapeleleziMasomo Unayoweza Kujifunza Katika Biblia
-
-
SOMO LA 30
Rahabu Awaficha Wapelelezi
Wapelelezi Waisraeli walipoenda kwenye jiji la Yeriko, walikaa katika nyumba ya mwanamke aliyeitwa Rahabu. Mfalme wa Yeriko akatambua jambo hilo na kuwatuma askari kwenye nyumba ya Rahabu. Lakini Rahabu akawaficha wapelelezi hao wawili kwenye dari la nyumba yake na kuwaelekeza askari upande mwingine. Kisha Rahabu akawaambia wapelelezi hao hivi: ‘Nitawasaidia kwa sababu ninajua kwamba Yehova yuko upande wenu na kwamba mtaishinda nchi hii. Tafadhali mniahidi kwamba mtaiokoa familia yangu.’
Wapelelezi wakamwambia Rahabu hivi: ‘Tunaahidi kwamba hakuna mtu ndani ya nyumba yako atakayeumia.’ Walimwambia hivi: ‘Funga kamba nyekundu dirishani, na watu wa familia yako wataokolewa.’
Rahabu akawashusha wapelelezi hao kwa kamba kupitia dirisha lake. Wakaenda milimani na kujificha kwa siku tatu kabla ya kurudi kwa Yoshua. Kisha Waisraeli wakavuka Mto Yordani na kujitayarisha kuishinda nchi. Yeriko lilikuwa jiji la kwanza walilolishinda. Yehova aliwaambia walizunguke jiji mara moja kila siku kwa siku sita. Siku ya saba, walilizunguka jiji mara saba. Kisha makuhani wakapiga tarumbeta, nao askari wakapaaza sauti kwa kelele kadiri walivyoweza. Kuta za jiji hilo zikaanguka chini! Lakini nyumba ya Rahabu, ambayo ilikuwa kwenye ukuta, ikaendelea kusimama. Rahabu na familia yake wakaokolewa kwa sababu alimtegemea Yehova.
“Vivyo hivyo, je, Rahabu . . . hakutangazwa pia kuwa mwadilifu kwa matendo, baada ya kuwakaribisha wale wajumbe na kuwatoa nje kupitia njia nyingine?”—Yakobo 2:25
-
-
Yoshua na WagibeoniMasomo Unayoweza Kujifunza Katika Biblia
-
-
SOMO LA 31
Yoshua na Wagibeoni
Habari kuhusu kuanguka kwa Yeriko zilienea katika mataifa mengine ya Kanaani. Wafalme wao wakaamua kuungana ili wapigane na Waisraeli. Lakini Wagibeoni wakaamua kufanya jambo tofauti. Wakiwa wamevalia mavazi yaliyochakaa wakamwendea Yoshua na kusema hivi: ‘Tumetoka nchi ya mbali sana. Tumesikia kumhusu Yehova na yote aliyowafanyia mlipokuwa Misri na Moabu. Tunaomba mtuahidi kwamba hamtatushambulia, nasi tutakuwa watumishi wenu.’
Yoshua aliwaamini na akawaahidi kwamba hatawashambulia. Siku tatu baadaye, akagundua kwamba hawakuwa wametoka nchi ya mbali. Walikuwa wakaaji wa nchi ya Kanaani. Yoshua akawauliza Wagibeoni hivi: ‘Kwa nini mlitudanganya?’ Wakamjibu: ‘Tuliogopa! Tunajua kwamba Yehova Mungu wenu anawapigania. Tafadhali msituue.’ Yoshua akatimiza ahadi yake na kuwaacha waendelee kuishi.
Baada ya muda mfupi, wafalme watano Wakanaani na majeshi yao wakatishia kuwashambulia Wagibeoni. Yoshua na jeshi lake wakatembea usiku mzima ili kuwaokoa Wagibeoni. Vita vikaanza mapema asubuhi siku iliyofuata. Wakanaani wakaanza kukimbia kuelekea pande zote. Kila mahali walipokimbilia Yehova aliangusha mvua ya mawe makubwa juu yao. Kisha Yoshua akamwomba Yehova alifanye jua lisimame tuli. Kwa nini Yoshua amwombe Yehova afanye hivyo wakati jua halikuwahi kusimama tuli kabla ya hapo? Kwa sababu Yoshua alimwamini Yehova. Jua halikutua kwa siku nzima hadi Waisraeli walipowashinda wafalme Wakanaani na majeshi yao.
“‘Ndiyo’ yenu imaanishe ndiyo, na ‘Siyo’ yenu, siyo, kwa maana linalozidi hayo linatoka kwa yule mwovu.”—Mathayo 5:37
-