-
MajaliwaKutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko
-
-
Aliwaambia Wababiloni hivi: “Na wasimame, sasa, na kukuokoa, wanaoabudu mbingu, watazamaji wa nyota, ambao kwenye miezi mipya wanajulisha habari za mambo yatakayokuja juu yako. Tazama! Wamekuwa kama majani makavu. . . . Wale ambao umefanya kazi pamoja nao kama wachawi wako tangu ujana wako. Kwa kweli watatanga-tanga, kila mmoja kwenda katika eneo lake mwenyewe. Hakutakuwa na yeyote wa kukuokoa.”—Isa. 47:13-15.
-
-
Manabii wa UwongoKutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko
-
-
Manabii wa Uwongo
Maana: Mtu mmoja-mmoja na mashirika yanayotangaza ujumbe ambao wanadai hautoki kwa wanadamu, lakini ujumbe huo hautoki kwa Mungu wa kweli na haupatani na mapenzi yake yaliyofunuliwa.
Manabii wa kweli na wa uwongo wanaweza kutambuliwaje?
Manabii wa kweli hutangaza imani yao katika Yesu, lakini mengi yanahitajiwa kuliko kudai kuhubiri katika jina lake
1 Yoh. 4:1-3: “Yajaribuni maneno yaliyoongozwa na roho ili kuona kama yanatokana na Mungu, kwa sababu manabii wengi wa uwongo wameingia ulimwenguni. Mnalijua neno lililoongozwa na roho kutoka kwa Mungu kwa njia hii: Kila neno lililoongozwa na roho linalomkiri Yesu Kristo kuwa alikuja katika mwili hutokana na Mungu, lakini kila neno lililoongozwa na roho ambalo halimkiri Yesu halitokani na Mungu.”
Mt. 7:21-23: “Si kila mtu anayeniambia, ‘Bwana, Bwana,’ atakayeingia katika ufalme wa mbinguni, bali yule anayefanya mapenzi ya Baba yangu aliye mbinguni ndiye atakayeingia. Wengi wataniambia siku hiyo, ‘Bwana, Bwana, hatukutoa unabii katika jina lako . . . ?’ Na hata hivyo nitawaambia waziwazi: Sikuwajua ninyi kamwe! Ondokeni kwangu, ninyi wenye matendo ya uasi-sheria.”
Manabii wa kweli hutumia jina la Mungu, lakini kudai tu kumwakilisha hakutoshi
Kum. 18:18-20: “Nitawainulia wao nabii kutoka katikati ya ndugu zao, kama wewe; nami nitaweka maneno yangu katika kinywa chake, naye atasema nao yote nitakayomwamuru. Na itatukia kwamba mtu ambaye hatasikiliza maneno yangu ambayo atayasema katika jina langu, mimi mwenyewe nitamtaka ajibu. Hata hivyo, nabii atakayethubutu kusema katika jina langu neno ambalo sijamwamuru kusema au atakayesema katika jina la miungu mingine, nabii huyo lazima afe.” (Linganisha na Yeremia 14:14; 28:11, 15.)
Yesu alisema: “Sifanyi jambo lolote kwa uamuzi wangu mwenyewe; bali kama vile Baba alivyonifundisha, ndivyo ninavyosema mambo haya.” (Yoh. 8:28) Yeye alisema: “Nimekuja katika jina la Baba yangu.” (Yoh. 5:43) Pia Yesu alisema: “Yule ambaye husema mambo aliyotunga yeye mwenyewe anatafuta utukufu wake mwenyewe.”—Yoh. 7:18.
Ikiwa mtu mmoja-mmoja au mashirika yanadai kumwakilisha Mungu lakini yanakataa kulitumia jina la kibinafsi la Mungu, nao huzoea kutoa maoni yao wenyewe juu ya mambo, je, wanatimiza sifa hiyo muhimu ya nabii wa kweli?
Uwezo wa kufanya “ishara kubwa,” au “miujiza,” si lazima uwe uthibitisho wa nabii wa kweli
Mt. 24:24: “Makristo wa uwongo na manabii wa uwongo watatokea na kutoa ishara kubwa [“miujiza,” NAJ] na maajabu ili kuwapotosha, ikiwezekana, hata wale waliochaguliwa.”
2 The. 2:9, 10: “Kuwapo kwa huyo mwasi-sheria ni kulingana na utendaji wa Shetani pamoja na kila tendo lenye nguvu na ishara za uwongo na mambo ya ajabu na pamoja na kila udanganyifu usio wa uadilifu kwa wale wanaoangamia, kuwa malipo kwa sababu hawakukubali kuipenda ile kweli ili wapate kuokolewa.”
Kwa upande mwingine, Musa alifanya miujiza kwa mwelekezo wa Yehova. (Kut. 4:1-9) Yehova pia alimpa Yesu uwezo wa kufanya miujiza. (Mdo. 2:22) Lakini mbali na miujiza hiyo, mambo mengine zaidi yalithibitisha kwamba kweli Mungu alimtuma.
Yale ambayo manabii wa kweli wanatabiri hutimia, lakini huenda wasifahamu mambo hayo yatatimizwa wakati gani au jinsi gani
Dan. 12:9: “Nenda, Danieli, kwa sababu maneno hayo yamewekwa siri na kufungwa kwa muhuri mpaka wakati wa mwisho.”
1 Pet. 1:10, 11: “Manabii . . . waliendelea kuchunguza ni majira gani hasa au ni majira ya namna gani ambayo roho iliyokuwa ndani yao ilikuwa ikionyesha kumhusu Kristo ilipokuwa ikitoa ushahidi kimbele juu ya mateso ya Kristo na juu ya utukufu ambao ungefuata hayo.”
1 Kor. 13:9, 10: “Tuna ujuzi wa sehemu tu nasi tunatoa unabii kwa sehemu tu; lakini wakati kile kilicho kamili kitakapofika, kile kilicho kwa sehemu tu kitaondolewa mbali.”
Met. 4:18: “Lakini njia ya waadilifu ni kama nuru inayong’aa, inayozidi kuongezeka mpaka mchana mkamilifu.”
Mitume na wanafunzi wengine wa kwanza wa Kristo walikuwa na matarajio fulani yenye makosa, lakini Biblia haiwahesabu pamoja na “manabii wa uwongo.”—Ona Luka 19:11; Yohana 21:22, 23; Matendo 1:6, 7.
Nathani nabii alimtia moyo Mfalme Daudi afanye yale yaliyokuwa moyoni mwake kuhusu kujenga nyumba kwa ajili ya ibada ya Yehova. Lakini baadaye Yehova alimwambia Nathani amwambie Daudi kwamba si yeye atakayeijenga. Yehova hakumkataa Nathani kwa sababu ya yale aliyokuwa amesema mapema bali aliendelea kumtumia kwa sababu alisahihisha jambo hilo kwa unyenyekevu Yehova alipomweleza waziwazi.—1 Nya. 17:1-4, 15.
Maneno ya nabii wa kweli huendeleza ibada ya kweli na hupatana na mapenzi ya Mungu yaliyofunuliwa
Kum. 13:1-4: “Ikiwa nabii au mwotaji wa ndoto atainuka katikati yenu naye awape ishara au kitu cha ajabu, nayo ishara hiyo au kitu hicho cha ajabu kiwe kweli alichokuambia, akisema, ‘Na tuifuate miungu mingine, ambayo wewe hukuijua, nasi tuitumikie,’ usisikilize maneno ya nabii huyo au mwotaji huyo wa ndoto, kwa sababu Yehova Mungu wenu anawajaribu apate kujua ikiwa ninyi mnampenda Yehova Mungu wenu kwa moyo wenu wote na kwa nafsi yenu yote. Mnapaswa kumfuata Yehova Mungu wenu, nanyi mnapaswa kumwogopa yeye, nanyi mnapaswa kuzishika amri zake, nanyi mnapaswa kuisikiliza sauti yake, nanyi mnapaswa kumtumikia yeye, nanyi mnapaswa kushikamana naye.”
Kwa kuwa Biblia inasema kwamba “rafiki ya ulimwengu” ni adui ya Mungu, je, makasisi wanaowahimiza waumini wao wajiingize katika mambo ya ulimwengu wanaendeleza ibada ya kweli? (Yak. 4:4; 1 Yoh. 2:15-17) Mungu wa kweli alisema kwamba mataifa “watalazimika kujua kwamba mimi ni Yehova,” na Biblia inasema kwamba Mungu angechukua kutoka katika mataifa “watu kwa ajili ya jina lake,” lakini je, mashirika ya kidini yanayopuuza umuhimu wa kulitumia jina la kibinafsi la Mungu yanatenda kupatana na mapenzi hayo ya Mungu yaliyofunuliwa? (Eze. 38:23; Mdo. 15:14) Yesu aliwafundisha wafuasi wake wasali kuhusu Ufalme wa Mungu, na Biblia inaonya mtu asiwatumaini watu wa udongo, kwa hiyo je, makasisi au mashirika ya kisiasa yanayowahimiza watu wautumaini utawala wa wanadamu ni manabii wa kweli?—Mt. 6:9, 10; Zab. 146:3-6; linganisha na Ufunuo 16:13, 14.
Manabii wa kweli na wa uwongo wanaweza kutambuliwa kwa matunda wanayoonyesha katika maisha yao na maisha ya wafuasi wao
Mt. 7:15-20: “Jihadharini na manabii wa uwongo ambao wanakuja kwenu katika mavazi ya kondoo, lakini ndani wao ni mbwa-mwitu wenye kunyafua. Kwa matunda yao mtawatambua. . . . Kila mti mzuri huzaa matunda mazuri, lakini kila mti uliooza huzaa matunda yasiyofaa . . . Basi, kwa kweli kwa matunda yao mtawatambua watu hao.”
Wana maisha ya aina gani? “Matendo ya mwili ni . . . uasherati, uchafu, mwenendo mpotovu, ibada ya sanamu, mazoea ya kuwasiliana na pepo, uadui, mizozo, wivu, milipuko ya hasira, magomvi, migawanyiko, madhehebu, husuda, vipindi vya kulewa, karamu za kupindukia, na mambo kama hayo. . . . Wale walio na mazoea ya kufanya mambo ya namna hiyo hawataurithi ufalme wa Mungu. Kwa upande mwingine, matunda ya roho [ya Mungu] ni upendo, shangwe, amani, ustahimilivu, fadhili, wema, imani, upole, kujizuia.”—Gal. 5:19-23; 2 Pet. 2:1-3.
Je, Mashahidi wa Yehova hawajawahi kukosea katika mafundisho yao?
Mashahidi wa Yehova hawadai kuwa manabii wanaoongozwa na roho. Nyakati nyingine wao hukosea. Kama mitume wa Yesu Kristo, mara nyingine wao wamekuwa na matarajio fulani yenye makosa.—Luka 19:11; Mdo. 1:6.
Maandiko hutaja wakati mbalimbali kuhusiana na kuwapo kwa Kristo, na Mashahidi wa Yehova wamejifunza mambo hayo kwa makini sana. (Luka 21:24; Dan. 4:10-17) Yesu pia alisimulia ishara yenye mambo mengi, ambayo ingeambatana na utimizo wa unabii mbalimbali unaohusu wakati, ili kutambulisha kizazi ambacho kingeishi kione mwisho wa mfumo mbovu wa mambo wa Shetani. (Luka 21:7-36) Mashahidi wa Yehova wameonyesha uthibitisho wa kutimizwa kwa ishara hiyo. Ni kweli kwamba nyakati nyingine Mashahidi wamekosea katika kuelewa yale ambayo yangetukia kwenye mwisho wa vipindi fulani vya wakati, lakini hawajafanya kosa la kupoteza imani wala kuacha kukesha kuhusiana na kutimia kwa makusudi ya Yehova. Wameendelea kukumbuka kabisa shauri hili ambalo Yesu alitoa: “Endeleeni kukesha kwa sababu hamjui ni siku gani Bwana yenu atakuja.”—Mt. 24:42.
-