-
SerikaliKutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko
-
-
Hata watawala wafisadi wakipinduliwa na sheria zisizo za haki kutupiliwa mbali, serikali mpya itakuwa na wanadamu wasiokamilika na bado watakuwa sehemu ya mfumo wa kisiasa ambao Biblia inasema waziwazi kwamba uko chini ya uongozi wa Shetani.
Mt. 26:52: “Rudisha upanga wako mahali pake, kwa maana wale wote wanaouchukua upanga wataangamia kwa upanga.” (Yesu alimwambia hayo mmoja wa mitume wake wakati ambapo mamlaka ya serikali ilikuwa ikitumiwa isivyo haki dhidi ya Mwana wa Mungu mwenyewe. Je, hiyo haingekuwa sababu nzuri zaidi ya mtu kupigana, ikiwa hilo lingekuwa jambo zuri la kufanya?)
Met. 24:21, 22: “Mwanangu, mwogope Yehova na mfalme. Usishirikiane na watu wanaotaka badiliko. Kwa maana msiba wao utakuja ghafula, hivi kwamba ni nani anayejua juu ya kuangamizwa kwa watu wanaotaka badiliko?”
Basi suluhisho ni nini kwa matatizo ya ufisadi na ukandamizaji?
Dan. 2:44: “Mungu wa mbinguni atausimamisha ufalme [serikali] ambao hautaharibiwa kamwe. Na ufalme huo hautapewa watu wengine wowote. Utazivunja na kuzikomesha falme hizi zote, nao utasimama mpaka wakati usio na kipimo.”
Zab. 72:12-14: “[Yesu Kristo, mfalme aliyewekwa na Yehova] atamkomboa maskini anayelilia msaada, pia mwenye kuteseka na yeyote ambaye hana msaidizi. Atamsikitikia mtu wa hali ya chini na maskini, naye ataziokoa nafsi za maskini. Ataikomboa nafsi yao kutoka katika ukandamizaji na katika jeuri, nayo damu yao itakuwa na thamani machoni pake.” (Jinsi alivyowahangaikia watu hao alipokuwa duniani—alivyowaponya, alivyolisha umati wa watu, hata kutoa uhai wake kwa ajili yao—huonyesha kwamba yeye kwa kweli ndiye mtawala aliyetabiriwa katika unabii huo.)
Ona pia ukurasa wa 313-318, chini ya kichwa “Ufalme.”
Kwa nini tunapaswa kufikiria kwa uzito yale ambayo Biblia inasema kuhusu wakati ujao wa serikali?
Watawala wa kibinadamu hawatoi yale ambayo wanadamu wanahitaji kwa haraka
Fikiria mambo haya ambayo watu kila mahali wanahitaji, ambayo serikali za kibinadamu hazitoi lakini ambayo Mungu ameahidi: (1) Maisha katika ulimwengu usio na tisho la vita.—Isa. 2:4; Zab. 46:9, 10. (2) Chakula cha kumtosha kila mtu.—Zab. 72:16. (3) Nyumba nzuri kwa kila mtu.—Isa. 65:21. (4) Kazi ya kuridhisha kwa wote wanaoihitaji, ili waweze kujiruzuku wenyewe na familia zao.—Isa. 65:22. (5) Maisha yasiyoharibiwa na magonjwa na maradhi.—Ufu. 21:3, 4. (6) Haki; uhuru bila ubaguzi wa kidini, wa rangi, wa kiuchumi, na wa kikabila na kitaifa.—Isa. 9:7; 11:3-5. (7) Kuwa na usalama, bila wahalifu kuhatarisha maisha ya watu au mali zao.—Mika 4:4; Met. 2:22. (8) Ulimwengu ambamo sifa zenye kuthaminiwa zaidi zitatia ndani upendo, fadhili, watu kuhangaikiana, na ukweli.—Zab. 85:10, 11; Gal. 5:22, 23.
Kwa maelfu ya miaka, watawala wa kisiasa wamekuwa wakiwaahidi watu wao hali zilizo bora. Kukiwa na matokeo gani? Ijapokuwa watu katika mataifa mengi wana mali nyingi zaidi, si wenye furaha zaidi, nayo matatizo yanayowakabili ni mengi kuliko zamani.
Unabii wa Biblia umekuwa wenye kutegemeka kabisa
Karne moja mapema neno la Mungu lilitabiri cheo cha Babiloni cha kutawala ulimwengu, pia jinsi ambavyo mamlaka yake yangevunjwa mwishowe, na uhakika wa kwamba, ikiisha kuharibiwa, jiji lake kuu halingekaliwa tena kamwe. (Isa. 13:17-22) Karibu karne mbili mapema, hata kabla Koreshi hajazaliwa, Biblia ilitabiri kumhusu kwa kumtaja jina na pia daraka lake katika mambo ya kimataifa. (Isa. 44:28; 45:1, 2) Kabla Umedi na Uajemi hazijawa mamlaka ya ulimwengu, kuinuka kwake, ukiwa muungano wa mamlaka mbili, na jinsi ambavyo ungekoma, yote hayo yalitabiriwa. Zaidi ya karne mbili mapema mwendo wa milki ya ulimwengu ya Ugiriki chini ya mfalme wake wa kwanza ulitabiriwa, pia mgawanyiko wa baadaye wa milki hiyo kuwa sehemu nne.—Dan. 8:1-8, 20-22,
Biblia ilitabiri kirefu hali za ulimwengu za wakati wetu, na inatupasha habari kwamba serikali zote za kibinadamu zitakomeshwa mikononi mwa Mungu na kwamba Ufalme wa Mungu mikononi mwa Mwanawe, Yesu Kristo, utawatawala wanadamu wote.—Dan. 2:44; 7:13, 14.
Je, si jambo la hekima kutii chanzo cha habari ambacho kimetegemeka sana bila kugeuka-geuka?
Serikali ya Mungu ndiyo suluhisho pekee la kweli kwa matatizo ya wanadamu
Matatizo yanayohitaji kusuluhishwa yanataka nguvu, uwezo, na sifa ambazo wanadamu hawana. Mungu anaweza kuwaweka huru wanadamu kutoka katika uvutano wa Ibilisi na roho wake waovu, na Mungu ameahidi kufanya hivyo, lakini hakuna mwanadamu anayeweza kufanya hivyo. Mungu amefanya uandalizi wa kufanya yale ambayo sayansi ya tiba haiwezi kamwe kutimiza—kuondoa dhambi, hivyo kukomesha magonjwa na kifo na kufanya iwezekane watu wawe jinsi wanavyotaka kuwa kikweli. Muumba ana ujuzi unaohitajiwa (kuhusu dunia na taratibu zote za uhai) ili kusuluhisha matatizo ya uzalishaji wa chakula na kuzuia uchafuzi hatari, lakini mara nyingi jitihada za wanadamu huleta matatizo zaidi. Neno la Mungu tayari linageuza maisha ya watu hivi kwamba wale wanaoitikia uongozi wake wanakuwa wenye fadhili, watu wenye upendo na maadili bora, jamii ya watu wanaokataa kutumia silaha dhidi ya wanadamu wenzao na wanaoishi kwa amani na undugu wa kweli ijapokuwa wanatoka katika mataifa, rangi, na makabila yote.
Ufalme wa Mungu utaondoa wakati gani mfumo wa ulimwengu uliopo sasa? Ona vichwa “Vipindi vya Wakati” na “Siku za Mwisho.”
-
-
Shetani IbilisiKutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko
-
-
Shetani Ibilisi
Maana: Kiumbe wa roho ambaye ni mpinzani mkuu wa Yehova Mungu na wa wote wanaomwabudu Mungu wa kweli. Alipewa jina Shetani kwa sababu alianza kumpinga Yehova. Shetani pia anaitwa Ibilisi, kwa sababu yeye ndiye mchongezi mkuu wa Mungu. Shetani anaitwa nyoka wa zamani, labda kwa sababu alimtumia nyoka katika Edeni kumdanganya Hawa, na kwa sababu hiyo jina “nyoka” likaja kumaanisha “mdanganyifu.” Katika kitabu cha Ufunuo, mfano wa joka mkubwa anayenyafua unatumiwa kumhusu Shetani.
Tunaweza kujuaje kama kweli kuna mtu huyo wa roho?
Biblia ndiyo chanzo kikuu cha uthibitisho. Humo anaitwa kwa jina mara nyingi (Shetani mara 52, Ibilisi mara 33). Pia ushahidi wa kuwako kwa Shetani unaotoka kwa mtu aliyejionea kwa macho umeandikwa humo. Shahidi huyo aliyemwona kwa macho ni nani? Yesu Kristo, aliyeishi mbinguni kabla ya kuja duniani, mara nyingi alisema kumhusu mwovu huyo kwa kumtaja jina.—Luka 22:31; 10:18; Mt. 25:41.
-