Kazi Yetu ya Kuhubiri Ni Kazi Inayoonyesha Sifa ya Huruma
1 Yesu aliona kwamba watu wengi waliosikiliza mahubiri yake walikuwa “wamechunwa ngozi na kutupwa huku na huku kama kondoo wasio na mchungaji.” (Mt. 9:36) Kwa huruma na upendo, aliwafundisha njia za Yehova, akawafariji, na kuwasaidia wamjue Mungu. Tunapofikiri juu ya matendo ya Yesu, tunajifunza kuwaza na kujisikia kama yeye, na sifa hiyo ya huruma inaonekana wazi tunapohubiria watu.
2 Fikiri kidogo jambo ambalo Yesu alifanya wakati watu waliokosa tumaini lolote walipokuja kwake. (Luka 5:12, 13; 8:43-48) Alifikiria wale waliokuwa katika hali za kipekee. (Marko 7:31-35) Alitambua jinsi wengine walivyojisikia na akawahangaikia. Yeye hakuangalia tu hali ya inje ya mtu. (Luka 7:36-40) Bila shaka, Yesu alionyesha kabisa sifa ya huruma ya Mungu wetu.
3 ‘Aliwasikitikia’: Yesu hakufanya kazi yake ya kuhubiri kama mtu mwenye kulazimishwa. Yeye ‘aliwasikitikia’ watu. (Marko 6:34) Vilevile leo, sisi hatutolee tu watu habari lakini tunajaribu pia kuokoa maisha yao ambayo ndio ya maana sana. Tafuta kujua sababu gani watu wanakubali au wanakataa. Kwa nini wanakuwa wenye kuogopa au hawasikilize mambo unayosema? Je, wamepuuzwa (au kuzarauliwa) na pia kupofushwa na viongozi wa dini za uongo? Ikiwa tunapendezwa kweli na wengine, hilo litawachochea kusikiliza habari njema.—2 Kor. 6:4, 6.
4 Sifa ya huruma inagusa mioyo. Kwa mfano: Mwanamke mmoja aliteseka sana na kifo chenye kuhuzunisha cha binti wake wa miezi mitatu. Dada wawili walio Mashahidi walipogonga kwenye mlango wake, aliwakaribisha akiwa na wazo la kupinga maelezo yao kuhusu sababu inayomfanya Mungu aruhusu watu wateseke. Lakini, baadaye mwanamke huyo alisema hivi: “Walinisikiliza kwa huruma sana, na walipokuwa wakiondoka, nilijisikia vizuri sana hivi kwamba nikakubali warudi tena kunitembelea.” Unapohubiri, je, unajikaza kuonyesha sifa ya huruma kwa kila mtu unayekutana naye?
5 Kuonyesha sifa ya huruma kutatusaidia tuwafariji wengine kwelikweli. Tunapofanya hivyo, tunamtukuza Yehova, “Baba ya rehema nyororo.”—2 Kor. 1:3.