Tuunge Mkono Maoni ya Biblia Kuhusu Mazishi—Sehemu ya 3
Wakristo Wanafanya Mazishi kwa Njia Rahisi, Yenye Kiasi, na Yenye Kuheshimika
1. (a) Kwa nini wasio Mashahidi wanafanya mazishi makubwa na yenye kuvutia watu? (b) Watu fulani wanafanya nini ili kuvutia watu wengi zaidi kwenye mazishi?
1 Wale ambao hawaelewi hali ya wafu wanaamini kwamba kufanya mazishi makubwa yenye kuvutia watu ni kwa maana ili kufurahisha yule aliyekufa na kuepuka kuwakwaza wale waliofiwa. Wasio Mashahidi wanaona kuwa ni jambo la maana ‘kuonyesha’ cheo na mali ya yule aliyekufa ao ya familia yake. (1 Yoh. 2:16) Mara nyingi roho ya kushindana isiyo ya Kikristo inaonekana wakati wengi wanapojaribu kufanya mazishi ya hali ya juu kupita ya wengine. Ili kuwavuta watu wengi iwezekanavyo, vikaratasi vya kutangazia watu kuhusu mipango ya mazishi vinabandikwa huku na huku. Watu fulani wanaweza kuchelewesha mazishi kwa muda wa siku nyingi ao hata zaidi ya juma moja ili kukusanya feza zaidi kwa ajili ya mazishi makubwa na yenye sherehe nyingi zaidi. Wanaona hilo kuwa jambo la maana sana hivi kwamba hata familia zilizo maskini sana zinajisumbua mpaka kujiingiza katika madeni ili tu kupata feza kwa ajili ya “mazishi makubwa” yanayofanywa kulingana na nia ya watu wa jamaa na majirani.
2. (a) Jinsi gani Wakristo wanafanya mazishi kwa njia tofauti na ya watu wa ulimwengu? (b) Kulingana na Yohana 17:16 na Methali 11:2, kwa nini ni jambo la maana watu wa Mungu wafanye mazishi kwa njia rahisi na yenye kiasi?
2 Tofauti na hilo, watu wa Mungu wanaelewa wazi kwamba wafu hawajui kitu, hawajui kwamba wengine wanaendelea kuwaheshimu na kuwasifu. Wakristo wa kweli hawafanyi mazishi wakiwa na kusudi la kutafuta kujionyesha ili kuvutia wengine. Ikiwa tunafuata mazoea hayo, je, tutaonekana kuwa tofauti na ulimwengu kuhusiana na mafundisho tunayoamini? (Yoh. 17:16) Je, watu hawataona kwamba sisi pia tunawaogopa wafu? Kwa kuwa tunajua kwamba kuogopa wafu ni desturi ya mahali petu na kwamba inapendwa na watu wengi, jambo hilo litatusaidia tuwe waangalifu na kuona kwamba ni jambo la hekima kufanya mazishi kwa njia yenye kiasi na rahisi. (Met. 11:2) Namna gani tunaweza kufanya hivyo?
3. (a) Watu fulani wanatumia njia gani ili kukusanya feza kwa ajili ya mazishi? (b) Namna gani watu wa Yehova wanaona njia hizo?
3 Garama za Mazishi: Katika maeneo fulani, ndugu fulani wamekutana mbele mazishi yafanywe ili kupanga jinsi ya kupata feza kwa ajili ya mazishi. Wametuma barua kwa makutaniko mengine ili kuomba msaada wa feza. Ili kulipa garama za mazishi, ndugu wengine wameunda kati yao kisanduku kinachoitwa “feza kwa ajili ya mazishi.” Mbele ya kufanya mazishi, ndugu fulani, aliyechaguliwa na baraza la wazee, anaenda nyumba kwa nyumba ili kukusanya feza ao anafanya hivyo kwenye Jumba la Ufalme. Visanduku vya michango vinatayarishwa ili wale walio hapo watoe feza. Kwenye kilio, risiti (reçus) zinatolewa na matangazo yanafanywa kuhusu watu ao vikundi vya watu waliotoa michango na hesabu ya feza zilizotolewa. Chakula na pombe vinatolewa kwenye nafasi hiyo ili kuwachochea wale walio hapo watoe michango yao. Matendo hayo yanapaswa kuonwa namna gani? Wakristo wa kweli hawapaswi kuomba msaada wa feza kwa ajili ya mazishi kwa kutumia njia hizo.
4. (a) Ni nani aliye na daraka la kushugulikia garama za mazishi? (Ona maelezo ya chinic) (b) Ikiwa familia haina kabisa uwezo, inaweza kupata msaada wapi? (Ona maelezo ya chinid) (c) Kukubali feza kutoka kwa watu wa jamaa wasio Mashahidi kuna hatari gani, na namna gani Methali 27:12 inasaidia?
4 Watu wa familia ya Kikristo wanapaswa kujua kwamba ni wao walio na daraka la kushugulikia garama za mazishi.a Ikiwa familia fulani haina kabisa uwezo wa kulipia garama za mazishi rahisi, kwa hiyo watu wengine wa jamaa wa karibu wanaweza kusaidia.b (1 Tim. 5:3; Ona od uku. 132, fu. 1) Ikiwa hata hivyo hawafikie kupata feza za kufanya mazishi, basi ndugu na dada kibinafsi wanaweza kusaidia ao kutaniko. (1 Yoh. 3:17, 18) Hata hivyo, inaomba kuwa waangalifu. Wakati watu wa jamaa wasio Mashahidi wanaombwa kutoa msaada kwa ajili ya mazishi, hapo wanaweza kuona kwamba wana haki ya kutoa maoni yao kuhusu mipango ya mazishi. Jambo hilo linaweza kutokeza matatizo makubwa wakati tunapenda kufanya mazishi bila kuingiza mazoea yasiyo safi. Hilo halimaanishi kwamba Wakristo wa kweli hawatakubali michango ambayo watu wa jamaa wanatoa kwa kujipendea. Lakini ikiwa ndugu wanafikiri kwamba kukubali mchango wa wasio Mashahidi kutawafanya waingilie sana mipango ya mazishi na waombe kuongoza sherehe fulani za mazishi, hivyo inaomba kukataa kwa hekima mchango huo.—Met. 27:12.
5. (a) Soma Waefeso 4:17-19 na Waroma 12:2. Namna gani kanuni hizi zinatusaidia tunapofanya mipango ya mazishi? (b) Namna gani Yesu alizikwa, na hilo linaweza kutusadia jinsi gani? (c) Soma Luka 14:28 na 2 Wakorintho 8:12. Ili kuepuka kuomba michango, kukopesha feza, ao kujitia katika madeni, watu wa familia ya Kikristo watafanya mipango ya mazishi ya namna gani?
5 Kwa kuwa tunaelewa waziwazi hali ya wafu, hilo litatutia moyo kabisa kufanya mazishi yetu bila kufuata hata kidogo mazoea ya ulimwengu ambayo ni kawaida kati ya wale wasioelewa vizuri mafundisho ya Biblia. (Efe. 4:17-19) Ijapokuwa hatutaki kuwakwaza wengine kwa kurahisisha sana mipango ya mazishi, haturuhusu ulimwengu utukaze kuiga wale walio katika giza la kiroho. (Rom. 12:2) Tunaweza kukumbuka kwamba Yesu alikuwa mutu mkuu zaidi aliyepata kuishi; lakini alizikwa kwa njia rahisi na yenye kuheshimika. (Yoh. 19:40-42) Kwa wale walio na “akili ya Yesu,” kufuata mfano huu si kumkosea heshima yule aliyekufa. (1 Kor. 2:15, 16) Kwa hiyo, ili kuepuka kuomba msaada, kukopesha feza, ao kujiingiza katika madeni, watu wa familia ya Kikristo watatumia hekima kwa kufanya mipango ya mazishi iliyo rahisi na yenye kiasi kulingana na mapato yao.—Luka 14:28; linganisha 2 Kor. 8:12.
6. (a) Kwa nini si lazima kutuma matangazo kuhusu kifo na mipango ya mazishi kwa makutaniko mengine? (b) Kwa nini si jambo lenye kufaa kuvunja programu za mikutano ya mahubiri ao kubadili saa za mikutano kwa sababu ya mazishi? Soma na onyesha jinsi ya kutumia andiko la Mathayo 6:33, 34.
6 Kuendesha Mipango ya Mazishi: Habari ya kifo inafikia watu kwa haraka, kwa hiyo si lazima kutangaza habari ya kifo na mipango ya mazishi kwenye mikutano ya makutaniko mengine isipokuwa tu katika kutaniko la yule aliyekufa. Pia, si lazima kuandikia makutaniko mengine kwa kusudi hilo. Bila shaka, haitakuwa vizuri kuacha kufanya mikutano ao kubadili saa za mikutano ya kutaniko kwa sababu ya mazishi. Kwa kutia mambo ya kiroho pa nafasi ya kwanza, hilo linatusaidia kuendelea kuwa na maoni yenye kusawazika kuhusu kifo na kuendelea kutia faida za Ufalme pa nafasi ya kwanza katika maisha yetu.—Mt. 6:33, 34.
7. (a) Ni jambo gani litafanywa ikiwa hotuba ya Biblia inatolewa kwenye mazishi? (b) Msemaji ataepuka kufanya nini anapotoa hotuba?
7 Ikiwa wazee wa kutaniko wanakubali, hotuba ya Biblia inaweza kutolewa kwenye Jumba la Ufalme, ao ikiwa familia inataka, hotuba inaweza kutolewa kwenye nyumba ya yule aliyekufa ao mahali pengine. Msemaji aliyechaguliwa na familia iliyofiwa anapaswa kutumia plan ya hotuba iliyotayarishwa na tengenezo la Yehova. Hotuba ya mazishi inapaswa kuwa yenye kufariji, yenye kutia moyo, na yenye kujenga kiroho. Msemaji atazungumzia habari iliyo kwenye plan bila kuongeza mambo mengine yanayotegemea mafundisho ya uongo. Kwa mfano, kusema kwamba labda kifo kilitokana na laana ao na watu wengine hakupatani na kweli ya Biblia na kunakana uwezo wa Yehova wa kuwalinda watumishi wake. (Met. 18:10) Pia, msemaji atakuwa mwangalifu kwamba mambo anayosema katika hotuba ao katika sala yasifanye watu wafikiri kwamba anazungumza na yule aliyekufa. (Mhu. 9:5, 10) Ikiwa mtumishi mwaminifu wa Yehova amekufa, msemaji anaweza kuongeza katika hotuba maneno machache kuhusu maisha ya ushikamanifu ya ndugu huyo aliyekufa. (Ebr. 6:12) Lakini, wakati wa hotuba ya mazishi, halitakuwa jambo lenye kufaa kuruhusu watu wasimame na kusema maneno ya kumsifu yule aliyekufa, wala hawataruhusiwa kufanya hivyo mbele ya mazishi, wakati wa mazishi ao kisha hapo.
8. (a) Ndugu wengi wamekuwa na zoezi gani, na kwa nini tunapaswa kuepuka kufanya hivyo? (b) Tunapopanga hotuba ya mazishi, jinsi gani tutakuwa waangalifu kuhusu wakati na sala? (c) Ikiwa kutakuwa msimamizi wa hotuba, ataepuka kufanya nini?
8 Ndugu wamekuwa na zoezi la kukutana kwenye Jumba la Ufalme siku ambayo hotuba ya mazishi itatolewa ili kuimba nyimbo za Ufalme kwa muda wa saa nyingi mbele hotuba ianze. Ijapokuwa nyimbo za Ufalme zinaweza kutumiwa ili kuanza na kumalizia hotuba ya mazishi, itaonekana kuwa tunawaiga wale wanaojiita Wakristo ikiwa vikundi vya ndugu wanakutana ili kuimba kwa muda mrefu mbele hotuba ianze. Kwa kawaida, hotuba ya mazishi inafanya dakika 30 na inapaswa kuanza kwa wakati. Hotuba inaweza kuanza na sala ao hapana. Si lazima kuwe msimamizi wa hotuba atakayesema maneno ya utangulizi na kualika msemaji, na kisha hotuba, kusema maneno ya kumalizia. Lakini ikiwa kutakuwa mpango huo, maelezo ya ndugu huyo yatakuwa machache na yenye kuhusu tukio hilo. Si lazima arudilie mambo ambayo msemaji alizungumzia ao kutoa “maneno ya shukrani” kwa wale waliohuzuria hotuba. Ikiwa familia inataka, kisha kumzika mutu, maneno machache yanaweza kusemwa na sala kutolewa kwenye kaburi ili kumalizia. Tusisahau kwamba mutu asiye Shahidi hataruhusiwa kuongoza sehemu yoyote ya mazishi wala kusema maneno fulani kwenye Jumba la Ufalme ao kwenye kaburi.—2 Kor. 6:14-18.
9. Tunatiwa moyo kufanya nini tunapohuzuria hotuba ya mazishi?
9 Kuwa na Maoni Yenye Kufaa: Tunapaswa kuwa na maoni gani tunapohuzuria mazishi? Ijapokuwa tunaweza kuwa na moyo wenye huzuni nyingi, tunataka kufarijiwa na Maandiko. Kwa hivyo, wale wanaohuzuria hotuba ya mazishi watakumbuka kila wakati kuja na Biblia zao. Msemaji anaposoma na kuonyesha jinsi ya kutumia Maandiko ya Biblia, sisi pia tufuatane naye katika Biblia zetu, hivyo imani yetu itajengwa katika tumaini la ufufuo la wakati ujao, wakati ambapo “kifo hakitakuwapo tena.” (Ufu. 21:4) Pia, tuna nafasi ya kuwafariji wale waliofiwa na wageni wengine walio hapo. Tunapokuwa na maoni yanayofaa, tunaweza kuwafariji wengine na kutuliza huzuni yetu kwa kufikiria sana tumaini letu nzuri la wakati ujao, wakati ambapo Mungu atameza kifo milele.—Isa. 25:8.
10. (a) Namna gani wale walio katika giza la kiroho wanaonyesha huzuni yao? (b) Wale walio na uelewevu wa kiroho wanatenda namna gani, na kwa nini? Soma na onyesha jinsi ya kutumia 1 Wathesalonike 4:13.
10 Watu wengi wanafikiri kwamba kuhuzunika sana ndilo jambo linaloonyesha kwamba tunaheshimu na tunampenda mpendwa aliyekufa. Ndiyo sababu, wakati wa kuangalia mwili wa yule aliyekufa, wakati wa hotuba ya mazishi, ao kwenye kaburi, watu fulani wanalia kupita kiasi, wanajitupa chini, wanasemasema maneno kwenye sanduku kana kwamba yule aliyekufa angali hai. Wengine wamefikia hata kukumbatia mwili wa yule aliyekufa, kuingia katika sanduku ao kujaribu kujitupa katika kaburi. Ijapokuwa kifo kinaletea wote huzuni nyingi, watu wa Mungu hawaonyeshi huzuni yao kwa njia yenye kukosa usawaziko. Kwa nini? Kwa kuwa sisi si kama watu ‘wasiojua lolote kuhusu wale walalao usingizi katika kifo.’ Tunaelewa vizuri hali ya wafu. Tuna tumaini hakika katika ufufuo. (Yoh. 5:28, 29) Tunafarijiwa na ahadi hizo na hivyo ‘hatuna huzuni kama wale watu wengine wasio na tumaini.’—1 The. 4:13.
Desturi za Kisha Mazishi
11. (a) Baada ya mazishi, jinsi gani tunaweza kuhangaikia kwa upendo familia iliyofiwa? (b) Hatupaswi kutazamia kupata nini tunapotembelea familia iliyofiwa, na jinsi gani andiko la Matendo 20:35 linahusu jambo hilo?
11 Mwili ukiisha kuzikwa, kilio kinakwisha. Hakuna jambo lingine linaloweza kufanywa kwa ajili ya yule aliyekufa. Kisha mazishi, watu wanaweza kutembelea familia iliyofiwa ili kuifariji. Wakati kama huo, tunapata nafasi ya kufikiri kwa utulivu kuhusu uzima, kuona jinsi uzima ulivyo mfupi kabisa na kwamba ‘siku ya kufa ni bora kuliko siku ya kuzaliwa kwa mutu.’ (Mhu. 7:1) Si kuonyesha wema ikiwa wale wanaofariji wanaongezea mizigo wale waliofiwa kwa kuwalazimisha wawatolee chakula, pombe, na labda mahali pa kulala. Watu wa Yehova wanaamini kwamba kuna “furaha zaidi katika kutoa kuliko ilivyo katika kupokea.” (Mdo 20:35) Kwa hivyo, ni vizuri tufikirie yale tunayoweza kuwatolea wale waliofiwa; yaani, faraja kutokana na Maandiko na msaada wa kimwili, kuliko kufikiria tu kula chakula, kunywa pombe na kujifurahisha. Tunapofikiria mahitaji ya wale waliofiwa na kuepuka kuwa mzigo kwao, tunaonyesha upendo wa Kikristo na wema.—Gal. 6:2.
12. (a) Wale wasioelewa vizuri kweli ya Biblia wanafanya nini kisha mazishi? (b) Kwa nini watu wanapanga kukutana hivyo, na ni fundisho gani lisilo la Kikristo ambalo wanaamini?
12 Tuepuke Sherehe za Kisha Mazishi: Wale wasioelewa vizuri kweli ya Biblia wanatenda kwa njia iliyo tofauti wakati ambapo mazishi yamekwisha. Watu wa jamaa, majirani, na wengine wanakutana pamoja ili kula, kunywa, na kucheza muziki wenye sauti kubwa. Wengi wanaita hiyo “mazishi ya kweli.” Mara nyingi, kwenye pindi kama hizo, watu wanakula na kunywa kupita kiasi, wanacheza michezo yenye kuamsha tamaa mbaya, na wanatenda matendo yasiyofaa. Watu wengi, wanaposikia muziki huo wenye kuchezwa kwa sauti kubwa, wanakuja kujiunga kwenye sherehe hii hata ikiwa hawakumjua yule aliyekufa ao hawajui familia iliyofiwa. Watu fulani wamefikiri kwamba sherehe hiyo inawasaidia wasahau huzuni ya kifo. Hata hivyo, Wakristo wa kweli wanapaswa kujua kwamba watu wengi wanaamini kwamba sherehe kama hizo wakati wa kifo zina kusudi la kuheshimu wafu na kufungulia njia roho ya yule aliyekufa ili iwafikie mababu wake.
13. (a) Jinsi gani sherehe zinazofanywa kisha mazishi zinalingana na matukio yanayoelezwa katika andiko la Kutoka 32:1-6? (b) Soma Mhubiri 3:1, 4. Kwa nini sherehe kama hizo hazifai kwa watu wa Mungu? (c) Kulingana na andiko la Yohana 17:16 na 1 Wakorintho 10:7, kwa nini Wakristo wa kweli wanapaswa kuepuka kufanya ao kuhuzuria sherehe kama hizo?
13 Kulingana na maoni ya watu wengi, sherehe kama hizo zinaweza kuonwa kuwa sehemu ya desturi ya kwao. Hata hivyo, hatutafuata hata kidogo tabia isiyo ya Kikristo eti kwa sababu ni desturi ya kwetu. Kwa mfano, Waisraeli walikuwa na zoea ya kuimba na kucheza kulingana na desturi yao. Lakini walipochanga desturi yao na mazoea yasiyomheshimu Mungu, jambo hilo liliharibu uhusiano wao pamoja na Yehova. (Kut. 32:1-6) Ndivyo ilivyo kuhusiana na desturi ya kucheza na sherehe ambazo ni kawaida kwenye kilio. Mpendwa anapokufa si wakati wa kujifurahisha ao kufanya sherehe. (Mhu. 3:1, 4) Biblia inashauri kwa hekima hivi: “Afadhali sikitiko kuliko kicheko, maana kwa kukunjamana uso moyo huwa afadhali.” (Mhu. 7:3) Kwa kuwa mara nyingi sherehe hizo za kisha mazishi zinahusiana na mwenendo usiofaa na pia mambo ya mashetani, Wakristo wa kweli wanapaswa kuepuka kufanya ao kuhuzuria sherehe kama hizo. Tunapoepuka desturi kama hizo, tunaonyesha kwamba sisi “si sehemu ya ulimwengu” na kwamba tunamheshimu Mungu wa kweli na pia tunaheshimu zamiri za wengine.—Yoh. 17:16; 1 Kor. 10:7.
14. (a) Ni sherehe gani zinazofanywa mara nyingi kisha mazishi, na kwa kawaida zinafanywa wakati gani? (b) Kwa wale Wasio Mashahidi, sherehe hizo zina maana gani yenye kuhusiana na imani katika roho?
14 Sherehe ya Kumalizia Kilio na ya Ukumbusho wa Kifo: Kisha mazishi, watu fulani wa jamaa wanafanya mipango kwa ajili ya ile wanayoita sherehe ya “kumalizia kilio.” Wengine wanafanya ukumbusho wa kifo kila mwaka ili kumheshimu na kumkumbuka yule aliyekufa. Kwenye sherehe hizo, watu wanakula na kunywa pombe, muziki unachezwa na wanakusanya michango mingi. Ijapokuwa kipindi cha wakati wa kumalizia kilio kinaweza kutofautiana kuhusiana na muda, mara nyingi sherehe hiyo inafanywa siku ya 40, ao zaidi, kisha mazishi. Watu wengi wanaona sherehe ya kumalizia kilio na ya ukumbusho wa kifo kuwa sehemu ya maana ya kilio, kwa kuwa wanaamini kwamba roho ya yule aliyekufa haiwezi kufunguliwa mpaka wakati sherehe hizo zitakapofanywa.
15. (a) Kwa nini watu fulani wamefanya sherehe za kisha mazishi? (b) Ni ulizo gani linalotokezwa sasa?
15 Kuhuzuria ao kufanya sherehe ya mazishi majuma ao miezi kisha mazishi kunaweza kuonekana kuwa nafasi ya kupata ao kutoa faraja ya zaidi kwa waliofiwa. Inaweza kuonwa kuwa njia ya kuruhusu wale ambao hawakupata nafasi ya kuhuzuria mazishi wapate nafasi ya kuaga yule aliyekufa. Wengine wanachukua nafasi hiyo ili kuwashukuru wale waliotegemeza mipango ya mazishi. Je, tunaweza kusema kwamba kufanya sherehe za kisha mazishi ni jambo lenye kufaa kwa kutaniko na watu wa jamaa, kwa kuwa hakuna desturi za kipagani zinazofuatwa?
16 Kisha mazishi, watu wa jamaa wa karibu wanaweza kuamua kukutana kwa siri ili kuzungumzia garama za mazishi na mambo ya sheria yanayohusiana na kifo. Zaidi ya hiyo, kisha mazishi, watu fulani wanaweza kutaka kutolea wale waliofiwa msaada wa kimwili na wa kiroho. Hayo ni mambo ambayo mutu anaweza kufanya peke yake na haiombi kutaniko lote liingilie. Itakuwa namna gani ikiwa familia fulani inatayarisha kukusanya kutaniko, watu wa jamaa, na marafiki kisha mazishi? Kufanya mipango kama hiyo kunaweza kufanya wengine wafikiri kwamba Mashahidi wa Yehova wana namna yao ya kumalizia kilio ao wanafanya ukumbusho wa kifo. Kufanya hivyo kunaweza kuwakwaza kwa urahisi wale wanaojua mambo ambayo Mashahidi wa Yehova wanaamini na kufundisha kuhusu wafu. (1 Kor. 10:32) Kwa kuwa sherehe ya kumalizia kilio na ya ukumbusho wa kifo vinategemea kabisa imani katika roho za mababu, waabudu wa kweli wa Mungu wanaepuka jambo lolote linalofanana na sherehe za kisha mazishi. (2 Kor. 6:17) Tunapofanya hivyo, tunaonyesha kweli kwamba ‘tunachukia yaliyo mabaya’ na kupenda mambo yaliyo safi, na haki. (Zab. 97:10; Rom. 12:9) Acheni basi kila mmoja wetu aweke moyoni kanuni nzuri ambazo tumezungumzia, ili kuhakikisha kwamba sisi Wakristo tunafanya mazishi kwa njia rahisi, yenye kiasi, na isiyo na mazoea machafu.
[Maelezo ya Chini]
a Hapa tunazungumzia watu wa familia wa karibu, yaani wazazi na watoto wao.
b Hapa tunazungumzia watu wa jamaa wasio wa karibu, kama vile shangazi, wajomba, binamu (watoto wa shangazi na wa wajomba), na wengine.
16. (a) Ijapokuwa hakuna ubaya wowote kutembelea familia iliyofiwa, Wakristo wa kweli wataepuka kufanya nini? (b) Kulingana na 1 Wakorintho 10:32, 2 Wakorintho 6:17, na Zaburi 97:10, kwa nini inaomba tuepuke kufanya ao kuhuzuria sherehe yoyote inayofanywa kisha mazishi?
[Maulizo ya Funzo]
c Hapa tunazungumzia watu wa familia wa karibu, yaani wazazi na watoto wao.
d Hapa tunazungumzia watu wa jamaa wasio wa karibu, kama vile shangazi, wajomba, binamu (watoto wa shangazi na wa wajomba), na wengine.