Somo 11
Ikatae Dini Isiyo Ya Kweli!
Shetani na roho wake waovu hawataki wewe umtumikie Mungu. Wanataka ikiwezekana wamgeuze kila mtu kutoka kwa Mungu. Wao hujaribu jinsi gani kufanya hivyo? Njia moja wanayotumia ni dini isiyo ya kweli. (2 Wakorintho 11:13-15) Dini ambayo haifundishi kweli kutoka katika Biblia ni dini isiyo ya kweli. Dini isiyo ya kweli ni kama fedha za uwongo—huenda zikaonekana kuwa za kwelikweli, lakini hazina thamani yoyote. Dini isiyo ya kweli yaweza kukuletea matatizo mengi.
Mambo ya kidini yasiyo ya kweli hayawezi kumpendeza Yehova, Mungu wa kweli. Yesu alipokuwa duniani, kulikuwepo kikundi cha watu wa kidini waliotaka kumwua. Walifikiri kwamba ibada yao ndiyo ya kweli. Walisema hivi: “Tuna Baba mmoja, Mungu.” Je, Yesu alikubaliana nao? Hapana! Aliwaambia hivi: “Nyinyi mwatoka kwa baba yenu Ibilisi.” (Yohana 8:41, 44) Leo, watu wengi hufikiri kuwa wanamwabudu Mungu, na kumbe, wanamtumikia hasa Shetani na roho wake waovu!—1 Wakorintho 10:20.
Kama vile mti uliooza unavyozaa matunda mabaya, ndivyo dini isiyo ya kweli inavyotokeza watu wanaofanya mambo mabaya. Ulimwengu umejaa matatizo kwa sababu ya mambo mabaya ambayo watu hufanya. Kuna ukosefu wa adili, mapigano, wizi, kuonewa, mauaji, na kulala wanawake kinguvu. Watu wengi wanaofanya mambo mabaya hayo wana dini, lakini dini yao haiwachochei kutenda mambo mazuri. Hawawezi kuwa marafiki wa Mungu isipokuwa wanaacha kutenda mambo mabaya.—Mathayo 7:17, 18.
Dini isiyo ya kweli huwafundisha watu waombe sanamu. Mungu anasema watu wasiombe sanamu. Na kwa kweli haifai kufanya hivyo. Je, ungefurahi ikiwa mtu fulani angeongea na picha yako tu, wala haongei nawe kamwe? Je, mtu huyo angeweza kuwa rafiki yako wa kweli? Hapana, haingewezekana. Yehova anataka watu waongee naye, wala hataki waongee na sanamu au picha, ambazo hazina uhai.—Kutoka 20:4, 5.
Dini isiyo ya kweli hufundisha kwamba ni sawa kuwaua watu wakati wa vita. Yesu alisema kwamba marafiki wa Mungu wangependana. Hatuui watu tunaowapenda. (Yohana 13:35) Hata ni makosa kwetu kuwaua watu wabaya. Maadui wa Yesu walipokuja kumkamata, hakuwaruhusu wanafunzi wake wampiganie.—Mathayo 26:51, 52.
Dini isiyo ya kweli hufundisha kwamba watu waovu watateseka katika moto wa helo. Ingawa hivyo, Biblia hufundisha kwamba dhambi huongoza kwenye kifo. (Waroma 6:23) Yehova ni Mungu wa upendo. Je, Mungu mwenye upendo angeweza kutesatesa watu milele? Bila shaka hapana! Katika Paradiso, kutakuwako dini moja tu, ile inayokubaliwa na Yehova. (Ufunuo 15:4) Dini zote zinazotegemea uwongo wa Shetani zitaondolewa.