Watchtower—MAKTABA KU ENTERNETE
Watchtower
MAKTABA KU ENTERNETE
Kiswahili (Congo)
  • BIBLIA
  • VICHAPO
  • MIKUTANO
  • Biblia Iliokoka Hatari ya Kuharibika
    Munara wa Mulinzi (Gazeti la Watu Wote)—2016 | No. 4
    • HABARI KUBWA | BIBLIA ILIOKOKA NAMNA GANI?

      Biblia Iliokoka Hatari ya Kuharibika

      HATARI: Zamani, waandikaji wa Biblia na wale wenye walifanya kopi ya maandishi ya Biblia walitumia mafunjoa na ngozi za nyama. (2 Timotheo 4:13) Namna gani mafunjo na ngozi za nyama vilitia Biblia katika hatari?

      Mafunjo yanapasuka, yanapoteza rangi, na yanaregea haraka. Richard Parkinson na Stephen Quirke, wanasayansi wenye kujifunza mambo ya zamani ya Misri, wanasema hivi: “Kisha muda fulani, karatasi ya mafunjo inaweza kuanza kuharibika na kuwa kamba-kamba na kufikia kuwa vumbi. Wakati kitabu cha kukunjwa kinawekwa, kinaweza kuanza kuharibika ao kuoza kwa sababu ya baridi na kinaweza kukuliwa na panya ao vidudu, zaidi sana siafu wa rangi ya mweupe kama kinapatikana katika udongo.” Kisha kuvumbuliwa, mafunjo fulani yaliwekwa kwenye mwangaza mukubwa wa jua ao baridi kali, na hilo lilifanya mafunjo hayo yaharibike haraka.

      Ngozi za nyama zinakawia kuliko mafunjo, lakini zinaharibika pia kama zinatumiwa mubaya ao kama zinawekwa nafasi ya kifukutu ao ya baridi sana, na nafasi ya mwangaza mukubwa wa jua.b Ngozi ya nyama inaweza pia kukuliwa na vidudu. Ndiyo sababu kitabu kimoja kinasema hivi: “Ni nguvu sana maandishi ya zamani kuokoka.” (Everyday Writing in the Graeco-Roman East) Kama mafunjo ao ngozi za nyama zenye kuwa na maandishi ya Biblia zingeharibika, ujumbe wa Biblia ungepotea pia.

      NAMNA BIBLIA ILIOKOKA: Sheria ya Wayahudi ililazimisha kila mufalme ‘ajiandikie katika kitabu nakala ya Sheria hii,’ ni kusema, vitabu tano vya kwanza vya Biblia. (Kumbukumbu la Torati 17:18) Zaidi ya hilo, watu wenye kujua kufanya kopi waliandika kopi nyingi sana za maandishi kati ya mwaka wa 1 na 100 kisha kuzaliwa kwa Yesu. Kwa hiyo, Maandiko yangeweza kupatikana katika masinagogi ya Israeli yote na hata mbali katika Makedonia! (Luka 4:16, 17; Matendo 17:11) Sababu gani maandishi fulani ya zamani sana yanapatikana mupaka leo?

      [Picha katika ukurasa wa 4]

      Vitabu vya Kukunjwa vya Bahari ya Chumvi vimefanya mamia ya miaka bila kuharibika ndani ya mitungi ao ndani ya shimo nafasi yenye kukauka

      Philip Comfort, mwenye elimu ya Agano Jipya anasema hivi: “Wayahudi walijulikana kuwa watu wenye kuweka vitabu vya kukunjwa katika mitungi ili kuvilinda. Inawezekana Wakristo waliendelea pia na tabia hiyo. Ndiyo sababu maandishi fulani ya zamani ya Biblia yalivumbuliwa katika vyombo vya udongo, katika vyumba vidogo-vidogo, ndani ya mashimo, na mara fulani tu kwenye kukauka.

      MATOKEO: Maelfu ya sehemu ya maandishi ya Biblia yanapatikana mupaka leo. Maandishi fulani kati ya maandishi hayo yamefanya zaidi ya miaka 2000. Hakuna kitabu cha zamani chenye kuwa na maandishi mengi ya zamani sana kama Biblia.

      a Mafunjo (papyrus) ni karatasi zenye zilitengezwa kupitia mumea wenye kuitwa funjo. Mumea huo unaota nafasi kwenye kuwa maji.

      b Kwa mufano, Tangazo la Uhuru wa inchi ya États-Unis liliandikwa kwenye ngozi ya nyama. Sasa, kumepita karibu miaka 250 kisha tangazo hilo kuandikwa; lakini ngozi hiyo imepoteza rangi yake na kufanya ikuwe nguvu kusoma maandishi yenye kuwa ndani.

  • Biblia Iliokoka Hata Kama Kulikuwa Upinzani
    Munara wa Mulinzi (Gazeti la Watu Wote)—2016 | No. 4
    • HABARI KUBWA | BIBLIA ILIOKOKA NAMNA GANI?

      Biblia Iliokoka Hata Kama Kulikuwa Upinzani

      HATARI: Viongozi wengi wa politike na wa dini walikuwa na mipango yenye kupingana na ujumbe wa Biblia. Mara nyingi walitumia mamlaka yao ili kukataza watu kuwa na Biblia, kuichapisha, ao kuitafsiri. Tuone mifano mbili:

      • Mwaka wa 167 hivi mbele ya kuzaliwa kwa Yesu: Mufalme Antioko Epifane wa jamaa ya Seleuko, alitafuta kukaza Wayahudi wafuate dini ya Wagiriki. Kwa hiyo, alitoa amri ya kuharibu kopi zote za Maandiko ya Kiebrania. Mwanahistoria mwenye kuitwa Heinrich Graetz aliandika kwamba wakubwa katika utawala wa Antioko Epifane “walipasua na kuchoma vitabu vya kukunjwa vya Sheria kila wakati walivipata, na waliua wale wote wenye walikuwa wanatafuta nguvu na kitulizo kupitia usomaji wa vitabu hivyo.”

      • Katika kipindi cha 476-1500 hivi: Viongozi fulani wa dini ya Kikatoliki hawakufurahi kwa sababu waamini walihubiri mafundisho ya Biblia kuliko kuhubiri mafundisho ya dini ya Kikatoliki. Waliona kuwa mwasi-imani kila mwamini mwenye alikuwa na vitabu vya Biblia isipokuwa tu kitabu cha Zaburi katika luga ya Kilatini. Baraza fulani la kanisa lilitoa amri kwa kulazimisha watu wao “waendelee kutafuta waasi-imani kwa bidii na kwa uaminifu. . . kwa kuchunguza nyumba zote na vyumba vya chini ya udongo vya watu wenye waliwaziwa kuwa na vitabu vya Biblia. . . . Kila nyumba mwenye mwasi-imani atapatikana itabomolewa.”

      Kama maadui wa Biblia wangeweza kuiharibu, ujumbe wake ungepotea.

      [Picha katika ukurasa wa 5]

      Tafsiri ya Biblia ya Kiingereza ya William Tyndale iliokoka hata kama kopi za Biblia hiyo zilichomwa, zilikatazwa kutumiwa, na hata kama Tyndale aliuawa katika mwaka wa 1536

      NAMNA BIBLIA ILIOKOKA: Mufalme Antioko alikuwa na mupango mubaya juu ya inchi ya Israeli, lakini Wayahudi walikuwa tayari wanaishi katika inchi zingine nyingi. Watu wenye elimu wanafikiri kwamba kwa kila Wayahudi 100, zaidi ya 60 walikuwa tayari wanaishi inje ya Israeli kati ya mwaka wa 1 na 100 kisha kuzaliwa kwa Yesu. Wayahudi waliweka kopi za Maandiko katika masinagogi yao, na kopi hizo zilitumiwa pia na vizazi vyenye kufuata, hata Wakristo.—Matendo 15:21.

      Katika kipindi cha 476-1500 hivi, watu wenye walipenda Biblia hawakuogopa kuteswa na waliendelea kutafsiri na kufanya kopi za Maandiko. Inawezekana sehemu mbalimbali za Biblia zilipatikana katika luga 33 hivi katikati ya mwaka wa 1401 na 1500, mbele ya kutokea kwa mashini ya kuchapisha! Kwa hiyo, Biblia ilitafsiriwa na kuchapishwa sana kuliko zamani.

      MATOKEO: Wafalme wenye nguvu na viongozi wabaya wa dini walitaka kuharibu Biblia. Lakini, Biblia inaendelea kugawanywa na kutafsiriwa kuliko vitabu vyote katika historia. Biblia imekuwa na matokeo fulani juu ya sheria na luga za inchi nyingi, na juu ya maisha ya watu wengi.

  • Biblia Iliokoka Hata Kama Watu Walijaribu Kubadilisha Ujumbe Wake
    Munara wa Mulinzi (Gazeti la Watu Wote)—2016 | No. 4
    • [Picha katika ukurasa wa 7]

      Wamasora walifanya kopi za Maandiko kwa uangalifu

      HABARI KUBWA | BIBLIA ILIOKOKA NAMNA GANI?

      Biblia Iliokoka Hata Kama Watu Walijaribu Kubadilisha Ujumbe Wake

      HATARI: Biblia haikupotea hata kama kulikuwa hatari ya kuharibika na upinzani. Lakini, watafsiri na watu fulani wenye kufanya kopi walijaribu kubadilisha ujumbe wa Biblia. Wakati fulani, walijaribu kupatanisha Biblia na mafundisho yao kuliko kupatanisha mafundisho yao na Biblia. Tuchunguze mifano fulani:

      • Mahali pa kufanyia ibada: Kati ya mwaka wa 400 na 101 mbele ya kuzaliwa kwa Yesu, waandikaji wa Pantateki ya Wasamaria waliongeza kisha andiko la Kutoka 20:17 maneno “kwenye Mulima Gerizimu. Na hapo mutajenga mazabahu.” Kwa hiyo, Wasamaria walipenda watu waamini kwamba Maandiko yanaunga mukono kujenga hekalu kwenye Mulima Gerizimu.

      • Fundisho la utatu: Karibu miaka 300 kisha kumaliza kuandika Biblia, muandikaji mumoja mwenye kuunga mukono fundisho la utatu aliongeza kwenye 1 Yohana 5:7 maneno “mbinguni, Baba, Neno na Roho Mtakatifu, na watatu hawa ni moja.” Maneno hayo hayakupatikana katika maandishi ya kwanza ya Biblia. Bruce Metzger, mutu mwenye elimu ya Biblia, anasema kwamba “kuanzia mwaka wa 501 na kuendelea,” maneno hayo “yalipatikana mara kwa mara katika maandishi ya Kilatini cha Zamani na katika Vulgate [ya Kilatini].”

      • Jina la Mungu: Kwa kufuata desturi ya Wayahudi ya kukataa kutaja jina la Mungu, watafsiri wengi wa Biblia waliamua kuondoa jina la Mungu katika Maandiko. Walibadilisha jina la Mungu na majina ya cheo kama vile “Mungu” ao “Bwana.” Lakini katika Biblia, majina hayo yanatumiwa ili kuzungumuzia Muumbaji, wanadamu, vitu vyenye kutumiwa katika ibada ya uongo, na hata Shetani.—Yohana 10:34, 35; 1 Wakorintho 8:5, 6; 2 Wakorintho 4:4.a

      NAMNA BIBLIA ILIOKOKA: Kwanza, hata kama watu fulani wenye walifanya kopi za maandishi ya Biblia hawakuwa waangalifu ao hata kudanganya, wengine wengi walikuwa wenye ufundi na waangalifu sana. Wamasora walifanya kopi za Maandiko ya Kiebrania kati ya mwaka wa 501 na 1000 kisha kuzaliwa kwa Yesu. Kopi hizo zinaitwa Maandishi ya Wamasora. Inasemekana kwamba Wamasora walihesabu maneno na herufi ili kuhakikisha kama maandishi hayo hayana makosa. Kila nafasi waliwazia kwamba kulikuwa makosa katika maandishi yenye walitumia, waliandika pembeni. Wamasora walikataa kubadilisha maandishi ya Biblia. Profesa Moshe Goshen-Gottstein aliandika hivi: “Waliona kama kuyabadilisha kimakusudi ingekuwa kosa kubwa sana kwao.”

      Pili, maandishi mengi yenye kupatikana leo yanasaidia watu wenye elimu ya Biblia wavumbue makosa. Kwa mufano, viongozi wa dini walifundisha kwa miaka mingi kwamba tafsiri yao ya Biblia katika Kilatini haikuwa na makosa. Lakini, kwenye andiko la 1 Yohana 5:7, waliingiza makosa yenye tumetaja katika habari hii. Makosa hayo yaliingizwa hata katika Biblia ya Kiingereza yenye kupendwa sana ya King James Version! Lakini, wakati maandishi mengine yalivumbuliwa yalionyesha nini? Bruce Metzger aliandika hivi: “Maneno [yenye kuwa kwenye 1 Yohana 5:7] hayapatikane katika tafsiri zote za zamani (Kisiria, Kikoptiki, Kiarmenia, Kietiopia, Kiarabu, Kislavonia), isipokuwa tu katika tafsiri ya Kilatini.” Matokeo ni kwamba Biblia ya King James Version yenye iliandikwa upya na Biblia zingine ziliondoa makosa hayo.

      [Picha katika ukurasa wa 6]

      Chester Beatty P46, funjo la maandishi ya Biblia ya tangu mwaka wa 200 hivi kisha kuzaliwa kwa Yesu.

      Maandishi ya zamani yanashuhudia kwamba ujumbe wa Biblia haukubadilishwa? Wakati Vitabu vya Kukunjwa vya Bahari ya Chumvi vilivumbuliwa katika mwaka wa 1947, watu wenye elimu ya Biblia walilinganisha maandishi ya Kiebrania ya Wamasora na maandishi ya vitabu vya kukunjwa vya Biblia vyenye viliandikwa zaidi ya miaka elfu moja mbele. Mumoja kati ya watu wenye wanaandika habari juu ya Vitabu vya Kukunjwa vya Bahari ya Chumvi alisema kwamba kitabu kimoja kinatosha ili “kuhakikisha kabisa kwamba Wayahudi wenye walifanya kwa mikono kopi za maandishi ya Biblia kwa zaidi ya miaka elfu moja, walifanya hivyo kwa uaminifu na uangalifu sana.”

      Maktaba ya Chester Beatty ya Dublin, Irlande, iko na mafunjo yenye kuwa na karibu kila kitabu cha Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo. Kati ya mafunjo hayo kuna yale yenye yaliandikwa kati ya mwaka wa 101 na 200, miaka 100 tu kisha kumaliza kuandika Biblia. Kitabu kimoja chenye kufasiria maneno ya Biblia kinasema hivi: “Hata kama mafunjo hayo yanaleta habari ya mupya juu ya maandishi, yanaonyesha pia kwamba ujumbe wa Biblia haukubadilika wakati watu walikuwa wanafanya kopi ya maandishi ya Biblia.”—The Anchor Bible Dictionary.

      “Tunaweza kuhakikisha kwamba hakuna kitabu kingine cha zamani kimeandikwa hivyo bila makosa kutoka maandishi ya zamani”

      MATOKEO: Kuliko kuingiza makosa katika Biblia, kupatikana kwa maandishi mengi ya Biblia na miaka yenye maandishi hayo yamefanya, kumesaidia ujumbe wa Biblia ukuwe muzuri zaidi. Frederic Kenyon aliandika hivi juu ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo: “Hakuna kitabu kingine cha zamani chenye kuwa na ushuhuda mwingi na wa zamani juu ya maandishi yake, na kila mutu mwenye elimu na mawazo ya muzuri anaweza kukubali kwamba maandishi yenye tuko nayo hayana makosa.” Na William Henry Green, mutu mwenye elimu alisema hivi juu ya Maandiko ya Kiebrania: “Tunaweza kuhakikisha kwamba hakuna kitabu kingine cha zamani kimeandikwa hivyo bila makosa kutoka maandishi ya zamani.”

      a Ili kupata habari zaidi, ona kitabu Biblia Inafundisha Kabisa Nini? kwenye ukurasa wa 195-197, kinapatikana pia kwenye adresi ya Internete www.pr2711.com.

Vichapo vya Swahili (Congo) (1996-2026)
Toka
Ingia
  • Kiswahili (Congo)
  • Tumia Wengine
  • Préférences
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Kanuni za Matumizi
  • Kanuni za Kutunza Siri
  • Paramètres Kuhusu Kutunza Siri
  • JW.ORG
  • Ingia
Tumia Wengine