Somo 2
Mungu Ndiye Rafiki Bora Unayeweza Kuwa Naye
Kuwa rafiki ya Mungu ndilo jambo bora zaidi kwako. Mungu atakufundisha jinsi ya kuwa mwenye furaha na mwenye usalama; atakuweka huru kutokana na imani nyingi zisizo za kweli na mazoea yanayodhuru. Atasikiliza sala zako. Atakusaidia ufurahie amani ya ndani na uwe na uhakika. (Zaburi 71:5; 73:28) Mungu atakusaidia wakati wa matatizo. (Zaburi 18:18) Na Mungu anakutolea zawadi yake ya uhai udumuo milele.—Waroma 6:23.
Unapomkaribia Mungu, utawakaribia marafiki wa Mungu. Wao watakuwa marafiki wako pia. Kwa kweli, watakuwa kama ndugu na dada zako. Watafurahia kukufundisha juu ya Mungu nao watakusaidia na kukutia moyo.
Sisi hatulingani na Mungu. Unapojitahidi kuwa rafiki ya Mungu, lazima uelewe jambo moja la maana. Kuwa rafiki ya Mungu si sawa na kuwa rafiki ya mtu unayelingana naye. Mungu ni wa kale zaidi na mwenye hekima zaidi, naye ana nguvu zaidi kuliko sisi. Yeye ndiye Mtawala aliye na haki ya kututawala. Basi tukitaka kuwa marafiki wake, ni lazima tumsikilize na kufanya mambo anayotuambia tufanye. Tukifanya hivyo, tutapata mema sikuzote.—Isaya 48:18.