Somo 3
Unahitaji Kujifunza Juu Ya Mungu
Ili uwe rafiki ya Mungu, unahitaji kujifunza juu yake. Je, marafiki wako wanajua jina lako, nao hulitumia? Ndiyo. Mungu pia anataka ujue jina lake na kulitumia. Jina la Mungu ni Yehova. (Zaburi 83:18; Mathayo 6:9) Lazima pia ujifunze mambo yanayompendeza na yale yasiyompendeza. Unahitaji kujua marafiki wake na maadui wake. Kumjua mtu huchukua muda. Biblia inasema kwamba ni jambo la hekima kuweka kando wakati wa kujifunza juu ya Yehova.—Waefeso 5:15, 16.
Marafiki wa Mungu hufanya mambo yanayompendeza. Wafikirie marafiki wako. Ukiwatendea mabaya na kufanya mambo wanayochukia, je, wataendelea kuwa marafiki wako? Bila shaka hapana! Vivyo hivyo, ukitaka kuwa rafiki ya Mungu, unahitaji kufanya mambo yanayompendeza.—Yohana 4:24.
Si dini zote hutokeza urafiki na Mungu. Yesu, ambaye ndiye rafiki wa karibu zaidi wa Mungu, alizungumza juu ya barabara mbili. Barabara moja ni pana, nayo imejaa watu. Barabara hiyo huongoza kwenye uharibifu. Barabara ile nyingine ni nyembamba, nayo ina watu wachache wanaoitembea. Barabara hiyo huongoza kwenye uhai udumuo milele. Kwa hiyo, ukitaka kuwa rafiki ya Mungu, lazima ujifunze njia ya kweli ya kumwabudu.—Mathayo 7:13, 14.